Kigezo cha Kuiga
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA CHILE
Giacomo Castelli ana nyumba katika Antofagasta, jiji lenye wakazi karibu 170,000, lililoko kaskazini mwa Chile. Juni iliyopita, akiwa katika roshani yake aliona kikundi cha watu katika bustani ya mahali hapo. “Jambo la kushangaza lilikuwa kuwaona matineja wakicheka na kujifurahisha pamoja na wazazi wao,” aliandika katika barua kwa gazeti El Mercurio. Ili kuthibitisha mwono huu usio wa kawaida, alienda katika bustani hiyo.
“Nilipata mshangao mwingine,” aliandika mwandikaji huyo mdadisi. “Baadhi ya familia zilipomaliza chakula cha mchana, kila mmoja wa washiriki wao alianza kuokota kile kilichodondoshwa bila kukusudiwa kwenye nyasi na kukiweka katika mfuko wake wa takataka. . . .
“Nilitaka kujua hawa watu wasio wa kawaida walikuwa nani,” aliendelea mwandikaji huyo. “Nilimwendea msichana mrembo ambaye angeweza kuwa mshindi wa mashindano ya uzuri, naye aliniambia kwa upole: ‘Sisi ni Mashahidi wa Yehova, na tunakutana katika Regional Stadium kwa ajili ya kusanyiko.’” Wakati wa pumziko la mchana, vikundi kutoka kusanyiko la mzunguko lililohudhuriwa na watu zaidi ya 3,000 vilikuwa vimeenda katika bustani hiyo kwa ajili ya chakula cha mchana.
“Mimi ni mfuasi wa Katoliki ya Kiroma ya Kimitume,” alisema mwandikaji huyo. “Kwa uaminifu huhudhuria Misa takatifu na miaka iliyopita hata nilisafiri Lourdes, katika Ufaransa.
“Lakini, kwa heshima ya malezi yangu ya Kikristo yenye uvutano sana, kwa unyofu lazima nijiulize: Wao wana nini ambacho sisi Wakatoliki, dini ya watu wengi katika Chile, hatuna? Kwa nini hawa matineja waonekana wako huru sana kwa wazazi wao wakati binti zangu watatu huondoka nipendekezapo tu wazo la kwenda nje pamoja?
“Kwa nini watoto wetu wa Kikatoliki ni wenye jeuri; kwa nini hupiga kelele na kuiga vipindi vya ‘Power Rangers’ wakiwapiga watoto wengine, . . . ilhali watoto hawa ni wenye amani, ni wenye furaha kweli kweli, na wenye kufikiria ikolojia? Kwa nini sisi Wakatoliki hatuwezi kukutana pamoja katika makusanyiko bila ya kujiingiza katika biashara ya aibu sana ambayo huzunguka sehemu zetu takatifu zaidi za kidini kama vile vihekalu vya La Tirana, Andacollo, na vinginevyo?
Mwandikaji huyo, Bw. Castelli, alimalizia barua yake kwa gazeti hilo kwa swali hili: “Wale miongoni mwetu ambao tunajihesabu kuwa ni Wakatoliki na Wakristo je, tutakuwa kama wao? Mungu na Bikira na watubariki kuwa hivyo.”