Njia ya Kurudia Paradiso
KWA sababu ya tamaa ya mwanadamu ya kupata Paradiso na majaribio makubwa na madogo ya kuifanyiza tena, mtu angedhani kwamba kufikia sasa dunia ingekuwa paradiso halisi. Lakini sivyo ilivyo.
Badala ya hivyo, mwanadamu ametanguliza pupa, ambayo mara nyingi hutawala kwa hasara ya mazingira na unamna-namna wa viumbe vilivyo hai. Wakiamini kwamba utajiri ndio jambo kuu, watu wengi wamepoteza tumaini kabisa kwamba dunia haitapata kamwe kufanywa kuwa paradiso ya Kiedeni. Badala ya hivyo, wao hutazamia maisha baada ya kifo mbinguni kuwa tumaini lao la pekee kwa Paradiso. Maoni hayo yadokeza kwamba, kwanza, tamaa yetu ya kibinadamu kwa Edeni itafadhaishwa milele na, pili, Mungu ameiacha dunia hii kwa sababu ya upumbavu na pupa ya wanadamu. Je, ndivyo ilivyo? Wakati ujao una nini hasa? Na wakati ujao huo utakuwa wapi?
Paradiso—Itakuwa Mbinguni au Duniani?
Karibu miaka 2,000 iliyopita, Yesu Kristo alisema hivi alipokuwa akizungumza na mwizi aliyetubu aliyekuwa ametundikwa mtini kando yake: “Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:43) Je, Yesu alimaanisha kwamba mwizi huyo angeenda mbinguni pamoja naye? La.
Huyo mtenda-maovu hata hangalifikiria jambo hilo. Kwa nini? Kwa sababu labda alikuwa amefahamu mafungu katika Maandiko ya Kiebrania, ambayo yalikuwapo katika wakati wake, kama vile sehemu ya kwanza ya Zaburi 37:29: “Wenye haki watairithi nchi.” (Italiki ni zetu.) Yesu alifundisha kweli iyo hiyo, akitangaza hivi: “Wenye furaha ni wenye tabia-pole, kwa kuwa wao watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Andiko hili lapatana na ile ambayo kwa kawaida huitwa Sala ya Bwana, inayosema: “Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:9, 10.
Biblia yafundisha kwamba Mungu aliumba dunia, bali si mbingu, kuwa makao ya familia ya wanadamu. Neno lake lataarifu kwamba yeye “hakuiumba [dunia] ukiwa” bali “aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Kwa muda gani? ‘Aliiweka nchi juu ya misingi yake; isitikisike milele.’ (Zaburi 104:5) Ndiyo, “dunia hudumu daima.”—Mhubiri 1:4.
Ni kusudi la Mungu kwamba watu wengi zaidi kati ya wale wanaomtumikia waifanye dunia hii kuwa makao yao milele. Ona jinsi Neno la Mungu, Biblia, linavyoeleza jambo hili. Zaburi 37:11 latabiri: “Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” Kwa muda gani? Zaburi 37:29 lasema: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Italiki ni zetu.) Wakati huo andiko lisemalo hivi litatimizwa: “[Wewe Mungu] waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake,” yaani, matakwa yanayopatana na mapenzi ya Mungu.—Zaburi 145:16.
Vipi kuhusu wale ambao hawataki kufanya mapenzi ya Mungu? Mithali 2:21, 22 lasema: “Maana wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”
Paradiso Inarudishwa
Sasa upesi, hukumu za Mungu zitatekelezwa dhidi ya ulimwengu huu mwovu. (Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5, 13) Lakini Mungu atahifadhi “umati mkubwa” wa watu waokoke huo uharibifu unaokuja na kuingia katika ulimwengu mpya alioufanyiza.—Ufunuo 7:9-17.
Kisha, Mungu ataelekeza kazi hiyo yenye shangwe ambayo raia wake wa kibinadamu watafanya ya kugeuza dunia nzima kuwa makao ya paradiso ya wanadamu. Biblia yaahidi: “Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi: jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi. . . . Maana katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani.”—Isaya 35:1, 6.
Katika Paradiso hiyo yenye kupanuka, hakutakuwa tena na njaa, umaskini, mitaa ya mabanda, watu wasio na makao, au maeneo yenye kujaa uhalifu. “Na nafaka zitakuwa nyingi.” (Zaburi 72:16, Zaire Swahili Bible) “Na mti wa kondeni utazaa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake.” (Ezekieli 34:27) “Nao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine.” (Isaya 65:21, 22) “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.”—Mika 4:4.
Sababu Inayofanya Wengine Waende Mbinguni
Labda watu wengi watakiri kwamba wana tamaa ya kuishi katika paradiso ya kidunia. Hilo ni jambo la kawaida, kwa kuwa Mungu hakupata kuwawekea tamaa ya kwenda mbinguni; wao hata hawawezi kuwazia jinsi maisha ya mbinguni yalivyo. Kwa mfano, katika mazungumzo na mhudumu wake wa Kanisa la Uingereza, ingawa Pat alikuwa mshiriki wa dhati wa kanisa hilo, alisema: “Sijapata kamwe kuwa na mawazo yoyote kuhusu kwenda mbinguni. Mimi sitaki kwenda, na hata hivyo nitafanya nini huko?”—Linganisha Zaburi 115:16.
Ni kweli Biblia hufundisha kwamba idadi ndogo ya wanadamu, 144,000, wanaenda mbinguni. (Ufunuo 14:1, 4) Pia yaeleza sababu: “Ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:9, 10) Pamoja na Mfalme wao, Yesu Kristo, hao wafanyiza “ufalme,” ambao ni serikali mpya ya kimbingu juu ya dunia, ambayo Wakristo husali juu yayo. Serikali hiyo itasimamia kazi ya kugeuza kabisa dunia na wanadamu pia.—Danieli 2:44; 2 Petro 3:13.
Hata hivyo, kwa kuwa tamaa ya kuishi mbinguni haimo kiasili katika wanadamu, utendaji wa kipekee wa roho ya Mungu “hutoa ushahidi” kwa wale 144,000 ili wahisi “mwito [huo] wa kimbingu” wa kipekee. (Waroma 8:16, 17; Wafilipi 3:14) Ingawa hivyo, bila shaka utendaji kama huo wa roho takatifu hauhitajiki kwa wanadamu kwa ujumla kwa sababu makao yao ya milele ni hapa katika dunia paradiso.
Paradiso ya Kiroho Yatayarisha Njia
Mtu anastahilije kupata uhai wa milele katika Paradiso duniani? “Hii yamaanisha uhai udumuo milele,” Yesu alisema, “wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Likihusianisha mahusiano ya amani kati ya wanadamu na ujuzi wa Mungu, Isaya 11:9 lasema: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Linganisha Isaya 48:18.
Bila shaka, ujuzi huu si ujuzi wa akilini tu. Huo huathiri utu wa mtu na kukuza sifa za kimungu, kama vile “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.” (Wagalatia 5:22, 23) Mashahidi wa Yehova hujaribu kukuza sifa hizi, na hivyo, hata sasa, wao wamebarikiwa na paradiso nzuri ya kiroho.—Isaya 65:13, 14.
Hali yao ya kiroho yatofautiana kama nini na ile ya ulimwengu, ambao unazidi kudidimia katika hali ya kutomcha Mungu na ufisadi! Hata hivyo, upesi ulimwengu huu utaangamizwa na Mungu. Kwa wakati huu, Mashahidi wa Yehova wakualika kuzuru—ndiyo uchunguze—paradiso ya kiroho ambayo wanafurahia. Jionee mwenyewe kwamba sasa hivi Yesu, Mfalme wa kimbingu asiyeonekana, anaongoza kwa utulivu wakazi wa wakati ujao wa ulimwengu huo mpya katika barabara nyembamba ielekeayo kwenye Paradiso ya kidunia na uhai wa milele!—Mathayo 7:13, 14; Ufunuo 7:17; 21:3, 4.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Waokokaji wa mwisho wa ulimwengu huu watafurahia kushiriki katika kugeuza dunia kuwa paradiso