“Kubaliana na Mteja Sikuzote”
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA WEI TUNG CHIN
Mume wangu alizoea kuniambia kwamba nisijishughulishe na “wale watu wa kidini wafinyao kengele za milango.” Hivyo Mashahidi wa Yehova walipokuja katika mlango wetu, ningesema hatukupendezwa. Lakini pia aliniambia “kubaliana na mteja sikuzote,” hivyo Shahidi alipokuja katika mkahawa wetu uitwao Red Dragon na kutaka kuongea na mimi kuhusu dini yake, nilihisi kwamba ni lazima nisikilize.
MUME wangu Tong Y., alimiliki Red Dragon, mkahawa wa Kichina katika St. Clair Avenue, katika Cleveland, Ohio. Hapo, baada ya kufunga ndoa aliniambia wito huu, “Kubaliana na mteja sikuzote.”
T.Y. alikuwa amekuja Marekani ili kusoma katika Chuo Kikuu cha New York. Baada ya kuhitimu katika 1927, alikwenda kufanya kazi katika mkahawa katika sehemu ya Times Square ya New York. Aliwaona watu wakila chakula katika kaunta za duka la dawa, ambapo vifaa vya kupikia vilikuwa vichache. Hivyo alikuwa na wazo la kuwauzia chakula moto aina ya chow mein.
Baada ya muda mfupi, mkahawa alioufungua katika Kijiji cha Greenwich ulikuwa ukifanikiwa sana. Katika mwaka 1932 alihamisha biashara yake hadi Cleveland, Ohio, na kufungua Red Dragon, ambayo iliwatosha watu 200. Gazeti moja la habari la Cleveland liliripoti katika Septemba 1932: “Akivamia eneo la Maziwa Makubwa baada ya kukazia fikira kutosheleza hamu ya chakula ya mamilioni ya watu katika mashariki yote, Tong Y. Chin ameleta katika Cleveland mkahawa wake wa kwanza wa chow mein mpya katika eneo la magharibi ya kati ambao ameusitawisha katika miaka mitano kuwa biashara yenye kuchuma dola milioni moja kwa mwaka.”
Kabla ya kueleza jinsi nilivyokutana na T.Y., acha nieleze kuhusu maisha yangu katika China, hali iliyochangia sana maisha yangu ya baadaye.
Malezi ya Umaskini
Kumbukumbu zangu za mapema ni kumwona Mama akiondoka katika kijiji chetu kilichoko China barani akitafuta chakula. Wazazi wangu walikuwa maskini sana kiasi cha kwamba walilazimika kutoa baadhi ya watoto wao waasilishwe. Siku moja, nilipokuwa na umri wa karibu miaka miwili au mitatu tu, Baba alirudi nyumbani akiwa na mtazamo fulani katika macho yake. Nilifikiri, ‘Ana habari mbaya kwangu.’
Baada ya muda mfupi, Mama alinishika mkono, tukapitia kijia chembamba, chenye matope, kilichoko kati ya mashamba ya mpunga, tukiwa waangalifu tusiangukie majini katika upande wowote. Tulisimama katika nyumba moja ambapo Mama alizungumza na msichana aliyekuwa akitabasamu, kisha katika nyumba nyingine ambapo msichana mchanga alionekana kuwa na hofu na bila tabasamu. Sikumbuki kupata kuwaona wasichana hawa. Walikuwa dada zangu wakubwa. Waliponiaga, nilihisi kwamba hatutaonana tena kamwe.
Tulipoendelea kutembea, mama yangu aliongea mfululizo, akiniambia mambo kumhusu, baba yangu, na ndugu na dada zangu. Bado ninaweza kuyaona macho ya Mama yenye fadhili na huzuni. Tulipofika mwisho wa safari yetu, ilionekana kama kuna tatizo. Nyumba hiyo ilionekana yenye kusikitisha na isiyo na furaha. Hii ilikuwa makao yangu mapya. Sikutaka kulala, lakini mama yangu na wazazi wangu wa kambo walinifanya nilale. Baada ya muda mfupi nililala, na nilipoamka, Mama alikuwa amekwenda. Sikumwona tena kamwe.
Utoto Wenye Huzuni
Ingawa sasa kulikuwa na chakula cha kutosha, hakukuwa na upendo, na moyo wangu ulikuwa na huzuni sana. Kila asubuhi niliamka na kulia. Niliwatamani Mama na kaka yangu, ambaye alibaki nyumbani pamoja na mama. Mara nyingi nilifikiria kujiua. Nilipokuwa mkubwa kiasi, nilitamani sana kwenda shule, lakini wazazi wangu wa kambo waliendelea kuniweka nyumbani ili nifanye kazi.
Nilipokuwa na umri wa miaka tisa, tulihamia mbali sana huko Shanghai. “Sasa una umri wa kutosha kuweza kwenda kununua vitu dukani na kupika chakula,” niliambiwa. Hivyo kazi hizo ziliongezwa katika kazi zangu za kila siku. Kila siku wazazi wangu wa kambo wangenipa fedha kiasi cha kutosha kununua chakula cha milo mitatu. Njiani kuelekea sokoni, niliwapita ombaomba na kuwasikitikia sana kwa sababu walikuwa na njaa. Hivyo niliweza kuwapa sarafu moja au mbili na bado nikabakisha fedha za kununua chakula nilichohitaji.
Jinsi nilivyotaka kwenda shule na kujifunza! “Katika kipindi cha miezi sita tutakuandikisha,” waliahidi wazazi wangu wa kambo. Muda huo ulipopita, waliniambia: “Miezi sita kuanzia sasa.” Baada ya muda mfupi, nilitambua kwamba nisingepelekwa kamwe shule. Nilihuzunika sana. Nilianza kumchukia kila mtu katika nyumba hiyo. Mara nyingi, ningejifungia bafuni na kusali. Ingawa tuliamini miungu mingi, lakini kwa kiasi fulani nilijua kwamba kulikuwa na Mungu mkuu, mwenye nguvu kuliko miungu mingine yote. Kwa hiyo nilimwambia hivi katika sala: “Kwa nini kuna maumivu na huzuni nyingi sana?” Hii ilikuwa sala yangu kwa miaka mingi.
Ndoa Yabadili Maisha Yangu
Siku hizo katika China, ndoa zilizopangwa na watu wa ukoo zilikuwa za kawaida. Mmoja kati ya marafiki wa T.Y. wa chuo kikuu ambaye alikuwa amerudi China alimwandikia: “Umepita umri wa miaka 30 na bado hujaoa.” Kisha aliongea kunihusu na kuongeza: “Ana umri wa miaka 18; ana sura nzuri, na tabia nzuri pia. . . . Kama ningekuwa wewe Tong Y. Chin, ningechukua jambo hili kwa uzito.” Rafiki yake alitia ndani picha.
T.Y. aliwaandikia wazazi wangu wa kambo: “Nimeiona picha ya binti yenu mwenye kuheshimika. Nitamwoa, ikiwa, baada ya kuonana na kutumia wakati pamoja, twagundua kwamba twapendana.” T.Y. alikuja Shanghai, tukakutana. Ingawa nilifikiri kwamba alikuwa amekomaa sana kwangu, niliamua kwamba angalau ndoa itaniwezesha kuondoka katika nyumba hii. Hivyo tukafunga ndoa katika mwaka 1935 na mara moja tulisafiri kwa meli kwenda Marekani. Hivyo ndivyo nilivyokuja Cleveland.
Matatizo Makubwa Japo Utajiri
Mwanzoni, kulikuwa na matatizo ya uwasiliano na mume wangu. Aliongea lahaja mojawapo ya Kichina, Kikanton, na niliongea nyingine, Kishanghai. Ilikuwa kana kwamba tulikuwa tukiongea lugha mbili tofauti. Pia nililazimika kujifunza lugha ya Kiingereza na desturi mpya. Vipi kazi yangu mpya? Nilipaswa kuwa mhudumu wa mkahawa mwenye kupendeza, mwenye neema, wakati wote nikitaka kuwapendeza wateja. Ndiyo, nilipaswa kukumbuka, “Kubaliana na mteja sikuzote.”
Nilifanya kazi ngumu kwa saa 16 au zaidi kwa siku pamoja na mume wangu, na wakati mwingi nikiwa mjamzito. Binti yetu wa kwanza, Gloria, alizaliwa mwaka 1936. Baada ya hapo, nilizaa watoto sita katika kipindi cha miaka tisa—wavulana watatu na wasichana watatu zaidi, mmoja wao akifa alipokuwa na umri wa mwaka mmoja tu.
Wakati huohuo, T.Y. alikuwa ameanza kuendesha mikahawa na klabu nyingi za usiku. Baadhi ya watumbuizaji ambao walianza kazi-maisha yao katika hizi, kama vile Keye Luke, Jack Soo, na Kaye Ballard, wakaja kuwa watu maarufu sana. Pia vyakula vyetu vya Kichina viliuzwa sana na kuwa maarufu.
Kufikia katikati ya miaka 1930, T.Y. alijulikana kuwa mfalme wa chow mein. Pia alikuwa msimamizi wa Chama cha Wafanyabiashara wa Kichina na mhadhiri juu ya China. Nilijihusisha katika mambo mengi ya hisani, kijamii, kiraia, na ya jumuiya. Kuonekana mbele ya watu na kutembea katika gwaride kulikuwa sehemu ya maisha yangu. Picha zetu na majina yetu yalionekana kwa kawaida katika magazeti ya habari ya Cleveland; kila kitu tulichofanya au kusema kilionekana kuripotiwa—kutoka shughuli za biashara hadi likizo na hata saizi ya kiatu changu!
Katika mwaka wa 1941, wakati majeshi ya anga ya Japani yalipopiga Pearl Harbor kwa mabomu, Marekani ilianza vita na Japani. Kwa sababu tulikuwa watu wa kutoka nchi za Mashariki, tulibaguliwa. Hata kabla ya vita, tulipokuwa tukijenga nyumba yetu katika ujirani mzuri, tulipokea barua za vitisho vya kutuua. Lakini ilikwisha, na tuliwalea watoto wetu humo.
Hivyo, nilikuwa na nyumba nzuri, yenye nafasi, mume na familia yenye kustahiwa, ndiyo, hata mavazi maridadi na vito. Lakini, furaha iliendelea kuwa ndoto kwangu. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba hatukuwa na wakati sana tukiwa familia. Ingawa nilifanikiwa kuamka kila asubuhi kuwaona watoto wakienda shule, kwa kawaida tulikuwa tukifanya kazi walipoenda kulala. Mtunza-nyumba alishughulikia mahitaji yao ya kila siku.
Tulikuwa Wabuddha, na bado miungu ya dini yetu haikunituliza. T.Y., akiandamana na mwana wetu mkubwa zaidi, angetembea katika nyumba yote akiwasha mishumaa na kuweka chakula mbele ya sanamu, ili miungu ile. Lakini hawakula kamwe chakula hicho, hivyo watoto walikuwa wakifurahia sana kula baadaye.
Hatimaye, baada ya kupatwa na uchovu sana bila kuona suluhisho, nilifikiri kwamba familia yangu ingekuwa na furaha zaidi bila ya mimi. Nilichanganyikiwa sana akilini nikajaribu kujiua. Kwa uzuri, nilikimbizwa hospitalini, na nikapona.
Jibu kwa Sala Zangu
Wakati fulani baadaye, katika mwaka wa 1950, mwanamke mmoja mwenye nywele nzuri nyeupe aliingia katika mkahawa wetu akiwa na mume wake. Nilipokuwa nikiwakaribisha na kuona kwamba wameketi kwa starehe, aliongea nami kuhusu Mungu. Sikupendezwa. Mashahidi wa Yehova walikuwa wakitutembelea nyumbani na kujaribu kuongea na mimi, lakini sikuzote niliwaambia waende haraka. Lakini, katika mkahawa, hali ilikuwa tofauti—“Kubaliana na mteja sikuzote!”
Mwanamke huyo, Helen Winters, aliniuliza ikiwa niliamini Biblia. “Biblia ipi?” Nilijibu. “Kuna nyingi sana!” Kila wakati aliporudi, nilijiambia, ‘Yule msumbufu aja tena!’ Lakini alikuwa mwenye fadhili na mdumifu. Na kile alichosema kuhusu dunia iliyo paradiso ambayo isingekuwa na maumivu tena au kuteseka kilivutia.—2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.
Katika mojawapo ya ziara zake, aliacha mwaliko wa kwenda kwenye mikutano katika Jumba la Ufalme na alionyesha ujumbe mfupi katika upande wa pili ambao ulielezea baraka za Ufalme wa Mungu. Nakumbuka nikiuangalia baadaye na kufikiri, ‘Laiti hili lingekuwa kweli!’ Alinitolea funzo la Biblia pamoja nami nyumbani, na hatimaye nikakubali.
Kila juma tulijikusanya kuzunguka meza yetu kwa ajili ya funzo—Helen nami pamoja na watoto wangu sita, wakati huo wakiwa na umri wa miaka kati ya 5 hadi 14. Mara nyingi nilimsikitikia kwani wakati mwingine watoto walionekana kupoteza upendezi. Katika mwaka wa 1951 tulianza kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme. Baada ya muda mfupi niling’amua kwamba kile nilichokuwa nikijifunza kilikuwa jibu la sala zangu. Hivyo niliamua kwamba nilihitaji kwelikweli kujifunza kusoma Kiingereza vizuri, ambalo lilikuwa tatizo kubwa kwangu.
Kupata Furaha ya Kweli
Baada ya muda mfupi, nilianza kufanya maendeleo ya haraka katika ujuzi nikaweka maisha yangu wakfu kwa Yehova Mungu. Kisha, katika Oktoba 13, 1951, katika mkusanyiko mkubwa Washington, D.C., nilibatizwa pamoja na watoto wangu wawili wakubwa, Gloria na Tom. Kwa mara ya kwanza, maisha yangu yalikuwa ya maana. Ulikuwa mwanzo wa miaka yangu ya furaha zaidi.
Katika maisha yangu yote nimekuwa nikitumikia wanadamu wengine, lakini sasa niliazimia kitu cha kwanza kabisa ni kumtumikia Muumba wetu! Nilianza kushiriki ujumbe wa Ufalme na wote ambao wangesikiliza. Pia nilijaribu kukazia watoto wangu umaana wa kuhudhuria mikutano ya Kikristo na umuhimu wa kuongea na wengine juu ya mambo ya kupendeza katika Neno la Mungu.
Katika mwaka wa 1953 tulianza kuwa na Funzo la Kitabu la Kutaniko katika nyumba yetu. Karibu miaka 45 baadaye, funzo bado linaendelea kufanyika hapa. Katika miaka hiyo yote funzo la kitabu limekuwa na msaada mkubwa wa kiroho kwa familia yetu.
Kuendelea kuwa watendaji kiroho na bado kudumisha biashara yetu ya mkahawa lilikuwa jambo gumu sana. Lakini, niliweza kujifunza Biblia na watu wengi. Baadhi ya watu hawa walipokea kweli ya Biblia na baadaye wakawa mapainia, kama watumishi wa wakati wote wanavyoitwa. Wakati wa miaka ya 1950, watoto wetu wanne wachanga waliweka maisha yao wakfu kwa Yehova wakabatizwa. T.Y. hakuwa anapendezwa na Biblia, lakini bado angetupeleka na kuturudisha kutoka mikutanoni. Tuliamua tusimhubirie lakini tuongee tu miongoni mwetu wenyewe tulipokuwa tukirudi nyumbani kuhusu jambo moja au mawili tulilolifurahia katika mkutano.
Wakati huo, T.Y. alikuwa akifunga safari nyingi katika miji mingi kotekote Marekani. Nilipiga simu kwenye makao makuu ya Watch Tower Society katika Brooklyn, New York, na kueleza hali yetu. Grant Suiter, aliyekuwa wakati huo katibu-mweka-hazina wa Sosaiti, alitukaribisha tutembelee mahali hapo tulipokuwa New York. T.Y. alivutiwa sana, hasa juu ya usafi wa jikoni, ambayo wakati huo ilitayarishwa kulisha watu 500.
Wakati wa ziara yetu tulionana na Russell Kurzen, ambaye baadaye alimpelekea T.Y. Biblia ambayo aliisoma kila usiku hadi alipoimaliza. Baadaye, wakati wa mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova katika New York katika mwaka wa 1958, mume wangu alibatizwa! Kwa mshangao wetu, mwana wetu mkubwa zaidi, ambaye wakati huo alikuwa akitumika akiwa mshiriki wa familia ya makao makuu, alikuwa na sehemu fupi katika programu.
Mwaminifu Hadi Kifo Chake
Mara nyingi mimi na T.Y. tulishiriki pamoja katika huduma ya mlango hadi mlango. Wakati uwezo wa macho yake ulipoanza kupungua, tulishiriki kwa ukawaida katika ushahidi wa barabarani. Gazeti la The Cleveland Press lilikuwa na kichwa “Mgeuko Katika Red Dragon” pamoja na picha yetu tukitoa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa wapita-njia. Habari hiyo ilieleza jinsi tulivyopata kuwa Mashahidi. Ilitukia kwamba Red Dragon ilibadilishwa jina, ikawa Chin’s Restaurant.
Kwa miaka mingi, mume wangu nami tuliwapokea katika mkahawa wetu ndugu na dada wengi Wakristo kutoka sehemu mbalimbali ulimwenguni. Tulikumbuka vizuri shauri la Ndugu Fred Franz, ambaye alitumikia akiwa msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society. Alipotutembelea, alituhimiza: “Iweni waaminifu, na mshikamane kwa ukaribu na tengenezo la Yehova.”
Mwanzoni mwa miaka ya 1970, T.Y. alipatwa na mishtuko ya akili mara kadhaa naye akafa Agosti 20, 1975. Gazeti la habari la kila siku la kwetu lilichapisha tanzia ndefu pamoja na picha yake akitoa Mnara wa Mlinzi katika huduma. Miaka yetu ya mwisho tukiwa pamoja ilikuwa bora zaidi. Baada ya kufanya kazi kwa miaka zaidi ya 60, Chin’s Restaurant ilifungwa katika Aprili 1995. Kwa baadhi ya watu, hiyo ilionekana kuwa mwisho wa muhula fulani.
Kudumisha Miradi ya Kiroho
Wakati fulani ilikuwa tamaa yetu kwamba wana wetu watatu waendeshe biashara ya familia. Lakini, tamaa hiyo ilibadilika; tulitaka wafuate hatua za Yesu na kuwa wahudumu wa wakati wote. Tuliwauliza kila mmoja wao ikiwa yeyote angependa kupainia katika Hong Kong na kuwasaidia Wachina wengine kujifunza kile ambacho tulikuwa tumejifunza. Tuliwatolea msaada wa kifedha ili wapainie katika Hong Kong. Ingawa hakuna hata mmoja kati yao aliyekuwa amejifunza kuongea Kichina kwa ufasaha, Winifred, Victoria, na Richard walichagua kuhamia Hong Kong.
Binti yetu Winifred amepainia huko kwa zaidi ya miaka 34! Victoria aliolewa na Marcus Gum, na hatimaye walirudi Marekani. Wamelea watoto watatu—Stephanie na Seraiah, ambao wapo katika utumishi wa wakati wote katika Cleveland, na Symeon, ambaye anatumikia pamoja na mke wake Morfydd katika Watchtower Farms, Wallkill, New York. Victoria na Marcus sasa wanaishi karibu, ambapo waweza kunitunza. Yeye ni mwangalizi-msimamizi wa Kutaniko la Coventry katika Cleveland.
Binti yetu mkubwa zaidi, Gloria, amelazimika kubaki katika kiti cha magurudumu kwani alishambuliwa na polio katika mwaka 1955. Yeye na mume wake, Ben, waishi katika Escondido, California, ambapo aendelea kutumikia kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri. Tom amekuwa mhudumu wa wakati wote kwa miaka zaidi ya 22. Yeye na mke wake Esther, kwa sasa wanafanya kazi katika Watchtower Educational Center, Patterson, New York. Richard na mke wake, Amy, walirudi kutoka Hong Kong kusaidia kumtunza T.Y. kabla ya kifo chake. Sasa wao pia watumikia katika Patterson. Kitindamimba wetu, Walden, ametumia zaidi ya miaka 30 katika utumishi wa wakati wote. Kwa miaka 22 iliyopita, yeye na mke wake, Mary Lou, wametumikia makutaniko ya Marekani katika kazi ya mzunguko na ya wilaya.
Si kwamba watoto wetu hawakutupatia kamwe matatizo yoyote. Akiwa tineja, mmoja alitoroka nyumbani na hatukusikia kumhusu kwa miezi mitatu. Kwa muda fulani mwana wetu mwingine alipendezwa na michezo zaidi kuliko mambo ya kiroho, akiepa funzo la Biblia la familia la kila juma ili aende akashindane katika michezo. Hata alipokea matoleo ya msaada wa masomo kwa sababu ya michezo. Alipoamua kuingia katika utumishi wa wakati wote badala ya kupokea moja ya hii misaada ya masomo ya chuo kikuu, nilihisi kitulizo kikubwa sana kwangu!
Nashukuru Kwamba Nilisikiliza
Ingawa watoto wangu wametawanyika kihalisi ulimwenguni, nafurahi kujua kwamba wanamtumikia Yehova kwa uaminifu. Sasa nina miaka 81, na ugonjwa wa baridi-yabisi na magonjwa mengine yamepunguza mwendo wangu, lakini bidii yangu kwa Yehova haijapungua. Najitahidi kujitunza ili mtoto wangu yeyote asiache utumishi wa wakati wote ili aje kunitunza.
Ninatazamia kwa shauku wakati ujao ambapo makusudi ya Mungu yatatimizwa na nitawaona tena wapendwa wangu waliokufa, kutia ndani mume wangu, wazazi wangu wa asili, na Helen Winters, ambaye alijifunza pamoja nasi. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Ninaterema kama nini kwamba nilimsikiliza yule mwanamke mpendwa mwenye nywele nyeupe zaidi ya miaka 46 iliyopita! Kwa kweli, nilikubaliana na yule mteja!
[Picha katika ukurasa wa 21]
Tulipofunga ndoa
[Picha katika ukurasa wa 23]
Familia yetu katika mwaka 1961. Kutoka kushoto kwenda kulia: Victoria, Wei, Richard, Walden, Tom, T.Y., Winifred, na Gloria mbele
[Picha katika ukurasa wa 24]
Wei Chin leo