Uongo wa Kwanza—Nani Aliyeusema?
KATIKA mji mmoja katika upande wa kusini wa Afrika wanaume wawili wakiwa ndani ya motokaa waliendesha motokaa hiyo kupitia mahali palipokuwa makutano ya barabara. Taa za kuongozea motokaa zilikuwa zinaonyesha rangi ya chanikiwiti (kijani kibichi), walakini walisimamishwa na ofisa wa kuongoza magari (polisi) ambaye aliwauliza hivi: “Kwa sababu gani mkaendesha motokaa hali taa zilikuwa nyekundu?” Wanaume wote hao wawili walikana hawakufanya hivyo. Walakini ofisa huyo alisema: “Ati, mnaniambia siwezi kuona?” Halafu akaanza kuandika shtaka la kuwafikisha mahakamani. Yule dereva akajibu kwa upole: “Kuna Mtu huko juu anayejua unayofanya.” Ofisa huyo akasita . . . akaenda zake.
Ndiyo, polisi huyo alikuwa akisema uongo. Je! hilo ni jambo la kushangaza? Sivyo. Kusema uongo kumetia mizizi sana katika ujamii wa kibinadamu. Kama ambavyo imesemwa mara nyingi: “Sema uongo mara nyingi kutosha na watu watausadiki.” Wanasiasa wengi wanaelekea kukubaliana na jambo hilo, na, katika akili za wengi, siasa zinahusiana sana na kusema uongo.
Watu wanasema uongo kwa ajili ya sababu nyingi. Mkristo mnyofu aliyekuwa hana kazi kwa muda fulani alitoa ombi la kuajiriwa kazi na kampuni fulani ya kibiashara. Walakini meneja (msimamizi) alimwonya hivi: “Ili uuze bidhaa zangu lazima uweze kusema uongo kwa ufundi mwingi zaidi ya mtu yule mwingine!” Mkristo huyo aliikataa kazi hiyo.
Hata watu wenye kufuata dini, kama hawashikilii kanuni za kimungu, wanasema uongo. Je! unakumbuka itikio la viongozi wa kidini Wayahudi waliposikia kwamba Yesu Kristo wa Nazareti aliyekuwa ameuawa, alikuwa amefufuliwa? Waliwahonga (waliwapa rushwa) askari waliokuwa wakilinda kaburi la Yesu waseme: “Wanafunzi wake walikuja usiku, wakamwiba, sisi tulipokuwa tumelala.”—Mathayo 28:12-15.
Hata hivyo inaonekana kwamba si asili ya wanadamu kusema uongo. Dakt. Lewis Thomas aliandika hivi: “Kama ninavyofahamu, mwanadamu hawezi kusema uongo, hata ule mdogo, pasipo kupiga namna fulani ya kamsa (king’ora) iliyomo ndani sana mahali fulani katika kisehemu cha ubongo cha utusitusi, na kutokeza kwa ghafula misukumo ya kutendesha katika neva, au umwagaji wa ghafula wa homoni za neva za ubongo za namna fulani... Basi, kusema uongo kunaleta wasiwasi, hata tunapofanya hivyo ili kujilinda, au kujifariji, au kuepa, au kujipatia faida.” (Discover, Desemba 1980) Maitikio hayo ya kimwili ndiyo yanayotendesha kitambua uongo.
Kwa kuwa kusema uongo kunaleta wasi-wasi mwingi, kulianzaje?
Ni Nani Aliyesema Uongo wa Kwanza?
Yesu Kristo alitambulisha mwongo wa kwanza, na alionyesha kwamba huyo hakuwa mwanadamu. Yeye alisema: “[Shetani] asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo.” (Yohana 8:44) Kwa hiyo mwongo wa kwanza alikuwa ni Shetani Ibilisi. Yeye alianza kusema uongo wakati gani? Kulingana na Biblia, ilikuwa muda mfupi baada ya jamii ya kibinadamu kuanza.
Tukio hilo limeandikwa katika kitabu cha Biblia, Mwanzo, na uongo huo ulikuwa jambo la kumaanisha uzima au kifo kwa wanadamu. Mungu alimwonyesha mwanadamu wa kwanza, Adamu, kwamba uendelevu wa uhai wake ulitegemea utii. Yeye alimpa Adamu sheria rahisi ya kutiiwa na akamwambia kwamba akishindwa kutii sheria hiyo ‘angekufa hakika.’ Walakini Shetani alisema uongo wenye kuumiza: “Hakika hamtakufa.” Huo ndio uliokuwa uongo wa kwanza kati ya mabilioni ya uongo ambayo yamesemwa juu ya Dunia.—Mwanzo 2:17; 3:4.
Watu wengi leo hawaamini masimulizi hayo katika Biblia. Lakini Yesu, mtu mwenye kusema kweli zaidi ya wote ambao wamepata kuishi, alithibitisha kwamba maandishi katika Mwanzo si hadithi za kizee tu bali ni mambo ya kweli. (Mathay0 19:4, 5) Hakika, matokeo ya uongo huo yangali yanatupata. Uliletea jamii ya kibinadamu msiba.