Kweli Ilinirudishia Uhai Wangu
Wengi wa rafiki zangu wa zamani wamekufa kutokana na UKIMWI. Kabla ya vifo vyao, niliwaona kwa ukawaida barabarani. Ningekuwa mfu pia kama si kwa sababu ya kweli. Ebu nieleze.
NILIZALIWA Desemba 11, 1954, nikiwa mtoto wa pili na wa mwisho wa John na Dorothy Horry. Walinipa jina Dolores, lakini wakati wa kuzaliwa mama aliniita Dolly kwa sababu alifikiri nilionekana kama mwanasesere. Lakabu hiyo ilidumu, lakini watu hawakufahamu wakati huo kwamba ningekuja kuwa tatizo kubwa sana kwa mama yangu.
Tuliishi katika nyumba za reli—ziliitwa hivyo kwa sababu ya muundo wazo mrefu na mwembamba. Zilikuwa katika barabara ya 61st Street katika New York City. Nyumba hiyo haikuwa nzuri sana; na panya walikuwapo pia. Walakini, baada ya kuumwa na panya usiku mmoja, mara moja tulihama.
Katika 1957, tulihamia upande wa mashariki wa Manhattan ya chini. Ikilinganishwa na mahali tulipohama, hapa palikuwa mahali pazuri sana—vyumba vizuri vya kulala, bustani kubwa nje ya dirisha langu na mandhari ya East River. Ningeweza kuona boti zikipita na watoto wakicheza mpira wa mguu wa Kimarekani na besiboli katika uwanja. Ndiyo, hii ilikuwa paradiso kwangu. Kisha maisha yangu yaliyo salama yakaanza kuharibika.
Uraibu wa Alkoholi na Dawa za Kulevya
Mama na baba walikuwa wakibishana sana. Kwanza sikuelewa sababu, lakini nilianza kuona kwamba baba yangu alikuwa mlevi wakati wote. Hangeweza kutunza kazi, na ni mama pekee aliyekuwa anafanya kazi. Rafiki zangu walipojua kwamba baba alikuwa mraibu wa alkoholi, dhihaka niliyopata ilifanya maisha yangu kuwa mabaya sana.
Hali iliendelea kuwa mbaya sana. Hatimaye, baba alikuwa mjeuri sana naye mama akamfukuza nyumbani. Hivyo tukawa familia ya mzazi mmoja. Nilikuwa na umri wa miaka minane au tisa, na nilihisi nimelemezwa na hali ya familia yetu. Mama alilazimika kufanya kazi kwa kuendelea ili kupata pato la kulipia gharama, akituacha dada yangu na mimi kwa majirani baada ya shule.
Nilipofika darasa la sita, nikawa mwasi sana. Ningetoroka masomo na kwenda kwenye Tompkins Square Park na kunywa alkoholi ili kusahau matatizo yangu. Baada ya muda mfupi nilianza kushirikiana na umati wa rafiki wenye umri mkubwa zaidi. Nilikuwa na umri wa miaka 11 tu, lakini nilionekana mkubwa kwa umri wangu, hivyo niliweza kuonekana mwenye umri wa miaka 16 au 17. Umati huu wa marafiki wapya, ulikunywa, ulivuta bangi, ulitumia dawa za kulevya za LSD nao walijidunga heroini. Naam, nilitaka kuwa kama wao, hivyo nilianza kutumia vitu hivyo. Nilipofika umri wa miaka 14, nilikuwa mraibu wa vitu hivyo.
Mama Agundua
“Nilikuzaa na nitakuua.” Huo ulikuwa usemi katika ujirani wetu wa akina mama ambao wameumizwa sana na kutamaushwa na watoto wao. Mama, ambaye wakati wote ni mtulivu na mwenye kujiweza, alipogundua kwamba binti yake mwenye umri wa miaka 14 alikuwa akitumia heroini, alisema atafanya hivyo hasa—kuniua.
Nilikimbilia chumba cha kuogea na kujaribu kujifungia kwa kuzuia mlango kwa kujitegemeza kwa besheni kubwa ya kuogea, lakini nilichelewa sana. Sasa nilikuwa kwenye taabu kwelikweli! Bila haja ya kusema, nilipigwa vilivyo. Kitu tu kilichoniokoa na hasira ya mama ni kwamba dada yangu na mtu aliyeniripoti kwa mama, walifanikiwa kuingia bafuni na kumshika mama yangu ndipo nilipoweza kutoroka nyumbani. Hatimaye niliporudi nyumbani—kwani nilitoroka kwa siku kadhaa—nilikubali kupata msaada kwa tatizo langu la dawa za kulevya.
Napata Msaada wa Kitaalamu
Miezi michache baadaye, niliona tangazo katika televisheni kuhusu kituo cha urekebishaji wa wale walioathiriwa na dawa za kulevya. Ni mahali ambapo watu wenye kuhitaji msaada kikweli wa kushinda matatizo yao ya matumizi ya dawa za kulevya wanaweza kupata msaada huo. Nilizungumzia yale niliyoyaona pamoja na mama, naye alinipeleka katika mojawapo vituo hivyo katika New York City. Kituo hicho huandaa mazingira ya kifamilia ambako watu hupata kitia-moyo kubadilisha mtindo-maisha wao wote. Niliishi hapo kwa karibu miaka miwili na nusu.
Ingawa nilifaidika kutokana na msaada uliotolewa, nilitamaushwa sana nilipogundua kwamba baadhi ya wafanyakazi wa kituo hicho ambao niliwatumaini na kuwaheshimu—ambao walipaswa kuwa wameacha kutumia dawa za kulevya—walirudia kuzitumia tena. Nilihisi nimesalitiwa na kuwa mpumbavu. Walitufundisha kwamba ule msemo wa zamani, “Ukiisha kuwa mraibu, daima utakuwa mraibu,” ulikuwa ni uwongo. Lakini sasa niliwaona wakiwa ushahidi halisi kwamba ule msemo wa zamani haukuwa uwongo.
Hata hivyo, nikiwa na miaka 17, nilirudi nyumbani nikiwa si mtumiaji tena wa dawa za kulevya na nikiazimia kufanya yote niwezayo nisitumie heroini tena. Wakati huo, mama yangu na dada yangu walikuwa wameanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.
Bado Mshiriki Asiyefaa wa Familia
Ingawa nilikuwa nimeacha kutumia dawa za kulevya, bado nilihisi kama mshiriki asiyefaa wa familia. Hii ni kwa sababu sikuwa tayari kuishi kupatana na sheria mpya za nyumbani, ambazo zilitia ndani kutovuta sigareti, kutoenda disko na kadhalika. Haikuwa muda mrefu kabla mama hajanifukuza nyumbani kwa sababu nilikataa kubadili mashirika yangu na mtazamo wangu wa kilimwengu. Kwa kweli nilimchukia kwa sababu ya hilo, lakini kwa kweli hilo lilikuwa jambo bora ambalo angeweza kunifanyia. Alishikilia kanuni za uadilifu na kamwe hakuyumba.
Hivyo niliondoka nyumbani ili nijifanyie maisha mapya yaliyo bora. Nilirudi shule kujifunza ustadi fulani ili kunisaidia kulipia gharama za chuo. Nilifanya vizuri sana nikawa mshiriki mwenye faida kwa jumuiya. Nilipata kazi yenye mshahara mzuri na nyumba yangu mwenyewe. Kisha mapenzi yalianza nilipokutana na rafiki yangu wa zamani. Tulianzisha upya uhusiano wetu na tulikusudia kufanya kila kitu sawasawa na kufunga ndoa.
Hata hivyo, hatimaye rafiki yangu alianza kutumia dawa za kulevya, na mambo yakaanza kutuharibikia sisi sote. Nikishindwa kuvumilia maumivu ya kihisia-moyo, nilifanya kile nilichoona ni bora—nilitumia dawa za kulevya ili kutuliza hisia zangu. Nilijihusisha na kokeini, ambayo iliandaa kile kilichoitwa ulevi wa matajiri. Kokeini ilikubalika wakati huo kwa sababu wengi hawakuifikiria kuwa inaleta uraibu. Lakini kwangu, hiyo ilikuwa mbaya kuliko heroini.
Katika miaka ya katikati ya 1970, nilikuwa mtumiaji kwa miaka mitatu hivi. Hatimaye, nilianza kufikiria maisha mabaya niliyokuwa ninaishi, nilianza kujiuliza, ‘Je, maisha ni haya tu?’ Nilifikia mkataa kwamba ikiwa ndivyo, basi nilikuwa nimechoshwa nayo. Nilimrudia mama na kumwambia kwamba nimechoka na mtindo-maisha huu na kwamba nilikuwa ninarudi kwenye kituo cha urekebishaji. Baada ya kuwa hapo kwa mwaka mmoja na nusu mwingine, nikaacha dawa za kulevya.
Karibu Nipate Kweli
Kwa mara nyingine nilipata kazi nzuri, nyumba nzuri, na rafiki wa kiume. Tukachumbiana. Wakati huohuo, mama aliendelea kuwasiliana nami kwa ukawaida. Angeongea nami kuhusu Biblia na kunitumia Mnara wa Mlinzi na Amkeni! lakini kamwe sikuyaangalia. Nilimwambia mama mipango yangu ya kufunga ndoa na kuwa na familia. Hivyo alinitumia kitabu ambacho kilibadili maisha yangu kabisa—Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha.
Kadiri nilivyosoma kitabu hiki, nilijua kile nilichotaka na kwamba nimekuwa nikienda katika njia isiyo sawa. Hatimaye, mtu fulani alielewa jinsi nilivyohisi na kile hasa kilichokuwamo katika moyo wangu. Sikuwa tofauti kwa kuwa na hisia hizo—nilikuwa kawaida! Hata hivyo, mtu niliyekuwa nikijihusisha naye alinicheka nilipomwonyesha kitabu Maisha ya Jamaa na Biblia. Asingeweza kufanya mabadiliko ya lazima ili kuwa na maisha ya familia yenye furaha. Hivyo nilikuwa na uamuzi mgumu wa kufanya—kuishi naye au kuachana naye. Niliamua kwamba ni wakati wa kumwacha na kwenda sehemu nyingine.
Rafiki yangu alikasirika sana. Siku moja niliporudi nyumbani, nilipata kwamba alikuwa amechana nguo zangu zote vipande-vipande kwa kutumia wembe. Karibu kila kitu nilichomiliki kilikuwa kimeenda—viatu, makoti, fanicha—zilikuwa zimechanwa ama kuuzwa. Nilibakiwa tu na nguo nilizovaa. Nilitaka kulala chini na kufa. Nyakati nyingine unachoshwa na mapambano ya maisha. Hivyo unarudia kufanya kile ambacho wakati wote umekuwa ukipambana nacho—kutuliza hisia zako kwa kutumia dawa za kulevya. Nilifikiria ama nifanye hivyo ama nijiue.
Ingawa nilirudia kutumia dawa za kulevya tena, mama kamwe hakuacha kunisaidia. Angenitembelea na kuniletea nakala za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Jioni moja katika mazungumzo, nilimwambia jinsi nilivyohisi—kwamba nilichoka kujaribu na nilikuwa nimechoshwa na matatizo hayo. Kwa urahisi alisema: “Umejaribu kila kitu, kwa nini usimjaribu Yehova?”
Naokolewa na Kweli
Ilikuwa katika 1982 kwamba nilikubali kufanya kile alichokuwa amenisihi kwa miaka yote kufanya. Nilianza kujifunza Biblia kwa uzito. Baada ya muda mfupi nilianza kusisimka kuhusu yale niliyokuwa ninajifunza. Nilianza kutambua kwamba uhai wangu ni wenye thamani sana kwa Yehova na kwamba kuna kusudi la kweli katika maisha. Lakini nilitambua kwamba ikiwa nilikuwa ninataka kumtumikia Yehova, nilipaswa kufanya mabadiliko mengi na kwamba nilihitaji utegemezo wa kihisia-moyo na kiroho. Hivyo, nilimwomba mama ikiwa ningeweza kurudi nyumbani tena.
Mama alikuwa mwenye tahadhari, kwani mara nyingi nilikuwa nimemtamausha. Aliongea na mzee Mkristo kuhusu ombi langu la kurudi na kuishi naye. Alipogundua kwamba mama alihisi kuna uwezekano mkubwa kwamba wakati huu ningeweza kuwa nimebadilika kweli kweli, alisihi: “Kwa nini usimpe fursa nyingine?”
Kwa shukrani, wakati huu sikumtamausha mama. Niliendelea kujifunza Biblia na kuanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Kwa msaada wa Yehova, nilibadili kabisa mtindo-maisha wangu. Shauri liandaliwalo na Biblia, Neno la Mungu la kweli, liliniwezesha kupitia hali ngumu. (Yohana 17:17) Hata niliacha kuvuta sigareti, uraibu ambao ulikuwa mgumu kwangu kuushinda kuliko uraibu wa heroini na kokeini. Kwa mara ya kwanza nilihisi furaha kuwa hai.
Miezi michache baadaye, katika Desemba 24, 1983, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Aprili iliyofuata, nilianza upainia-msaidizi, namna mojawapo ya kuongeza utumishi. Kwanza, washiriki wangu wa zamani waliponiona katika utumishi wa shambani walinidhihaki. Ilikuwa kama vile mtume Petro alivyoonya kimbele: “Mambo ambayo wao huona kuwa ni ajabu ya ninyi kutokwenda mbio pamoja nao katika ufisadi ule ule usio na kiasi, wakiwatukana.”—1 Petro 4:4.
Katika Septemba 1984, nikawa painia wa kawaida, na mara nilikuwa ninaongoza mafunzo kumi ya Biblia kwa juma. Baadhi ya mafunzo haya ni wale waliokuwa wamenidhihaki nilipoanza utumishi kwa mara ya kwanza. Huu ulikuwa wakati wa kusisimua sana katika maisha yangu kwa sababu niliweza kusaidia vijana kadhaa waikubali kweli ya Biblia. Wakati wote nilitaka kuwa na watoto, hivyo kuwa mama, kitamathali, kwa wototo wa kiroho kumekuwa chanzo cha shangwe ya wakati wote kwangu.—Linganisha 1 Wakorintho 4:15.
Kadiri miaka ilivyopita, ningewaona barabarani karibu na nyumbani kwetu rafiki wa zamani ambao nilikuwa ninatumia dawa za kulevya pamoja nao. Likiwa tokeo la kushirikiana sindano na watu walioambukizwa, wameambukizwa UKIMWI na kuwa hoi kwelikweli. Wengi wamekufa tayari. Ninajua kwamba ningeweza kuwa mfu ikiwa si kweli ya Biblia. Kwa maana hiyo, imenirudishia uhai wangu.
Epuka Maumivu
Mara nyingi mimi hutamani kwamba nilipokuwa mtoto ningeijua kweli na kuepuka maisha yaliyojaa maumivu na taabu. Sasa Yehova hunisaidia kukabili maumivu yanayotokana na kutumia ujana vibaya, hata hivyo nitalazimika kungoja mpaka mfumo mpya ili kuondoa kabisa makovu ya kihisia-moyo. (Ufunuo 21:3, 4) Leo, ninajitahidi sana kuwaambia wachanga kwamba wao wamebarikiwa kumjua Yehova na kuwa na msaada wa tengenezo lake ili kutumia kile anachofundisha.
Ulimwengu waweza kuonekana umemeremeta na kuvutia. Na unataka uamini kwamba unaweza kufurahia aina yao ya furaha bila ya maumivu. Lakini bila shaka hili haliwezekani. Ulimwengu utakutumia na utakapokwisha kumaliza kukutumia, utakutupa mbali. Biblia inasema kweli kwamba Ibilisi ni mtawala wa ulimwengu huu—kwelikweli yeye ni mungu wao—na kwamba hatupaswi kuupenda ulimwengu wala vitu vilivyomo. (Yohana 12:31; 14:30; 16:11; 2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 2:15-17; 5:19) Kwa vile watu wa ulimwengu wanaishi wakiwa watumwa wa ufisadi, ushirika wao hauwezi kukuletea furaha ya kweli.—2 Petro 2:19.
Tumaini langu ni kwamba kwa kueleza mambo haya kunihusu kutasaidia wengine kuona kwamba “uhai ulio halisi”—uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu—ndio uhai pekee unaostahili kufuatwa. Bila kujali mambo mazuri na mabaya tuwezayo kukabili kadiri tutembeavyo katika kweli, hali katika ulimwengu wa Shetani si nzuri hata kidogo. Shetani hujitahidi kufanya ionekane kuwa nzuri. Mimi husali kwamba, pamoja na ndugu na dada zangu Wakristo, niweze kukaza macho yangu juu ya uhai halisi, ndiyo juu ya uhai wa milele katika dunia iliyo paradiso. (1 Timotheo 6:19)—Kama ilivyosimuliwa na Dolly Horry.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Nikiwa pamoja na mama yangu, tukitoa ushahidi katika Tompkins Square Park