Sura 1
Unaweza Kuwa na Wakati Ujao Wenye Furaha!
1, 2. Muumba wako anataka uwe na nini?
KUMBATIO changamfu kutoka kwa mtu fulani umpendaye. Kicheko cha kutoka moyoni wakati wa mlo mzuri pamoja na marafiki wapendwa. Furaha ya kutazama watoto wako wakicheza kwa uchangamfu. Pindi kama hizi ni nyakati zenye furaha maishani. Hata hivyo, kwa wengi, maisha huonekana yakitokeza tatizo moja zito baada ya jingine. Ikiwa imekuwa hivyo kwako, jipe moyo.
2 Mapenzi ya Mungu ni kwamba uwe na furaha yenye kudumu ukiwa chini ya hali bora kabisa katika mazingira mazuri ajabu. Hiyo si ndoto tu, kwani Mungu kwa kweli anakutolea ufunguo uongozao kwenye wakati ujao kama huo wenye furaha. Ufunguo huo ni ujuzi.
3. Ni ujuzi upi ulio ufunguo uongozao kwenye furaha, na sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu aweza kutoa ujuzi huo?
3 Tunaongea juu ya ujuzi wa aina ya pekee ulio mkubwa zaidi ya hekima ya binadamu. Huo ndio “ujuzi wenyewe juu ya Mungu.” (Mithali 2:5, New World Translation) Miaka karibu 2,000 iliyopita, mwandikaji fulani wa Biblia alisema hivi: “Kila nyumba hujengwa na mjenzi fulani—na Mungu ndiye mjenzi wa vitu vyote.” (Waebrania 3:4, Habari Njema kwa Watu Wote) Fikiria huo ujuzi ambao bila shaka Mfanyi wa vitu vyote anao! Biblia husema kwamba Mungu huhesabu na huzipa majina nyota zote. Hilo ni wazo la kustaajabisha kama nini, kwa kuwa kuna mamia ya maelfu ya mamilioni ya nyota katika galaksi yetu wenyewe, na wataalamu wa nyota husema kwamba kuna galaksi nyinginezo karibu milioni elfu mia moja! (Zaburi 147:4) Mungu ajua pia habari zote juu yetu, kwa hiyo ni nani mwingine ambaye angeweza kutoa majibu mazuri zaidi kwa maswali yenye maana maishani?—Mathayo 10:30.
4. Sababu gani tumtazamie Mungu atoe maagizo ya kutuongoza, na ni kitabu kipi kinachotimiza uhitaji huo?
4 Ebu wazia watu wawili wakijaribu kurekebisha magari yao. Kwa kuchukizwa sana, mtu mmoja anaiacha kazi yake ya kurekebisha gari lake. Yule mwingine analisahihisha tatizo kwa utulivu, aliwasha moto gari, na kutabasamu gari lianzapo na kuendelea bila shida. Isingekuwa vigumu kwako kukisia ni nani kati ya hao watu wawili aliyekuwa na kitabu chenye maagizo kutoka kwa wafanyiza-gari. Je! si jambo la akili kwamba Mungu angetupa maagizo ili kutuongoza maishani? Kama vile huenda ukajua, Biblia hudai kuwa hivyo hasa—kitabu chenye maagizo na mwongozo kutoka kwa Muumba wetu, kilichokusudiwa kutoa ujuzi juu ya Mungu.—2 Timotheo 3:16.
5. Ujuzi uliomo katika Biblia ni wenye thamani jinsi gani?
5 Ikiwa dai la Biblia ni kweli, ebu fikiria zile hazina za ujuzi ambazo bila shaka zimo katika kitabu hicho! Kwenye Mithali 2:1-5 (NW) hiyo hutuhimiza tuitafute hekima, tuchimbe ili kuipata kama vile tungechimba tupate hazina iliyofichwa—si katika udongo wa fikira za binadamu, bali katika Neno la Mungu mwenyewe. Tukitafuta-tafuta humo, ‘tutapata ujuzi wenyewe juu ya Mungu.’ Kwa kuwa Mungu aelewa mipaka na mahitaji yetu, yeye hutupa sisi maagizo ambayo yatatusaidia kuongoza maisha zenye amani na furaha. (Zaburi 103:14; Isaya 48:17) Zaidi ya hayo, huo ujuzi juu ya Mungu hututolea habari njema yenye kusisimua.
UHAI UDUMUO MILELE!
6. Yesu Kristo alitoa uhakikishio upi kuhusu ujuzi juu ya Mungu?
6 Yesu Kristo, yule mtu ajulikanaye vizuri kutokana na historia alieleza kwa wazi jambo hili kuhusu ujuzi juu ya Mungu. Yeye alisema hivi: “Hii yamaanisha uhai udumuo milele, kuendelea kwao kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3, NW) Ebu wazia—ujuzi uongozao kwenye uhai udumuo milele!
7. Kuna uthibitisho gani kwamba halikuwa kusudi la Mungu tufe?
7 Usikate maneno upesi kwamba uhai udumuo milele ni ndoto tu. Badala ya hivyo, fikiria njia ambayo mwili wa binadamu umeumbwa. Umebuniwa vizuri sana ili uweze kuonja, kusikia, kunusa, kuona, na kuhisi. Kuna mambo mengi sana duniani yanayopendeza hisi zetu—chakula chenye ladha sana, nyimbo za ndege zenye kufurahisha, maua yenye kunukia, mandhari nzuri, urafiki wenye kupendeza! Na ubongo wetu wa ajabu ni bora zaidi kuliko kompyuta ya hali ya juu sana, kwani hutuwezesha tuthamini na kufurahia mambo yote hayo. Je, unafikiri Muumba wetu ataka tufe na kupoteza yote hayo? Je, halingekuwa jambo lenye kupatana na akili zaidi kukata maneno kwamba yeye anatutaka tuishi kwa furaha na kufurahia uhai milele? Basi, ujuzi juu ya Mungu unaweza kumaanisha hivyo kwako.
UHAI KATIKA PARADISO
8. Biblia husema nini juu ya wakati ujao wa wanadamu?
8 Yale ambayo Biblia husema juu ya wakati ujao wa dunia na wanadamu yaweza kujumlishwa katika neno moja—Paradiso! Yesu Kristo alisema juu yayo alipomwambia hivi mtu fulani aliyekuwa akifa: “Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:43, NW) Mtajo wa Paradiso bila shaka ulimkumbusha mtu huyo ile hali yenye furaha ya wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. Mungu alipowaumba, wao walikuwa wakamilifu nao waliishi katika shamba lililokuwa kama bustani ambalo Muumba alikuwa amebuni na kupanda. Liliitwa kwa kufaa bustani ya Edeni, jina limaanishalo raha.
9. Uhai ulikuwaje katika Paradiso ya kwanza?
9 Bustani hiyo ilikuwa yenye kupendeza kama nini! Ilikuwa paradiso halisi. Miongoni mwa miti yayo mizuri kulikuwa na ile iliyozaa matunda yenye ladha sana. Adamu na Hawa walipochunguza makao yao, wakanywa kutokana na maji yayo matamu, na kukusanya matunda kutokana na miti yayo, hawakuwa na sababu ya kuhangaika au kuwa wenye hofu. Hata wanyama hawakuwa hatari, kwani Mungu alikuwa amemweka mwanamume pamoja na mke wake katika utawala wenye upendo juu yao wote. Kwa kuongezea, watu wawili wa kwanza walikuwa wenye afya nzuri sana. Maadamu wangeendelea kuwa watiifu kwa Mungu, wakati ujao wa milele na wenye furaha ungekuwa mbele yao. Walipewa kazi yenye kuridhisha ya kutunza makao yao mazuri ajabu ya Paradiso. Zaidi ya hayo, Mungu aliwapa Adamu na Hawa agizo la ‘kuijaza dunia, na kuitiisha.’ Wao na wazao wao walipaswa kuipanua mipaka ya Paradiso mpaka sayari yetu yote ingekuwa mahali penye uzuri na pa kupendeza.—Mwanzo 1:28.
10. Yesu aliposema juu ya Paradiso, yeye alimaanisha nini?
10 Hata hivyo, Yesu alipotaja Paradiso, yeye hakuwa akimwomba mtu aliyekuwa akifa afikirie wakati uliopita zamani. La, Yesu alikuwa akisema juu ya wakati ujao! Yeye alijua kwamba makao yetu yote ya kidunia yangekuwa paradiso. Hivyo ndivyo Mungu angetimiza kusudi lake la kwanza kwa ajili ya wanadamu na dunia yetu. (Isaya 55:10, 11) Ndiyo, Paradiso itarudishwa! Nayo itakuwaje? Acha Neno la Mungu, Biblia Takatifu, lijibu.
UHAI KATIKA PARADISO ITAKAYORUDISHWA
11. Katika ile Paradiso itakayorudishwa, hali itakuwaje kuhusu ugonjwa, uzee, na kifo?
11 Ugonjwa, uzee, na kifo havitakuwako tena. “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.” (Isaya 35:5, 6) “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao [wanadamu]. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.
12. Sababu gani tunaweza kuwa na hakika kwamba hakutakuwa na uhalifu, ujeuri, wala uovu katika ile Paradiso ya wakati ujao?
12 Uhalifu, ujeuri, na uovu utatoweka milele. “Watenda mabaya wataharibiwa . . . Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo . . . Bali wamngojao BWANA ndio watakaoirithi nchi.” (Zaburi 37:9-11) “Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”—Mithali 2:22.
13. Mungu ataletaje amani?
13 Amani itaenea duniani pote. “[Mungu] avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki.” (Zaburi 46:9) “Mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma.”—Zaburi 72:7.
14, 15. Biblia husema nini juu ya makao, kazi, na chakula katika ile Paradiso itakayorudishwa?
14 Kutakuwa na makao salama na kazi yenye kuridhisha. “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake . . . Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu.”—Isaya 65:21-23.
15 Chakula chenye afya kitapatikana kwa wingi. “Kutakuwako na nafaka tele juu ya dunia; na juu ya milima kutakuwako mfuriko.” (Zaburi 72:16, NW) “Dunia yenyewe hakika itatoa mazao yayo; Mungu, Mungu wetu, atatubariki.”—Zaburi 67:6, NW.
16. Sababu gani uhai katika Paradiso utakuwa wenye kupendeza?
16 Uhai udumuo milele juu ya dunia iliyo paradiso utakuwa wenye kupendeza. “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yayo.” (Zaburi 37:29, NW) “Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi.”—Isaya 35:1.
UJUZI NA WAKATI WAKO UJAO
17. (a) Unapaswa kufanya nini ikiwa unavutiwa na uhai katika Paradiso? (b) Tunajuaje kwamba Mungu ataleta mabadiliko makubwa duniani?
17 Ikiwa unavutiwa na uhai katika Paradiso, usiruhusu lolote likuzuie usipate ujuzi juu ya Mungu. Yeye anawapenda wanadamu naye ataleta mabadiliko yanayohitajiwa ili kufanya dunia iwe paradiso. Kwa vyovyote vile, ikiwa wewe ungekuwa na nguvu za kukomesha huzuni na ukosefu wa haki ambao umeenea sana ulimwenguni, je, usingefanya hivyo? Je, tusingemtazamia Mungu afanye hivyohivyo? Kwa kweli, Biblia husema waziwazi juu ya wakati Mungu atakapoondolea mbali mfumo huu uliojaa ugomvi na kuweka mahali pao utawala mkamilifu, wa uadilifu. (Danieli 2:44) Lakini Biblia haituambii yote hayo tu. Hiyo hutuonyesha jinsi tuwezavyo kuokoka ili kuingia ndani ya ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa.—2 Petro 3:13; 1 Yohana 2:17.
18. Ujuzi juu ya Mungu unaweza kukufanyia nini sasa?
18 Ujuzi juu ya Mungu unaweza pia kukunufaisha sana sasa hivi. Maswali yenye kina zaidi na yanayosumbua zaidi maishani yanajibiwa katika Biblia. Kukubali mwongozo wayo kutakusaidia usitawishe urafiki pamoja na Mungu. Hilo ni pendeleo lililoje! Na hili litakusaidia ufurahie amani ambayo ni Mungu peke yake anayeweza kukupa. (Warumi 15:13, 33) Uanzapo kutwaa ujuzi huu wa muhimu, unaingia katika jitihada ya maana na yenye kuthawabisha zaidi maishani mwako. Hutajuta kamwe ukijipatia ujuzi juu ya Mungu uongozao kwenye uhai udumuo milele.
19. Tutazungumzia swali jipi katika sura ifuatayo?
19 Tumerejezea Biblia kuwa kitabu chenye ujuzi juu ya Mungu. Hata hivyo, tunajuaje kwamba, si kitabu chenye hekima ya binadamu, bali ni chenye hekima ya juu zaidi? Tutazungumzia swali hilo katika sura ifuatayo.
TAHINI UJUZI WAKO
Sababu gani ujuzi juu ya Mungu unaweza kukuongoza kwenye furaha ya milele?
Uhai utakuwaje katika Paradiso ya kidunia inayokuja?
Sababu gani wewe utanufaika kutokana na kutwaa ujuzi juu ya Mungu sasa?