Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 12/8 kur. 9-12
  • Malezi ya Mtoto—Maoni Yaliyosawazika

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Malezi ya Mtoto—Maoni Yaliyosawazika
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kukubali Sababu
  • Malezi ya Pamoja
  • Malezi ya Mzazi Mmoja
  • Mapendeleo ya Kutumia Wakati Pamoja na Mtoto
  • Hauwi Peke Yako Kamwe
  • Wengine Waweza Kusaidia
  • Matatizo ya Jamaa Yatatuliwa na Mashauri ya Biblia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Malezi ya Mtoto—Dini na Sheria
    Amkeni!—1997
  • Ni Nini Kingekuwa Bora Zaidi kwa Mtoto?
    Amkeni!—1997
  • Mzazi Mmoja, Matatizo Mengi
    Amkeni!—2002
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 12/8 kur. 9-12

Malezi ya Mtoto—Maoni Yaliyosawazika

MARA nyingi magumu hasa hutokea baada ya talaka, kung’ang’ania shauku na udhibiti wa mtoto. Ule msemo “Kwahitaji wawili ili kupigana vita” si kweli sikuzote. Huenda ikahitaji mzazi mmoja tu aliye na jeuri atakaye mambo yafanywe atakavyo. Mwanasheria wa familia katika Toronto, Kanada, alionelea: “Katika sheria za familia, kila kitu huongozwa na hisia-moyo na hisia za watu zahusika.”

Badala ya kufikiria lililo bora zaidi kwa mtoto, wazazi wengine huendeleza mabishano kwa muda mrefu kwa kuanzisha majadiliano kuhusu masuala yasiyofaa. Kwa kielelezo, wengine wamejaribu kuthibitisha kuwa malezi yapaswa kubadilishwa kwa kuwa mzazi yule mwingine ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova na atamnyima mtoto ‘njia ya kawaida ya maisha.’

Yule asiye Shahidi aweza kutoa suala kuhusu kusherehekea sikukuu za kuzaliwa, Krismasi, au hata Halowini. Wengine huenda wakalalamika kuwa ushirika wa mtoto na marekebisho ya kijamii yangezuiwa ikiwa mtoto angeamua kutoisalimu bendera. Au huenda wengine wakapendekeza kuwa mtoto angedhuriwa kisaikolojia kwa kuandamana na mzazi katika kuzungumza na wengine kuhusu Biblia. Wazazi fulani wasio Mashahidi hata wamedai kuwa maisha ya mtoto yangehatarishwa kwa sababu mzazi aliye Shahidi hangetoa idhini kwa mtoto ili atiwe damu mishipani.

Mkristo hukabilije ugumu wa mabishano kama hayo yenye kujaa hisia? Jibu lenye kujaa hisia—“kuzima moto kwa moto”—halitakuwa na matokeo. Ikiwa jambo hilo lapelekwa mbele ya hakimu, kila mzazi atakuwa na fursa ya kusikiwa. Ni jambo la maana zaidi kukumbuka shauri la Biblia lisemalo: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 55:22) Kwa kutafakari juu ya kanuni hizi za Biblia na kuzitumia, wazazi wanaweza, kwa msaada wa Yehova, kukabiliana na tukio lolote la mwisho linalohusu malezi ya mtoto.—Mithali 15:28.

Kukubali Sababu

Suala kuu ni hali njema ya mtoto. Ikiwa mzazi ni mwenye kudai sana, aweza kupoteza malezi ya mtoto na hata apate kwamba mapendeleo yake ya kutumia wakati na mtoto yamewekewa vikwazo. Mzazi mwenye hekima hujiendesha kwa njia yenye amani, akikumbuka shauri la Biblia lisemalo: “Msirudishe ovu kwa ovu kwa yeyote. . . . Iachieni nafasi hasira ya kisasi . . . Usijiache mwenyewe ushindwe na lililo ovu, bali fuliza kushinda lililo ovu kwa lililo jema.” (Waroma 12:17-21) Iwe ni mahakamani, katika ofisi ya wakili, au pamoja na mkadiriaji wa malezi ya mtoto, wazazi wapaswa ‘kuacha hali yao ya kukubali sababu ijulikane kwa watu wote.’—Wafilipi 4:5.

Nyakati fulani mwenzi aliyetenganishwa atajaribu kuwadanganya wengine kwa kutokeza matatizo yenye kuongoza vibaya na ya kukisiwa tu. Ni jambo la hekima kupigana dhidi ya mwelekeo wa kibinadamu wa kuitikia kupita kiasi mashambulizi haya ya maneno. Afya, dini, na elimu ni mambo yanayopendwa sana na wenzi waliotenganishwa kwa kutunga hila katika kusikizwa kwa kesi ya kubishania malezi.—Mithali 14:22.

Kukubali sababu kwatia ndani uwezo wa kufikiria kwa uangalifu mambo ya hakika na kuzungumza ili kufikia makubaliano ya kiasi. Hakuna mzazi apaswaye kusahau kuwa hata baada ya talaka, mtoto bado ana wazazi wawili. Wazazi wametalikana lakini hawajamtaliki mtoto. Kwa hiyo, isipokuwa katika hali zenye kupita kiasi, kila mzazi apaswa kuwa na uhuru wa kutenda kama mzazi wakati anapokuwa na mtoto. Kila mmoja apaswa kuwa na uhuru wa kueleza hisia zake na kanuni zake na kushiriki pamoja na mtoto katika utendaji unaokubalika kisheria, wa kidini au mwingineo.

Ebu tuchunguze matokeo ya maamuzi yawezayo kufanywa na mahakama: (1) malezi ya pamoja, (2) malezi ya mzazi mmoja, na (3) kuwekewa mipaka kwa mapendeleo ya kuwa na mtoto. Tofauti ni nini kati ya malezi ya pamoja na malezi ya mzazi mmoja? Waweza kukabilianaje unapopoteza malezi? Namna gani ikiwa mzazi mmoja ametengwa na ushirika?

Malezi ya Pamoja

Mahakimu wengine huhisi kwamba ni muhimu kusitawisha uwasiliano kati ya mtoto na wazazi wote wawili. Kusababu kwao kwategemezwa na chunguzi za utafiti zinazoonyesha kwamba watoto wanaweza kupatwa na mkazo na madhara ya kihisia-moyo kidogo zaidi baada ya talaka ikiwa wazazi wataweza kushiriki malezi. Badala ya kuhisi kuwa ametupwa na mzazi mmoja, mtoto huyo atakuwa na hisi ya kupendwa na wazazi wote wawili na kushirikishwa katika nyumba zote mbili. “Malezi ya pamoja ni njia ya kuwahusisha wazazi wote wawili,” asema mwanasheria mmoja wa familia.

Hata hivyo, Dakt. Judith Wallerstein, mkurugenzi mkuu wa Kitovu cha Mabadiliko Katika Familia, katika Corte Madera, California, aonya kwamba kufanya malezi ya pamoja yafaulu, yahitaji wazazi wenye ushirikiano na mtoto ambaye ni mwenye kubadilikana na mwenye kupatana na watu. Sifa hizi ni za maana kwa sababu katika malezi ya pamoja wazazi wote wawili hudumisha haki ya kisheria ya kushiriki katika kufanya uamuzi kuhusu masuala makuu yanayohusu afya, elimu, malezi ya kidini, na maisha ya kijamii ya mtoto wao. Lakini hili hufanikiwa tu ikiwa wazazi wote wawili wanabaki wakiwa wenye kukubali sababu katika kufikiria lililo jema zaidi kwa mtoto wao badala ya linalowapendeza kibinafsi.

Malezi ya Mzazi Mmoja

Huenda mahakama ikampa malezi mzazi ambaye, katika maoni yake, aweza kuandaa vizuri zaidi mahitaji ya mtoto. Huenda hakimu akaamua kwamba mzazi mlezi awe ndiye pekee afanyaye maamuzi kwa habari ya masuala ya maana yanayohusu hali njema ya mtoto. Mara nyingi, mahakama hufikia uamuzi huo baada ya kusikiliza matokeo ya uchunguzi wa wakadiriaji—hawa kwa kawaida huwa ni wanasaikolojia, madaktari wa magonjwa ya akili, au wafanyakazi wa umma.

Watetezi wa malezi ya mzazi mmoja huhisi kuwa mpango huo humwezesha mtoto kuwa imara zaidi. Wazazi wanaposhindwa kuwasiliana au wanapoelekea kutowasiliana pamoja kwa matokeo, mahakimu wengi wa kesi hupendelea mpango huu wa malezi. Bila shaka, mzazi asiye mlezi haachwi nje kabisa ya maisha ya mtoto. Haki za kutumia wakati pamoja na mtoto kwa kawaida hupewa mzazi asiye mlezi, na wazazi wote wawili wanaweza kuendelea kumwandalia mtoto mwongozo, upendo, na shauku inayohitajiwa.

Mapendeleo ya Kutumia Wakati Pamoja na Mtoto

Ni jambo lisilo la hekima kwa wazazi kuona malezi ya mtoto kama kuna “mshindi” na “aliyeshindwa.” Wazazi hufanikiwa na wanakuwa “washindi” wanapowaona watoto wao wakikua kuwa watu wazima waliokomaa, hodari, na wenye kuheshimika. Kufaulu katika kulea mtoto hakutegemei ni nani amepewa malezi ya mtoto na sheria. Kwa kutii masharti ya sheria za mahakama katika mambo ya malezi ya mtoto, hata wakati yaonekanapo kuwa yasiyo haki, Mkristo ataonyesha “ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa.” (Waroma 13:1) Ni la maana pia kukumbuka kuwa huu si wakati wa kupigania shauku au uaminifu-mshikamanifu wa watoto wako kwa kumdharau yule mzazi mwingine katika jaribio la kuharibu uhusiano wake nao.

Kuna vielelezo vya Biblia vya wazazi wenye kumhofu Mungu ambao, kwa sababu tofauti-tofauti walitenganishwa na watoto wao. Kwa kielelezo, Amramu na Yokebedi, wazazi wa Musa, wakitenda kwa hali njema zaidi ya mtoto wao, walimweka katika kisafina chenye kuelea “akakiweka katika majani kando ya mto.” Wakati huyu mtoto mchanga sana alipopatikana na binti Farao, walidumisha tumaini lao katika Yehova. Wazazi hawa wenye hekima na wenye imani walithawabishwa kwa kupewa mapendeleo ya “kutumia wakati pamoja naye” ambao waliutumia kwa matokeo kumzoeza mvulana huyo katika njia ya Yehova. Musa akakua kuwa mtumishi mwenye kutokeza wa Mungu wa kweli.—Kutoka 2:1-10; 6:20.

Ingawa hivyo, namna gani ikiwa mzazi mmoja ametengwa na ushirika? Je, mzazi aliye Mkristo apaswa kumruhusu kutumia wakati na mtoto? Hatua ya kutenga na ushirika wa kutaniko hubadili tu uhusiano wa kiroho kati ya mtu huyo na kutaniko la Kikristo. Kwa kweli, hutenganisha vifungo vya kiroho. Lakini uhusiano wa mzazi na mtoto hubaki bila kuguswa. Mzazi aliyepewa malezi anapaswa kuheshimu haki za mzazi aliyetengwa na ushirika za kutumia wakati pamoja na mtoto. Hata hivyo, ikiwa mzazi aliye mlezi atokeza tisho la papohapo au kubwa kwa hali njema ya mtoto ya kimwili au ya kihisia-moyo, basi mahakama (si mzazi mlezi) yaweza kupanga kuwe na mtu wa tatu mtoto anapotumia wakati na mzazi huyo mwingine.

Hauwi Peke Yako Kamwe

Mashauri ya talaka na mabishano ya malezi ya mtoto ya baadaye huwa yenye kuchosha kihisia-moyo. Ndoa ambayo ilianza kukiwa na matumaini sasa imevunjwa-vunjwa pamoja na miradi walioitamani, mipango, na matarajio ya wenzi hao. Kwa kielelezo, kukosa uaminifu au kutendwa vibaya sana kwaweza kumfanya mke mwaminifu-mshikamanifu kutafuta ulinzi wa kisheria kwake na kwa mtoto wake. Lakini, hisia za hatia na za kutostahili zaweza kuendelea anapofikiria kwa makini kosa lilikuwa nini au jinsi ambavyo mambo yangaliweza kushughulikiwa kwa matokeo zaidi. Wenzi wengi wa ndoa huhofia jinsi watoto wao watakavyotenda kuelekea kuvunjika kwa familia. Kushindana mahakamani kwa ajili ya malezi kwaweza kuwa hali ya kubadilika-badilika kihisia-moyo ambayo haitahini tu uaminifu-maadili wa mtu akiwa mzazi, bali pia hujaribu imani ya mtu na itibari yake katika Yehova.—Linganisha Zaburi 34:15, 18, 19, 22.

Mwenzi asiye na hatia achaguapo kuchukua hatua kwa sababu ya kutendwa vibaya kwa mtoto au kutendwa vibaya kupita kiasi kwa mwenzi au kulinda afya yake dhidi ya hatari ya maradhi yenye kuambukizwa kingono kutoka kwa mwenzi asiye mwaminifu, hakuna sababu kwa mwenzi huyo asiye na hatia kuhisi hatia au kuhisi kwamba ameachwa na Yehova. (Zaburi 37:28) Mwenzi asiye mwaminifu au mwenye kutenda vibaya ndiye ameuchafua mkataba mtakatifu wa ndoa na ‘ametenda kwa hiana’ kwa mwenzi wake.—Malaki 2:14.

Endelea kuwa na “dhamiri njema” mbele ya wanadamu na mbele ya Yehova kwa kutumia kanuni za Biblia, ukimtendea mwenzi wako mliyetenganishwa naye kwa kufuatia haki, na kuonyesha kunyumbulika katika mapatano yenu ya malezi. “Ni bora kuteseka kwa sababu mnatenda mema, ikiwa mapenzi ya Mungu yataka hivyo, kuliko kwa sababu mnatenda ovu.”—1 Petro 3:16, 17.

Kwa habari ya watoto, wanahitaji uhakikishio kwamba mvunjiko wa familia haukuwa kosa lao. Wakati mwingine mambo hayaendi vile yalivyopangiwa. Lakini kutumia kanuni za Biblia kwaweza kupunguza athari ya talaka kwa kutia moyo kuwe na mazungumzo ya wazi na yenye uelewevu kati ya wazazi na watoto. Kwa kielelezo, hili laweza kufanywa kwa kuwaruhusu watoto wawe na sehemu katika kupangia maisha ya familia ya baada ya talaka. Kwa kuwa na subira na mwenye fadhili na kwa kupendezwa na hisia za watoto na kusikiliza maelezo yao, utafanya mengi katika kuwasaidia kujipatanisha na ratiba na mipango mipya ya kuishi.

Wengine Waweza Kusaidia

Si wazazi tu wanaoweza kumsaidia mtoto anayepitia mvunjiko wa familia. Washiriki wa familia, walimu, na marafiki waweza kufanya mengi kuunga mkono na kuwatia moyo watoto wa talaka. Hasa wazakuu waweza kufanya mengi kuchangia usawaziko wa watoto na hali njema ya kihisia-moyo.

Wazakuu Wakristo waweza kuwaandalia watoto mafunzo ya kiroho na utendaji wenye kujenga, lakini wapaswa kuwa wenye staha kuelekea maamuzi ya wazazi kuhusu mazoezi ya kidini, kwa kuwa ni wazazi, si wazakuu, walio na mamlaka ya kiadili na kisheria ya kufanya maamuzi haya.—Waefeso 6:2-4.

Wakiwa na tegemezo kama hilo, watoto wa talaka waweza kuvumilia mvunjiko wa ndoa ya wazazi wao. Na waweza kuendelea kutazamia mbele baraka za ulimwengu mpya wa Mungu, ambapo familia zote zitakuwa huru kutoka katika “utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Waroma 8:21; 2 Petro 3:13.

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Kusahihisha Kutoelewana

“Ulimi wa mwenye hekima hutamka maarifa vizuri,” na mzazi Mkristo ana fursa nzuri ya kusahihisha kutoelewana au kweli nusu. (Mithali 15:2) Kwa kielelezo, kwa habari ya utunzaji wa afya ya watoto wao, “Mashahidi wa Yehova hukubali tiba ya dawa na upasuaji,” lakini anapokuwa mzazi mlezi, Shahidi ana haki ya kuarifiwa na kutoa idhini juu ya utaratibu wowote wa kitiba.a—The Journal of the American Medical Association.

Mashahidi wa Yehova huchukua dini yao, inayotegemezwa na Neno la Mungu, Biblia, kwa uzito. Hii huwafanya wawe baba, mama, watoto, rafiki, majirani, na raia bora. Wazazi Wakristo hutoa nidhamu kwa upendo, wakijenga staha kwa mamlaka na kuwaandalia watoto wao maadili bora ya maisha.b—Mithali 13:18.

Elimu ya kilimwengu ni sehemu muhimu katika kumlea mtoto, na Mashahidi wa Yehova hutaka watoto wao wapate iliyo bora kabisa ipatikanayo.c—Mithali 13:20.

[Maelezo ya Chini]

a Ona broshua Damu Yaweza Kuokoaje Uhai Wako?, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b Ona kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, sura ya 5-7, 9, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

c Ona broshua Mashahidi wa Yehova na Elimu, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mzazi mlezi apaswa kusikiliza kwa subira wakati mtoto aelezapo kuhusu wakati aliotumia pamoja na mzazi asiye mlezi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki