Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 11/22 kur. 26-27
  • Baraza la Kisheria la Urusi Latetea

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Baraza la Kisheria la Urusi Latetea
  • Amkeni!—1998
  • Habari Zinazolingana
  • Mashahidi wa Yehova Nchini Urusi
    Amkeni!—1997
  • Dini Zitapatwa na Nini?
    Amkeni!—2001
  • Kutetea Imani Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Je, Mashahidi wa Yehova ni Wakristo wa kweli?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 11/22 kur. 26-27

Baraza la Kisheria la Urusi Latetea

Mashahidi wa Yehova

MASHAHIDI WA YEHOVA hufurahia ripoti zenye msingi mzuri kuwahusu zinazoripotiwa kwenye vyombo vya habari. Zaidi ya hayo, Mashahidi wa Yehova wako tayari kutoa habari za kweli kujihusu na kuhusu itikadi zao na utendaji wao wa kidini. Lakini, makala zisizosema ukweli au zenye kuwachongea zinapoandikwa kuwahusu, nyakati nyingine Mashahidi huomba msaada wa wenye mamlaka wa serikali ili kutetea haki zao za kidini na za kiraia. Chukua mfano mmoja wa majuzi.

Mnamo Agosti 1, 1997, nyongeza ya gazeti mashuhuri la Urusi ya eneo la St. Petersburg, Komsomolskaya pravda, ilichapisha makala moja yenye kupotosha kabisa juu ya Mashahidi wa Yehova. Katika makala hiyo, yenye kichwa “Farakano la Petersburg. Kutakuwa na Jiji-Hekalu Hapa,” mwandikaji, Oleg Zasorin, alidai kwamba Mashahidi wa Yehova ni wenye madhara kwa itikadi zao na kwamba utendaji wao wakiuka Katiba ya Urusi. Mashambulizi yake hasa yalikazia kupotoshwa kwa itikadi za Mashahidi zinazotegemea Biblia, kwa mfano, utiwaji-damu mishipani na mahusiano ya familia. Isitoshe, makala hiyo iliwaita Mashahidi wa Yehova “farakano,” ikidai kwamba wao, kwa maoni ya watu fulani, “ni hatari kuliko mafarakano yote.”

Kituo cha Usimamizi cha Shirika la Kidini la Eneo hilo la Mashahidi wa Yehova nchini Urusi kiliomba msaada wa baraza la sheria la Presidential Judicial Chamber for Media Disputes la Muungano wa Urusi lipitie taarifa zilizokuwa katika makala hiyo, ambazo Mashahidi wa Yehova waliziona kuwa zenye ulaghai. Kwenye mkutano wa Baraza la Sheria mnamo Februari 12, 1998, wawakilishi wa Mashahidi wa Yehova walikuwapo wakajibu maswali mengi yaliyoulizwa na washiriki wa baraza hilo, na vilevile waandishi wa habari na mawakili. Ili kuthibitisha mambo ambayo kwa hakika Mashahidi wa Yehova huamini na kufundisha, washiriki wa Baraza la Sheria walichunguza kwa makini vichapo vya Mashahidi wa Yehova, na hasa kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia.

V. V. Borshchyov, mshiriki wa Baraza la Muungano wa Urusi, alisema kwamba wazo la “mafarakano” hasa humaanisha mambo yasiyofaa. Bw. Borshchyov alisema: “[Kuwa huru hivyo na kubandika wengine majina ni hatari sana. Kwa Baraza la Sheria kukubali ombi la Mashahidi wa Yehova lisikilizwe kwamaanisha kwamba hili ni jambo muhimu. Ni lazima maneno na matukano tele dhidi ya shirika la kidini lililosajiliwa rasmi yakomeshwe.”

Baada ya kusikia uthibitisho wote, Baraza la Sheria lilikata kauli ya kwamba makala hiyo iliyotokea katika Komsomolskaya pravda si halali na haifuati maadili; pia lilipata kwamba makala hiyo ilijaa makosa na haikuwa na msingi. “Mwandishi hataji mambo yoyote hususa . . . Mwandishi wa makala hiyo alieneza porojo eti ni habari zenye kutegemeka, akikiuka haki za uandishi wa habari,” likasema Baraza la Sheria. Tofauti na ripoti ya makala hiyo katika gazeti la habari hilo, Baraza la Sheria lilipata kwamba Mashahidi wa Yehova ni wenye kutii sheria na kwamba wao hufundisha washiriki wao waishi kwa amani na familia zao na marafiki wao ambao si wa dini yao.

Muda wa saa moja baada ya ushuhuda wa mwisho kusikizwa, Baraza la Sheria lilitoa uamuzi wake:

“1. Kutambua kwamba kuchapishwa kwa makala ‘Farakano la Petersburg. Kutakuwako Jiji-Hekalu Hapa’ ni ukiukaji wa matakwa ya Fungu la 4, 49, na 51 la Sheria ya Muungano wa Urusi ‘Kuhusu Vyombo vya Habari.’

“2. Kupendekeza kwamba Kamati ya Serikali ya Muungano wa Urusi Inayosimamia Mambo Yanayochapishwa ipitie suala la kuonya kamati ya uhariri ya gazeti Komsomolskaya pravda.

“3. Kumwadhibu mwandishi wa habari O. Zasorin.

“4. Kupendekeza kwamba kamati ya uhariri ya gazeti Komsomolskaya pravda iombe radhi kwa kuchapisha habari zisizo na msingi ambazo zinaharibu sifa ya shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova.”

Uamuzi huo wa Baraza la Sheria wakubaliana na mikataa iliyofikiwa na msomi wa mambo ya kidini na mgombea-ufalsafa Sergei Ivanenko. Baada ya kuchunguza kwa makini itikadi za Mashahidi wa Yehova na kushirikiana nao, Bw. Ivanenko, ambaye si mmoja wa Mashahidi wa Yehova, aliandika makala iliyotokea kwenye toleo la Februari 20-26, 1997, la Moscow News.a Bw. Ivanenko alimalizia: “Mashahidi wa Yehova [wamejulikana] kwa itikadi yao thabiti ya kuishi kulingana na Biblia. . . . Kwa Mashahidi wa Yehova, Biblia ni katiba, kanuni ya kuongoza watu na wonyesho bora sana wa kweli. . . . Mashahidi wa Yehova waweza kuonwa kuwa vielelezo kwa raia wenzao kwa ajili ya ujitoaji wao kwa kweli ya Biblia na utayari wao wa kutetea itikadi zao bila ubinafsi.”

Uamuzi wa Baraza la Sheria na maelezo ya Bw. Ivanenko yathibitisha tena kwamba dini ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova si tisho kwa jumuiya, lakini badala yake, inanufaisha watu wote wenye mioyo minyofu. Mashahidi wa Yehova huwa ‘tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hudai kwao sababu ya tumaini lililo katika wao, lakini wakifanya hivyo kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.’—1 Petro 3:15.

[Maelezo ya Chini]

a Sehemu kubwa ya makala ya Bw. Ivanenko yenye kichwa “Je, Tuwaogope Mashahidi wa Yehova?” ilichapishwa tena, baada ya kupokea idhini, katika toleo la Amkeni! la Agosti 22, 1997, ukurasa wa 22-27.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki