Paradiso Isiyo na Taabu—Karibuni Itakuwa Halisi
“UTAKUWA pamoja na mimi katika Paradiso.” Maneno hayo yalimtumainisha kama nini huyo mtu aliyekuwa na historia ya uhalifu! La, si kwamba alihisi angeponea helo yenye kuwaka moto na kwenda mbinguni wakati afapo. Badala ya hivyo, huyo mwizi aliyekuwa kando ya Yesu alifarijika kutokana na tumaini la kwamba angefufuliwa kwenye uhai wakati ambapo Paradiso ingerudishwa katika sayari hii. Tafadhali, ona ni nani aliyeitoa taarifa hiyo yenye kutokeza juu ya Paradiso—Mwana wa Mungu mwenyewe, Yesu Kristo.—Luka 23:43.
Ni nini lililozusha ahadi ya Kristo ya Paradiso? Yule mwizi alikuwa ameomba: “Nikumbuke mimi uingiapo katika ufalme wako.” (Luka 23:42) Ufalme huu ni nini, na kuna uhusiano gani kati yake na paradiso ya kidunia? Na huo unahakikishaje kwamba hiyo Paradiso haitakuwa na taabu?
Nguvu Itakayoleta Paradiso
Utakubali kwamba paradiso ya kweli inaweza tu kuja duniani wakati ambapo taabu zote za siku hizi zimetoweka. Kufikia wakati huu jitihada za wanadamu za kuondoa taabu zimeambulia patupu, kama ambavyo historia yashuhudia vizuri. Nabii Mwebrania Yeremia alikiri hivi: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Basi, ni nani awezaye kuondoa kabisa taabu zote za siku hizi?
Halihewa Zenye Kupita Kiasi na Uchafuzi. Dhoruba kali ya upepo katika Bahari ya Galilaya ilipokuwa ikipeleka mawimbi makubwa yenye uwezo wa kuvunja meli, mabaharia walimwamsha mwandamani wao safarini kutoka usingizini. Naye akaiambia tu bahari: “Usu! Nyamaa!” Simulizi la Gospeli la Marko laeleza lililotukia: “Upepo ukapunguka, kukawa shwari kubwa.” (Marko 4:39) Mwandamani huyo safarini hakuwa mwingine ila Yesu. Yeye alikuwa na nguvu za kudhibiti halihewa.
Ni Yesu uyo huyo aliyetabiri kupitia mtume Yohana kwamba wakati ungekuja ambapo ‘Mungu angewaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.’ (Ufunuo 1:1; 11:18) Hili si jambo lisilowezekana kwa Yule ambaye aliondoa ulimwengu mzima wa watu wasiomcha Mungu katika Furiko la siku ya Noa.—2 Petro 3:5, 6.
Uhalifu na Ujeuri. Biblia yaahidi: “Watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao BWANA ndio watakaoirithi nchi. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:9, 11) Tena, ni Mungu, Yehova, aahidiye kuondoa uhalifu na ujeuri wote, akihifadhi Paradiso kwa wenye upole.
Umaskini na Njaa. Ukosefu wa haki wa siku hizi huzifanya serikali katika eneo moja la ulimwengu kurundika “milima” ya vyakula vya ziada na kwa wakati uo huo nchi zilizo maskini ziking’ang’ana na umaskini. Mashirika ya kutoa kitulizo, yakiungwa mkono na watu wenye kuhangaika ulimwenguni pote, hujaribu kuandaa mahitaji ya msingi lakini mara nyingi wao hushindwa wakati mipango ya ugawanyaji inapotibuka kwa sababu ya ukosefu wa kudumisha sheria na utengamano. Tofautisha hali hiyo na yale yaliyorekodiwa na nabii Isaya: “Katika mlima huu BWANA wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, karamu ya vinono vilivyojaa mafuta, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, iliyochujwa sana.” (Isaya 25:6) Je, hiyo haionyeshi kwamba njaa kuu na njaa haitakuwapo tena? Bila shaka.
Vita. Majaribio ya kutawala tufe hili kupitia mamlaka ya mataifa yote hayakufua dafu. Ule Ushirika wa Mataifa ulioanzishwa mwaka wa 1920, ulishindwa kuzuia kuzuka kwa Vita ya Ulimwengu ya Pili nao ukaanguka pu! Umoja wa Mataifa, ambao mara nyingi umesifiwa kuwa tumaini bora zaidi la kupata amani, hung’ang’ana kuamua pande zenye kupigana katika maeneo ya mapambano. Japo jitihada zake za kutafuta amani ambazo zimetangazwa sana, vita zimejaa tele, ziwe ni za wenyewe kwa wenyewe, za kikabila, au za kijumuiya. Serikali ya Ufalme wa Mungu yaahidi kuondoa makundi yenye kupigana siku hizi na kuelimisha raia zake kufuatia njia za amani.—Isaya 2:2-4; Danieli 2:44.
Mvunjiko wa Familia na wa Maadili. Kuvunjika kwa familia kumeenea. Uhalifu wa watoto umejaa. Ukosefu wa maadili umesambaa katika matabaka yote ya jamii ya kibinadamu. Lakini, viwango vya Mungu vimedumu bila kubadilishwa tangu mwanzo. Yesu alitoa ushuhuda kwamba “mtu ataacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja . . . Kwa hiyo, kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.” (Mathayo 19:5, 6) Yehova Mungu akaamuru zaidi: “Heshimu baba yako na mama yako . . . ili ipate kuwa vema kwako nawe upate kudumu muda mrefu juu ya dunia.” (Waefeso 6:2, 3) Viwango kama hivyo vitaenea katika dunia itakayokuwa chini ya Ufalme wa Mungu.
Ugonjwa na Kifo. “BWANA . . . ndiye atakayetuokoa,” akaahidi nabii Isaya, “wala hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:22, 24) “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” akakiri mtume Mkristo Paulo, “lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uhai udumuo milele kwa njia ya Kristo Yesu.”—Waroma 6:23.
Yehova Mungu ataondoa taabu hizi zote kupitia serikali yake ya kimbingu iliyo mikononi mwa Mwana wake, Kristo Yesu. Lakini, huenda ukasema, ‘Ufafanuzi huu ni kama ndoto tu ya Utopia. Kwa hakika ungefurahisha kama ungekuwa hivyo, lakini je, ndivyo utakavyokuwa?’
Uhalisi wa Wakati Huu
Kwa watu wengi, uwezekano wa kuishi katika paradiso isiyo na taabu hapahapa duniani waonekana kuwa tazamio lisilowezekana. Ikiwa ndivyo unavyohisi, chunguza ithibati inayothibitisha kwamba kwa kweli hili litatukia.
Mashahidi wa Yehova ni jumuiya ya kimataifa ya siku hizi yenye zaidi ya watu milioni tano ambao tayari kwa kadiri fulani wana mazingira yasiyo na taabu katika makutaniko yao 82,000 ambayo yameenea kotekote katika nchi 233. Unaweza kuzuru wowote wa mikusanyiko yao, mikubwa kwa midogo, na utapata nini?
(1) Mazingira Safi na Yenye Kupendeza. Akieleza juu ya mkusanyiko mmoja wa Mashahidi wa Yehova kule Norwich, Uingereza, meneja wa stediamu ya mchezo wa mpira wa mguu alisema: “Mazingira yenye amani katika hizo siku nne . . . yanavutia sana. Mna utulivu wa binafsi ambao hutofautiana sana na ule wa siku nyinginezo zozote nne katika ulimwengu wa biashara wenye mkazo na maisha ya kila siku yanayotuzingira. Kwa kweli Mashahidi wana jambo fulani ambalo ni tofauti na lililo gumu kueleza.”
Mshauri mmoja wa mazoezi ya mambo ya ujenzi ambaye alizuru ofisi za London za Mashahidi wa Yehova alisema: “Nilivutiwa sana na yale niliyoona na kusikia nami nilishangaa sana kwa mazingira yenye amani kabisa na utulivu ambazo ziko si katika majengo yenu tu bali pia miongoni mwa [wanaume na wanawake]. Nahisi kwamba njia yenu ya maisha na furaha ina mengi ya kufundisha ulimwengu huu wote ulio na taabu.”
(2) Usalama na Amani. Mwandikaji wa makala za gazeti Journal de Montréal katika Kanada aliandika: “Mimi si Shahidi. Lakini mimi nimeshuhudia jambo la kwamba Mashahidi hushuhudia ubora na mwenendo ufaao. . . . Ikiwa ni wao pekee wangekuwa ulimwenguni, hatungehitaji kuifunga milango yetu usiku na kuweka king’ora cha kuzuia wezi.”
(3) Uaminifu-Mshikamanifu kwa serikali ya Ufalme wa Mungu hutambulisha Mashahidi. Msimamo wao wa kutokuwamo huwaudhi wengine, ingawa haipasi kuwa hivyo. Kutokuwamo kwao katika mipango ya siku hizi ya kisiasa iliyo dhaifu hakutokani na kukataa kwao kutaka kuboresha jamii. Badala ya hivyo, wao hujaribu kutenda kwa njia ambayo hupendeza yule ambaye anatawala kupitia serikali ya kimbingu, yaani, Muumba wa dunia, Yehova Mungu.
Itikadi za Mashahidi, zikitegemea kabisa Neno la Mungu, Biblia, huwazuia wasiangukie mtego wa kuwa farakano au madhehebu. Wao hupendezwa kwa fadhili na watu wengine wote, hata wawe wa dini gani. La, wao hawajaribu kuwalazimisha watu hao wabadili maoni yao. Wao hujaribu kumwiga Kiongozi wao, Kristo Yesu, kwa kutoa uthibitisho wa Kimaandiko juu ya Paradiso isiyo na taabu ambayo itaanzishwa karibuni hapa duniani.—Mathayo 28:19, 20; 1 Petro 2:21.
(4) Afya ya Kiroho na Furaha. Kwa uhalisi, Mashahidi wa Yehova hawadai kuwa hawana taabu kabisa wakati huu. Hili haliwezekani miongoni mwa watu ambao wamerithi dhambi kutoka kwa Adamu. Lakini kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu, wao hujitahidi kusitawisha sifa za binafsi kama vile “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.” (Wagalatia 5:22, 23) Ni ibada yao kwa Yehova kupitia Kristo Yesu ambayo huwaunganisha na kudumisha matumaini yao.
Twatumaini kwamba kuzuru mahali pa kwenu ambapo Mashahidi hukutania kutakusadikisha kwamba Mungu atageuza dunia kuwa paradiso halisi.
Taabu za siku hizi zitakoma. Hata kutokamilika kunakoendelea kutapotea polepole wakati manufaa za dhabihu ya fidia ya Kristo zinapotumiwa kwa wanadamu watiifu. Ndiyo, unaweza kupata afya kamili na furaha.
Matayarisho sahili yatakusaidia kufurahia tazamio kama hilo. Omba Mashahidi wakupe nakala yako binafsi ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele.a Ukiwa nacho, kwa muda mfupi unaweza kujifunza jambo ambalo Mungu anataka ufanye ili wewe pia uweze kufurahia milele maisha katika paradiso isiyo na taabu.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Blabu katika ukurasa wa 10]
Itikadi za Mashahidi, zikitegemea kabisa Biblia, huwazuia wasiwe farakano au madhehebu
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Msingi unawekwa sasa kwa ajili ya paradiso isiyo na taabu
Karibuni paradiso halisi itakuwako duniani pote