Yehova Alinyoosha Njia Yetu
NILIZALIWA 1924, karibu na Cham, mji ulio katika mkoa wa Uswisi wa Zug. Wazazi wangu walikuwa na watoto 13—wavulana 10 na wasichana 3. Nilikuwa mzaliwa wa kwanza, mvulana. Wavulana wawili walikufa walipokuwa wachanga sana. Tuliobaki tulipokea malezi madhubuti ya Kikatoliki kwenye shamba wakati wa Mshuko Mkubwa wa Kiuchumi.
Baba alikuwa mtu mwenye kufuatia haki, mtu mwema kiasili, lakini alikuwa na mwelekeo wa kufoka kwa hasira kali. Katika pindi moja, hata alimpiga vibaya Mama alipomshutumu isivyo haki kwa sababu ya wivu wake. Mama hakuweza kuvumilia kumwona akizungumza na wanawake wa ujirani wetu, ingawa hakuwa na sababu ya kutilia shaka uaminifu wake. Jambo hilo lilikuwa likinitaabisha sana.
Mama alikuwa mshirikina sana. Alikuwa akifasiri hata matukio madogo kuwa ishara kutoka kwa “nafsi zenye kuteseka katika purgatori.” Nilichukia wepesi huo wa kuamini bila ushuhuda. Lakini makasisi walikuwa wakiendeleza itikadi zake za kishirikina kwa kumpa habari za kusoma zilizounga mkono mawazo yake ya kidini yasiyo ya kweli.
Nilikuwa na Maswali
Tokea uvulana wangu na kuendelea, maswali kuhusu Mungu na yale yatakayompata mwanadamu yalikaa akilini mwangu. Nilijaribu kufikia mikataa ya kiakili, lakini mambo mengi yalionekana kupingana! Nilisoma vichapo vya Kikatoliki kuhusu watakatifu, miujiza, na kadhalika. Hata hivyo, havikutosheleza kufikiri kwangu. Nilihisi kana kwamba nilikuwa nikipapasa-papasa gizani.
Kasisi wa kwetu alinionya kwa upole nisitafakari juu ya maswali niliyokuwa nayo. Alisema kwamba kutaka kuelewa kila kitu kulikuwa ishara ya majivuno na kwamba Mungu hukinza wenye kiburi. Fundisho lililokuwa lenye kunichukiza hasa lilikuwa kwamba Mungu angetesa milele katika helo yenye kuwaka moto wowote waliokufa bila kuungama dhambi zao. Kwa kuwa hilo lilimaanisha kwamba wanadamu walio wengi zaidi duniani wangeteswa milele, mara nyingi nilijiuliza, ‘Hii yaweza kupatanishwaje na upendo wa Mungu?’
Pia nilitilia shaka zoea la Kikatoliki la kuungama. Nilihofu tulipoambiwa kwenye shule ya Kikatoliki kwamba mawazo yasiyo safi yalikuwa dhambi kubwa iliyohitaji kuungamwa kwa kasisi. Nilikuwa nikijiuliza, ‘Je, nilikumbuka kuungama kila kitu? Au nilikuwa nimesahau jambo fulani, likifanya kuungama kwangu kuwe bure na dhambi zangu zisisamehewe?’ Hivyo nikawa na shaka moyoni kuhusu rehema ya Mungu na utayari wake wa kusamehe.
Kwa miaka mitatu au minne, nilipambana na mawazo yenye kushusha moyo yaliyonilemea. Nilifikiria kuacha kuamini Mungu kabisa. Lakini kisha ningefikiri, ‘Nikivumilia, bila shaka nitapata njia ifaayo.’ Baada ya muda fulani, nilisitawisha uhakika katika kuwako kwa Mungu, lakini nikawa na tashwishi nyingi juu ya itikadi zangu za kidini.
Kwa sababu ya yale niliyofundishwa mapema, niliamini kwamba Yesu Kristo alikuwa akifikiria Kanisa la Katoliki ya Kiroma alipomwambia mtume Petro hivi: “Juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu.” (Mathayo 16:18, Douay Version ya Katoliki) Nilikuja kuamini kwamba hatimaye sehemu nzuri katika kanisa zingeshinda, na nilitaka kushirikiana na kanisa ili kufikia lengo hilo.
Ndoa na Familia
Nikiwa mwana mwenye umri mkubwa zaidi katika familia, nilifanya kazi pamoja na baba yangu shambani hadi mdogo wangu anayenifuata alipoweza kuchukua mahali pangu. Kisha nikaenda katika shule ya kilimo ya Kikatoliki, nilikopata shahada ya pili. Baadaye, nilianza kutafuta mwenzi wa ndoa.
Kupitia mmoja wa dada zangu, nilipata kumjua Maria. Nilipata kujua kwamba alikuwa amesali apate mume ambaye wangejitahidi naye kupata uhai udumuo milele. Tuliandika hivi kwenye tangazo letu la ndoa: “Tukiwa tumeunganishwa katika upendo twatafuta furaha, macho yetu tumeyaelekeza kwa Mungu. Njia yetu ni uhai, na mradi wetu ni raha mustarehe ya milele.” Tulifunga ndoa Juni 26, 1958, katika makazi ya watawa wanawake ya Fahr, karibu na Zurich.
Maria nami tulikuwa na malezi yaliyofanana. Alitoka katika familia ya kidini sana naye alikuwa mkubwa kati ya watoto saba. Wote walikuwa na shughuli nyingi za kazi za shamba, shule, na kuhudhuria kanisa, kwa hiyo kulikuwa na wakati mchache sana wa kucheza. Miaka ya kwanza ya ndoa yetu haikuwa rahisi. Kwa sababu ya maswali mengi niliyokuwa nayo kuhusu mambo ya kidini, Maria alianza kutia shaka kama alikuwa ameolewa na mtu afaaye. Alikataa kutilia shaka mafundisho ya kanisa au zoea lake la kuunga mkono vita, Krusedi, na Mabaraza ya Kuhukumu Wazushi. Hata hivyo, sote wawili tuliitibari katika Mungu na tulisadiki kwamba maadamu tulikuwa tukitafuta kufanya mapenzi yake kadiri tuwezavyo, hangetuacha kamwe.
Katika 1959 tulikodi shamba karibu na Homburg mashariki mwa Uswisi. Haya yalikuwa makao yetu kwa miaka 31. Machi 6, 1960, mwana wetu wa kwanza, Josef, alizaliwa. Akafuatiwa na ndugu sita na dada mmoja, Rachel. Maria amethibitika kuwa mama asiyependelea, mwaminifu kwa kanuni zilizoimarika. Amekuwa baraka kwelikweli kwa familia.
Kutafuta Kweli ya Biblia
Hatua kwa hatua, tulishindwa kuvumilia kutokuwa kwetu na ujuzi wa kidini. Mwisho-mwisho wa miaka ya 1960, tulianza kuhudhuria mihadhara kwenye Shule ya Kikatoliki ya Watu Wazima, lakini tulikuwa tukirudi nyumbani tukiwa tumetatanishwa zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Wasemaji walifafanua maoni yao wenyewe, pasipo uthibitisho wa Kimaandiko. Katika sehemu ya mapema ya 1970, niliyafikiria maneno ya Yesu: “Ukimwomba Baba chochote kwa jina langu, atakupatia. . . . Omba, na utapokea.”—Yohana 16:23, 24, Dy.
Uhakikisho ulio juu kutoka Neno la Mungu ulinifanya nisali hivi kwa kurudia: “Baba, ikiwa Kanisa Katoliki ndilo dini ya kweli, tafadhali nionyeshe waziwazi. Lakini ikiwa si la kweli, nionyeshe waziwazi pia nami nitatangazia kila mtu.” Niliomba tena na tena kupatana na agizo la Yesu katika Mahubiri ya Mlimani la “fulizeni kuomba.”—Mathayo 7:7, 8.
Mazungumzo yangu na Maria—hasa juu ya mabadiliko ya mafundisho ya Kikatoliki katika miaka ya 1960 kuhusu ibada ya “watakatifu,” kula nyama kila Ijumaa, na kadhalika — mwishowe yalimfanya awe na tashwishi. Wakati mmoja, alipokuwa akihudhuria Misa katika masika ya 1970, alisali hivi: “Ee Mungu, tuonyeshe njia ya uhai wa milele. Hatujui tena ni ipi iliyo njia ya kweli. Nitakubali chochote, lakini onyesha familia yote njia ya kweli.” Sikujua juu ya sala yake, wala yeye hakujua juu ya yangu, hadi tulipotambua kwamba sala zetu zilikuwa zimesikiwa.
Kupata Kweli ya Biblia
Baada ya kurudi kutoka kanisani Jumapili moja asubuhi mapema katika 1970, mtu alibisha mlangoni. Mwanamume mmoja aliyeandamana na mwana wake mwenye umri wa miaka kumi alijijulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilikubali mazungumzo ya Biblia. Nilifikiria ningeweza kumthibitisha kuwa amekosea kwa sababu kutokana na mambo niliyokuwa nimeambiwa kuhusu Mashahidi wa Yehova, sikuamini walijua mambo sana.
Mazungumzo yetu yaliendelea kwa muda wa saa mbili bila matokeo yenye kutosheleza, na ilikuwa hivyohivyo Jumapili iliyofuata. Nilikuwa nikitazamia kwa hamu mazungumzo ya mara ya tatu, lakini yule Shahidi hakuja. Maria alisema kwamba lazima awe alitambua kwamba ilikuwa ni kazi bure. Nilifurahi aliporudi majuma mawili baadaye. Mara moja nilisema: “Nimekuwa nikijiuliza juu ya helo kwa miaka 35. Siwezi kukubali kamwe kwamba Mungu, ambaye ni upendo, atese viumbe kwa njia hiyo ya ukatili.”
“Wasema kweli,” akajibu yule Shahidi. “Biblia haifundishi kwamba helo ni mahali pa mateso.” Alinionyesha kwamba neno la Kiebrania na la Kigiriki limaanishalo Sheoli na Hadesi, ambalo mara nyingi limetafsiriwa “helo” katika Biblia ya Katoliki, hurejezea tu kaburi la kawaida. (Mwanzo 37:35; Ayubu 14:13; Matendo 2:31) Pia, alisoma maandiko yaliyothibitisha kwamba nafsi ya binadamu inaweza kufa na kwamba hukumu ya dhambi ni kifo, si mateso. (Ezekieli 18:4; Waroma 6:23) Kutokana na hayo, nilianza kuona waziwazi kwamba nilikuwa nimepofushwa na mambo ya kidini yasiyo ya kweli maisha yangu yote. Sasa nilianza kujiuliza kama mafundisho mengine ya kanisa hayakuwa sawa.
Sikutaka kudanganywa tena, kwa hiyo nilinunua kamusi ya Biblia ya Katoliki na mabuku matano ya historia ya mapapa. Vichapo hivi vilikuwa na kibali, yaani, mamlaka ya episkopali ya Katoliki ya Kiroma ilikuwa imekubali vichapwe. Kusoma historia ya mapapa kulinifanya nijue kwamba baadhi yao walikuwa miongoni mwa wahalifu wabaya zaidi ulimwenguni! Na kwa kuchunguza kamusi ya Biblia, nilijifunza kwamba Utatu, moto wa helo, purgatori, na mafundisho mengineyo mengi ya kanisa hayategemei Biblia.
Sasa nilikuwa tayari kujifunza Biblia na Mashahidi. Mwanzoni, Maria alikuwapo ili aonekane kuwa mwungwana tu, lakini upesi alikubali yale aliyokuwa akijifunza. Baada ya miezi minne niliacha Kanisa Katoliki na kumjulisha kasisi kwamba watoto wetu hawangehudhuria tena masomo ya kidini. Jumapili iliyofuata kasisi alionya wakazi wa parokia yake juu ya Mashahidi wa Yehova. Nilijitolea kutetea itikadi zangu nikitumia Biblia, lakini kasisi alikataa mazungumzo hayo.
Baada ya hapo tulifanya maendeleo ya haraka. Hatimaye, mke wangu nami tulifananisha wakfu wetu kwa Yehova kupitia ubatizo wa maji Desemba 13, 1970. Mwaka mmoja baadaye, ilinibidi nifungwe miezi miwili gerezani kwa sababu ya suala ya kutokuwamo kwa Kikristo. (Isaya 2:4) Haikuwa rahisi kuacha mke wangu na watoto wanane, hata kwa kipindi hicho kifupi. Watoto walikuwa na umri wa miezi 4 tu hadi miaka 12. Mbali na hilo, tulikuwa na shamba na mifugo wa kutunza. Lakini kwa msaada wa Yehova, waliweza kukabiliana na hali bila ya mimi kuwepo.
Kufuliza Kutanguliza Masilahi ya Ufalme
Mtu yeyote katika familia yetu hangekosa mkutano wa kutaniko kamwe isipokuwa awe alikuwa mgonjwa. Na tulipanga kazi yetu katika njia ya kwamba hatukukosa kamwe yoyote ya mikusanyiko mikubwa. Upesi michezo ya watoto darini mwetu ilikuwa kuigiza yale waliyoona kwenye mikutano yetu ya Kikristo. Kwa mfano, wangepeana migawo ya hotuba za wanafunzi na kujizoeza utoaji mbalimbali. Kwa furaha, wote waliitikia mafundisho yetu ya kiroho. Napenda sana kumbukumbu la mke wangu nami tukihojiwa kwenye kusanyiko la mzunguko, na watoto wetu wanane wakiketi kwa kufuatana—kuanzia yule mwenye umri mkubwa zaidi hadi yule mchanga zaidi — wakisikiliza kwa makini.
Kulea watoto wetu katika “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova” kulikuwa hangaiko letu kubwa. (Waefeso 6:4) Tuliamua kuondoa televisheni yetu, nasi mara nyingi tungealika Wakristo wenzetu wenye bidii nyumbani kwetu ili watoto wetu waweze kunufaika kutokana na mambo yao yaliyoonwa na idili yao. Tulikuwa waangalifu kuepuka mazungumzo ya kutofikiria wengine na kuchambua wengine. Ikiwa mtu alikosea, tulizungumzia hilo na kuangalia mambo yaliyomsababisha akosee. Tulijaribu kusaidia watoto wetu wakadirie hali kwa kusababu kuzuri na kwa haki. Tuliepuka kwa uangalifu kuwalinganisha na vijana wengine. Na tulitambua umaana wa wazazi kutowaendekeza au kutowakinga watoto na matokeo ya matendo yao.—Mithali 29:21.
Hata hivyo, kulea watoto wetu hakukuwa bila matatizo. Kwa mfano, wakati mmoja, wanashule wenzi waliwashawishi wachukue peremende kutoka kwenye duka bila ya kuzilipia. Tulipojua lililotokea, tulifanya watoto wetu warudi dukani na kuzilipia na waombe msamaha. Lilikuwa jambo lenye kuaibisha kwao, lakini walijifunza somo la ufuatiaji wa haki.
Badala ya kulazimisha watoto wetu waandamane nasi tu katika utendaji wa kuhubiri, tuliweka kielelezo kwa kuutanguliza utendaji huo. Watoto waliona kwamba sisi tulitanguliza mikutano na huduma ya shambani mbele ya kazi iliyohitaji kufanywa shambani. Jitihada zetu za kulea watoto wetu wanane katika njia ya Yehova zilibarikiwa kwa hakika.
Mwana wetu mkubwa zaidi, Josef, sasa ni mzee Mkristo na alitumikia kwa miaka kadhaa katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova Uswisi pamoja na mke wake. Thomas ni mzee, na yeye na mke wake ni mapainia, kama watumishi wa wakati wote wanavyoitwa. Daniel, aliyeacha kazi-maisha yake ya ubingwa wa mbio za baiskeli, ni mzee, naye na mke wake ni mapainia katika kutaniko jingine. Benno na mke wake ni wahudumu watendaji katika Uswisi ya kati. Mwana wetu wa tano, Christian, anatumikia akiwa mzee katika kutaniko tunalohudhuria. Ameoa na ana watoto wawili. Franz ni painia na mzee katika kutaniko moja la Bern, na Urs, ambaye wakati mmoja alitumikia katika ofisi ya tawi ya Uswisi, ameoa naye anatumikia akiwa painia. Binti yetu wa pekee, Rachel, na mume wake walikuwa mapainia pia kwa miaka kadhaa.
Kwa kufuata kielelezo cha watoto wangu, mimi pia nimekuwa painia, baada ya kustaafu kutoka kazi ya kimwili Juni 1990. Nikitazama nyuma kwenye maisha yangu na yale ya familia yangu, kwa hakika naweza kusema kwamba Yehova amenyoosha njia yangu na kutupa baraka “hata isiwepo nafasi ya kutosha.”—Malaki 3:10.
Andiko la Biblia apendalo sana mke wangu mpendwa ni hili: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 55:22) Nalo langu ni hili: ‘Jifurahishe kwa BWANA, naye atakupa haja za moyo wako.’ (Zaburi 37:4) Sote wawili tumeona ukweli wa maelezo haya yenye kupendeza. Mradi wetu ni kumsifu Mungu wetu, Yehova, milele, pamoja na watoto wetu na familia zao.—Kama ilivyosimuliwa na Josef Heggli.