Wenye Kubadilikana, Hata Hivyo Wenye Wajibu Kuelekea Viwango vya Kimungu
“WATU wastahimilivu si wapumbavu kamwe, na watu wapumbavu si wastahimilivu kamwe,” yasema methali moja ya Kichina. Kuna mengi ya kweli katika methali hii, kwa sababu kuwa mstahimilivu ni jambo gumu, lenye kuhitaji kuwa na wajibu kwa viwango vifaavyo vya mwenendo. Lakini twapaswa kujiwajibisha kwa viwango gani? Je, halingekuwa jambo la akili kufuata viwango vilivyowekwa na Mfanyi wa wanadamu, kama vinavyoelezwa katika Neno lake, Biblia Takatifu? Mungu mwenyewe huweka kielelezo cha kufuata viwango vyake.
Muumba—Kielelezo Chetu Kikuu
Mungu Mweza Yote, Yehova, amesawazika kabisa katika ustahimilivu, akionyesha ustahimilivu usio mwingi kupita kiasi wala usio mchache kupita kiasi. Kwa maelfu ya miaka, amestahimili wale wanaoharibia sifa jina lake, wanadamu wafisadi, na wale wanaoitumia dunia vibaya. Mtume Paulo aliandika, kama ilivyorekodiwa kwenye Waroma 9:22, kwamba Mungu “alivumilia kwa ustahimilivu mwingi vyombo vya hasira ya kisasi vilivyofanywa kufaa kwa ajili ya uharibifu.” Kwa nini Mungu amekuwa mstahimilivu kwa muda mrefu hivyo? Kwa sababu ustahimilivu wake una kusudi.
Mungu ni mwenye subira kuelekea wanadamu “kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Muumba amepatia wanadamu Biblia na amepatia watumishi wake utume wa kujulisha kila mahali viwango vyake vya mwenendo. Wakristo wa kweli wanawajibika kwa viwango hivi. Lakini je, hilo lamaanisha kwamba ni lazima watumishi wa Mungu wawe wagumu katika kila hali?
Wenye Uthabiti, Hata Hivyo Wenye Kubadilikana
Yesu Kristo alitia moyo wale wanaotafuta uhai wa milele ‘waingie kupitia lango jembamba.’ Lakini kuingia kupitia lango jembamba hakumaanishi kuwa na akili iliyofungika. Ikiwa tuna mwelekeo wa kutawala au kutaka watu wafuate maoni yetu tunapokuwa na wengine, kwa hakika itafanya maisha yawe yenye kufurahisha kwa kila mtu ikiwa tutazuia mwelekeo huu. Lakini jinsi gani?—Mathayo 7:13; 1 Petro 4:15.
Theofano, mwanafunzi Mgiriki, aliyeeleza kwamba wakati uliotumiwa pamoja na watu wa malezi tofauti-tofauti uliongoza katika kuwafahamu vizuri zaidi, alisema: “Ni jambo la muhimu kwamba tujaribu kuona jinsi wanavyofikiri badala ya kuwalazimisha kufuata njia yetu ya kufikiri.”Kwa hiyo, kwa kupata kumjua mtu vyema zaidi, twaweza kugundua kwamba ladha yake katika chakula na hata lahaja yake si ya ajabu kama tulivyofikiri. Badala ya nyakati zote kuwa na mengi ya kusema kuliko wengine au kusisitiza kusema neno la mwisho, twajifunza mambo yenye mafaa kwa kusikiliza maoni ya mwingine. Kwa hakika, watu wenye akili iliyofunguka hupata maisha yakiwa yenye kuthawabisha sana.
Wakati wowote upendezi wa kibinafsi unapohusika, twapaswa kuwa wenye kubadilikana na kuruhusu wengine wafurahie chaguo lao wenyewe. Lakini wakati mwenendo ni jambo la utii kwa Muumba wetu, twapaswa kuwa thabiti. Mungu Mweza Yote havumilii aina zote za mwenendo. Alionyesha hili kwa shughuli zake pamoja na watumishi wake wakati uliopita.
Mtego wa Kuwa Mstahimilivu Kupita Kiasi
Eli, kuhani mkuu wa taifa la kale la Israeli, alikuwa mtumishi wa Mungu ambaye alinaswa katika mtego wa kuwa mstahimilivu kupita kiasi. Waisraeli walikuwa wameingia katika uhusiano wa kiagano pamoja na Mungu, wakikubali kutii sheria zake. Lakini wana wawili wa Eli, Hofni na Finehasi, walikuwa wenye pupa na wasio na adili na walikosa staha sana kwa Mweza Yote. Eli, ingawa aliijua vema sana Sheria ya Mungu, alitoa karipio pole tu na alilegea katika kutoa nidhamu. Alifanya kosa la kufikiri kwamba Mungu angestahimili uovu. Muumba hutofautisha udhaifu na uovu. Kwa sababu ya kuasi kimakusudi Sheria ya Mungu, wana waovu wa Eli waliadhibiwa vikali—na ilikuwa hivyo kwa kufaa.—1 Samweli 2:12-17, 22-25; 3:11-14; 4:17.
Lingekuwa jambo la huzuni kubwa kama nini kwetu kuwa wenye ustahimilivu kupita kiasi katika familia yetu kwa kujifanya hatuoni makosa yenye kurudiwa ya watoto wetu! Ni jambo zuri zaidi kama nini kuwalea “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova”! Hili lamaanisha kwamba ni lazima tushikamane na viwango vya kimungu vya mwenendo sisi wenyewe na kuvikaza katika watoto wetu.—Waefeso 6:4.
Vivyo hivyo, kutaniko la Kikristo haliwezi kustahimili uovu. Ikiwa mshiriki azoea kutenda makosa na kukataa kutubu, ni lazima aondoshwe. (1 Wakorintho 5:9-13) Hata hivyo, nje ya mzingo wa familia na kutaniko, Wakristo wa kweli hawajaribu kubadili jamii kwa ujumla.
Uhusiano Imara Pamoja na Yehova
Ukosefu wa ustahimilivu hutokea katika mazingira ya hangaiko. Hata hivyo, ikiwa tuna uhusiano wa karibu pamoja na Mungu, sisi hufurahia hisi ya usalama ambayo hutusaidia kudumisha usawaziko ufaao. “Jina la BWANA ni ngome imara; mwenye haki huikimbilia akawa salama,” ndivyo tusomavyo kwenye Mithali 18:10. Kwa hakika hakuna madhara yawezayo kutupata au kupata wapendwa wetu ambayo Muumba hatayashughulikia kwa wakati wake.
Mtu aliyenufaika sana kutokana na uhusiano mzuri pamoja na Mungu alikuwa mtume Paulo. Akiwa Myahudi aliyeitwa Sauli, yeye aliwanyanyasa wafuasi wa Yesu Kristo na alikuwa na hatia ya umwagaji wa damu. Lakini Sauli mwenyewe alikuja kuwa Mkristo, na akiwa mtume Paulo, baadaye alieneza evanjeli kwa wakati wote. Paulo alidhihirisha mtazamo wa akili iliyofunguka kwa kuhubiria watu wote, “kwa Wagiriki na kwa Wabaribari pia, kwa wenye hekima na kwa wasio na akili pia.”—Waroma 1:14, 15; Matendo 8:1-3.
Yeye alifauluje kubadilika? Kwa kupata ujuzi sahihi wa Maandiko na kukua katika upendo kwa Muumba, ambaye hana upendeleo. Paulo alijifunza kwamba Mungu ni mwenye haki katika njia ya kwamba Yeye huhukumu watu wakiwa mtu mmoja-mmoja, si kulingana na utamaduni au jamii, lakini kulingana na kile alicho mtu na anachofanya. Ndiyo, kwa Mungu, matendo ni ya muhimu. Petro alitaja kwamba “Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Mungu Mweza Yote hana upendeleo. Ni tofauti na viongozi fulani wa ulimwengu, ambao huenda wakatumia ukosefu wa ustahimilivu kimakusudi kwa makusudi yao wenyewe.
Nyakati Zinabadilika
Kulingana na John Gray, wa Chuo Kikuu cha Oxford katika Uingereza, ustahimilivu ni “sifa ambayo siku hizi imekuwa nadra sana kupatikana.” Lakini hilo litabadilika. Ustahimilivu uliosawazishwa na hekima ya kimungu utaenea.
Katika ulimwengu mpya wa Mungu ulio karibu, ukosefu wa ustahimilivu utatoweka. Namna mbaya za ukosefu wa ustahimilivu, kama vile ubaguzi na ushupavu, zitatoweka. Kuwa na akili iliyofungika hakutazuia tena furaha katika maisha. Kisha, kutakuwa na paradiso tukufu sana kuliko yoyote ile ambayo imewezekana kuwapo katika Bonde la Kashmir.—Isaya 65:17, 21-25.
Je, unatazamia kuishi katika ulimwengu huo mpya? Ni pendeleo lililoje na litafurahisha kama nini!
[Picha katika ukurasa wa 8]
Mtume Paulo alionyesha usawaziko ufaao kwa sababu alikuwa na uhusiano pamoja na Mungu