Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 1/8 kur. 26-27
  • Unaweza Kumhofuje Mungu wa Upendo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unaweza Kumhofuje Mungu wa Upendo?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mbingu na Utukufu Mwingi wa Mungu
  • Mungu Mwenye Kusamehe
  • Kuhofu Hukumu ya Mungu
  • Sitawisha Moyo wa Kumhofu Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kwa Nini Tunapaswa Kuhofu Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kuogopa Mungu Je! Kunaweza Kukunufaisha Wewe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Kwa Nini Ujifunze Biblia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 1/8 kur. 26-27

Maoni ya Biblia

Unaweza Kumhofuje Mungu wa Upendo?

“HERI MTU YULE AMCHAYE [“AMHOFUYE,” NW] BWANA.”—Zaburi 112:1.

IKIWA “Mungu ni upendo,” kama Biblia inavyomfafanua, kwa nini twapaswa kumhofu? (1 Yohana 4:16) Kwa ujumla maneno upendo na hofu huonwa kuwa hayapatani. Kwa hiyo, hofu yapaswa kuwa na fungu gani katika uhusiano wetu na Mungu? Kwa nini umhofu Mungu wa upendo? Uchunguzi wa makini wa jinsi neno “hofu” linavyotumika katika Biblia unaweza kutuandalia uelewevu bora juu ya jambo hili.

Katika lugha nyingi neno moja laweza kuwa na maana mbalimbali, likitegemea muktadha. Mathalani, katika lugha nyinginezo mtu aweza kusema: “Ninapenda aiskrimu” na pia, “Ninawapenda watoto wangu.” Kuna tofauti kubwa katika mkazo wa aina za upendo unaoonyeshwa. Vivyo hivyo, Biblia huzungumzia aina tofauti za hofu. Wakati inapotumia neno hilo kuhusu kuabudu Mungu, hairejezei ogofyo, tisho, au hisi ya adhabu inayokaribia. Badala ya hivyo, hofu ya Mungu huwasilisha hisia nzuri—kicho, ustahifu, na staha yenye kina kirefu. Hisia-moyo hizi zilizo bora ziko na upendo kwa Mungu na uvutio kumwelekea, bali si silika ya kukimbia au kujificha kutoka kwake.

Kumhofu Mungu huondoa hofu mbaya ya kujikunyata. Kuhusu mtu anayemhofu Mungu, mtunga-zaburi aandika: “Hataogopa habari mbaya; moyo wake u imara ukimtumaini BWANA.” (Zaburi 112:7) Hakuna tisho kutoka kwa watu waovu au kutoka kwa Shetani mwenyewe linaloweza kushinda staha yetu nyingi na kicho kwa Yehova. (Luka 12:4, 5) Wala tusiogope kumfikia Mungu katika sala. Badala ya hivyo, katika muktadha huu, ‘upendo hutupa hofu nje.’—1 Yohana 4:18.

Mbingu na Utukufu Mwingi wa Mungu

Mfalme Daudi wa zamani za kale alikuwa mtu mwenye kuhofu Mungu. Yeye alikuwa na kicho wakati alipofikiria kwa makini uumbaji wenye uzuri na ulio tata. Alisema kwa mshangao: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu na nafsi yangu yajua sana.” (Zaburi 139:14) Akikodoa macho katika anga ya usiku, alisema kwa mshangao: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu.” (Zaburi 19:1) Je, wawazia kwamba Daudi alitiwa woga mwingi na jambo hili lililompata? Kinyume cha hilo, lilimsukuma amwimbie Yehova sifa.

Ujuzi ulioongezeka wa leo juu ya mbingu watupatia sababu yenye nguvu hata zaidi ya kuhisi kicho. Hivi karibuni, waastronomia wakitumia Darubini-Upeo ya Angani ya Hubble walichunguza kwa kina zaidi ndani ya mbingu kuliko wanadamu wowote waliokuwa mbele yao. Waliteua sehemu ya anga ambayo ilionekana tupu kwa darubini-upeo za ardhi na kulenga Hubble kwenye eneo dogo tu kama punje ya mchanga iliyoshikiliwa penye urefu wa mkono. Picha iliyotokea ilikuwa imesongamana, si na nyota mojamoja, lakini na magalaksi—mifumo mikubwa mno yenye mabilioni ya nyota—ambayo mwanadamu hajapata kamwe kuona!

Ule ukubwa, fumbo, na ajabu ya ulimwengu wote mzima hutia kicho ndani ya mtazamaji makini. Hata hivyo, maajabu kama hayo ni wonyesho tu wa utukufu na nguvu za Muumba. Biblia humwita Yehova Mungu “Baba wa mianga ya kimbingu” na kutuambia kwamba “huihesabu idadi ya nyota, huzipa zote majina.”—Yakobo 1:17; Zaburi 147:4.

Ukubwa wa ulimwengu wote mzima waonwa pia katika muda ambao matukio ya kimbingu yatukia. Nuru kutoka kwenye magalaksi iliyopigwa picha na Darubini-Upeo ya Angani ya Hubble ilikuwa imesafiri kupitia anga kwa mabilioni ya miaka! Je, kuwa kwetu wapya na udogo wetu kwa kulinganishwa na udumifu wa mbingu haupaswi kusababisha tuhisi kicho na staha yenye kina kirefu kwa ajili ya Yule aliyeziumba nyota? (Isaya 40:22, 26) Kung’amua kwamba yule Mungu aliyeumba vyote hivyo pia ‘humkumbuka mtu na kumwangalia’ huongeza kina cha staha yetu kwa Muumba wetu na hutufanya tutake kumjua na kumpendeza. (Zaburi 8:3, 4) Staha na uthamini za hali ya juu sana ndizo Biblia huita hofu ya Mungu.

Mungu Mwenye Kusamehe

Sisi sote ni wasiokamilika. Hata tunapojaribu kufanya lililo sawa twafanya dhambi bila kukusudia. Inapotukia hivyo, je, twapaswa kuogopa sana kupoteza upendeleo wa Mungu? Mtunga-zaburi aliandika: “Kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha, ili Wewe uogopwe.” (Zaburi 130:3, 4) Kwamba “Muumba” ni mwenye fadhili sana na mwenye kusamehe hutokeza uthamini na staha yenye kina kirefu katika waabudu wake.—Isaya 54:5-8.

Hofu ya Mungu hutuchochea tutende mema na pia tujiepushe kufanya lile Mungu analosema ni baya. Uhusiano wetu pamoja na Baba yetu wa kimbingu waweza kulinganishwa na ule wa baba mwema wa kibinadamu pamoja na watoto wake. Nyakati nyingine huenda watoto wasikumbuke kwa nini baba yao huwakataza kucheza barabarani. Na bado, wakati wanapohisi msukumo wa kufuata mpira mbio mpaka kwenye barabara, kufikiria katazo la baba yao huwazuia—labda kukiwaokoa kutoka kwenye kifo. Hivyohivyo, kumhofu Yehova kwa mtu mzima kwaweza kumzuia asifanye tendo ambalo lingeweza kuangamiza maisha—yake mwenyewe na ya wengine.—Mithali 14:27.

Kuhofu Hukumu ya Mungu

Kwa kutofautisha, mtu ambaye dhamiri yake haimzuii kutompendeza Mungu ana sababu ya kuhofu katika njia tofauti sana. Kama vile serikali za kibinadamu huadhibu wahalifu, Mungu ana haki ya kuchukua hatua dhidi ya wakosaji wa kukusudia, wasiotubu. Kuruhusu kwa Mungu uovu kwa muda kumefanya wengine wawe sugu katika mwendo wenye kosa. Lakini Biblia huonyesha waziwazi kwamba siku moja karibuni ataondoa watu wote waovu kutoka kwenye dunia. (Zaburi 37:9, 10; Mhubiri 8:11; 1 Timotheo 5:24) Waovu wasiotubu wana sababu ya kuhofu adhabu kutoka kwa Mungu. Na bado, hii si aina ya hofu ambayo Biblia hupendekeza.

Badala yake, Biblia hushirikisha kumhofu Yehova na mambo mazuri maishani—kuimba, shangwe, itibari, hekima, maisha marefu, uhakika, ufanisi, tumaini, na amani, kwa kutaja machache tu.a Tukiendelea kutembea katika hofu ya Yehova, tutafurahia baraka za namna hiyo milele.—Kumbukumbu la Torati 10:12-14.

[Maelezo ya Chini]

a Ona Kutoka 15:11; Zaburi 34:11, 12; 40:3; 111:10; Mithali 10:27; 14:26; 22:4; 23:17, 18; Matendo 9:31.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]

Kwa hisani ya Anglo-Australian Observatory, picha ya David Maliny

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki