Utafutaji Wetu wa Haki
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ANTONIO VILLA
Katika 1836 watu wote wa Texas waliokuwa wakilinda Alamo—wakipungua 200—waliuawa na jeshi la Mexico lenye wanaume wapatao 4,000. Baadaye, ile shime ya vita “Kumbukeni Alamo” ilitumiwa kuchochea yale mapigano ya kutaka uhuru, ambao ulipatikana baadaye mwaka huo. Katika 1845 lile eneo ambalo pindi moja lilikuwa sehemu ya Mexico likawa sehemu ya Marekani, nao Wamexico wakajikuta katika eneo wanamoonyeshwa uhasama. Tofauti za kijamii bado zinakumbukwa.
NILIZALIWA mwaka wa 1937, karibu na San Antonio, Texas, ambako Alamo lipo. Katika siku hizo bafu, chemchemi ya maji, na vifaa vingine vya umma vilikuwa na maandishi “Wazungu Pekee” na “Wengine.” Upesi nikafahamu kwamba lile neno “Wengine” lilitia ndani sisi ambao tulikuwa jamii ya Wamexico.
Wakati wa kuona sinema katika jumba la sinema, Wamexico na weusi waliruhusiwa kuketi kwenye roshani pekee, bali si katika ukumbi mkuu. Mikahawa mingi na biashara nyingi hazingewatumikia Wamexico. Pindi moja mke wangu, Velia, na dadake walipoingia duka ya kutengeneza nywele, wenye duka hiyo hata hawakuwa na adabu ya kusema: “Wamexico hawaruhusiwi hapa.” Wao waliwacheka tu mpaka Velia na dadake wakaaibika na kuondoka.
Nyakati nyingine, wanaume wazungu—mara nyingi wakiwa wamelewa—wangetafuta wanawake Wamexico, ambao wengi waliwaona kuwa wakosefu wa adili kiasili. Nikafikiria, ‘Wao hawashiriki bafu na chemchemi ya maji pamoja nasi, lakini wanalala na wanawake Wamexico.’ Mwanzoni, ukosefu huu wa haki ulinifanya nikose usalama, na baadaye kunifanya niwe mwasi.
Matatizo na Makanisa
Unafiki wa dini ulinichukiza hata zaidi. Wazungu, weusi, na Wamexico wote walikuwa na makanisa tofauti-tofauti. Nilipokuwa nikijitayarishia Komunyo yangu ya kwanza nikiwa Mkatoliki, padri alinipa bahasha fulani zilizowekewa tarehe za wakati ujao nikampe baba yangu. Kila juma tulipaswa kurudisha bahasha moja ikiwa na mchango. Muda mfupi baadaye, padri aliniambia: “Umwambie babako kwamba sijapokea zile bahasha.” Maneno makali ya babangu yakawa na uvutano kwangu: “Wao wanapenda kitu kimoja tu—pesa!”
Kwa ukawaida kulikuwa na kashfa nyingi za wahubiri kutoroka na wanawake katika makutaniko yao. Mambo kama hayo yalinifanya nitangaze kwa kurudia-rudia: “Dini ina mambo mawili tu—ama kuchukua pesa zako ama kuchukua mwanamke wako.” Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova walipozuru, nilikuwa nawaondosha, nikisema: “Nikitaka dini, nitajitafutia mwenyewe.”
Jeshi na Ndoa
Nilijiunga na Jeshi la Wanahewa la Marekani katika 1955, ambako nilitumaini kwamba kwa kufanya kazi yangu vizuri, ningepata heshima ambayo nilikuwa nimenyimwa kwa sababu ya kuwa Mmexico. Kwa kutia bidii, nilipata kutambuliwa, hatimaye nikiwekwa kuwa msimamizi wa kukadiria ubora wa kazi. Kazi hiyo ilihusisha uchanganuzi wa idara nyingine za utumishi wa kijeshi.
Katika 1959, nilimwoa Velia. Sikuzote Velia alikuwa amependa dini. Lakini, alikuwa ametamaushwa na makanisa kadhaa ambayo alikuwa amehudhuria. Siku moja katika 1960, akihisi ameshuka moyo sana, alisali: “Tafadhali, Mungu, kama upo, unijulishe. Nataka kukujua.” Siku iyo hiyo mmoja wa Mashahidi wa Yehova alikuja kwetu katika Petaluma, California.
Lakini, muda mfupi baadaye Velia hakuwaona tena wale Mashahidi kwa sababu nilipewa mgawo mwingine wa kijeshi. Basi haikuwa hadi 1966, nilipokuwa Vietnam, ndipo alianza tena kujifunza Biblia pamoja nao katika Seminole, Texas. Niliporudi nyumbani kutoka Vietnam mapema mwaka uliofuata, sikufurahi kumpata akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi.
Upinzani Wangu wa Kishupavu
Nilihisi kwamba Velia angedanganywa na kutamaushwa na dini. Kwa hiyo nikawapo wakati wa funzo na kutafuta fursa ndogo tu ya kufichua dalili yoyote ya unafiki. Mwanamke huyo aliposema kwamba Mashahidi hawajihusishi kisiasa, niliingilia: “Mume wako hufanya kazi gani?”
“Yeye ni mkulima wa pamba,” akajibu.
“Ha!” nikajibu kwa ufidhuli. “Yunifomu za kijeshi hutengenezwa kwa pamba. Kwa hiyo mnaunga mkono vita!” Nikawa nasema kwa sauti ya juu na kukosa kiasi.
Ingawa katika Juni 1967 mgawo mpya wa kijeshi ulitupeleka mbali sana, hadi Minot, North Dakota, Mashahidi wa huko waliwasiliana na Velia na kuanzisha tena funzo lake la Biblia. Nikaanza kupinga kwa njia za kitoto. Ningefika kimakusudi wakati wa funzo lao na kugongesha milango, kupanda ngazi kwa kelele nyingi, kuangusha buti zangu kwa kelele sakafuni, na kuvuta maji ya choo mara kadhaa.
Velia alikuwa mke mpole na mnyenyekevu ambaye hakupata kufanya jambo lolote bila idhini yangu. Ingawa kwa shingo upande nilimruhusu kuwa na funzo la Biblia, alijua kwamba kungekuwa na matatizo makubwa zaidi kuhudhuria mikutano ya Mashahidi. Alipohimizwa ahudhurie, sikuzote alikuwa akijibu: “Afadhali nisiende. Sitaki kumkasirisha Tony.”
Hata hivyo, siku moja Velia alisoma katika Biblia: “Msiwe mkiitia kihoro roho takatifu ya Mungu.” (Waefeso 4:30) “Hiyo yamaanisha nini?” akauliza. Shahidi aliyeongoza funzo hilo akaeleza: “Roho takatifu ya Mungu imepulizia uandikaji wa Biblia. Kwa hiyo tusipotii isemalo Biblia, basi twaitia kihoro roho takatifu ya Mungu. Kwa mfano, wengine hawaendi mikutanoni, hata ingawa wanajua kwamba Neno la Mungu lasema twapaswa kwenda.” (Waebrania 10:24, 25) Moyo mnyenyekevu wa Velia ulihitaji kichocheo hicho tu. Tangu siku hiyo alihudhuria kila mkutano japo upinzani wangu.
Ningesema kwa ukali: “Unaweza kuondokaje nyumbani na hujaniandalia chakula mezani?” Upesi Velia akajifunza sikuzote awe akiacha chakula changu kikiwa moto na tayari. Kwa hiyo nikatumia visababu vingine: “Wewe hunipendi wala hupendi watoto wetu. Wewe hutuacha kwa ajili ya mikutano hiyo.” Au kama ningeshambulia itikadi za Mashahidi na kama Velia angejaribu kwa upole kuzitetea, ningetumia neno nilipendalo bocona—“domokaya”—nikimwita bocona asiye na staha wala unyenyekevu.
Hata hivyo, Velia alihudhuria mikutano, mara nyingi akiondoka nyumbani kwa machozi tele kwa sababu ya kumshambulia na maneno. Lakini nilikuwa nimeshikilia kanuni fulani. Sikupata kamwe kumpiga mke wangu wala sikupata kufikiria kumwacha kwa sababu ya imani yake. Lakini nilikuwa na wasiwasi kwamba mtu fulani mwenye sura nzuri katika mikutano hiyo angependezwa naye. Na bado nilifikiri kwamba kwa habari ya dini, ‘Wao hutaka tu ama pesa ama mwanamke.’ Mara nyingi nilimlalamikia Velia alipokuwa akivaa ili kwenda mikutano: “Unajirembesha kwa ajili ya mtu mwingine lakini hujirembeshi kamwe kwa ajili yangu.” Kwa hiyo mara ya kwanza nilipoamua kuhudhuria mkutano, nilisema: “Ninaenda—lakini ili nikuchunguze vizuri tu!”
Hata hivyo, kusudi langu hasa lilikuwa kupata jambo fulani dhidi ya Mashahidi. Katika mmojawapo wa mikutano niliyohudhuria kwa mara ya kwanza, hotuba ilitolewa kuhusu kufunga ndoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Tulipofika nyumbani, nililalamika vikali: “Waona! Wako tu kama wengine wote—wakibagua mtu yeyote ambaye si wa dini yao.” Velia akaeleza kwa upole: “Lakini si wao wanaosema hivyo, ni Biblia inayosema hivyo.” Nikajibu haraka kwa kupiga ukuta ngumi na kusema: “Umekuwa kama bocona tena!” Kwa hakika, nilikuwa nimefadhaika kwa sababu nilijua alikuwa amesema kweli.
Niliendelea kuhudhuria mikutano na kusoma fasihi za Mashahidi, lakini kusudi langu lilikuwa kujaribu kuwakosoa. Hata nikaanza kutoa maelezo katika mikutano—lakini ili tu kuonyesha watu kwamba sikuwa “Mmexico mjinga.”
Utafutaji Wangu wa Haki Waridhishwa
Kufikia mwaka wa 1971 kazi yangu ya jeshi ilikuwa imetupeleka Arkansas. Niliendelea kuhudhuria mikutano na Velia, ambaye mnamo Desemba 1969 alikuwa amebatizwa katika wonyesho wa wakfu wake kwa Yehova. Sikumpinga tena, lakini sikutaka mtu yeyote anifunze Biblia. Ujuzi wangu kutokana na kusoma fasihi za Biblia ulikuwa umeongezeka sana. Lakini huo ulikuwa tu ujuzi wa akilini—tokeo la tamaa yangu ya kuwa bora katika kitu chochote nilichofanya. Hata hivyo, polepole, kushirikiana na Mashahidi wa Yehova kulianza kuwa na uvutano moyoni mwangu.
Kwa kielelezo, niliona kwamba weusi walikuwa wanashiriki katika kufundisha kwenye mikutano ya kutaniko. Lakini kwanza nilijiambia, ‘Ndiyo, wao wafanya hivyo ndani ya Jumba la Ufalme pekee.’ Lakini tulipohudhuria mkusanyiko katika stediamu kubwa ya besiboli, nilishangaa kuona kwamba hata huko weusi walikuwa na sehemu katika programu. Nikalazimika kukiri kwamba Mashahidi hawana ubaguzi. Wao hufuata haki ya kweli.
Pia nikaja kutambua kwamba Mashahidi wa Yehova wanapendana kikweli. (Yohana 13:34, 35) Na nilipokuwa nafanya kazi pamoja nao kwenye ujenzi wa Jumba la Ufalme lao, ningeweza kuona kwamba walikuwa watu wa kawaida tu. Niliwaona wakichoka, wakifanya makosa, na hata kuambiana maneno yasiyo ya kirafiki mambo yalipoenda vibaya. Badala ya kutenganishwa na ukosefu huo wa ukamilifu, nikaja kuhisi usalama zaidi nikiwa miongoni mwao. Labda nilitambua kwamba nina tumaini japo kasoro zangu nyingi.
Hatimaye Moyo Wangu Ulifikiwa
Nilitambua kwa mara ya kwanza kwamba nilikuwa nasitawisha uhusiano na Yehova wakati ambapo katika 1973, Mnara wa Mlinzi lilipoeleza kwamba kuvuta sigareti ni “unajisi wa mwili” na ni kosa la kutenga na ushirika. (2 Wakorintho 7:1) Wakati huo nilikuwa nikivuta kati ya pakiti moja na pakiti mbili za sigareti kwa siku. Awali nilikuwa nimejaribu mara nyingi kuacha sigareti lakini sikufua dafu. Lakini sasa, kila wakati nilipohisi tamaa ya kuvuta sigareti, ningesali kimyakimya ili Yehova anisaidie kuacha tabia hiyo chafu. Kwa mshangao wa kila mtu, sikuvuta sigareti tena.
Nilipaswa kustaafu jeshi Julai 1, 1975. Nilitambua kwamba ikiwa nilitaka kufanya yale ambayo Biblia inafundisha, ni lazima niweke wakfu maisha yangu kwa Yehova. Sikuwa nimepata kamwe kuwa na funzo la Biblia, kwa hiyo wazee wa kutaniko walishangaa kama nini wakati, mnamo Juni 1975, nilipowaambia kwamba nilitaka kubatizwa mara tu baada ya kazi yangu ya jeshi kwisha. Walieleza kwamba kwanza ni lazima nitimize amri ya Yesu ya kushiriki katika kazi ya kuhubiri. (Mathayo 28:19, 20) Nilifanya hivyo Jumamosi ya kwanza katika Julai. Siku iyo hiyo nilikutana na mzee mmoja na kujibu maswali ya Biblia yanayoulizwa wanaotaka kubatizwa. Majuma matatu baadaye nilibatizwa.
Walipoona nimebatizwa, watoto wetu watatu—Vito, Venelda, na Veronica—wakaanza kufanya maendeleo ya kiroho. Kwa miaka miwili iliyofuata, watoto wakubwa wawili walibatizwa, wakifuatiwa na aliye mdogo zaidi miaka minne baadaye. Nizungumzapo na wanaume wanaojua kweli ya Biblia na hawataki kuifuata, mimi huwaeleza matokeo ya kukosa kuchukua hatua. Nawaambia kwamba ingawa watoto wao hawawezi kuwaeleza, wao hufikiri, ‘Ikiwa kweli si muhimu kwa baba, basi si muhimu kwetu.’
Kufuatia Huduma ya Wakati Wote
Familia yetu yote ikaanza huduma ya wakati wote tukiwa mapainia katika Marshall, Arkansas. Mimi na Velia tulianza katika 1979, na watoto walitufuata katika kazi ya upainia katika miaka iliyofuata kila mmoja wao alipomaliza shule ya sekondari.
Mapema katika miaka ya 1980, tulisikia ripoti kuhusu tamaa ya kupata ujuzi wa Biblia miongoni mwa watu wa Ekuado, Amerika Kusini, nasi tukaweka mradi wa kuhamia huko. Kufikia 1989 watoto wetu walikuwa watu wazima ambao wangeweza kujitunza. Basi, katika mwaka huo tulizuru kifupi Ekuado ili “kuipeleleza nchi.”—Linganisha Hesabu 13:1, 2.
Mnamo Aprili 1990 tulifika Ekuado, makao yetu mapya. Kwa kuwa hatukuwa na fedha za kutosha—kwa sababu tulitegemea malipo ya uzeeni ya kijeshi—tulilazimika kupanga bajeti kwa uangalifu sana. Lakini shangwe za huduma ya wakati wote katika eneo hili lenye matokeo kiroho zimeshinda kwa mbali dhabihu zozote za kifedha tulizofanya. Kwanza, tulihubiri katika jiji la bandari la Manta, ambako kila mmoja wetu aliongoza mafunzo 10 hadi 12 ya Biblia kila juma. Kisha, katika 1992, nilianza kutumikia nikiwa mwangalizi asafiriye, nikiandamana na mke wangu. Sisi huzuru kutaniko tofauti kila juma.
Haki Inapopatikana Kikamili
Nikikumbuka, mimi na Velia twaweza kuona kwamba ukosefu wa haki tuliotendewa tulipokuwa tukikua sasa hutusaidia katika huduma yetu. Sisi huwa waangalifu hasa tusidharau mtu kamwe ambaye huenda ni maskini au asiye na elimu kuliko sisi au ambaye ni wa jamii tofauti na yetu. Pia, twaona kwamba wengi wa ndugu zetu na dada zetu Wakristo huona ukosefu wa haki wa kijamii ulio mbaya zaidi ya ule tuliotendewa. Lakini, hawalalamiki. Wao hukazia macho Ufalme wa Mungu unaokuja, na sisi tumejifunza kufanya hivyo. Tuliacha zamani kujaribu kupata haki katika mfumo huu; lakini badala ya hivyo, twatumia maisha zetu kuelekeza watu kwenye suluhisho la pekee kwa ukosefu wa haki, Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14.
Pia tumejifunza kwamba wale miongoni mwetu ambao wamekuwa wanyetivu sana kwa ukosefu wa haki ni lazima wawe waangalifu wasitazamie haki kamili miongoni mwa watu wa Mungu. Hiyo ni kwa sababu sisi sote hatujakamilika na huelekea kufanya mabaya. (Waroma 7:18-20) Lakini kwa unyoofu twaweza kusema kwamba tumepata ushirika wa kimataifa wenye upendo wa ndugu ambao wanajaribu kufanya yaliyo sawa kwa kadiri wawezavyo. Tunatumaini kwamba tukiwa pamoja na watu wa Mungu kila mahali, tutaingia katika ulimwengu mpya wa Mungu ambamo uadilifu utakuwapo.—2 Petro 3:13.
[Blabu katika ukurasa wa 20]
Nikajibu haraka kwa kupiga ukuta ngumi
[Picha katika ukurasa wa 21]
Nikiwa na Velia, nilipojiunga na jeshi la wanahewa
[Picha katika ukurasa wa 23]
Nikiwa na Velia, 1996