“Nimeshika Imani”
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MARAFIKI WA BRUNELLA INCONDITI
“SIKU ya Jumamosi ilisonga polepole sana na ikawa yenye upweke sana. Nilikuwa peke yangu chumbani, nikiwa bila tumaini lolote. Ilikuwa ni kama kutembea katika ujia ulioko katikati ya vyumba. Kila kitu kilikuwa kikiendelea sawa, na kwa ghafula mtu fulani akafunga mlango kwa kishindo mbele yangu, na hakukuwa na njia ya kutoka, hata nilipojaribu kwa kadiri gani.”
Brunella Inconditi mwenye miaka 15 alikuwa ametamauka sana moyoni mwake. Siku ya maana zaidi maishani mwake ilikuwa ikipita. Mapema mwaka huo upendo wake uliokuwa ukizidi kukua kwa ajili ya Yehova na Biblia ulikuwa umemsukuma aweke maisha yake wakfu kwake. Alikuwa abatizwe mnamo Julai 1990 katika “Lugha Iliyo Safi” Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova katika Montreal, Kanada. Badala ya hivyo, Brunella alikuwa karibu kukabili jaribu kwa imani yake ambalo lingedumu maishani mwake mwote.
Siku mbili kabla ya siku aliyotazamia kuonyesha wakfu wake kwa ubatizo wa maji, Brunella aligundua kwamba alikuwa na leukemia. Madaktari katika hospitali ya huko ya watoto walitaka kuanza kumtibu mara hiyo, kwa hiyo Brunella alibaki hospitalini.
Maneno Yake Mwenyewe Yagusa Mioyo ya Madaktari
Brunella alijua kwamba damu ni kitu kitakatifu kwa Yehova Mungu. (Mambo ya Walawi 17:11) Wazazi wake, Edmondo na Nicoletta, walikuwa wametaja kwamba binti yao asitiwe damu mishipani wakati wa kutibiwa. “Brunella alitaka madaktari wasikie kutoka kwake pia, ingawa alikuwa mtoto,” baba yake akumbuka. “Aliwaambia kwa uthabiti kwamba yeye hakutaka tiba ambayo ingevunja amri ya Biblia ya ‘kuepukana na damu.’”—Matendo 15:20.
Mnamo Julai 10, 1990, madaktari watatu na mfanyakazi wa jamii walikutana na wazazi wa Brunella na wahudumu wawili kutoka kutaniko la huko la Mashahidi wa Yehova. Uchunguzi ulithibitisha kwamba Brunella alikuwa na leukemia aina ya limfoblasti. Madaktari hao walieleza mipango yao ya kukabili maradhi hayo. Walieleza kwa njia ya busara kwamba ilikuwa vigumu sana kutibu maradhi hayo. “Mwenendo wa Brunella na azimio lake la kumtii Mungu lilikuwa limegusa sana mioyo ya madaktari hao na yule mfanyakazi wa jamii. Walivutiwa sana na jinsi wazazi wake walivyompenda na vilevile ule utegemezo wa marafiki kutoka kutaniko la Kikristo. Wao pia walithamini jinsi tulivyoelewa na kustahi msimamo wao,” akumbuka mmoja wa wazee wa kutaniko.
Madaktari walikusudia kuepuka kumtia damu mishipani. Brunella angetibiwa sana kwa njia ya tiba ya kemotherapi (tiba ya kemikali), lakini isiyo na nguvu kama kawaida. Jambo hilo lingepunguza madhara ya chembe za damu yasababishwayo na tiba hiyo. “Madaktari walifikiria mahitaji ya kimwili, kihisia-moyo, na ya kiroho ya Brunella,” aeleza Nicoletta. “Tulipowaomba washauriane na daktari mwenye ujuzi wa muda mrefu wa kutibu leukemia ya watoto bila kutumia damu, walikubali.” Brunella na wafanyakazi wa hospitali hiyo walisitawisha upendo mchangamfu kati yao.
Miradi ya Kiroho
Ingawa tiba ya kwanza ilitokeza matokeo fulani mazuri, majaribio makali ya Brunella ndiyo yalikuwa tu yanaanza. Kufikia Novemba 1990 maradhi yake yalipungua, kwa hiyo bila kuchelewa alibatizwa. Akifikiria miezi michache iliyopita, Brunella alikiri hivi: “Haikuwa rahisi kamwe. Unahitaji nguvu nyingi sana, na unahitaji kufikiria mambo yafaayo. . . . Imani yangu ilijaribiwa, lakini nilibaki imara, na ningali ninapanga kuchukua upainia wa kawaida [mhudumu wa wakati wote] ukiwa kazi ya maisha yangu.”
Mapema katika 1991, Brunella alirudiwa na maradhi yake. Nusura afe akitibiwa kwa njia ya kemotherapi, lakini kwa mshangao na furaha ya kila mtu, alipata nafuu. Kufikia Agosti alikuwa na afya njema kiasi cha kumwezesha kutumia mwezi mzima katika huduma ya peupe akiwa painia-msaidizi. Ugonjwa wake ukaongezeka tena, na kufikia Novemba 1991 alikuwa na kansa katika sehemu kadhaa za mwili wake. Madaktari wengine katika hospitali nyingine wakaanza kumtibu kwa tiba ya aina ya mnururisho.
Hata chini ya hali ngumu kama hizo, Brunella alibaki imara na kujiwekea miradi ya kiroho. Alipojua kwa mara ya kwanza kwamba ana leukemia, aliambiwa huenda angeishi kwa miezi sita pekee. Sasa, karibu mwaka moja na nusu baadaye, Brunella alikuwa angali anafanya mipango ya wakati ujao. “Hakukawia kujaribu kutimiza miradi yake,” mzee mmoja wa kutaniko akasema. “Imani ya Brunella kwa Paradiso iliyoahidiwa na Mungu ilimdumisha katika majaribu yake. Akakomaa Kikristo ingawa alikuwa mchanga kwa umri. Mwenendo wake na mtazamo wake ulichochea kutaniko na kufanya wale waliomjua wampende sana, kutia ndani wafanyakazi wa hospitali.” Mama yake akumbuka hivi: “Hakulalamika kamwe. Mtu alipomwuliza anahisije, yeye angejibu hivi, ‘Vizuri’ au, ‘Si vibaya, na wewe je?’”
Wakati Ujao Salama
Brunella alipanga kuhudhuria “Wachukuaji Nuru” Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova mnamo Julai 1992. Hata hivyo, kufikia wakati wa mkusanyiko, Brunella alilazwa hospitalini, na afya yake ilikuwa ikiendelea kudhoofika. Hata hivyo, yeye alihudhuria mkusanyiko katika kiti cha magurudumu, akitazamia kuona ile drama Kufanya Yaliyo Sawa Machoni pa Yehova.
Alirudi nyumbani kwa familia yake kwa siku chache za mwisho za maisha yake. “Kwa habari hiyo, alihangaikia wengine sana kuliko alivyojihangaikia mwenyewe,” asema Nicoletta. “Angewatia moyo kujifunza Biblia, akiwaambia, ‘Tutakuwa pamoja katika Paradiso.’”
Brunella alikufa Julai 27, 1992, akiwa na tumaini thabiti la ufufuo wa kupata uhai katika Paradiso duniani. Alikuwa tu ameanza kufuatia miradi yake, lakini alikuwa amepanga aendelee na mwendo wake wa kujiweka wakfu baada ya kufufuliwa kwake. Siku chache tu kabla hajafa, Brunella aliandika barua hii ifuatayo, iliyosomwa katika hotuba ya maziko yake.
“Marafiki Wapendwa:
“Asanteni sana kwa kuja. Kuwapo kwenu kwamaanisha mambo mengi kwa familia yangu.
“Kwa watu waliokuwa karibu nami—tumepitia mambo mengi. Tulikuwa na pindi zilizokuwa mbaya, lakini kulikuwa na pindi zenye kuchekesha pia. Lilikuwa ni pigano gumu na lenye kudumu sana, lakini sihisi kwamba nimeshindwa. Kama Maandiko yasemavyo, ‘Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo hadi mwisho, nimeshika imani.’—2 Timotheo 4:7, NW.
“Nimejifunza mengi pia, na nikakua sana, na marafiki wangu na wale waliokuwa karibu nami waliona badiliko hilo. Ningependa kuwashukuru watu wote walionitegemeza.
“Nyinyi mwaminio mfumo mpya na Yehova mwajua kutakuwa na ufufuo, kama Yohana 5:28, 29 isemavyo. Kwa hiyo iweni imara katika kweli, na tutaweza kuonana tena.
“Ninataka kuwashukuru watu wanaojua mambo ambayo nimepitia. Ninampa kila mmoja wenu kumbatio na busu. Ninawapenda nyinyi nyote.”
Brunella hakuacha ujana wake wala ugonjwa wake umfanye aahirishe wakfu wake kwa Mungu. Kielelezo chake cha imani na azimio lake latia moyo vijana kwa wazee kuondoa kitu chochote kinachoweza kuwazuia wasikimbie mbio ya uhai.—Waebrania 12:1.