Vijana Huuliza . . .
Naweza Kukabilianaje na Kuwa Mgonjwa Sana?
JASON alikuwa na umri wa miaka 18 tu, lakini ilionekana kana kwamba miradi yake yote ya maisha sasa ilikuwa isiyofikika. Alikuwa ametumaini kutumikia akiwa mhudumu Mkristo wa wakati wote, lakini ndipo akapata kujua kwamba alikuwa na maradhi ya Crohn—tatizo lenye maumivu na lenye kudhoofisha la matumbo. Hata hivyo, leo, Jason anakabili hali zake kwa mafanikio.
Labda wewe pia unapambana na ugonjwa mbaya. Katika makala moja iliyotangulia, Amkeni! lilizungumzia matatizo yanayokabiliwa na vijana kama wewe.a Acha sasa tutazame jinsi uwezavyo kushughulikia hali yako kwa mafanikio.
Mtazamo Chanya wa Akilini
Kukabili ugonjwa wowote kwa mafanikio huhusisha mtazamo chanya wa akilini. Biblia husema hivi: “Roho ya mtu itastahimili udhaifu wake; bali roho iliyovunjika nani awezaye kuistahimili?” (Mithali 18:14) Mawazo na hisia za huzuni za kutotazamia mazuri hufanya iwe vigumu kupona. Jason alipata hilo kuwa kweli.
Mwanzoni, ilimlazimu Jason kupambana na hisia hasi, kama vile hasira, ambazo zilikuwa zikimfanya ashuke moyo sana. Ni nini kilichosaidia? Yeye aeleza: “Makala katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kuhusu mshuko-moyo zilinisaidia sana kudumisha mtazamo chanya. Sasa najaribu kukabili siku moja kwa wakati mmoja.”b
Carmen mwenye umri wa miaka 17 vivyohivyo alijifunza kufikiria sehemu chanya za hali yake. Ingawa anaugua anemia ya sickle-cell, yeye hufikiria hali zake zilizo nzuri. “Mimi hufikiri juu ya wengine ambao wako katika hali mbaya kuliko mimi na ambao hawawezi kufanya mambo ambayo naweza kufanya,” yeye asema. “Na nahisi nikiwa mwenye shukrani na sijisikitikii.”
Mithali 17:22 husema: “Moyo uliochangamka ni dawa nzuri.” Wengine huenda wakahisi kwamba kicheko hakifai wakati wa ugonjwa mbaya. Lakini ucheshi wenye nia nzuri na uandamani mzuri huburudisha akili yako na kuongeza tamaa yako ya kuishi. Kwa hakika, shangwe ni sifa ya kimungu, moja ya matunda ya roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Roho hiyo yaweza kukusaidia kuhisi shangwe hata ingawa unapambana na ugonjwa.—Zaburi 41:3.
Kupata Daktari Mwenye Kuelewa
Kuwa na daktari ambaye anaelewa vijana ni msaada mkubwa sana. Mahitaji ya kijana ya kiakili na ya kihisia-moyo kwa kawaida ni tofauti na yale ya mtu mzima. Ashley alikuwa na umri wa miaka kumi tu wakati alipokwenda hospitali ili kutibiwa uvimbe katika ubongo uwezao kuleta kifo. Daktari wa Ashley alishughulika naye kwa huruma na kwa maneno ambayo angeelewa. Alimwambia jinsi ugonjwa wa utotoni mwake mwenyewe ulivyomchochea kuwa daktari. Yeye alimwelezea kwa uanana lakini waziwazi, tiba ambayo Ashley alipaswa kupokea, kwa hiyo alijua cha kutarajia.
Wewe na wazazi wako mtataka kutafuta wafanyakazi wa kitiba wanaowastahi na wanaoelewa mahitaji yako. Ikiwa kwa sababu fulani huhisi kustarehe kiasi fulani na utunzi unaopata, jihisi huru kueleza mahangaiko yako kwa wazazi wako.
Pigania Afya Yako!
Ni jambo la muhimu pia kwamba upigane na ugonjwa wako katika kila njia uwezayo. Kwa mfano, jifunze mengi kadiri uwezavyo kuhusu hali yako. “Mtu mwenye hekima ana nguvu,” yaonelea methali ya Biblia. (Mithali 24:5) Ujuzi huondosha hofu ya mambo yasiyojulikana.
Kwa kuongezea, kijana mwenye ufahamu aweza kujihusisha zaidi katika matibabu yake na yuko katika hali nzuri ya kushirikiana katika matibabu yake. Kwa kielelezo, huenda akajua kwamba hapaswi kuacha kutumia dawa alizoagizwa bila pendekezo la daktari wake. Carmen aliyetajwa hapo juu, alisoma vitabu kuhusu anemia ya sickle-cell, kama walivyofanya wazazi wake. Walichojifunza kiliwasaidia kupata matibabu ambayo yangeweza kumsaidia Carmen sana.
Mwulize daktari wako maswali hususa—zaidi ya mara moja ikilazimu—ikiwa hujafahamu jambo fulani waziwazi. Badala ya kusema kile ambacho unafikiri daktari ataka kusikia, eleza kwa weupe wa moyo kile unachofikiri na kuhisi. Kama Biblia isemavyo, “pasipo mashauri makusudi hubatilika.”—Mithali 15:22.
Katika hatua fulani Ashley alionekana kuwa mwenye kutowasiliana sana kuhusu ugonjwa wake. Yeye alikuwa akizungumza na mama yake tu kuuhusu. Mfanyakazi wa kijamii mwenye hekima alimwuliza hivi faraghani: “Je, wahisi kwamba huenda huambiwi kila kitu?” Ashley alisema kutoka moyoni kwamba ndivyo alivyohisi. Kwa hiyo mwanamke huyo akamwonyesha Ashley rekodi zake za kitiba na kumweleza kuzihusu. Yeye pia aliwaomba madaktari watumie wakati mwingi kuzungumza na Ashley moja kwa moja, badala ya kuzungumza na wazazi wake kumhusu. Kwa kujieleza hatimaye, Ashley aliweza kupata msaada aliohitaji.
Utegemezo Kutoka kwa Walio Karibu Nawe
Wakati mshiriki yeyote wa familia awapo mgonjwa sana, hali hiyo huwa jambo la familia, ikihitaji jitihada ya pamoja. Familia ya Ashley na kutaniko la Kikristo zilijiunga pamoja ili kumtegemeza. Kutaniko lilikumbushwa pindi kwa pindi kwamba alikuwa hospitalini. Washiriki wa kutaniko walimtembelea kwa ukawaida, na walisaidia familia yake na kazi ya nyumbani na kutayarisha milo hadi familia ilipoweza kurudia kawaida yayo. Watoto kutanikoni walimtembelea Ashley hospitalini wakati hakuwa mgonjwa sana kiasi cha kutoweza kupata uandamani. Hilo halikuwa zuri kwa Ashley tu bali pia kwa rafiki zake wachanga.
Ingawa hivyo, kabla ya wengine kuweza kukupa msaada, ni lazima wajue kwamba unauhitaji. Carmen hutazamia kupata utegemezo wa kihisia-moyo na kiroho kutoka kwa wazazi wake na wazee wa kutaniko. Yeye pia huwatazamia wenzake shuleni wanaoshiriki itikadi zake za Kikristo wampe utegemezo. “Wao hunihangaikia,” asema Carmen, “na nahisi kuwa natunzwa.”
Shule yako huenda ikaweza kuandaa shauri lenye msaada la kitiba na kifedha na kuweza hata kutoa utegemezo wa kibinafsi. Kwa mfano, mwalimu wa Ashley alitia moyo darasa lake limwandikie barua Ashley na kumtembelea. Ikiwa walimu wako hawafahamu magumu unayokabili, huenda ikalazimu wazazi wako kuzungumzia hali yako kwa staha na mamlaka ya shule.
Tumia Akili na Mwili kwa Hekima
Unapokuwa mgonjwa sana, huenda usiweze kufanya lolote ila kufikiria sana nishati uliyo nayo ya kupata nafuu. Ikiwa hujadhoofishwa kabisa, kuna mambo mengi yenye kujenga uwezayo kufanya. Mtungaji Jill Krementz alitoa maelezo kuhusu kile alichoona alipokuwa akifanyia utafiti kitabu chake How It Feels to Fight for Your Life: “Limekuwa jambo lenye kunihuzunisha kutumia miaka miwili nikitembea kwenye kumbi za hospitali na kuona watoto wengi sana wakitazama televisheni. Twahitaji kuwatia moyo wachanga hawa wasome zaidi. Kwenye kitanda cha hospitali ni mahali pazuri pa mtu kufanyisha ubongo wake mazoezi.”
Iwe uko nyumbani au hospitalini, kufanyisha stadi zako za kiakili mazoezi kwaweza mara nyingi kukusaidia uhisi vizuri zaidi. Je, umepata kujaribu kuandika barua au mashairi? Kuchora au kupaka rangi? Namna gani kujifunza kucheza ala ya muziki ikiwa hali yako yaruhusu? Hata ukiwa na mapungukio ya kiafya, kuna uwezekano mwingi. Kwa hakika, jambo bora zaidi uwezalo kufanya ni kusitawisha zoea la kusali kwa Mungu na kusoma Neno lake, Biblia.—Zaburi 63:6.
Hali yako ikiruhusu, utendaji ufaao wa kimwili waweza kukusaidia uhisi vizuri zaidi. Kwa sababu hii makao ya kitiba mara nyingi huwa na programu za tiba ya mazoezi kwa wagonjwa wachanga. Katika visa vingi mazoezi yafaayo hayaendelezi kupona kimwili tu bali pia husaidia kufanya uwe mchangamfu.
Usife Moyo!
Alipokuwa akiteseka sana, Yesu alisali kwa Mungu, Akamtumaini, na akakazia fikira wakati ujao wake mwenyewe wenye shangwe badala ya maumivu aliyokuwa akipata. (Waebrania 12:2) Alijifunza kutokana na maono yake yenye maumivu. (Waebrania 4:15, 16; 5:7-9) Alikubali msaada na kitia-moyo. (Luka 22:43) Yeye alikazia hali-njema ya wengine badala ya hali yake mbaya.—Luka 23:39-43; Yohana 19:26, 27.
Ingawa huenda ukawa mgonjwa sana, wewe pia waweza kuwa kichocheo kwa wengine. Katika ripoti ya shule, dada ya Ashley, Abigail, aliandika hivi: “Mtu ninayevutiwa naye sana ni dada yangu. Hata ingawa ni lazima aende hospitali kutiwa dawa kupitia mishipa na kudungwa sindano nyingi, bado yeye huonekana akitabasamu!”c
Jason hajaacha miradi yake, ameibadili kwa namna fulani tu. Sasa mradi wake ni kwenda kutumikia mahali palipo na uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme wa Mungu. Kama ilivyo katika kisa cha Jason, huenda usiweze kufanya yote uwezayo. Jambo la maana ni kujifunza kuishi kulingana na mapungukio yako mwenyewe, kutojikinga kupita kiasi wala kutokuwa mzembe. Mtegemee Yehova akupe hekima na nguvu ya kufanya kadiri uwezavyo. (2 Wakorintho 4:16; Yakobo 1:5) Na kumbuka, wakati utafika ambapo dunia hii itakuwa paradiso, ambapo “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Ndiyo, siku moja utakuwa na afya njema tena!
[Maelezo ya Chini]
b Ona Mnara wa Mlinzi, Oktoba 1, 1991, ukurasa wa 15; Machi 1, 1990, ukurasa wa 3-9; na Amkeni!, Oktoba 8, 1988, ukurasa wa 2-16; Novemba 8, 1988, ukurasa wa 10-14.
c Ona pia Siri ya Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., ukurasa wa 116-127.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Dada mkubwa Abigail huvutiwa na moyo mkuu wa Ashley