Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 1/8 kur. 10-12
  • Jinsi Uwezavyo Kukabiliana na Hii Enzi ya Habari

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Uwezavyo Kukabiliana na Hii Enzi ya Habari
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wapokeaji na Watoaji wa Habari
  • Je, Twahitaji Habari Nyingi Hivi Zisizo na Maana?
  • Habari Nyingi Kupita Kiasi
    Amkeni!—1998
  • Hangaiko la Habari Husababishwa na Nini?
    Amkeni!—1998
  • Matumizi ya Internet—Uwe Chonjo Kuhusu Hatari Zake!
    Huduma Yetu ya Ufalme—1999
  • Intaneti Kutumia kwa Hekima Kifaa cha Ulimwenguni Pote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 1/8 kur. 10-12

Jinsi Uwezavyo Kukabiliana na Hii Enzi ya Habari

LAZIMA tukabili uhakika wa kwamba kuna pande nyingi za enzi ya habari ya miaka ya 1990 ambazo zitaendelea kutufanya tuwe na hangaiko. Tuna udhibiti kidogo tu au hatuna udhibiti wowote juu ya baadhi ya hizi. Kwa upande ule mwingine, kuna hatua tuwezazo kuchukua ili kuondosha mengi, ikiwa si yote, ya mahangaiko kama hayo. Kwa hiyo twaweza kusema kuwa, kuokoka katika enzi ya habari ni kazi ngumu lakini yenye kuthawabisha.

Wapokeaji na Watoaji wa Habari

Kama tumejiainisha kwa njia hii au la, katika maisha yetu yote kwa kadiri fulani sisi ni wapokeaji na watoaji wa habari. Hata hivyo, ubongo wetu hupokea na kushughulikia habari kwa njia tofauti-tofauti. Njia moja yahusu uwezo wa ajabu wa ubongo wa kushughulikia habari bila sisi kufahamu.

Njia nyingine yahusu kushughulikia habari tukiwa na ufahamu kama vile wakati wa maongezi. Tuna udhibiti mkubwa juu ya aina hii ya kushughulikia mambo—tukiwa watoaji na wapokeaji. Juu ya maongezi yasiyo na maana, Biblia huonya kuhusu wale “wasio na shughuli tu, bali pia wapiga-porojo na wajiingizaji katika mambo ya watu wengine, wakiongea juu ya mambo yasiyowapasa.” (1 Timotheo 5:13) Yaani, jihadhari usitumie wakati mwingi kupita kiasi ukiongea kuhusu mambo yasiyo na maana au hata habari yenye kudhuru. Usiwe aina ya mtu ambaye mapendezi yake makuu katika maisha ni kujua porojo ya karibuni zaidi. Wakati na nishati zenye thamani zaweza kupotezwa, na hii yaweza kutufanya sisi na wengine tuhangaike. Waweza kukosa fursa za kufyonza na kugawanya habari ambayo ni yenye kujenga na yaliyo muhimu ili kuokoka katika ulimwengu huu wenye matatizo.

Habari ipatikanayo kwa kusoma hushughulikiwa tukiwa na ufahamu na kwa sababu hiyo huchukua muda mrefu zaidi. Maombolezo haya yenye kujaa hangaiko, “Nimeshindwa kumaliza usomaji wangu!” husikika sana. Je, wahisi kuwa una mengi ya kusoma na wakati mchache sana wa kufanya hivyo? Kwa sababu ya hali ya kusoma ya kuchukua wakati mwingi, usanifu na raha ya kusoma hupotezwa katika enzi hii ya habari ya papo hapo. Watu wengi huruhusu televisheni kuhodhi wakati wao. Na bado, habari iliyoandikwa ingali njia yenye nguvu zaidi ya kuchochea mawazo na kupeleka habari, maoni, na mawazo.

Twaweza kukabilianaje wakati vifaa vingi vya kusoma vinapotaka uangalifu wetu na vyashindana na televisheni, michezo ya kompyuta, na mambo mengine ya kupisha wakati? Jibu ni kuchuja. Kuchuja, kuchanganua au kuweka mambo ya kutanguliza, kile tuhitajicho kusikia, kuona, kusema, au kusoma kwaweza kuondosha hangaiko jingi la habari. Kuchuja kwenye matokeo kwaweza kufanywa katika viwango viwili.

Je, Twahitaji Habari Nyingi Hivi Zisizo na Maana?

Utambuzi wa mahitaji yetu mara nyingi hupotoshwa na yale wengine hufikiri kuwa twahitaji au hupotoshwa na ustadi wa vyombo vya habari wa kutangaza ambao hutuongoza tuamini kuwa tuna uhitaji. Ili kukabili mchafuko huu wa mchanganyiko wa mambo mengi ya habari, tumia kanuni hii ya msingi: Weka mambo yakiwa sahili! Richard S. Wurman aieleza hivi: “Siri ya kushughulikia habari ni kupunguza eneo lako la kupokea habari liwe lile linalohusu maisha yako . . . Naamini kuwa ni ngano kwamba kadiri uwavyo na machaguo mengi, ndivyo uwezavyo kuchukua hatua zifaazo na ndivyo utakavyofurahia uhuru mwingi. Badala ya hivyo, machaguo mengi yaelekea kutokeza hangaiko jingi.”

Kwa hiyo, kwa habari ya kusoma na kutazama televisheni, ni vizuri kuchunguza mazoea yako. Jiulize: ‘Je, hili ni muhimu katika kazi yangu au maisha yangu? Je, nahitaji kweli kujua habari zote zisizo na maana na porojo kuhusu watu mashuhuri na waitwao eti watu warembo katika ulimwengu? Maisha yangu yangebadilikaje ikiwa singetazama programu hii ya televisheni, nisingesoma kitabu hiki au gazeti lile, au nisingetumia wakati mwingi sana nikisoma gazeti la habari?’ Wengi wameweza kuchanganua usomaji wao na utazamaji wao wa televisheni na wameweza kufutilia mbali mambo ambayo yalivuruga akili zao na pia nyumba zao. Kwa kielelezo, wameamua kufanya andikisho la gazeti moja tu la habari kila siku. Hata hivyo, magazeti mengi ya habari huwa na habari ileile. Watu wengine wameomba kihususa kwamba wasipokee barua za matangazo ambazo hawajaomba.

Kuweka maisha yakiwa sahili na bila mchanganyiko wa mambo kulipendekezwa na mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, Yesu Kristo. (Mathayo 6:25-34) Usahili wapendekezwa na watumika katika tamaduni nyingi za Kiasia na hata unatambuliwa na wengi katika tamaduni za nchi za Magharibi kuwa njia bora zaidi ya kuishi. Mwandishi Duane Elgin alitaarifu: “Kuishi kwa usahili zaidi ni kuishi maisha yenye kusudi zaidi yenye vikengeusha-fikira vichache zaidi visivyohitajiwa.”

Sasa, ukiwa umeweka mambo ya kutangulizwa katika kupokea habari kwa kulingana na mahitaji yako, fanya hivyohivyo na mapendezi yako, kwa kuwa mapendezi ndiyo nguvu yenye kuchochea ya kujifunza. Hata hivyo, tatizo hapa ni kutofautisha kati ya yale yakupendezayo hasa, na yale ambayo huenda ukafikiri kuwa yapaswa kukupendeza ili uwapendeze wengine—labda watu katika mahali pako pa kazi. Lakini ikiwa waweza kupangia kusoma kwako na kutazama televisheni au kutumia kompyuta kama vile tu uwezavyo kupangia utendaji mwingine wowote, utapata kuwa kupangia mapendezi halisi kwaweza kufanya maisha yako yapendeze zaidi bila hangaiko lisilofaa.

Kwa hiyo, waweza kukabilianaje na hangaiko la habari? Huenda usiweze kuliondoa kabisa, lakini kufuata kanuni chache sahili ambazo tumeorodhesha kwaweza kusaidia sana. Weka upokezi na mapendezi yako ya habari yakiwa sahili, na uchanganue habari kulingana na mahitaji na mapendezi ya kibinafsi. Wakati unakuja ambapo matatanisho yote ya maisha kutia ndani hangaiko la habari, yatakuwa mambo yaliyopita, lakini kwa wakati huu, weka staajabu za tekinolojia ya sasa mahali pake. Zione kuwa njia ya kutimiza kusudi lako. Usiwe mtumwa wake wala kuipatia kicho. Hivyo, habari yenye mafaa itakuwa yenye kujenga, yenye kutia moyo, na yenye faida, bila kukusababishia hangaiko.

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Jaribu Kubadilishana

“Katisha huduma za televisheni ya kulipwa, . . . na utumie [pesa] hizo kwa mwezi kununua kitabu kimoja au zaidi vizuri. Vitabu ni kinyume cha televisheni: Ni vya polepole, vyenye kuhusisha, vyenye kutia moyo, vyenye kuamsha kufikiri, na kuchochea ubunifu.”

“Waweza pia kufikiria kujiwekea mpaka kwa muda wa saa utakazotumia kwenye Internet kila juma, au angalau kusawazisha muda wa wakati utakaotumia kwenye Internet na kutumia muda huohuo katika kusoma vitabu.”—Data Smog—Surviving the Information Glut.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Uwe Bwana-Mkubwa, Si Mtumwa

“Zima televisheni. Hakuna njia ya haraka zaidi ya kudhibiti maisha yako, amani ya nyumba yako, na uradhi wa kufikiri kwako kuliko kuzima kifaa ambacho huongoza maisha ya wengi wetu. Mamilioni ya Wamarekani wamegundua utulivu na utiwaji-nguvu unaotokana na kutumia swichi ya kuzimia televisheni, bila kutaja saa nyingi zipatikanazo za wakati usioratibiwa mambo ambazo wanaweza kuanza kufanya mambo ambayo hawakupata kamwe nafasi ya kuyafanya muda uliopita.”—Data Smog—Surviving the Information Glut.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Jihadhari na Internet

Watu wasio na adili hutumia Internet kufuatia mapotovu yao ya kingono na kujaribu kuwasiliana na watu wanaokubali mambo hayo au na wahasiriwa wasio na hatia. Wengine huitumia Internet kuendeleza mambo yao wenyewe ya kibinafsi. Waasi-imani pia huweka mahali pao katika Internet ili kunasa watu wasio na habari.

Tahadhari kubwa inahitajiwa wakati Internet inapotumiwa, na bila shaka wazazi wapaswa kusimamia kwa uangalifu watoto wao wowote ambao huenda wanaitumia. Ni kweli kwamba kuna habari nyingi nzuri zinazopatikana, kama vile maktaba za kufanyia utafiti, habari za kununua vitabu, na vituo vya habari. Kwa mfano, hivi karibuni Watchtower Society ilitangaza mahali pake katika Internet (http://www.watchtower.org), ambayo inatumika kutoa habari za kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova. Lakini, ni lazima mtu atambue kwamba kuna mambo yenye kudhuru sana huko, kutia ndani ponografia na uasi-imani.

Mkristo apaswa kufahamu shauri la Paulo: “Kwa hiyo, nasema hili na kutoa ushahidi katika Bwana, kwamba nyinyi msiendelee tena kutembea kama vile mataifa watembeavyo pia katika ukosefu wa faida wa akili zao . . . Wakiisha kuishiwa na hisia zote za adili, walijikabidhi wenyewe kwenye mwenendo mlegevu ili wafanye ukosefu wa usafi wa kila namna pamoja na pupa. Lakini nyinyi hamkujifunza Kristo kuwa hivyo.” (Waefeso 4:17-20) Pia, “Acheni uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa hata visitajwe hata miongoni mwenu, kama vile ifaavyo watu watakatifu; wala mwenendo wa aibu wala maongezi ya kipumbavu wala kufanya mzaha wenye aibu, mambo yasiyofaa, bali badala ya hivyo utoaji-shukrani.” (Waefeso 5:3, 4) Ni lazima tutambue kwamba mahali pengi katika Internet pamefanyizwa na watu wenye makusudi yasiyo ya adili au yasiyo ya haki. Na mahali pengi ambapo huenda ukosefu wa adili au ukosefu wa haki haupatikani, kama vile vikundi vya mazungumzo, kwa wazi ni upotezo wa wakati. Achana na hayo yote!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki