Magonjwa ya Kuambukiza—Je, Ni Ishara ya Siku za Mwisho?
JE, MAGONJWA ya kuambukiza ya siku yetu yadokeza kuwa mwisho wa ulimwengu u karibu? Kabla ya kujibu swali hilo, ebu tufikirie kwa uangalifu ni nini kinachomaanishwa na msemo “mwisho wa ulimwengu.”
Watu wengi huamini kuwa mwisho wa ulimwengu humaanisha kwamba Mungu ataharibu dunia na uhai wote uliomo ndani yake. Hata hivyo, Neno la Mungu husema kuwa “aliiumba [dunia] ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Kusudi lake ni kuijaza sayari na watu wenye afya na furaha, wanaotaka kufuata viwango vyake vya uadilifu. Kwa hiyo, mwisho wa ulimwengu haumaanishi mwisho wa dunia na wakazi wake wote. Badala ya hivyo, wamaanisha mwisho wa mfumo wa sasa na wa waliopo ndani yake wanaokataa kufanya mapenzi ya Mungu.
Hili lilionyeshwa na mtume Petro, aliyeandika hivi: “Ulimwengu wa wakati [wa Noa] ulipatwa na uangamizo ulipogharikishwa kwa maji.” Ulimwengu ulipoharibiwa wakati wa Noa, ni watu wabaya walioangamia. Dunia ilibaki na ndivyo na Noa mwadilifu na familia yake. Kama Petro aendeleavyo kusema, Mungu atachukua hatua wakati ujao kuleta “uangamizo wa watu wasiomwogopa Mungu.”—2 Petro 3:6, 7.
Maandishi mengine ya Biblia hutegemeza kwa upatano maoni haya. Kwa kielelezo, Mithali 2:21, 22 lataarifu: “Wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”—Ona pia Zaburi 37:9-11.
Magonjwa ya Kuambukiza na Mwisho wa Ulimwengu
Lakini hili litatukia lini? Wanne kati ya mitume wa Yesu walimwuliza swali hilo. Waliuliza: “Ni wakati gani mambo haya yatakuwa, nayo itakuwa ni nini ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo [au, kama tafsiri nyingine za Biblia zisemavyo, “mwisho wa ulimwengu”]?” Yesu akajibu: “Taifa litainuka dhidi ya taifa na ufalme dhidi ya ufalme, na kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya dunia mahali pamoja baada ya pengine.” (Mathayo 24:3, 7) Katika simulizi linalofanana na hilo kwenye Luka 21:10, 11, Yesu aliongezea: “Kutakuwa . . . katika mahali pamoja baada ya pengine magonjwa ya kuambukiza . . . , na kutakuwa na mambo ya kuonwa yenye kutia hofu na kutoka mbinguni ishara zilizo kubwa.”
Ona kwamba Yesu hakusema kuwa magonjwa ya kuambukiza peke yake ndiyo yangeonyesha kuwa mwisho u karibu. Badala ya hivyo, aliorodhesha pia vita, matetemeko ya dunia, na upungufu wa chakula. Katika unabii wake upatikanao katika Mathayo 24 na 25, Marko 13, na Luka 21, Yesu alitabiri kuwa mambo mengine mengi pia yangetokea. Hayo yote yangetukia pamoja kabla Mungu hajachukua hatua ya kuleta mwisho wa uovu duniani. Kuna uthibitisho wenye nguvu kuwa sasa tunaishi katika kipindi hicho.
Paradiso Itakayokuja
Wakati ujao hautaleta maangamizo ya jamii ya binadamu, ama kwa magonjwa ya kuambukiza ama kwa mkono wa Mungu. Yehova Mungu aahidi kufanya upya dunia hii iwe paradiso. (Luka 23:43) Kati ya mambo mengine, atamaliza maradhi yanayowataabisha wanadamu.
Tunahakikishiwa hili tunapofikiria huduma ya Yesu Kristo, ambaye alidhihirisha sifa za Baba yake kikamilifu. Akiwezeshwa na Baba yake wa kimbingu, Yesu aliwaponya waliokuwa vilema, walioharibika viungo, walio vipofu, au mabubu. (Mathayo 15:30, 31) Pia aliwaponya wenye ukoma. (Luka 17:12-14) Alimponya mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu, mtu mwenye mkono ulionyauka, na mtu mwenye ugonjwa wa chovya. (Marko 3:3-5; 5:25-29; Luka 14:2-4) Alirudisha afya ya watu “wenye kifafa na watu waliopooza.” (Mathayo 4:24) Katika pindi tatu hata alifufua wafu!—Luka 7:11-15; 8:49-56; Yohana 11:38-44.
Maponyo haya ya kimuujiza hutoa uhakika wa ahadi ya Mungu kwamba wakati ujao anaofanyiza, “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Magonjwa ya kuambukiza hayatawanyang’anya watu afya na uhai wao tena kamwe. Twaweza kuwa na shukrani iliyoje kwa sababu Muumba wetu mwenye upendo ana uwezo na nia ya kuondoa kabisa ugonjwa na maradhi, milele!—Ufunuo 21:3, 4.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Yesu aliwezeshwa na Mungu kuwaponya wagonjwa
[Picha katika ukurasa wa 10]
Katika Paradiso ya kidunia ijayo, Yehova atafuta kabisa ugonjwa na maradhi