Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 6/8 kur. 11-14
  • Katika Masikio ya Kitoto

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Katika Masikio ya Kitoto
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tamaa ya Dini
  • Ndoa na Familia
  • Kuacha Hilo Kanisa
  • Kujifunza Kweli ya Biblia
  • Upinzani wa Familia
  • Mkutano wa Kukumbukwa
  • Mkaribie Msikiaji wa Sala
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Sababu kwa Nini Watu wa Namna Zote Wanakuwa Mashahidi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • “Yehova, Umenipata!”
    Amkeni!—2004
  • Biblia Inabadili Maisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 6/8 kur. 11-14

Katika Masikio ya Kitoto

SIKU moja, nilipokuwa msichana mdogo, mwanamume mmoja alifika nyumbani kwetu katika Coeburn, Virginia, Marekani, na wakati alipokuwa akiongea na baba yangu, mwandamani wake aliongea nami ili kunifanya niwe na shughuli. Maneno yake yalichora akilini picha ya dunia iliyo paradiso, ambapo ningeweza kucheza na wanyama wa pori ambao wasingenidhuru. (Isaya 11:6-9) Alieleza kwamba hata nisingelazimika kufa lakini ningeweza kuishi milele hapa duniani. Wakati ujao ulionekana mzuri sana! Kile ambacho mwanamume yule alisema kuhusu kuishi katika dunia kilikuwa na uvutano sana juu yangu.—Isaya 25:8; Ufunuo 21:3, 4.

Tamaa ya Dini

Wazazi wangu, ambao walikuwa na matatizo mengi ya ndoa, walitalikana miaka michache iliyofuata, na niliishi na mama. Hakupendezwa hata kidogo na dini. Hivyo nilijiendea shule ya Jumapili katika kanisa lolote ambalo lilikuwa umbali wa kutembea kutoka makao yetu. Baada ya muda mfupi mama aliolewa tena, na tulihama na baba wa kambo hadi jimbo la Indiana. Lakini, kila wakati wa kiangazi, nilirudi Virginia ili kumtembelea baba yangu.

Mara baada ya talaka baba mzazi akawa Mmormoni, na alijitahidi kunifundisha dini yake mpya. Wakati wa kiangazi cha 1960, nilipokuwa na miaka minane, alinibatiza. Lakini, nilipokuwa Indiana, nilihudhuria kanisa lolote ambalo lilikuwa karibu na nyumbani. Yote yalifundisha kwamba ikiwa tungekuwa wenye wema wa adili, tungeenda mbinguni, na ikiwa tungekuwa wabaya tungeenda helo, ambapo tungeteswa. Kwa kuwa nilifikiri kwamba hakuna mtu angeelewa hisia zangu za kutaka kuishi katika dunia badala ya mbinguni, sikumwambia mtu yeyote kamwe.

Nilipokuwa na miaka 11, baba alihamia jimbo la Oregon. Nilihisi vibaya sana na nikawa mwenye uchungu sana. Baba yangu wa kambo alikuwa mwatheisti na mraibu wa alkoholi, na alinitatiza sana kuhusu imani yangu. Aliniita Kibinti Kitakatifu, na nilipoanza kulia, angesema: “Kwa nini usimwite Mungu wako akusaidie?” Nyumbani hakuna mtu aliyeonekana kujali kuhusu Mungu. Hiyo ilikuwa miaka ya giza na yenye ugumu. Nilitendwa vibaya kimwili, kwa maneno, na kingono. Nilifarijika kwa kuongea na Mungu kwa sababu mara nyingi nilihisi kwamba ni yeye pekee aliyekuwa ananijali.

Mama alimwacha baba yangu wa kambo, na kutendwa vibaya kukaisha. Lakini tulikuwa maskini sana, na lilikuwa jambo gumu kwa mama kutimiza mahitaji ya kila siku. Nilipokuwa na miaka 13, tulirudi Virginia tena kumtembelea mama mkubwa. Alikuwa mwanamke Mbaptisti mwenye fadhili na moyo mweupe. Nilimpenda sana. Aliponiomba niandamane naye kanisani, nilikubali. Pia mama alikwenda, na ninakumbuka jinsi nilivyohisi vizuri sana kuwa na familia yangu hapo pamoja nami. Baada ya ziara, niliogopa kurudi nyumbani. Niliogopa kwamba ikiwa ningeenda, ningejihusisha katika ukosefu wa adili. Hivyo nilimsihi mama mkubwa niishi na yeye, na mama alikubali.

Mama mkubwa alininunulia tafsiri ya Biblia ya King James. Nilijivunia sana Biblia hiyo na nilisoma sehemu yayo kila siku. Nilisoma katika sura ya mwisho ya Biblia hiyo kwamba “ikiwa mtu yeyote ataongeza katika maneno haya, Mungu atamwongezea mapigo yaliyoandikwa katika kitabu hiki.” (Ufunuo 22:18, 19, King James Version) Hivyo nilifikiri, ‘Ninaweza kuaminije kwamba Kitabu cha Mormon ni sehemu ya Maandiko matakatifu?’ Kwa hiyo, niliamua kuwa Mbaptisti.

Ingawa nina hakika kwamba baba alikasirika nilipomwandikia na kumwambia kuhusu uamuzi wangu, elezo lake pekee lilikuwa kwamba alifurahi nilikuwa ninaenda kanisani. Niliandamana kwa ukawaida na mhudumu Mbaptisti katika nyumba za watu ili kuwaalika kwenye mikutano ya roho iliyofanyiwa katika hema. Nilihisi kwamba nilikuwa ninafanya mapenzi ya Mungu kwa kuwatembelea watu katika nyumba zao na kuongea nao katika njia aliyofanya Yesu.

Bado, nilikuwa na tamaa ya kuishi katika paradiso ya kidunia badala ya mbinguni. Ndipo niliposoma sehemu hii ifuatayo ya Biblia, na ilinipa tumaini: “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa.”—Mathayo 7:7, 8, Union Version.

Ndoa na Familia

Mwaka uliofuata nilirudi Indiana tena ili kuishi na mama. Nilipokuwa bado na miaka 15 tu, niliolewa, nikawa mjamzito, na nilikuwa ninasafiri kwa basi kuelekea kusini mwa California. Sikuijua vizuri familia ya mume wangu, lakini nilitaka nikubaliwe nao. Walikuwa Wapentekoste, na dada ya mume wangu aliniambia kuhusu zawadi ya kuongea katika ndimi. Hivyo nilipoenda nao katika ibada ya sala zao usiku mmoja, nilisali kwamba niruhusiwe kuongea katika ndimi.

Kwa ghafula, wakati wa ibada hisia ya ajabu ilinijia. Nilianza kutetemeka mwili mzima, na ulimi wangu ulianza kubwabwaja bila ya kuzuilika. Mhubiri alipiga kelele kwamba roho ilikuwa inakuja kupitia kwangu, na alianza kunipongeza. Baadaye, kila mtu alinikumbatia na kuniambia ni jambo zuri kama nini kwamba Mungu amenitumia katika njia hiyo. Lakini nilihisi kutatanishwa na kuogopa. Sikuwa hata na wazo la kile nilichosema.

Muda mfupi baadaye, kulikuwa na matatizo ya kujifungua mtoto wangu wa kwanza. Pasta wa kanisa hilo alimwambia mume wangu kwamba Mungu alikuwa anauzidisha uchungu wangu wa kuzaa kwa sababu hakuwa Mkristo. Mume wangu alinijia huku akilia na kuniambia kwamba ikiwa nilifikiri ingesaidia kupunguza uchungu wangu wa kuzaa, angebatizwa. Nilimwambia kwamba nilikuwa na uhakika kabisa kwamba Mungu hatishi watu ili wamtumikie.

Kuacha Hilo Kanisa

Jumapili moja, baada ya hotuba yake, pasta huyo aliliomba kutaniko michango. Kanisa lilihitaji kurekebishwa kwa sababu ya hasara iliyosababishwa na tetemeko la dunia la karibuni. Sahani ya mchango ilipopitishwa, niliweka fedha zote nilizokuwa nazo. Baada ya kuhesabu fedha hizo, badala ya pasta kushukuru kutaniko, alilisihi kufungua mifuko na mioyo yao kwa ajili ya jambo hili listahililo. Kisha alipitisha sahani tena. Sikuwa na fedha zaidi, hivyo kwa aibu kubwa, niliipitisha sahani haraka-haraka. Kwa haraka pasta huyo alihesabu fedha hizo tena na bila ya kuwashukuru, alisema tu kwamba hazikutosha. “Kwa hakika hakuna mtu atakayeondoka hadi tutakapopata fedha zihitajiwazo ili kufanya mapenzi ya Mungu,” akasema.

Mume wangu alikuwa anangojea nje, na nilijua kwamba alikuwa anakosa subira. Si yeye peke yake alikosa subira. Nilikosa subira kutokana na kukosa shukrani kwa pasta. Nikiwa na mtoto wangu mikononi mwangu na machozi yakinitiririka, nilitoka nje ya kanisa huku kila mtu akiangalia. Niliazimia kwamba sitajihusisha tena kamwe na kanisa. Ingawa niliacha kwenda kanisani, sikuacha kuamini Mungu. Bado niliendelea kusoma Biblia na kujaribu kuwa mke mzuri.

Kujifunza Kweli ya Biblia

Baada ya mtoto wetu wa pili kuzaliwa, rafiki zetu waliokuwa wanahamia jimbo la Texas waliongea na mwenye nyumba ili tupangishe nyumba walimoishi. Rafiki yangu Pat alipokuwa akiondoka, alisema kwamba mwanamke fulani alikuwa na fedha zake na angekuja nazo. Pat aliniomba nimtumie fedha hizo Texas. Siku chache baadaye, wanawake wawili walibisha mlango. Nikifiri walikuwa na fedha hizo, mara moja niliwakaribisha ndani. Nilieleza kwamba Pat alihama lakini alikuwa ameniambia kwamba wangepitia. “Naam, Pat alifanya vema,” Charlene Perrin, mmoja wa wanawake hao akasema. “Tulifurahia kwelikweli kujifunza naye.”

“Nini?” niliuliza. “Kujifunza? Ni lazima mmekosea.” Charlene alieleza kwamba walikuwa wameanza funzo la Biblia na Pat. Baada ya kujua kwamba Pat amehama, Charlene aliniuliza ikiwa ningependa kujifunza Biblia. “Ndiyo,” nilijibu kwa uhakika. “Nitawafundisha kila kitu mnachotaka kujua.” Nilijivunia usomaji wangu wa Biblia ambao nilikuwa nimefanya, na nilihisi kwamba ningeweza kuwatia moyo.

Charlene alinionyesha kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, na tulisoma Zaburi 37:9: “Watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao BWANA ndio watakaoirithi nchi [“dunia,” NW].” Nilishangaa. Hapo, katika Biblia yangu, palisema kwamba watu wangeirithi dunia. Baada ya hayo, niliuliza maswali mengi kwa wakati mmoja. Charlene alitabasamu na kusema: “Ala! Polepole! Tutajibu maswali yako moja baada ya jingine.” Alieleza umuhimu wa funzo la Biblia la kawaida, la utaratibu. Mara moja, alinikaribisha kwenye Jumba la Ufalme, jina la mahali pa kukutania pa Mashahidi wa Yehova.

Nilimweleza Charlene kuhusu jambo lililonipata kuhusu sahani ya mchango na kwamba sikutaka kurudi kanisani. Alisoma pamoja nami, Mathayo 10:8 ambalo husema: “Mlipokea bure, toeni bure.” Alisema kwamba hakuna sahani ya mchango ipitishwayo katika mikutano ya Mashahidi wa Yehova na kwamba michango yote ni ya hiari. Pia alisema kwamba kuna sanduku la mchango katika jumba na kwamba watu watakao kuchanga waweza kuweka michango katika hilo sanduku. Niliamua kujaribu dini tena.

Nilipoendelea kujifunza, nilijifunza kwa nini nilikuwa nimehisi vibaya sana wakati niliposema katika ndimi katika kanisa la Pentekoste. Zawadi ya Mungu ya kusema katika lugha tofauti-tofauti ilipewa Wakristo wa mapema ili kuwa uthibitisho wa kwamba walikuwa na roho takatifu yake. Zawadi hii ya kimuujiza ilitumikia kusudi linalofaa la kufanya kweli za Biblia kupatikana kwa watu wa mabara mbalimbali ambao walikusanyika pamoja katika Pentekoste 33 W.K. (Matendo 2:5-11) Lakini, Biblia yasema kwamba zawadi ya Mungu ya kusema katika lugha ingekoma, jambo ambalo kwa wazi lilitokea baada ya vifo vya mitume. (1 Wakorintho 13:8) Lakini ili kupofusha akili za watu, Shetani na roho waovu wake wamesababisha baadhi ya watu kubwabwaja maneno yasiyojulikana, katika njia ambayo imewafanya watu wengi waamini kwamba hawa wana roho takatifu ya Mungu.—2 Wakorintho 4:4.

Upinzani wa Familia

Baada ya muda mfupi, nilianza kuelewa kusudi la Mungu kwa dunia na kwamba sipaswi kuwa sehemu ya huu ulimwengu mwovu. (Yohana 17:16; 18:36) Pia nilijifunza kwamba nilipaswa kukata uhusiano wote na Babiloni Mkubwa, ambayo ni ishara itumiwayo katika Biblia kuwakilisha milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. (Ufunuo 18:2, 4) Nilipomwambia baba kwamba nilikuwa ninataka kubatizwa, wakati huu nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alihisi vibaya sana. Alinisihi sana nisiwe Shahidi. Ilikuwa mara ya kwanza kumwona akilia. Nililia pamoja naye, kwani kwa kweli sikutaka kumwumiza. Lakini nilijua kwamba nimepata kweli na kwamba nisingeweza kumkataa Yehova.

Familia yangu yote ilipinga kuwa kwangu mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwa muda fulani niliacha kuhudhuria mikutano. Hili lilipunguza upinzani kutoka kwa washiriki wa familia, lakini nilikuwa na hali mbaya sana. Nilijua kwamba nisingekuwa na amani kamwe hadi nifanye mapenzi ya Yehova. Siku moja wakati wa pumziko la mchana, nilipitia nyumbani kwa Charlene na kumwambia kwamba nilitaka kubatizwa. “Je, hufikiri kwamba jambo la kwanza ni kuanza kuja kwenye mikutano tena?” akauliza. Nilimwambia kwamba wakati huu niliazimia kwamba hakuna kitu kingekuja kati yangu na Yehova. Nilibatizwa Septemba 19, 1973.

Hiyo ilikuwa miaka 23 iliyopita. Kwa uzuri familia yangu imekuja kuheshimu uamuzi wangu, na hakuna yeyote kati yao anisongae niiache kweli ambayo ninaithamini sana. Lakini, Kim, binti yangu mkubwa zaidi, ndiye amekuwa Shahidi pekee kufikia sasa. Utumishi wake wenye uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova umekuwa chanzo cha kitia-moyo kwangu kwa miaka yote.

Mkutano wa Kukumbukwa

Katika 1990, wakati niliporudi Coeburn, Virginia, kwa ajili ya matembezi, nilimwomba mama tupitie Jumba la Ufalme ili nione saa za mikutano kuanza Jumapili. Tulipokuwa tukiingia njia ya kwenda Jumba la Ufalme, alisema kwamba tulikuwa tukiishi katika nyumba iliyokuwa nyuma tu ya jumba, baada ya kuvuka reli. Nyumba hiyo ilikuwa imeungua zamani, na kitu pekee kilichobaki ni dohani ya matofali. “Wakati huo ulikuwa msichana mdogo tu,” akasema, “si zaidi ya umri wa miaka mitatu au minne.”

Jumapili nilikaribishwa kwa shauku katika Jumba la Ufalme. Nilipoongea na Stafford Jordan, ilitukia nilitaja kwamba nilipokuwa mtoto nilikuwa nimeishi katika nyumba ambayo wakati huo ilikuwa nyuma ya Jumba la Ufalme. Aliniangalia kwa makini. “Ninakukumbuka!” akasema kwa mshangao. “Ulikuwa msichana mdogo mwenye nywele zilizosongamana wapata urefu huu [akaonyesha kwa mkono wake]. Tulikuwa tukihubiri katika eneo hili wakati mwandamani wangu alipoanzisha mazungumzo na baba yako. Nilijitahidi kukufanya uwe mwenye shughuli kwa kuongea nawe kuhusu Paradiso.”

Niliduwaa. Sauti yangu ilipaliwa na hisia-moyo nilipomwambia kuhusu jitihada yangu ya kuitafuta kweli ya Biblia. “Nilipokuwa bado kitoto ulipanda mbegu za kweli katika moyo wangu mdogo!” nikasema. Kisha aliniambia kwamba nilikuwa na mtu wa ukoo kwa upande wa babu yangu, Stephen Dingus, ambaye alikuwa amekuwa Shahidi mwaminifu. Familia haikuongea naye kamwe, kwani walikuwa wapinzani sana. “Angalikuonea fahari sana!” akasema Ndugu Jordan.

Niangaliapo miaka yangu ya nyuma katika tengenezo la Yehova, ninashukuru sana kwa upendo na fadhili ambazo nimeonyeshwa. Ndiyo, bado kuna nyakati ambazo nikiwa katika Jumba la Ufalme na kuona familia zikimtumikia Yehova pamoja nahisi huzuni kidogo, kwani karibu mara zote mimi huwa peke yangu. Lakini upesi hukumbuka kwamba Yehova yupo pamoja nami. Sikuzote alikuwa akinilinda, na wakati moyo wangu ulipoweza kuikubali kweli iliyokuwa imesemwa katika masikio ya mtoto mdogo miaka mingi sana iliyopita, aliiruhusu ichipuke na kuchanua.

“Asante sana, Ndugu Jordan,” nikasema, “kwa kutumia wakati kuongea kuhusu Paradiso na msichana mdogo mchangamfu!”—Kama ilivyosimuliwa na Louise Lawson.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Pamoja na Stafford Jordan nilipokutana naye tena katika 1990

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki