Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 1/22 kur. 4-8
  • Kujifunza Kuwaacha Waende

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujifunza Kuwaacha Waende
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuwafunza Watoto Wawe Wenye Madaraka
  • Rekebisho Lenye Upendo
  • Elimu kwa Ajili ya Uhai
  • Zoeza Mtoto Wako Tangu Utoto Mchanga Sana
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Wazazi—Wazoezeni Watoto Wenu Kwa Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Wafundishe Watoto Wako Kumpenda Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Kujenga Familia Yenye Nguvu Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 1/22 kur. 4-8

Kujifunza Kuwaacha Waende

“KAMA mishale mkononi mwa shujaa, ndivyo walivyo wana wa ujanani,” akaandika mtunga-zaburi wa Biblia. (Zaburi 127:4) Mshale haufikii shabaha yake kwa aksidenti. Lazima ulengwe kwa uangalifu. Kwa njia hiyohiyo, watoto hawawezi kufikia lengo la kuwa watu wazima wenye madaraka bila mwongozo wa wazazi. “Mlee mtoto katika njia impasayo,” Biblia yahimiza, “naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.”—Mithali 22:6.

Badiliko la kutoka kuwa mtoto mwenye kutegemea wazazi hadi kuwa mtu mzima mwenye kujitegemea haliwezi kufanywa usiku mmoja. Kwa hiyo wazazi wapaswa kuanza lini kuwazoeza watoto wao kuwa wenye kujitegemea? Mtume Paulo alimkumbusha mwanamume kijana aliyeitwa Timotheo hivi: “Tangu utoto sana umeyajua maandishi matakatifu, yawezayo kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu.” (2 Timotheo 3:15) Wazia, mama ya Timotheo alianza kumpa mazoezi ya kiroho akiwa angali mtoto mchanga sana!

Sasa, ikiwa watoto wachanga sana waweza kufaidika kutokana na mazoezi ya kiroho, je, si jambo lenye ukubalifu kuwapatia mazoezi kwa ajili ya utu mzima mapema iwezekanavyo? Njia moja ya kufanya hivyo ni kuwafunza kuchukua mambo kwa uzito, kufanya maamuzi yao wenyewe.

Kuwafunza Watoto Wawe Wenye Madaraka

Waweza kuwatiaje moyo watoto wako wawe wenye madaraka? Wenzi waliooana waitwao Jack na Nora wakumbuka kuhusiana na binti yao: “Kabla hajaweza kutembea kabisa, alijifunza kubeba soksi au vitu vidogo kupeleka kwenye chumba chake cha kulala na kuviweka katika mtoto wa meza anayefaa. Pia alijifunza kuweka vichezeo na vitabu mahali panapofaa.” Hii ni mianzo midogo, lakini tayari mtoto alikuwa akijifunza kufanya maamuzi yenye madaraka.

Kadiri mtoto aendeleavyo kuwa mkubwa, yeye aweza kukabidhiwa madaraka mazito zaidi. Hivyo Abra na Anita walimruhusu binti yao awe na mbwa kama mnyama-rafiki. Kijana huyo alikuwa na daraka kuelekea utunzaji wa mbwa huyo na hata alitoa pesa kutoka katika ruzuku yake kwa ajili ya gharama za kumtunza. Kuwazoeza watoto kuishi kulingana na madaraka yao kwahitaji subira. Lakini ni kwenye kufaa na kwachangia ukuzi wao wa kihisia-moyo.

Kazi za kila siku za nyumbani zatoa fursa nyingine ya kufunza watoto kuwa wenye madaraka. Wazazi wengine kwa kweli huwaachilia watoto wao kutokana na wajibu wa familia, wakiona kujihusisha kwao kuwa usumbufu kuliko kuwa msaada. Wengine hukata kauli kwamba watoto wapaswa ‘kuishi maisha bora zaidi kuliko waliyokuwa nayo wakiwa watoto.’ Huku ni kufikiri kwenye kasoro. Maandiko yasema “Ikiwa mtu anamwendekeza mtumishi wake tangu ujana na kuendelea, katika maisha yake ya baadaye atakuwa hata asiye na shukrani.” (Mithali 29:21, NW) Kanuni ya andiko hili bila shaka yatumika kwa watoto. Inahuzunisha wakati kijana afikiapo utu mzima akiwa si “asiye na shukrani” tu bali pia akiwa hawezi kushughulikia hata kazi rahisi kabisa za nyumbani.

Vijana katika nyakati za Biblia kwa kawaida waligawiwa kazi za kila siku za nyumbani. Kwa kielelezo, katika umri mchanga wa miaka 17, Yusufu mchanga alishiriki katika madaraka ya kutunza mifugo ya familia. (Mwanzo 37:2) Huu haukuwa mgawo mdogo kwani, mifugo ya baba yake ilikuwa mingi sana. (Mwanzo 32:13-15) Kwa kufikiria uhakika wa kwamba Yusufu alikua akawa kiongozi mwenye nguvu, yawezekana kuwa mazoezi yake ya mapema yalikuwa na sehemu kubwa katika kufanyiza tabia yake kwa njia chanya. Mfalme wa baadaye wa Israeli Daudi vilevile alipewa mifugo ya familia yake ili awatunze akiwa angali kijana.—1 Samweli 16:11.

Somo ni nini kwa wazazi leo? Wagawieni watoto wenu migawo ya kazi za kila siku za nyumbani zenye umaana. Kwa wakati, nishati, na subira, waweza kuwafunza wachanga kushiriki kusafisha, kupika, kutunza uwanja, na kurekebisha nyumba na gari. Ni kweli kuwa mengi yategemea umri na uwezo wa mtoto. Lakini hata watoto wadogo waweza kuwa na sehemu katika ‘kumsaidia Baba kurekebisha gari’ au katika ‘kumsaidia Mama kupika chakula.’

Kufunza kazi za kawaida za nyumbani pia kwahitaji wazazi wawape watoto zawadi ya thamani sana—wakati wao. Wenzi fulani waliooana, wazazi wa watoto wawili, waliulizwa siri ya kufaulu kuwazoeza watoto. Walijibu: “Wakati, wakati, wakati!”

Rekebisho Lenye Upendo

Watoto wafanyapo kazi yao vizuri, au angalau wawekapo jitihada kuifanya, watie moyo kwa sifa zenye ukarimu na za moyo mweupe! (Linganisha Mathayo 25:21.) Bila shaka, ni nadra kwa watoto kufanya mambo kwa uhodari wa watu wazima. Na wakati watoto wakubaliwapo kufanya maamuzi yao wenyewe, mara nyingi wao watafanya makosa. Lakini jihadhari usitende kupita kiasi! Je, hujafanya makosa ukiwa mtu mzima? Kwa hiyo, kwa nini usionyeshe subira mtoto wako akoseapo? (Linganisha Zaburi 103:13.) Acha nafasi kwa ajili ya makosa. Yaone kama sehemu ya hatua za kujifunza.

Watungaji Michael Schulman na Eva Mekler waonelea: “Watoto wanaotendewa kwa njia yenye urafiki hawaogopi kuwa wataadhibiwa kwa kufanya tendo la kujisimamia wenyewe.” Hata hivyo, “watoto walio na wazazi wasio na shauku au walio wakali wanaogopa kufanya tendo lolote la kujianzia, kutia ndani yawezayo kusaidia, kwa kuogopa kuwa wazazi wao watapata kosa katika yale ambayo wamefanya na kuwachambua au kuwaadhibu.” Elezo hili lapatana na onyo la Biblia kwa wazazi: “Msiwe mkichochea watoto wenu wakasirike, ili wasishuke moyo.” (Wakolosai 3:21) Kwa hiyo wakati jitihada za mtoto hazifikii yaliyotarajiwa, kwa nini usimsifu kwa kuwa angalau alijaribu? Mtie moyo afanye vizuri zaidi wakati ujao. Mwache ajue kwamba maendeleo yake yanakuletea furaha. Mhakikishie upendo wako.

Bila shaka, wakati mwingine rekebisho lahitajika. Hili laweza kuwa wazi hasa katika miaka ya ubalehe, wakati ambapo vijana hupigania utambulisho wao, ili wakubalike wakiwa watu binafsi walio na haki zao. Wazazi wanakuwa wenye hekima waonapo jitihada hizo kwa uelewevu badala ya kila mara kuzifasiri kuwa uasi.

Kweli, vijana wana mwelekeo wa kufanya mambo kwa msukumo au kujiruhusu kuathiriwa na “tamaa zenye kutukia ujanani.” (2 Timotheo 2:22) Kwa hiyo kukosa kuwekea mipaka tabia ya kijana kwaweza kumharibu mtoto kihisia-moyo; atakosa kujifunza kujidhibiti na hatakuwa na nidhamu ya kibinafsi. Biblia yaonya: “Mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye.” (Mithali 29:15) Lakini nidhamu inayofaa, ikitolewa kwa upendo, ni yenye manufaa na humtayarisha kijana kwa ajili ya madai na misongo ya utu mzima. Biblia yahimiza hivi: “Yeye asiyetumia fimbo yake humchukia mwanawe; bali yeye ampendaye humrudi mapema.” (Mithali 13:24) Hata hivyo, kumbuka kwamba, kiini cha nidhamu ni kufunza na kuzoeza—si kuadhibu. Hapa “fimbo” yaelekea yarejezea fimbo iliyotumiwa na wachungaji kuwaelekeza mifugo yao. (Zaburi 23:4) Ni ishara ya mwongozo wenye upendo—si unyama wenye kudhulumu.

Elimu kwa Ajili ya Uhai

Mwongozo wa wazazi wahitajika hasa elimu ya mtoto inapohusika. Pendezwa na elimu ya mtoto wako. Msaidie kuchagua masomo ya shuleni yanayofaa na uchukue daraka la kuamua ikiwa elimu yoyote ya ziada itahitajika.a

Bila shaka, elimu ya maana zaidi ya zote ni elimu ya kiroho. (Isaya 54:13) Watoto watahitaji kanuni za kimungu ili kuokoka katika ulimwengu wa utu mzima. “Nguvu zao za ufahamu” lazima zizoezwe. (Waebrania 5:14) Wazazi waweza kufanya mengi ili kuwasaidia watoto wao katika hili. Familia miongoni mwa Mashahidi wa Yehova zinatiwa moyo kuwa na funzo la Biblia la kawaida pamoja na watoto wao. Wakifuata kielelezo cha mama ya Timotheo, ambaye alimfunza Maandiko tangu utoto mchanga sana, wazazi Mashahidi vivyo hivyo huwafunza watoto wao wadogo.

Mzazi aliye pekee aitwaye Barbara hufanya funzo la familia la Biblia kuwa pindi yenye kupendeza zaidi kwa watoto wake. “Jioni hiyo nahakikisha kuwa nawapa watoto chakula kizuri, kamili na kitindamlo wanachofurahia. Nacheza kanda za Kingdom Melodies ili kufanyiza mandhari nzuri. Kisha, baada ya kufungua kwa sala, kwa kawaida sisi hujifunza gazeti Mnara wa Mlinzi. Lakini kukiwa na uhitaji maalumu, naweza kutumia vichapo kama vile Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi.”b Kulingana na Barbara, kujifunza Biblia huwasaidia watoto wake “kupata maoni ya Yehova kuhusu mambo.”

Ndiyo, hakuna zawadi kubwa kuliko ujuzi na uelewevu wa Neno la Mungu Biblia, ambayo mtoto aweza kupewa. Huo waweza kuwapa “wajinga werevu, na kijana maarifa na hadhari.” (Mithali 1:4) Hivyo, akiwa amejihami, kijana aingia utu mzima akiwa na uwezo wa kukabili misongo na hali mpya.

Hata hivyo, watoto wanapoondoka nyumbani, hilo husababisha badiliko kubwa katika mtindo-maisha wa wazazi wengi. Jinsi wawezavyo kukabiliana na kuondoka kwa watoto nyumbani kwazungumziwa katika makala yetu ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

a Ona ule mfululizo “Wazazi—Nyinyi Pia Mnayo Kazi ya Kufanya Nyumbani!” katika toleo la Amkeni! la Aprili 8, 1989.

b Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Watoto walio na wazazi wasio na shauku au walio wakali wanaogopa kufanya tendo lolote la kujianzishia, kutia ndani yawezayo kusaidia, kwa kuogopa kuwa wazazi wao watapata kosa katika yale ambayo wamefanya na kuwachambua au kuwaadhibu.”—Bringing Up a Moral Child, kilichoandikwa na Michael Schulman na Eva Mekler

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Wazazi Walio Pekee—Ule Ugumu wa Kuwaacha Waende

Mzazi aliye pekee aitwaye Rebecca aonelea: “Ni vigumu sana kwa wazazi walio pekee kuwaacha watoto wao waende. Ikiwa hatujiangalii, twaelekea kuwalinda kupita kiasi na kuzuia ukuzi wao wa utendaji.” Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia,c ukurasa wa 106-107 chatoa maoni haya yenye kusaidia:

“Ni jambo la asili kwa walio wazazi pekee kuwa karibu hasa na watoto wao, hata hivyo lazima kuwe na uangalifu kwamba mipaka iliyowekwa na Mungu kati ya wazazi na watoto hairukwi. Kwa kielelezo, magumu mazito yaweza kutokea ikiwa mama aliye mzazi pekee amtazamia mwana wake kuchukua madaraka ya kichwa cha nyumba au amtendea binti yake kama msiri wake, akimlemeza huyo msichana na matatizo ya kindani. Kufanya hivyo hakufai, kunaleta mkazo, na labda kumtatanisha mtoto. “Hakikishia watoto wako kwamba wewe, ukiwa mzazi, utawatunza—si wao wakutunze. (Linganisha 2 Wakorintho 12:14.) Nyakati nyingine, huenda ukahitaji shauri au tegemezo fulani. Utafute kutoka kwa wazee Wakristo au labda kutoka kwa wanawake Wakristo walio wakomavu, si kutoka kwa watoto wako wadogo.—Tito 2:3.” Wazazi walio pekee wawekapo mipaka inayofaa na kudumisha uhusiano mzuri kati yao na watoto wao, kwa kawaida inakuwa rahisi kuwaacha waende.

[Maelezo ya Chini]

c Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mazoezi yenye kutumika yaweza kuwasaidia watoto wawe watu wazima wenye madaraka zaidi

[Picha katika ukurasa wa 8]

Funzo la Biblia la familia laweza kuwapa watoto hekima inayohitajika ili kukabiliana na maisha ya utu mzima

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki