Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 4/22 kur. 17-19
  • Kwa Nini Ninalazimika Kuwa Mgonjwa Sana?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Ninalazimika Kuwa Mgonjwa Sana?
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Kwa Nini Hili Linanipata?’
  • Kushughulikia Hofu
  • Matatizo ya Kuwa Mgonjwa
  • Ziara za Kitiba—Si Jambo la Kupendeza
  • Mbona Niwe Mgonjwa Hivi?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Ugonjwa wa Kudumu—Hangaiko la Familia
    Amkeni!—2000
  • Kuishi kwa Mafanikio na Ugonjwa Wako—Jinsi Gani?
    Amkeni!—2001
  • Naweza Kukabilianaje na Kuwa Mgonjwa Sana?
    Amkeni!—1997
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 4/22 kur. 17-19

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Ninalazimika Kuwa Mgonjwa Sana?

JASON alipokuwa na umri wa miaka 13, alikusudia moyoni mwake kwamba wakati fulani baadaye angetumikia akiwa mhudumu wa wakati wote katika Betheli, makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York. Alijitengenezea sanduku la mbao na aliliita sanduku la Betheli. Alianza kukusanya vitu ndani yalo ambavyo alifikiri vingekuwa vyenye kufaa atakapoanza utumishi wake wa Betheli.

Lakini, miezi mitatu tu baada ya kutimiza miaka 18, Jason aligunduliwa kuwa ana maradhi ya Crohn—kasoro ya tumbo yenye maumivu makali yenye kudumu. “Yaliniangamiza kabisa,” akumbuka. “Nilichoweza tu kufanya ni kumpigia simu baba yangu kazini na kulia. Nilijua kwamba, angalau ndoto yangu ya kwenda Betheli imepatwa na kizuizi.”

Ugonjwa ni sababu ya msingi inayofanya ‘viumbe vyote vifulize kupiga kite pamoja na kuwa katika maumivu pamoja hadi sasa.’ (Waroma 8:22) Mamilioni ya vijana ni miongoni mwa wagonjwa. Hatimaye vijana wengi hupona. Lakini lazima wengine wapambane na magonjwa ambayo ni ya kudumu au, katika matukio fulani, ni yenye kutisha uhai. Miongoni mwa magonjwa ambayo husumbua vijana kwa kawaida ni pumu, kisukari, anemia ya sickle-cell, magonjwa ya kuambukiza, kifafa, magonjwa ya akili, na kansa. Baadhi ya vijana huishi na magonjwa mengi kwa wakati mmoja.

‘Kwa Nini Hili Linanipata?’

Kwa kawaida magonjwa hutokeza mkazo wa akili na kihisia-moyo, kuongezea taabu ya kimwili. Kwa mfano, ikiwa ugonjwa hukufanya usiende shule kwa miezi kadhaa, si kwamba utakuwa nyuma kimasomo tu bali pia utahisi uko mbali na jamii. Wakati Sunny mwenye umri wa miaka 12 alazimikapo kukosa shule kwa sababu ya kulazwa kila mara hospitalini, yeye huwa na wasiwasi, ‘Wanadarasa wenzangu wanafanya nini sasa? Jambo gani ninakosa leo?’

Vivyo hivyo, ukuzi wa kiroho pia waweza kuonekana kuathirika uwapo mgonjwa sana kiasi cha kushindwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo au hata kusoma Biblia. Katika hali kama hizo wahitaji tegemezo la ziada la kihisia-moyo na kiroho. Kwanza, huenda ukakataa kuamini ugunduzi wa ugonjwa. Baadaye, waweza kuhisi hasira sana, labda kwako mwenyewe, ukifikiri kwamba labda kwa njia fulani ungeweza kuepuka ugonjwa huo. Waweza kuhisi kulia, ‘Kwa nini Mungu aliruhusu hili linipate?’ (Linganisha Mathayo 27:46.) Kwa kweli, ni jambo la kawaida kupatwa na mshuko-moyo kwa kiasi fulani.

Kwa kuongezea, kijana aweza kufikiri kwamba ikiwa afanya juhudi za kipekee, kama vile kujaribu kuwa na tabia nzuri zaidi, Mungu ataondolea mbali ugonjwa wake. Lakini, kufikiri kwa namna hiyo kwaweza kuongoza katika kutamauka, kwani Mungu hatoi ahadi ya kuponyesha kimuujiza wakati huu.—1 Wakorintho 12:30; 13:8, 13.

Labda ulitumaini kwamba kamwe hutakufa—kwamba ungekuwa hai wakati Mungu aletapo “dhiki kubwa.” (Ufunuo 7:14, 15; Yohana 11:26) Ikiwa ndivyo, kujua kwamba una ugonjwa utishao uhai bila shaka utashtuka sana. Huenda ukastaajabu ikiwa umefanya kitu fulani cha kumchukiza Yehova, au waweza kufikiri kwamba Mungu amekuchagua wewe kwa jaribu fulani maalumu la uaminifu-maadili. Lakini, hiyo si mikataa inayofaa. “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote,” lasema Neno la Mungu, Biblia. (Yakobo 1:13) Ugonjwa na kifo ni sehemu za hali za sasa za mwanadamu, na sisi sote tunapatwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa.”—Mhubiri 9:11, NW.

Kushughulikia Hofu

Kupata ugonjwa mkubwa kwaweza kukufanya uwe na hofu kuu kwa mara ya kwanza. Kitabu How It Feels to Fight for Your Life hurekodi maoni ya vijana 14 wenye magonjwa makubwa. Kwa mfano, Anton, mwenye umri wa miaka kumi, aliogopa kwamba angekufa wakati wa shambulio kali la ugonjwa wa pumu. Na Elizabeth, mwenye umri wa miaka 16, ambaye alikuwa akipigana na kansa ya mifupa, aliogopa kulala usingizi kwa sababu huenda asiamke tena.

Ingawa, baadhi ya vijana, wana hofu ya namna nyingine—hofu kwamba hakuna mtu atakayetaka kufunga ndoa nao au hofu kwamba hawatakuwa na watoto wenye afya baadaye maishani. Vijana wengine huhofu kwamba waweza kuwapa washiriki wengine wa familia ugonjwa wao, ugonjwa wao uwe ni wenye kuambukiza au la.

Hata kama ugonjwa huo si hatari tena au upo katika hali ya kupungua, kujitokeza tena kwa ugonjwa huo kwaweza kutokeza tena hofu. Ikiwa uliwahi kupatwa na hofu kama hiyo, unajua kwamba hofu hizo ni kweli kabisa. Kwa uzuri, hisia-moyo nyingi za kwanza zisizofaa huelekea kupungua baada ya muda. Kisha waweza kuanza kupima hali zako kwa ufahamu zaidi.

Matatizo ya Kuwa Mgonjwa

“Uwapo kijana, wahisi ukiwa na nguvu za kuweza kufanya jambo lolote,” asema Jason, aliyetajwa mwanzoni. “Kisha kwa ghafula, uwapo mgonjwa sana watambua kwamba huna nguvu za kuweza kufanya jambo lolote. Wahisi kwamba umekuwa mzee kwa usiku mmoja, kwani walazimika kupunguza shughuli zako.” Naam, ni vigumu kupambana na vizuizi vipya.

Jason alipata kwamba tatizo jingine kubwa huja wakati wengine washindwapo kuelewa hali yako. Jason ana kile kiwezacho kuitwa “ugonjwa usioonekana.” Sura yake ya nje haionyeshi tatizo lake la ndani. “Mwili wangu haumeng’enyi chakula kama unavyopaswa,” aeleza Jason, “Hivyo ninalazimika kula mara kwa mara na ninakula chakula kingi zaidi ya wengine. Hata hivyo, bado mimi ni mwembamba. Pia, pindi nyingine mimi huchoka sana kiasi cha kushindwa kuwa macho wakati wa mchana. Lakini watu husema maneno yaonyeshayo kwamba mimi ni mwenye kujiachilia sana au mvivu. Wao husema maneno kama vile: ‘Wajua kwamba unaweza kufanya zaidi. Lakini hata hujaribu!’”

Jason ana ndugu na dada wachanga ambao hawaelewi mara zote kwa nini hawezi kufanya mambo ambayo alikuwa anafanya zamani, kama vile kuwapeleka kucheza mpira. “Lakini najua kwamba ikiwa nitaumia,” asema Jason, “yaweza kuchukua majuma kadhaa ili kupona. Waelekea kulinganisha maumivu yangu na yao na kusema, ‘Yeye apiga kite tu ili aangaliwe.’ Maumivu yao makubwa zaidi labda ni kuteguka kwa mguu, hivyo hawawezi kuwazia maumivu yangu yakoje hasa.”

Ikiwa ugonjwa wako unakuwa mzigo kwa familia, waweza kupambana na hatia. Wazazi wako pia waweza kuhisi hatia. “Wazazi wangu wote wawili waamini kwamba wamenirithisha tatizo hilo,” asema Jason. “Kwa kawaida watoto huweza kujirekebisha kwa tatizo baada ya kuukubali uhalisi wa tatizo hilo. Lakini wazazi wana wakati mgumu zaidi. Wao huniomba msamaha kwa kurudia-rudia. Ninalazimika kufanya yote niwezayo nyakati zote ili kujaribu kutuliza hisia zao za hatia.”

Ziara za Kitiba—Si Jambo la Kupendeza

Ziara za kawaida kwa daktari zaweza kuwa chanzo cha wasiwasi. Zaweza kukufanya uhisi mnyonge na bila msaada. Kukaa tu hospitalini katika chumba cha uchunguzi kungoja zamu yako kwaweza kuwa kwenye kutisha. “Wahisi . . . mpweke sana na ingekuwa vizuri ikiwa ungekuwa na mtu,” asema Joseph, mwenye umri wa miaka 14, ambaye ana ugonjwa wa moyo. Kwa kusikitisha, baadhi ya vijana hawapati aina hiyo ya utegemezo, hata kutoka kwa wazazi wao.

Hali kadhalika uchunguzi wa kitiba pia waweza kutokeza wasiwasi. Kwa kweli, baadhi ya chunguzi haziwezi kupendeza hata kidogo. Kisha, baadaye, waweza kulazimika kuvumilia kwa wasiwasi kwa siku au majuma kadhaa ungojapo matokeo. Lakini kumbuka hili: Kufanya uchunguzi wa kitiba si sawa na kufanya mtihani shuleni; kuwa na tatizo la kitiba hakumaanishi kwamba umeshindwa kwa kiasi fulani.

Kwa kweli, uchunguzi waweza kuandaa habari zenye kusaidia sana. Unaweza kuonyesha kwamba una tatizo la kitiba ambalo linaweza kutibiwa kwa urahisi. Au ikiwa sivyo, uchunguzi waweza kusaidia kuonyesha kile unachoweza kufanya ili kuishi na tatizo hilo. Unaweza hata kuonyesha kwamba kumbe huna tatizo fulani lililofikiriwa. Hivyo usiwe mwenye haraka kufikia mkataa kuhusu hali yako.

Kuwa na wasiwasi sana kutakuumiza tu. Biblia husema: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha.” (Mithali 12:25) Badala yake, Mungu atualika tumwambie kuhusu wasiwasi wetu. Twapaswa kuitibari kwamba yeye hutujali na kwamba atatupatia mwelekezo wake na hekima ili kushughulika na tatizo kwa njia bora zaidi.—Zaburi 41:3; Mithali 3:5, 6; Wafilipi 4:6, 7; Yakobo 1:5.

Twaweza kuwa wenye furaha kwamba Muumba wetu, Yehova Mungu, ameandaa uandalizi wa kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. Yeye hata atafufua wale ambao wamekufa, akiwapatia fursa ya kufurahia ulimwengu huo mpya. Wakati huo, Biblia yatuhakikishia kwamba “Wala hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.

Hadi wakati huo, waweza kuhitaji kukabiliana na ugonjwa hatari. Lakini, kuna mambo mengi yenye kutumika uwezayo kufanya ili kukabiliana kwa mafanikio na hali yako. Tutazungumza hayo katika makala ijayo.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Waweza kuuliza, ‘Kwa nini Mungu aliruhusu hili linipate?’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki