“Maangamizi ya Vitu vya Asili”
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA IRELAND
PUPA inatisha dunia. Inadhoofisha uwezo wa dunia wa kuandaa chakula na makao ambayo sote tunahitaji ili kuishi. Bila shaka tayari umejua jinsi pupa inavyoharibu dunia, lakini hapa pana vikumbusha vichache.
Kuchafuliwa kwa Dunia
Huko nyuma katika 1962, Rachel Carson, katika kitabu chake Silent Spring, alionya kuhusu kuchafua dunia kwa dawa za kuua wadudu na takataka zenye sumu. Kitabu The Naked Savage chasema hivi: “Mwanadamu alikuwa akichafua mazingira yake na kuyaharibu makao yake mwenyewe, jambo linalotoa ishara ya kutoweka kwa viumbe.” Wanadamu wangali wanachafua dunia kwa pupa. “Wakitafuta faida kubwa zaidi katika muda mfupi zaidi,” lasema World Hunger: Twelve Myths, “wakulima wa mashamba makubwa wako tayari kutumia kupita kiasi, maji, na kutumia kemikali nyingi bila kufikiria mmomonyoko wa udongo, kumalizwa kwa maji yatokayo chini, na kuchafuliwa kwa mazingira.”
Badala ya kulinda misitu ya mvua yenye thamani sana—ambayo ni muhimu sana kwa kuwapo kwa dunia—wanadamu wanaiharibu kwa kasi kuliko wakati mwingine wowote. “Misitu ya kitropiki yenye afya,” wasema waandikaji wa Far From Paradise—The Story of Man’s Impact on the Environment (1986), “karibu itapotea katika miaka 50 ijayo ikiwa mwendo wa uharibifu wa sasa waendelea bila kupunguzwa.”
Wavuvi wasio wanyoofu hutumia baruti na sumu za kemikali kuvua samaki kwenye miamba ya matumbawe—ambayo imefafanuliwa kuwa “vifanani vya misitu ya mvua ya kitropiki” kwa sababu ya uhai mwingi ambao matumbawe hutegemeza. Njia hizo katili za kuvua samaki pamoja na uchafuzi wa kemikali unaofanywa bila kujali “umeharibu kabisa” matumbawe mengi yenye afya.—The Toronto Star.
“Ni Sisi Wenyewe Ambao Tumejiletea Pigo”
Sir Shridath Ramphal, aliyekuwa msimamizi wa IUCN-Muungano wa Uhifadhi Ulimwenguni, tokea 1991 hadi 1993, afafanua aina hiyo ya matumizi mabaya ya mali za dunia kuwa “maangamizi ya vitu vya asili.” Maangamizi hayo ni mabaya kadiri gani? Akitoa mfano, Ramphal aandika: “Mito mingi ya India ni kama tu mabomba yaliyo wazi ya maji machafu ikibeba uchafu kutoka sehemu za mijini na mashambani kuelekea baharini.” Anakata kauli gani? “Ni sisi ambao wenyewe tumejiletea pigo.”
Pupa imetawala historia ya mwanadamu kwa karne nyingi, lakini tisho la dunia yetu kutoendelea kuwapo limeongezeka. Kwa nini? Kwa sababu uwezo wa mwanadamu wa kuharibu ni mkubwa zaidi sasa. “Kwa miaka hamsini [50] tu ambayo imepita,” chasema Far From Paradise, “tumekuwa na uwezo wa kemikali na kiufundi wa kuharibu kabisa namna nyingine za uhai katika dunia yetu. . . . Homo sapiens [Kilatini, mtu mwenye hekima], kama mwanadamu anavyojiita isivyofaa, ana karibu uwezo wote naye hajizuii.” Majuzi, shirika la mazingira la Greenpeace lilitoa shutuma kali, likisema: “Mwanadamu wa kisasa amefanya Paradiso [dunia] kuwa mahali pa takataka . . . na sasa amekaa kama kitoto kikatili . . . kwenye ukingo . . . wa kuharibu kabisa dunia hii yenye uhai mwingi.”
Lakini pupa inaathiri zaidi kuliko kutisha tu matazamio ya wakati ujao ya dunia. Inatisha furaha na usalama wako mwenyewe na wa familia yako. Kwa njia gani? Ona makala ifuatayo.