Mashahidi wa Yehova Nchini Urusi
Maoni ya Mwanatheolojia
JIJINI Roma, viongozi wa jumuiya ya Kiyahudi katika karne ya kwanza walisema hivi kuhusu Ukristo: “Kwa habari ya farakano hili yajulikana kwetu kwamba kila mahali huwa lasemwa vibaya.” Viongozi hao walifanya nini? Jambo la kustahili pongezi ni kwamba wao walimwendea mtume Paulo, ambaye wakati huo alikuwa amezuiliwa nyumbani, na kusema: “Twafikiri yafaa kusikia kutoka kwako fikira zako ni nini.” (Matendo 28:22) Wao walimsikiliza Mkristo mwenye ufahamu badala ya kuwasikiliza wale waliosema dhidi ya Ukristo.
Sergei Ivanenko, mwanatheolojia Mrusi aheshimiwaye, alifanya vivyo hivyo. Ingawa aliamini nyingi za ripoti hasi kuhusu Mashahidi wa Yehova ambazo zilikuwa zikisambaa nchini Urusi, aliamua kuulizia ofisi ya tawi ya Mashahidi, ambayo ilikuwa nje tu ya St. Petersburg, ili apate habari. Alikubali mwaliko wa kuzuru huko, aulize maswali, na ajionee mwenyewe Mashahidi.
Bw. Ivanenko alipofika mnamo Oktoba 1996, majengo ambayo ni makao ya washiriki karibu 200 wa wafanyakazi wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Urusi yalikuwa yakikaribia ukamilisho. Kwa siku tatu zilizofuata, alipewa fursa ya kupatazama mahali hapo pa ujenzi, kula milo katika chumba cha mlo, na kuhoji mtu awaye yote ambaye angependa.
Makala ambayo Bw. Ivanenko aliandika kuhusu Mashahidi ilichapishwa katika gazeti lipendwalo la kila juma la Urusi Moscow News la Februari 16-23, 1997. Makala hiyo, yenye kichwa “Je, Tuwaogope Mashahidi wa Yehova?,” pia ilitokea katika chapa ya Kiingereza ya Moscow News, ya Februari 20-26. Kwa kuwa wasomaji wengi wa Amkeni! wanapendezwa sana na utendaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Urusi, kwa idhini, twatokeza hapa sehemu kubwa ya makala hii. Bw. Ivanenko alianza makala hiyo kwa jambo lifuatalo lililoonwa, ambalo lilipigwa chapa kwa maandishi mazito:
“‘Enyi watu wa farakano, ondokeni Urusi!’ ndivyo vilivyosema vibandiko fulani vilivyokuwa vimebebwa na wanachama wa chama cha Zhirinovsky cha LDPR wakiandamana dhidi ya mkutano wa Mashahidi wa Yehova. ‘Ni nini hupendi kuhusu tengenezo hili?’ Nilimwuliza mmojawapo wa wale waliokuwa wakiandamana. Akanipa nakala ya gazeti Megapolis-Express lenye kichwa ‘Kaswende ya Kidini Yaibuka Kamchatka.’ Hilo gazeti lilisema kwamba ili kujaza makasha yao ya pesa, Mashahidi wa Yehova walikuwa makuwadi na kuendesha biashara haramu za umalaya, wakieneza maradhi yanayopitishwa kingono miongoni mwa mabaharia. ‘Je, wewe ni mmoja wa watu waliofanywa hivyo?’ nikamwuliza kwa huruma, ‘Je, waamini habari hii?’ ‘Hiyo si kitu,’ akajibu. ‘Jambo kubwa ni kwamba farakano hili la Kimarekani linaharibu hali ya kiroho na utamaduni wa Urusi, na ni lazima tulikomeshe.’”
Makala aliyoiandika Bw. Ivanenko ilianza kwa maandishi haya: “Imeandikwa na Sergei Ivanenko, mwanatheolojia, na anayewania ufalsafa.”
“Ufuatiaji haki kama huu ni nadra sana kupatikana, ingawa ni kweli kwamba Warusi wengi hawawapendi Mashahidi wa Yehova. Kutaja tu tengenezo hili hutokeza mfululizo wa maneno kuhusu ushupavu wake mbaya, chanzo chake cha Kimarekani, kuhusu imani ya kijinga ya wafuasi wa kawaida kwa viongozi wa tengenezo hilo, na itikadi ya kwamba mwisho wa ulimwengu umefika. Kwa wengi, Mashahidi wa Yehova hutokeza mchanganyiko wa hofu na udadisi.
“Hii ni Dini Gani, na Je, Twapaswa Kuihofu?
“Ili nipate jibu, nilizuru kijiji cha Solnechnoye, katika wilaya ya Kururtnoye, St. Petersburg, ambapo kipo kitovu cha usimamizi cha Mashahidi wa Yehova nchini Urusi.
***
“[Hapa] ni mahali ambapo zamani palikuwa kambi ya wakati wa kiangazi. Kufikia 1992 jengo [la awali] lilikuwa limechakaa sana, na badala ya watoto waliokuwa wakicheza kukawa na makundi ya panya. Yaonekana kwamba ni hali mbaya sana ya eneo hili iliyofanya Mashahidi wa Yehova wapokee ploti ya hekta saba [eka 17] watumie kwa muda usio dhahiri. Walirekebisha upya majengo ya zamani na kuanza kujenga majengo mapya, kutia ndani jengo la usimamizi lenye orofa nne, [Jumba la Ufalme] linalotoshea watu 500, na chumba cha kulia. Mashahidi wa Yehova pia wanapanda nyasi mpya (ambazo ziliagizwa rasmi kutoka Finland) na aina kadhaa za miti iliyo nadra kupatikana. Hiyo kazi inatazamiwa kukamilishwa katika kiangazi hiki kinachokuja. Kazi kubwa ya kitovu cha usimamizi ni kupanga utendaji wa kuhubiri na kusafirisha fasihi kwenye makutaniko ya mahali-mahali ya Mashahidi wa Yehova. Solnechnoye haina vifaa vyake vya uchapishaji, kwa hiyo fasihi za Kirusi huchapishwa Ujerumani, kisha hupelekwa St. Petersburg, na kutoka huko hizo husambazwa kwa maeneo mbalimbali. Watu wapatao 190 hufanya kazi katika kitovu hicho. Wao hufanya kazi kwa kujitolea na ingawa hawapokei mishahara, wao huandaliwa mahitaji yote ya kimsingi, kama vile mahali pa kuishi, chakula, na mavazi.
“Kazi ya kitovu hicho inaongozwa na halmashauri ya wazee 18. Vasily Kalin amekuwa mratibu wa hicho kitovu cha usimamizi tangu 1992. Alizaliwa katika Ivano-Frankovsk. Mnamo 1951, akiwa na umri wa miaka minne, yeye pamoja na wazazi wake walihamishwa Siberia (mwaka wa 1949 na 1951 familia zipatazo 5,000 zilinyanyaswa na wenye mamlaka kwa sababu ya kuwa Mashahidi wa Yehova). Alibatizwa mwaka wa 1965 na kuishi eneo la Irkutsk. Alikuwa mnyapara katika kiwanda cha mbao.
“Mbali na wajitoleaji wa hicho kitovu cha usimamizi kuna wafanyakazi wa ujenzi wenye kujitolea 200 ambao wametoka Urusi, Finland, Sweden na Norway wanaoishi Solnechnoye: Wengi wao walichukua likizo kutoka kwa kazi zao za kawaida. Pia kuna Mashahidi wa Yehova wengi kutoka Ukrainia, Moldova, Ujerumani, Marekani, Finland, Poland na nchi nyinginezo. (Mashahidi wa Yehova hawana ubaguzi wa kijamii. Japo uhakika wa kwamba Wageorgia, Waabkhazian, Waazerbaijan na Waarmenia wanaishi pamoja katika kitovu hicho, hakujapata kuwa na mgogoro wowote kwa miaka minne.)
“Vingi vya vifaa vya ujenzi vilitolewa na nchi za Skandinavia, na vingine vingi vilitolewa bila malipo na waamini wenzao. Nilionyeshwa buldoza ambayo Shahidi wa Yehova wa Sweden aliileta Solnechnoye mwaka wa 1993. Yeye aliitumia muda wote alipokuwa huko, na kabla ya kwenda nyumbani aliwapa ndugu zake katika imani. Wajenzi wanaishi katika mabweni mazuri na nyumba nzuri ndogondogo. Siku yao hufuata ratiba kama hii: saa 1:00 asubuhi—kiamsha kinywa na sala; wao hufanya kazi tokea saa 2:00 asubuhi hadi saa 11:00 jioni kukiwa na kipindi cha saa nzima cha mlo wa mchana. Siku za Jumamosi wao hufanya kazi mpaka wakati wa mlo wa mchana, na Jumapili ni siku ya kupumzika.
“Wao hula vizuri na sikuzote matunda ni sehemu ya mlo. Dini hii haifungi wala kukataza kabisa kula vyakula fulani kamwe. Baada ya kazi, wengi huenda kuoga kwenye bafu za mvuke na kisha kunywa bia moja au kuketi tu kusikiliza muziki. Hakuna walevi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, lakini alkoholi haikatazwi. Waamini hukubaliwa kunywa kwa kiasi divai, brandi, vodka na kadhalika. Lakini, Mashahidi wa Yehova hawavuti sigareti.
***
“Mara tatu kwa juma kuna masomo ya funzo la Biblia, ambayo mara nyingi huhudhuriwa na vijana. Lakini, ni kawaida kupata watu ambao wamekuwa Mashahidi wa Yehova kwa miaka 30 hadi 40. Karibu wote kati ya wenye umri mkubwa wamepata kufungwa gerezani, au kufungwa katika kambi za kazi ngumu na kupelekwa uhamishoni. Baada ya kipindi cha ukandamizi, madaktari, mawakili, wahandisi, walimu, wafanya-biashara, na wanafunzi wengi walijiunga na Mashahidi wa Yehova.
“Makutaniko hujaribu kudumisha hali ya usawa miongoni mwa washiriki wake. Kwa mfano, hata mratibu wa hicho kitovu cha usimamizi huosha vyombo jioni zamu yake ifikapo. Mashahidi wa Yehova hujiita kwa njia isiyo rasmi nao wataongeza pia ‘ndugu’ au ‘dada’ wanapoita mtu kwa jina lake.
“Shahidi wa Yehova avunjapo mafundisho ya Biblia na kukataa kutubu, yeye hupewa adhabu kali zaidi—yeye huondoshwa. Mtu huyo bado aweza kuhudhuria mikutano, lakini yeye hasalimiwi tena na waamini wenzake. Adhabu isiyo kali sana ingekuwa karipio.
***
“Niliwachunguza Mashahidi wa Yehova kwa muda mrefu nikijaribu kuona ni nini kilichowaleta watu tofauti-tofauti sana kwenye tengenezo hili la kidini. Kukiwa na tofauti hizo zote katika nyutu zao, viwango vyao vya elimu na mapendezi yao ya kibinafsi na mambo yasiyopendeza kibinafsi, [Mashahidi wa Yehova hawashiriki ibada na] dini nyinginezo ambazo huridhiana na ulimwengu huu wenye dhambi. Wao hawastarehe katika mahali ambapo ni lazima [watu] wafuate mamlaka bila kutumia akili, ambapo pana mafumbo, ambapo watu hugawanyika katika tabaka lenye kuongoza na la wengi wenye kuongozwa walio watiifu.
“Mashahidi wa Yehova hutofautishwa na itikadi yao thabiti ya kuishi kulingana na Biblia. Wao hujaribu kuthibitisha kila watendalo kwa kanuni hii au ile ya Biblia, au kwa kutaja fungu fulani katika Agano la Kale au Jipya. Mashahidi wa Yehova huamini kwamba Biblia na ni Biblia pekee ambayo ina majibu ya maswali yote. Kwa Mashahidi wa Yehova, Biblia ni katiba, kanuni ya kuongoza watu na wonyesho bora sana wa kweli.
“Kwa sababu hii Mashahidi wa Yehova wamejulikana kotekote ulimwenguni kuwa watu wenye kutii sheria sana na hasa kwa sababu ya mtazamo wao wa kulipa kodi bila kukwepa. Ofisi ya kukagua kodi mara nyingi huwakagua nayo hushangaa kwamba kila wakati hawavunji sheria yoyote ile. Bila shaka, Mashahidi wa Yehova wanaweza, kama ilivyo na wengine wengi, kujaribu kutafuta sababu ya kutolipa kodi, lakini Biblia yasema kwamba ni lazima mtu afuatie haki katika kulipa kodi, na kwa Mashahidi wa Yehova hiyo ndiyo mamlaka kuu zaidi.
“Hata hivyo, mtazamo wao usioridhiana juu ya Biblia mara nyingi hutokeza mizozo mikubwa baina ya Mashahidi wa Yehova na serikali. Msimamo wao wa kutojihusisha kabisa na siasa ni kisababishi kikuu cha mzozo, nao hudhihirika katika kukataa kwao kutumikia jeshini.
“Mashahidi wa Yehova hufasiri kihalisi maneno ya Yesu kuhusu jinsi ambavyo wanafunzi wake na ufalme wake si sehemu ya ulimwengu huu, na kwa sababu hii wao hukataa kushiriki katika siasa na vita, haidhuru vita hiyo iko wapi na inapiganwa kwa sababu gani. Kwa sababu Mashahidi wa Yehova walikataa kusema ‘Heil Hitler’ na kutumikia katika jeshi la Hitler, maelfu mengi ya waamini walipelekwa katika kambi za mateso za Nazi, na maelfu walikufa. Kila Shahidi wa Yehova Mjerumani ambaye alikufa kwa sababu ya kukataa kushiriki uchokozi dhidi ya Muungano wa Sovieti, huonwa na Warusi kuwa mtu ambaye alitenda tendo la maadili sana. Lakini, kwa wakati uo huo, Warusi wengi hawana mwelekeo wa kusikitikia wale Mashahidi wa Yehova [Warusi] ambao walifishwa kwa kukataa kuchukua silaha na kushiriki katika Vita ya Ulimwengu ya Pili, au ambao walihukumiwa kwa kukataa kutumikia katika jeshi katika nyakati za amani. Lakini katika hali hizo zote Mashahidi wa Yehova walikuwa wakitenda kulingana na itikadi zao za kidini wala si kulingana na masadikisho ya kisiasa.
“Muda usio mrefu tatizo kama hilo lilitokea nchini Japani, ambako wanafunzi fulani ambao walikuwa Mashahidi wa Yehova walikataa kujifunza mbinu za kupigana nao walijihatarisha kufukuzwa kutoka chuo kikuu. Mnamo 1996 Mahakama Kuu ya Japani ilitoa uamuzi ambao uliunga mkono haki za wanafunzi hao na kuwaruhusu kusoma masomo ya badala.
***
“Ni nini kuhusu Mashahidi wa Yehova ambacho hushangaza watu wenye kufikiri sasa? Jambo la kwanza ni kuhubiri kwao daima kwamba mwisho wa ulimwengu u karibu (wao hufanya kazi ya mishonari barabarani na nyumba hadi nyumba). Karibuni wazee wamewashauri wahubiri wasitilie mkazo sana ‘mwisho wa ulimwengu’ na hali mbaya itakayowapata watenda-dhambi, bali waeleze wasikilizaji kwamba Yehova anaandaa fursa ya wao kuweza kupata ‘uhai udumuo milele katika paradiso duniani.’
“Jambo jingine ambalo hukasirisha ni mtazamo hasi wa Mashahidi wa Yehova dhidi ya kuchangamana na dini nyinginezo, na kukataa kwao muungano wa kidini. Wao huamini kwamba ulimwengu wa Kikristo umemsaliti Mungu na Biblia, na kwamba dini nyinginezo zote zimekosea kabisa. Mashahidi wa Yehova hulinganisha dini hizi na ‘kahaba wa Babiloni,’ nao hudumisha kwamba dini hizo zitaharibiwa pia. Toleo la majuzi la ‘Amkeni!’ lasema kwamba mwisho wa dini nyingi u karibu, na kwamba dini moja tu itakayobaki ni ile ihubiriwayo na Mashahidi wa Yehova.
“Inatukia kwamba Mashahidi wa Yehova hukiri haki ya kila mtu ya kuwa na uhuru wa dhamiri.
***
“Nchi kadhaa tayari zimeonyesha hangaiko kuhusu kama mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni tisho kwa jumuiya au la. Mahakama Kuu ya jimbo la Connecticut, Marekani (1979) na New South Wales, Australia (1972), Mahakama ya Mkoa ya British Columbia, Kanada (1986) na mahakama nyinginezo zimetangaza kwamba hakuna uthibitisho kwamba Mashahidi wa Yehova ni tisho la kijamii, au kwamba wao huhatarisha afya za watu au hali zao za kihisia-moyo. Mahakama ya Haki za Kibinadamu ya Ulaya (1993) ilitetea haki ya Mashahidi wa Yehova ya uhuru wa kidini, ambayo ilikuwa imewekewa mipaka nchini Ugiriki na Austria. Leo Mashahidi wa Yehova hunyanyaswa katika nchi 25 . . .
“Mashahidi wa Yehova waweza kuonwa kuwa vielelezo kwa raia wenzao kwa ajili ya ujitoaji wao kwa kweli ya Biblia na utayari wao wa kutetea itikadi zao bila ubinafsi. Lakini swali lazuka: Je, jumuiya yetu iko tayari kuandaa haki za kikatiba za uhuru wa dhamiri kwa matengenezo ambayo husisitiza uelewevu wao wa Biblia kwa pande zote za maisha kwa njia shupavu kama hiyo na isiyo ya kuridhiana?”
Katika sentensi hii ya mwisho, Bw. Ivanenko alizusha swali muhimu. Katika karne ya kwanza, mtume Paulo, aliyechaguliwa moja kwa moja na Kristo ili atumikie akiwa mwakilishi wake, alikuwa ‘katika vifungo vya gereza’ isivyo haki. Hivyo, Paulo aliandikia waamini wenzake kuhusu jitihada zake za “kutetea na kuthibitisha kisheria habari njema.”—Wafilipi 1:7; Matendo 9:3-16.
Leo, Mashahidi wa Yehova huwakaribisha wote wachunguze utendaji wao kwa ukaribu, kama alivyofanya Bw. Ivanenko. Tuna uhakika kwamba watu wakifanya hivyo, wao watapata kwamba ripoti mbaya kuhusu Mashahidi si za kweli, kama vile ambavyo ripoti kuhusu Wakristo wa mapema hazikuwa za kweli pia. Kwa kutokeza, Mashahidi hutii “amri mpya” ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake: “Mpendane; kama vile nimewapenda nyinyi.”—Yohana 13:34, 35.
[Sanduku katika ukurasa wa 23]
Faili ya MN
(Habari ifuatayo ambayo ilitoka katika faili za gazeti Moscow News ilichapwa pamoja na makala hii ya Sergei Ivanenko.)
“Mashahidi wa Yehova Warusi ni sehemu ya tengenezo la Kikristo la ulimwenguni pote linalotenda katika nchi 233 na lenye washiriki milioni 5.4. Mashahidi wa Yehova hufuata mwongozo wa kiroho wa Baraza Linaloongoza lililoko Brooklyn, New York. Tengenezo la kisasa la Mashahidi wa Yehova lilitokana na darasa la funzo la Biblia lililofanyizwa mnamo 1870 na Charles Taze Russell kule Pittsburgh, Pennsylvania. Tengenezo hilo lilikuja Urusi mnamo 1887. Mmojawapo wa Mashahidi wa Yehova wa kwanza Warusi, Semyon Kozlitsky, alipelekwa uhamishoni kutoka Moscow hadi Siberia mwaka wa 1891. Japo mnyanyaso ambao tengenezo hilo lilivumilia, mwaka wa 1956 kulikuwa na Mashahidi wa Yehova 17,000 katika Muungano wa Sovieti. Mashahidi wa Yehova hawakutambuliwa rasmi nchini Urusi hadi Machi 1991, baada ya kupitishwa kwa sheria ‘Juu ya Uhuru wa Dini.’ Leo, kuna zaidi ya jumuiya 500 zenye washiriki wapatao 70,000 walio watendaji nchini Urusi. Tengenezo hilo hugawanya nakala za ‘Mnara wa Mlinzi’ (ambalo huchapishwa katika lugha 125, na kugawanywa kwa nakala milioni 20) na ‘Amkeni!’ (katika lugha 81, na kugawanywa kwa nakala milioni 18).”
[Picha katika ukurasa wa 23]
Sehemu ya jengo la ofisi ya tawi nchini Urusi
[Picha katika ukurasa wa 24]
Jumba la Ufalme ambako familia ya ofisi ya tawi nchini Urusi hukutanikia kwa ajili ya funzo la Biblia
[Picha katika ukurasa wa 25]
Familia za Mashahidi hujifunza na kufurahia tafrija pamoja
[Picha katika ukurasa wa 26]
Wao hushiriki ujuzi wa Biblia pamoja na wengine