Ni Nini Kingekuwa Bora Zaidi kwa Mtoto?
KUTALIKI au kutotaliki? Hili ni swali kuu katika akili za watu wengi waliooana wasio na furaha. Miaka mingi iliyopita talaka ilichukiwa, na mara nyingi ilishutumiwa, kwa sababu za kiadili na kidini. Na kwa kawaida wazazi wowote waliooana wasio na furaha walikaa pamoja kwa ajili ya watoto wao. Hata hivyo, katika nyakati za karibuni viwango vya ulimwengu huu vimebadilika sana. Leo, talaka yakubalika kwa wengi.
Lakini ijapokuwa talaka yakubalika, idadi yenye kuongezeka ya wazazi, mahakimu, wanasayansi wa kijamii, na wengine, wanaeleza hangaikio lao kuhusu matokeo mabaya ya talaka kwa watoto. Sasa maoni zaidi ya hadhari yanasikika. Uthibitisho wenye kuongezeka waonyesha kuwa talaka yaweza kuwa na matokeo yenye kuangamiza kabisa kwa mtoto. Wazazi wanasihiwa kufikiria matokeo ya talaka kwao wenyewe na kwa watoto wao. Mwanasoshiolojia Sara McLanahan, wa Chuo Kikuu cha Princeton, ataarifu kwamba “kati ya thuluthi mbili na robo tatu za familia zinazotaliki labda zapaswa kulipatia wakati zaidi na kulifikiria zaidi ikiwa wanafanya jambo lililo sawa.”
Uchunguzi wa hivi karibuni waonyesha kuwa watoto wa talaka wako katika hatari kubwa zaidi ya kupata mimba wakiwa matineja, kukataa shule, kushuka moyo, kutaliki katika ndoa zao wenyewe, na kuwa wapokeaji wa msaada. Katika nchi za Magharibi, mtoto 1 kati ya 6 huathiriwa na talaka. Mwanahistoria Mary Ann Mason, katika kitabu chake kuhusu malezi ya mtoto katika Marekani, aonelea hivi: “Mtoto aliyezaliwa katika 1990 alikuwa na karibu nafasi ya asilimia 50 ya kuwa katika mamlaka ya mahakama katika kesi inayohusu mahali mtoto huyo atakapoishi na ataishi na nani.”
Kwa kusikitisha, wakati wote uhasama hauishii na talaka, kwani wazazi waweza kuendelea kupigana katika mahakama kuhusu malezi ya watoto na haki za kutumia wakati nao, wakiwaongezea watoto wao mkazo. Makabiliano haya ya kihisia-moyo yenye upinzani katika mazingira ya chumba cha mahakama hujaribu uaminifu-mshikamanifu wa watoto kwa wazazi wao na mara nyingi huwafanya wajihisi kuwa wasio na nguvu na wenye hofu.
Mshauri wa familia alisema: “Talaka haiwaokoi watoto. Wakati mwingine huwaokoa watu wazima.” Uhalisi ni kwamba kwa kutalikana, wazazi waweza kutatua matatizo yao wenyewe, lakini kwa wakati uleule, wanaweza kusababisha hasara kwa watoto wao, ambao waweza kutumia muda uliobaki wa maisha yao wakijaribu kulipia hasara hiyo.
Machaguo ya Malezi ya Mtoto
Katika uhasama na mkazo wa kihisia-moyo katika talaka, ni vigumu sana kuzungumzia ni nani atakayepewa malezi ya watoto ya baadaye katika hali yenye utulivu na ya kimantiki. Ili kupunguza makabiliano ya wazazi na kuepuka upinzani katika mahakama, mamlaka fulani ya mahakama hutoa njia ya badala ya kusuluhisha mabishano, kama vile upatanisho nje ya mahakama.
Ukishughulikiwa vizuri, upatanisho huwaruhusu wazazi kufikia upatano badala ya kuachia hakimu uamuzi juu ya watoto. Ikiwa upatanisho hauwezekani, wazazi waweza kufikia upatano wa malezi na haki za kutumia wakati na watoto kupitia kwa mawakili wao. Wazazi wafikiapo upatano na kuuandika katika maandishi, hakimu aweza kuweka sahihi agizo lililo na matakwa yao.
Wakati wazazi hawawezi kukubaliana kuhusu mpango wa malezi, mfumo wa sheria katika nchi nyingi utatoa namna ya kujaribu kuhakikisha kuwa faida za watoto zinalindwa. Hangaikio kuu la hakimu litakuwa watoto, si wazazi. Hakimu atafikiria mambo mengi yanayohusiana, kama vile matakwa ya wazazi, uhusiano wa mtoto na wazazi wote wawili, upendeleo wa mtoto, na uwezo wa kila mzazi wa kuandaa utunzaji wa kila siku. Kisha hakimu ataamua mtoto ataishi wapi na ataishi na nani vilevile jinsi wazazi watakavyofikia maamuzi ya maana kuhusu wakati ujao wa mtoto.
Katika makubaliano ya mzazi mmoja kuwa mlezi, huenda mzazi huyo akawa na mamlaka ya kufanya maamuzi. Katika makubaliano ya malezi ya pamoja, wazazi wote wawili lazima wakubaliane katika maamuzi muhimu, kama vile utunzaji wa afya ya mtoto na elimu.
Maswali Yawezayo Kukabiliwa
Wanapokabili hali ya kwenda mahakamani kwa ajili ya malezi ya mtoto, wazazi walio Mashahidi wa Yehova ni lazima wafikirie pia kilicho bora zaidi kwa habari ya hali ya kiroho ya watoto. Kwa kielelezo, namna gani ikiwa mzazi asiye Shahidi anapinga kuwazoeza watoto kwa kupatana na Biblia? Au namna gani ikiwa mzazi asiye Shahidi ametengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo?
Hali kama hizi zaweza kufanya iwe vigumu zaidi kwa wazazi Wakristo kufanya maamuzi. Wanataka kutenda katika njia yenye hekima na yenye kiasi, na pia wanataka kudumisha dhamiri safi mbele ya Yehova wanapoyafikiria kwa sala yaliyo bora zaidi kwa watoto.
Katika makala zifuatazo, tutaangalia maswali kama haya: Inapompa mzazi malezi ya watoto, sheria husema nini kuhusu dini? Naweza kukabilianaje kwa mafanikio na magumu ya kesi ya malezi kwa mafanikio? Naweza kukabilianaje na kupoteza malezi ya watoto wangu? Nayaonaje makubaliano ya malezi pamoja na mzazi aliyetengwa na ushirika?