Mshangao Wenye Kusisimua
Dana Folz alikuwa na umri wa miaka minane alipogundua kwamba alikuwa ameasilishwa. Miaka mingi baadaye, alianza kujiuliza, ‘Mama yangu ni nani? Alifananaje? Kwa nini alifanya niasilishwe? Je, nina ndugu au dada?’ Soma simulizi la Dana la jinsi alivyompata mama yake mzazi hatimaye na mshangao wenye kusisimua uliofuata.
NILIZALIWA Agosti 1, 1966, katika Ketchikan, Alaska, Marekani. Dada yangu Pam alinizidi umri kwa miaka miwili. Baba yetu alikuwa mfanyakazi wa kijamii aliyeajiriwa na Ofisi ya Mambo ya Wahindi, naye alikuwa akihamishwa-hamishwa. Tulihama-hama sana katika Alaska. Baadaye tuliishi katika Iowa, Oklahoma, Arizona, na Oregon.
Tulipokuwa tukizuru watu wa ukoo katika Wisconsin katika kiangazi cha 1975, binamu fulani wangu walianza kumdhihaki binamu yangu mwingine. “Yeye ameasilishwa,” wao wakasema, “na hivyo yeye si wa akina Folz hasa.” Baada ya kurudi nyumbani, nilimwuliza mama kuhusu jambo hilo na nikashangaa kwa jinsi alivyoshtuka usoni. Akaeleza uasilishaji ni nini. Usiku huo, machozi yakimtiririka, alinieleza kwamba niliasilishwa na kwamba dada yangu aliasilishwa pia.
Wakati huo uasilishaji haukumaanisha kitu kwangu, na kwa muda fulani sikufikiria jambo hilo sana. Nilikuwa na mama na baba, na maisha yalikuwa kama kawaida. Wazazi wangu waliamua kuacha kuhama-hama ili familia ikae mahali pamoja pa kudumu. Nilipokuwa na umri wa miaka tisa, tulikaa Vancouver, Washington. Tulikuwa na uhusiano wa karibu sana na baba, lakini hatukuwa na uhusiano wa karibu sana na mama. Nyakati nyingine nilitaka kujifanyia mambo mwenyewe na nilikuwa mwasi, na fadhaiko ambalo mama alipata kutokana na hali hiyo linaweza kuwa ndiyo sababu iliyofanya ule ukaribu uzidi kupungua.
Mahaba na Chuo
Nilipokuwa katika shule ya sekondari, nilikutana na Trina, nasi tukawa marafiki mara hiyo. Baada ya kuhitimu nilikubali toleo la kusoma katika Chuo Kikuu cha Jimbo la Oregon, katika Corvallis, Oregon. Nilitumia wakati wa ziada nikisafiri kwenda na kutoka Vancouver ili kuwa na Trina, ambaye bado alibakiza mwaka mmoja ili kumaliza shule ya sekondari. Sikuwa nikisoma sana lakini niliona kama nitafanya tu vizuri chuoni. Ripoti yangu ya kwanza ya mtihani ilinishtua kabisa—ilikuwa mbaya zaidi niliyowahi kupata! Niliona aibu sana. Lakini sikuacha kumzuru Trina; nilibeba tu vitabu vyangu ili niweze kusoma ninapozuru.
Kisha, siku moja, nilipokuwa nikiendesha pikipiki nikirudi shuleni kutoka Vancouver, nilihusika katika aksidenti mbaya. Muda mfupi baadaye nilijeruhiwa hata vibaya zaidi nilipogongwa na gari nilipokuwa nikivuka barabara. Nikaanza kufanya kazi na kupoteza hamu ya kurudi chuoni.
Upendezi Katika Dini
Baada ya muda, tukaanza kuishi pamoja na Trina. Tulimwamini Mungu nasi tulitaka kumjua. Hata hivyo, tulihisi kwamba makanisa yalikuwa na unafiki. Basi tulijaribu kusoma Biblia kivyetu, lakini hatukuielewa.
Siku moja, nikiwa kazini katika Portland, Oregon, wafanyakazi wenzangu walianza kumdhihaki mtu ambaye nilimfikiria kuwa mmojawapo watu wazuri niliopata kukutana nao. Randy alistahimili mnyanyaso huo kwa utulivu. Baadaye siku hiyo nilimwuliza: “Nasikia kwamba wewe ni mhudumu?”
“Ndiyo, mimi ni mhudumu,” akasema.
“Katika dini gani?” nikauliza.
“Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.”
“Mashahidi wa Yehova ni nani?”
“Kweli hujui?” akauliza kwa mshangao.
“Ndiyo,” nikasema. “Mashahidi wa Yehova ni nani? Napaswa kuwajua?”
“Ndiyo,” akasema huku akitabasamu, “unapaswa kuwajua. Umepangia nini wakati wa chakula cha mchana?”
Hayo yalikuwa mazungumzo ya kwanza kati ya mazungumzo kadhaa ya Biblia tuliyofanya wakati wa chakula cha mchana. Usiku mmoja nilimwambia Trina kuyahusu. “Usizungumze na Mashahidi wa Yehova!” akasema. “Wao ni watu wa ajabu sana! Wao hata si Wakristo. Hawasherehekei Krismasi.” Naye akaniambia mambo mengine ambayo alikuwa amesikia juu ya Mashahidi wa Yehova.
“Mtu amekuambia mambo mengi ambayo si ya kweli,” nikasema. Baada ya mazungumzo marefu, niliweza kumsadikisha kwamba hakupata kujua ukweli wote. Baadaye, akaanza kunituma kuuliza Randy maswali, nami ningeleta majibu ya wazi ya Kimaandiko. Hatimaye, Trina akasema: “Sikujua kwamba mambo haya yote yalikuwa katika Biblia, lakini bado nafikiri wao ni watu wa ajabu. Ukitaka kuendelea kuzungumza naye kuhusu Biblia, mimi sijali; lakini usinilazimishe kukubali itikadi zao.”
Kipindi Chenye Hangaiko
Niliamini yale niliyokuwa nikijifunza katika Biblia, lakini nilihisi kwamba sikuweza kuishi kulingana nayo. Ilionekana kama tulikuwa tukigombana na Trina mara nyingi zaidi. Basi mimi na rafiki yangu mmoja tukaamua kuwaacha marafiki wetu wasichana na kuanza maisha mapya katika Oklahoma. Nikapanga kuchukua likizo kutoka kazini. Punde si punde mimi na rafiki yangu tukakaa katika nyumba ya kukodi katika mji fulani mdogo karibu na mpaka wa Texas. Haikuchukua muda mrefu kutambua jinsi nilivyomtamani sana Trina, lakini nikaamua kwamba hata hivyo nitajifurahisha.
Niligundua kwamba umri halali wa kuanza kunywa alkoholi katika Texas ulikuwa miaka 19, kwa hiyo rafiki yangu alipofunga safari, mimi nilivuka mpaka usiku mmoja na kujitumbuiza katika baa moja mashuhuri ya muziki aina ya rock-’n’-roll. Nikalewa chakari, nikaharibu gari langu kabisa, na kufungwa gerezani. Baada ya muda, niliweza kuwasiliana na baba yangu, akaniondoa gerezani kwa dhamana. Pia, Trina alinikubali tena, jambo lililofanya nishukuru sana! Nikarudia kazi yangu ya zamani na kurudia mazungumzo ya Biblia pamoja na Randy.
Nadhibiti Maisha Yangu
Ilikuwa karibu miaka miwili tangu niliposikia juu ya Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza, nikaamua kujihusisha zaidi na funzo langu la Biblia. Sasa nilikuwa na umri wa miaka 20, na maswali kuhusu uasilishaji ambayo niliyataja mwanzoni mwa makala hii yakaanza kunisumbua. Basi nikaanza kutafuta kwa bidii mama yangu mzazi.
Nilipigia simu hospitali katika Alaska ambamo nilizaliwa na kuomba habari ya hatua za kuchukua. Baada ya kujua hatua za kuchukua, nilipata nakala ya cheti changu cha kuzaliwa cha awali na kugundua kwamba jina la mamangu ni Sandra Lee Hirsch; lakini hakukuwa na rekodi ya jina la baba. Sandra alikuwa na umri wa miaka 19 tu nilipozaliwa, basi nikadhani kwamba ni lazima alikuwa msichana mseja mwoga ambaye alipata mimba bila kuolewa na aliyelazimika kufanya maamuzi magumu sana. Hakukuwa na habari za kutosha kwenye cheti cha kuzaliwa ambazo zingeniwezesha kumpata mama yangu.
Kwa wakati huo, kutokana na funzo langu la Biblia pamoja na Randy, nilisadiki kwamba nimepata dini ya kweli. Lakini mara nyingi nilishindwa kuacha matumizi yenye kuchafua ya tumbaku. (2 Wakorintho 7:1) Nilihisi kwamba Yehova ameniacha. Ndipo Shahidi mmoja katika Jumba la Ufalme akasema jambo ambalo lilinisaidia sana. Alitaja kwamba ni Shetani anayetutaka tushindwe na kwamba inahuzunisha sana kuona wengine wakipoteza uhai udumuo milele kwa kuacha washindwe. “Tunahitaji kumtwika Yehova mizigo yetu,” akasema, “na kumtegemea kabisa ili atusaidie katika nyakati zetu zenye magumu.”—Zaburi 55:22.
Hilo ndilo jambo nililohitaji kusikia! Nilianza kutumia yale aliyosema, nikisali mara nyingi nipate msaada wa Yehova. Punde si punde nikaacha kutumia tumbaku, tukafunga ndoa na Trina, na kuanza kuwa wa kawaida katika kujifunza Biblia. Baadaye, Trina pia alianza kujifunza. Nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji katika Juni 9, 1991. Na kabla ya majuma mawili kupita, binti yetu wa kwanza, Breanna Jean, alizaliwa.
Uhusiano Wangu na Baba
Tulikuwa na uhusiano wa karibu na baba. Alikuwa mtu mwenye fadhili sana ambaye sikuzote alinitia moyo nilipokuwa nimefadhaika. Lakini alikuwa thabiti nilipohitaji nidhamu. Basi, ulikuwa ni wakati mgumu mapema katika 1991 nilipopata habari kwamba baba alikuwa na kansa ya mapafu ya kufisha. Kufikia wakati huo mama na baba walikuwa wamehamia Hamilton, Montana. Mara nyingi tulisafiri huko kumwona na kumtia moyo mama.
Tuliweza kumpa baba kitabu Je! Uzima Ndio Uu Huu Tu? Aliahidi kukisoma na kusema kwamba alikuwa na wasiwasi kuhusu hali njema ya familia yake. Katika ziara yangu ya mwisho, aliniambia jinsi aonavyo fahari kwamba mimi ni mwana wake na kwamba ananipenda sana. Kisha, machozi yalipombubujika, aligeuza kichwa chake upande wa dirisha. Tulikumbatiana mara kadhaa kabla sijaondoka. Baba alisoma karibu thuluthi ya kitabu hicho kabla ya kufa, Novemba 21, 1991.
Baada ya kifo cha baba na kuhamia kwetu Moses Lake, Washington, nilipata tamaa hata zaidi ya kujifunza kuhusu historia yangu. Lakini japo wakati wote niliotumia katika utafutaji huo, hatukupuuza mambo ya kiroho. Trina alibatizwa Juni 5, 1993, na miezi sita baadaye alizaa binti yetu wa pili, Sierra Lynn.
Jinsi Nilivyompata Mama Yangu Mzazi
Niliendelea kuomba habari kutoka kwa mfumo wa kisheria wa Alaska, nikiandika barua baada ya nyingine kwa mashirika mbalimbali na vilevile kujifanyia utafiti wangu mwenyewe kwa kompyuta. Sikufua dafu. Kisha, kuelekea mwisho wa 1995, nilifanyiwa uchunguzi wa kitiba ambao ulifunua kwamba nilikuwa na kasoro fulani ya moyo. Nilikuwa na umri wa miaka 29 tu, na daktari alitaka kujua historia yangu ya kitiba.
Huyo daktari aliandika ombi lenye mambo mahususi lililo wazi, akisisitiza kwamba habari yoyote katika faili zangu za uasilishaji ni muhimu sana kwa hali-njema yangu. Baada ya muda tulipokea jibu. Jibu hilo lilikuwa na uamuzi wa hakimu kwamba hakuhisi uhitaji wangu wa kitiba ulikuwa mzito kiasi cha kufungua faili zangu. Nikawa hoi kabisa. Lakini majuma kadhaa baadaye, barua ilifika kutoka kwa hakimu wa pili. Uamuzi wa mahakama ulikuwa umeniruhusu kuona faili zangu za uasilishaji!
Faili zangu zenyewe za uasilishaji zilifika mapema Januari 1996. Zilikuwa na mji na historia ya familia ya mama yangu mzazi. Mara moja, nikatafuta katika kompyuta jina Sandra pamoja na mji wao nikapata nambari za simu za watu sita. Tuliamua na Trina kwamba ilifaa Trina apige hizo simu. Alipopiga simu ya tatu, mwanamke mmoja alisema kwamba Sandra alikuwa mpwa wake na akatupa nambari yake ya simu.
Simu na Mshangao
Trina alipopiga nambari hiyo ya simu, mwanamke aliyejibu alikataa kujitambulisha. Hatimaye, Trina akasema kinaganaga: “Mume wangu alizaliwa Ketchikan, Alaska, Agosti 1, 1966, na nahitaji kujua kama ni wewe ninayekutafuta.” Kimya kirefu kikatanda, ndipo, kwa sauti yenye kutetemeka, mwanamke huyo aliomba jina la Trina na nambari yake ya simu akasema kwamba angepiga simu baadaye. Sikufikiri kwamba angenipigia simu haraka, kwa hiyo nikaamua kwenda dukani kununua vitu fulani tulivyohitaji.
Niliporudi, Trina alikuwa kwenye simu macho yake yakiwa yamejaa machozi. Akanipa simu. Tulipokuwa tukisalimiana na mama na kuzungumza kidogo, Trina akanong’ona kwa hima, “Kweli alitaka kukulea.” Nikamsikitikia mama alipoanza kunieleza juu yake. “Nilitaka kukushukuru kwa uhai ulionipa,” nikasema. “Nina maisha mazuri na vitu vyote ambavyo nimehitaji. Nimekuwa na wazazi wazuri wenye upendo mwingi na sasa nina mke mzuri sana na binti wawili warembo. Nina furaha sana.”
Akaanza kulia. Tulipoendelea kuzungumza, aliniambia kwamba alibakwa, akawa mja-mzito, na kusongwa ili aniasilishe; kisha akaniambia kwamba baadaye alifunga ndoa na kwamba pindi fulani baadaye, alipokuwa hospitalini akipata nafuu kutokana na upasuaji aliofanyiwa, binti yake mchanga na mama yake walikufa kwa moto. Alisema kwamba wakati huo alihisi kwamba Mungu alikuwa amewachukua hao wapendwa wake ikiwa adhabu ya kumwasilisha mtoto wake. “La,” nikajibu mara moja, “Mungu hatendi kwa njia hiyo!” Akasema kwamba sasa anajua hivyo, kwa kuwa baada ya huo msiba, alikuwa ameanza “kutafuta kweli ya Biblia” na sasa alikuwa “mwanafunzi wa Biblia.”
Nikaanza kufikiri, ‘Hii si kweli,’ nilipouliza: “Ulijifunza na watu gani?” Kimya kirefu kikatanda. Kisha akasema: “Mashahidi wa Yehova.” Nilishtuka sana, nikashindwa kuongea. Kwa machozi, hatimaye nilijitahidi kusema, “hata mimi ni Shahidi.” Niliporudia kusema kwa wazi zaidi, alichachawa. Ilikuwa ajabu sana!
Mama alikuja kuwa Shahidi katika 1975, muda fulani baada ya kifo cha binti yake. Mume wake alipoanza kufanya maendeleo kiroho, alimwambia juu yangu. Mume wake alimfariji na kumwambia kwamba wangenitafuta. Lakini muda mfupi baadaye, alikufa katika aksidenti ya gari, akimwacha mama na watoto watatu wadogo wa kulea. Tulikuwa tukizungumza kwa muda wa saa nyingi katika jioni zilizofuata. Hatimaye, tuliamua kukutana Phoenix, Arizona, juma la pili la Februari 1996. Tayari mama alikuwa amepanga kuzuru huko pamoja na dada mwingine Mkristo.
Muungano wa Kukumbukwa
Tuliacha watoto wetu nyumbani katika ziara hii. Na niliposhuka kutoka kwenye ndege, nilimwona mama yangu na hatimaye niliweza kumkumbatia. Tulipokumbatiana, alisema alikuwa amengoja kwa miaka 29 kunikumbatia, naye alinishika kwa muda mrefu. Tulifurahia ziara na kupeana picha na kusimuliana hadithi. Hata hivyo, jambo kuu lilikuwa kuketi kando ya mama katika Jumba la Ufalme katika Phoenix! Tulisikiliza mkutano pamoja na kusimama pamoja tulipokuwa tukiimba nyimbo za Ufalme. Nilipata hisia nzuri sana ambayo nitakumbuka milele.
Mnamo Aprili 1996, dada yangu Laura alikuja kutoka kwake Iowa kutuzuru. Ilifurahisha kama nini kufurahia ushirika mchangamfu wa Kikristo pamoja naye! Pia nimeongea kwenye simu na ndugu zangu wawili ambao nimetoka kuwajua. Kuungana tena na familia yangu ni jambo la ajabu, lakini kuungana katika upendo katika tengenezo la Yehova ni zawadi ambayo ni Mungu wetu mkuu pekee, Yehova, awezaye kutoa.—Kama ilivyosimuliwa na Dana Folz.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Nikiwa na mama yangu mzazi