Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 2/22 kur. 17-19
  • Kweli Kuhusu Kusema Uwongo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kweli Kuhusu Kusema Uwongo
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uwongo wa Kwanza
  • Matokeo Yenye Kufisha
  • Zoea Lililotia Mizizi
  • Uwongo wa Kidini Leo
  • Uhitaji wa Kulinda
  • Kuchukua Msimamo kwa Ajili ya Ukweli
  • Kwa Nini Ni Rahisi Sana Kusema Uwongo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Semeni Ukweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Uongo wa Kwanza—Nani Aliyeusema?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Paradiso Yapotea
    Biblia—Ina Ujumbe Gani?
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 2/22 kur. 17-19

Kweli Kuhusu Kusema Uwongo

“MWONGO wewe!” Je, umepata kurushiwa maneno hayo yenye kuchoma? Ikiwa ndivyo, bila shaka unajua mpigo wa kihisia-moyo yaliyo nao.

Sawa tu na vile chombo cha kuwekea maua kipendwacho sana kiwezavyo kuvunjika vipande-vipande kigongeshwapo sakafuni, ndivyo uhusiano wenye thamani uwezavyo kuharibiwa na uwongo. Ni kweli, baada ya kipindi cha wakati, huenda ukaweza kurekebisha madhara hayo, lakini huenda uhusiano huo usiwe kamwe kama ulivyokuwa.

“Wale wapatao kujua kwamba wamedanganywa,” chasema kitabu Lying—Moral Choice in Public and Private Life, “wanakuwa na hadhari sana na jitihada za mwongo za kurudisha urafiki. Na wanatazama nyuma katika itikadi zao na matendo ya wakati uliopita wakikumbuka uwongo waliougundua.” Baada ya udanganyo kufunuliwa, huenda uhusiano ambao wakati mmoja ulisitawi kwa mazungumzo manyoofu na tumaini ukazimwa na hali ya kushuku na tashwishi.

Tukiwa na hisia zote zisizofaa zinazohusianishwa na kusema uwongo, ni lazima tuulize, ‘Zoea hilo potovu lilianzaje?’

Uwongo wa Kwanza

Yehova Mungu alipowaumba wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, aliwaweka katika makao mazuri ya shamba. Makao yao hayakuwa na namna yoyote ya udanganyo au ulaghai. Yalikuwa paradiso kwelikweli!

Hata hivyo, wakati fulani baada ya kuumbwa kwa Hawa, Shetani Ibilisi alimjia akiwa na toleo lenye kushawishi. Hawa aliambiwa kwamba ikiwa angekula “matunda ya mti huo,” ambao Mungu alikataza, hangekufa kama Mungu alivyokuwa amesema kwamba angekufa. Badala ya hivyo, ‘angekuwa kama Mungu, akijua mema na mabaya.’ (Mwanzo 2:17; 3:1-5) Hawa alimwamini Shetani. Akachukua tunda hilo, akalila, kisha akampa mumewe. Lakini badala ya kuwa kama Mungu kulingana na alivyoahidi Shetani, Adamu na Hawa wakawa watenda-dhambi wasiotii, watumwa wa ufisadi. (2 Petro 2:19) Na kwa kusema uwongo wa kwanza, Shetani akawa “baba wa uwongo wote.” (Yohana 8:44, Today’s English Version) Baada ya muda, wenye dhambi hawa watatu walijifunza kwamba hakuna manufaa wakati mtu anaposema uwongo au anapoamini uwongo.

Matokeo Yenye Kufisha

Yehova alitaka uumbaji wake wote—mbinguni na duniani—ujue kwamba kutotii kimakusudi hakutaepuka adhabu. Yeye alitenda kwa haraka kwa kumhukumia adhabu kiumbe huyo wa kiroho mwenye kuasi aishi muda wote wa maisha yake nje ya tengenezo la Mungu lililo takatifu. Isitoshe, Yehova Mungu atahakikisha hatimaye kwamba Shetani anaharibiwa kabisa. Hilo litatokea wakati “mbegu” aliyoahidi kuandaa Mungu itakapotia jeraha lenye kufisha kichwani.—Mwanzo 3:14, 15; Wagalatia 3:16.

Kwa upande wao Adamu na Hawa waliondoshwa kutoka shamba la Edeni. Mungu akampasisha adhabu Adamu, akisema: “Kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe nawe mavumbini utarudi.” Baada ya muda, wote Adamu na Hawa walikufa, sawa tu na alivyotabiri Mungu.—Mwanzo 3:19.

Wakiwa wazao wa Adamu, familia yote ya kibinadamu ‘imeuzwa chini ya dhambi.’ Wanadamu wote wamerithi kutokamilika kunakoongoza kwenye kifo. (Waroma 5:12; 6:23; 7:14) Matokeo ya uwongo wa kwanza ni yenye kufadhaisha kama nini!—Waroma 8:22.

Zoea Lililotia Mizizi

Kwa kuwa Shetani na malaika waliojiunga naye katika uasi dhidi ya Mungu hawajafishwa, hatupaswi kushangaa kwamba wanachochea wanadamu ‘kusema uwongo.’ (1 Timotheo 4:1-3) Likiwa tokeo, uwongo umetia mizizi sana katika jamii ya kibinadamu. “Uwongo umeingizwa sana katika jamii,” likataja Los Angeles Times, “hivi kwamba jamii sasa haihisi kama upo.” Wengi leo hushirikisha siasa na wanasiasa na uwongo, lakini je, ulijua kwamba viongozi wa kidini wamo miongoni mwa wasemaji uwongo sugu?

Wapinzani wa kidini wa Yesu walieneza uwongo kumhusu wakati wa huduma yake ya kidunia. (Yohana 8:48, 54, 55) Yeye aliwalaumu hadharani, akisema: “Nyinyi mwatoka kwa baba yenu Ibilisi, nanyi mwataka kufanya tamaa za baba yenu. . . . Wakati asemapo uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.”—Yohana 8:44.

Je, wakumbuka uwongo uliosambazwa wakati kaburi la Yesu lilipopatikana likiwa tupu baada ya ufufuo wake? Biblia yasema kwamba makuhani wakuu “wakawapa hao askari-jeshi kiasi cha kutosha cha vipande vya fedha na kusema: ‘Semeni, “Wanafunzi wake walikuja wakati wa usiku na kumwiba tulipokuwa tumelala usingizi.”’” Uwongo huu ulienezwa sana, na wengi walidanganywa kwa huo. Viongozi hao wa kidini walikuwa waovu kama nini!—Mathayo 28:11-15.

Uwongo wa Kidini Leo

Ni uwongo mkuu ambao unasemwa na viongozi wa kidini leo? Unafanana na ule ambao Shetani alimwambia Hawa: “Hakika hamtakufa.” (Mwanzo 3:4, italiki ni zetu.) Lakini Hawa alikufa, na kurudi ardhini, mavumbini ambapo kutoka huko alifanyizwa.

Hata hivyo, je, yeye alionekana kuwa amekufa tu na kwa hakika kuishi kwa umbo jingine? Je, kifo ni kiingilio cha uhai mwingine? Biblia haionyeshi kwamba sehemu fulani iliyo hai ya Hawa iliendelea kuishi. Nafsi yake haikuendelea kuishi. Kwa kukosa kumtii Mungu, yeye alikuwa ametenda dhambi, na Biblia yasema: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.” (Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible) Hawa, kama mume wake, aliumbwa kuwa nafsi inayoishi, na uhai wake akiwa nafsi inayoishi ulikoma. (Mwanzo 2:7) Kuhusu hali ya wafu, Biblia husema: “Wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Ingawa hivyo, ni nini ambacho makanisa hufundisha kwa kawaida?

Makanisa mara nyingi hufundisha kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa na kwamba kifo huiachilia ili ipate uhai mwingine—ama wa raha ama wa mateso. Kwa kielelezo, The Catholic Encyclopedia, husema: “Kanisa hufundisha waziwazi umilele wa maumivu ya helo kuwa kweli ya itikadi ambayo hakuna awezaye kuibishania au kuipinga bila uzushi wa wazi.”—Buku la 7, ukurasa 209, toleo la 1913.

Fundisho hilo ni tofauti kama nini na kile ambacho Biblia yasema waziwazi! Biblia yafundisha kwamba mtu anapokufa, “huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” (Zaburi 146:4) Kwa hiyo, kulingana na Biblia, wafu hawawezi kupata maumivu yoyote, kwa kuwa hawana ufahamu wa chochote kile. Kwa hiyo, Biblia huhimiza hivi: “Lo lote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako; kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [kaburi la kawaida la wanadamu] uendako wewe.”—Mhubiri 9:10.

Uhitaji wa Kulinda

Sawa na vile wengi walivyopotoshwa na uwongo wa makuhani katika siku ya Yesu, ndivyo kulivyo na hatari ya kudanganywa na mafundisho yasiyo ya kweli ya viongozi wa kidini wa leo. Watu hawa ‘wameibadili kweli ya Mungu kwa uwongo,’ na wanaendeleza mafundisho yasiyo ya kweli kama vile kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu na wazo la kwamba nafsi za wanadamu zitateswa katika moto wa helo.—Waroma 1:25.

Kwa kuongezea, dini za leo kwa kawaida huweka mapokeo na falsafa za kibinadamu katika kiwango kimoja na kweli ya Biblia. (Wakolosai 2:8) Hivyo, sheria za Mungu kuhusu adili—kutia ndani sheria juu ya ufuatiaji wa haki na mwenendo wa kingono—zaonwa kuwa za kadiri, si kamili. Tokeo ni kama inavyofafanuliwa katika gazeti Times: “Uwongo unasitawi katika ukosefu wa uhakika wa jamii, wakati ambapo watu hawafahamu tena, au kukubaliana juu ya kanuni zinazoongoza mwenendo wao kuelekeana.”—Linganisha Isaya 59:14, 15; Yeremia 9:5.

Kuishi katika mazingira ambayo kweli haionwi kuwa kitu cha maana hufanya iwe vigumu kutii onyo la Mungu la kutosema uwongo. Ni nini kiwezacho kutusaidia tuwe tukisema kweli sikuzote?

Kuchukua Msimamo kwa Ajili ya Ukweli

Tamaa yetu ya kumtukuza Muumba wetu hutuandalia kichocheo kizuri sana cha kusitawisha usemi wenye kweli. Kwa umaana, Biblia humwita “Mungu wa kweli.” (Zaburi 31:5) Kwa hiyo, ikiwa ni tamaa yetu kumpendeza Muumba wetu, ambaye huchukia “ulimi wa uwongo,” tutasukumwa kumwiga. (Mithali 6:17) Twaweza kufanyaje hilo?

Funzo lenye bidii la Neno la Mungu laweza kutupatia kinachohitajiwa ili ‘tuseme kweli kila mmoja wetu pamoja na jirani yake.’ (Waefeso 4:25) Hata hivyo, kujua tu kile Mungu anataka tufanye hakutoshi. Ikiwa kama wengi ulimwenguni leo, sikuzote hatujakuwa na mwelekeo wa kusema kweli, tutahitaji kufanya jitihada halisi ya kufanya hivyo. Huenda tukahitaji kufuata kielelezo cha mtume Paulo na kujiwekea viwango vigumu. “Napiga-piga mwili wangu ngumi na kuuongoza kama mtumwa,” Paulo aliandika.—1 Wakorintho 9:27.

Msaada wa ziada katika pigano la kusema kweli nyakati zote ni sala. Kwa kumwomba Yehova usaidizi, twaweza kuwa na “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida.” (2 Wakorintho 4:7) Kwa hakika, kudumisha “mdomo wa kweli” na kuondosha “ulimi wa uongo” kwaweza kuwa jambo la jitihada kwelikweli. (Mithali 12:19) Lakini kwa msaada wa Yehova hilo laweza kutimizwa.—Wafilipi 4:13.

Kumbuka sikuzote kwamba ni Shetani Ibilisi ambaye hufanya ionekane kwamba kusema uwongo ni jambo la kawaida. Yeye alimdanganya mwanamke wa kwanza, Hawa, akimwambia uwongo kwa hila. Hata hivyo, twajua vyema kabisa matokeo yenye kuleta msiba ya njia za kusema uwongo za Shetani. Mateseko yasiyoweza kusemeka yamepata familia ya kibinadamu kwa sababu ya uwongo mmoja wenye ubinafsi na watu watatu wenye ubinafsi—Adamu, Hawa, na Shetani.

Ndiyo, kweli kuhusu kusema uwongo ni kwamba kunalingana na sumu yenye kufisha. Ingawa hivyo, ni vizuri kwamba twaweza kufanya jambo kuuhusu. Twaweza kukomesha zoea la kusema uwongo na kufurahia kwa umilele upendeleo wa Yehova, Mungu “mwingi wa rehema na kweli.”—Kutoka 34:6.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Kusema uwongo kunalingana na sumu yenye kufisha

[Picha katika ukurasa wa 17]

Matokeo ya kusema uwongo ni kama kuvunjika-vunjika kwa chombo cha kuwekea maua

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki