Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Dyslexia Ninawaandikia ili kueleza shukrani zangu za moyo mweupe kwa makala “Kushinda Fadhaiko la Dyslexia.” (Agosti 8, 1996) Baada ya kusoma sanduku “Jinsi ya Kutambua Dyslexia Katika Watoto,” mume wangu nami tulihakikisha kwamba mtoto wetu mwenye miaka kumi amechunguzwa. Tuligundua kwamba ana tatizo la dyslexia, na sasa tunachukua hatua ili kumpa msaada anaouhitaji, kote nyumbani na shuleni. Wakati wote walimu wake wamekuwa wakituambia kwamba yeye ni mtoto mwenye uwezo sana lakini tu hana bidii. Hivyo mwaweza kuwazia jinsi gani tunashukuru kwamba makala hii ilichapishwa.
J. S., Scotland
Nikiwa mama ya watoto wawili wenye dyslexia, nilifurahia sana kusoma makala hii. Ilifanya kazi nzuri sana ya kuwaelimisha wengine jinsi udhaifu huu ulivyo halisi na jinsi ilivyo tatizo kwa wale wenye kuiugua. Je, mwaweza kuwazia kushindwa kusoma alama ya barabarani? Au kujaribu kuagiza chakula kutoka orodha ya vyakula wakati huwezi kusoma kile kinachosema? Nina uhakika kwamba wale wenye kusumbuka na tatizo hilo wataitumia habari hiyo vizuri.
M. K., Marekani
Spishi Zilizo Hatarini mwa Kutoweka Shukrani za kuhisiwa moyoni kutokana na mfululizo “Spishi Zilizo Hatarini mwa Kutoweka—Kwa Nini Tuhangaike?” (Agosti 8, 1996) Kwa kweli tupo katika hatari ya kupoteza hazina. Makala hiyo iliimarisha tamaa yangu ya kuishi katika ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu, ambapo wanyama wataweza kuishi bila hofu ya kutoweka.
D. I., Albania
Lile Tatizo la Wakimbizi Mimi ni mkimbizi kutoka Burundi, na ningependa kueleza uthamini wangu kutokana na mfululizo “Lile Tatizo la Wakimbizi—Je, Litapata Kwisha?” (Agosti 22, 1996) Nilitiwa moyo sana kujifunza maoni ya Yehova kuhusu jambo hili na jinsi, katika nyakati za kale, alivyotaka watu wake wawatendee wakimbizi kwa fadhili za upendo. Ninawashukuru kwa makala hizo; zilinitia moyo sana.
D. M., Kenya
Msiba wa Basi Wakati wa kusoma makala “Kushinda Msiba kwa Nguvu za Yehova” (Agosti 22, 1996), sikuweza kujizuia ila kulia kwani ni jambo lililonigusa kibinafsi. Mimi pia nilihusika katika aksidenti pamoja na rafiki yangu wa karibu zaidi. Alikufa saa chache baadaye kutokana na majeraha mabaya sana. Wakati wa kipindi cha miaka mitano iliyofuata, nilijifunza kukubali na kushughulika na hisia nzito za kihoro na hatia kwa sababu ya kwamba niliokoka naye alikufa. Ninaitibari katika Yehova kwamba atamkumbuka rafiki yangu mpendwa. Pia ninawasikitikia sana wale ambao wapendwa wao walikufa katika msiba huu katika Hispania.
J. T., Marekani
Kigugumizi Asanteni kwa ile makala ‘Na Ndimi za Wenye Kigugumizi Zitanena.’ (Agosti 22, 1996) mambo yaliyoonwa na Petr Kunc yaliniimarisha sana. Mimi pia ni mwenye kigugumizi. Kabla ya kutoa hotuba ya Biblia, wakati wote mimi humwomba Yehova ili anisaidie kujieleza kwa uwazi.
M. M., Italia
Nilipofikia miaka 20, nilijikuta nikiwa na wakati mgumu wa kuongea na wengine na kutoka katika jukwaa katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Baada ya mgawo, ningetoka jasho sana na kuhisi uchovu usio wa kawaida. Kwa kweli ni kitia-moyo kikubwa kusoma juu ya mambo aliyojionea Mkristo mwenzangu akimtumikia Yehova japo ana tatizo hili. Imenisaidia kuwa na maoni yanayofaa juu ya mambo.
M. S., Japani
Ninasukumwa sana kuwashukuru kwa kuchapisha mambo hayo aliyojionea. Nimekuwa na tatizo hili toka utotoni. Kama Petr, ninatumikia nikiwa mzee katika kutaniko, na ninalazimika kumtegemea Yehova ili anipe nguvu za kutimiza migawo yangu. Sasa ninaongoza Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, nikiwasaidia wengine na semi zao.
N. O. N., Nigeria