Maoni ya Biblia
Je, Biblia Inapinga Elimu?
“Ni watu wasio na ujuzi tu ndio hudharau elimu.”—Publilius Syrus, Moral Sayings, karne ya kwanza K.W.K.
BIBLIA hutusihi ‘tushike hekima kamili na busara.’ (Mithali 3:21) Yehova Mungu wa ujuzi, anataka waabudu wake wawe watu walioelimishwa. (1 Samweli 2:3; Mithali 1:5, 22) Lakini, taarifa fulani katika Biblia zaweza kuzusha maswali. Kwa kielelezo, akirejezea kwenye ufuatiaji wake wa hapo zamani, kutia na elimu yake ya juu, mtume Paulo aliandika: “Naiona kuwa kama takataka tu.” (Wafilipi 3:3-8, Today’s English Version) Katika barua nyingine yenye kupuliziwa, alisisitiza: “Hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu kwa Mungu.”—1 Wakorintho 3:19.
Basi je, Biblia, hupinga elimu? Mkristo apaswa kufikia kiwango gani katika kufuatia elimu ya kilimwengu? Je, elimu ya chini zaidi inayotakwa na sheria yatosha, au elimu ya ziada yapasa kufuatiwa?
Elimu Katika Karne ya Kwanza
Miongoni mwa Wakristo wa karne ya kwanza, kulikuwako namna nyingi za malezi ya kielimu. Watu fulani mashuhuri waliwaona mitume Wagalilaya Petro na Yohana kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Matendo 4:5, 6, 13) Je, hii ilimaanisha kwamba wanaume hawa wawili walikuwa hawajui kusoma na kuandika au hawakuwa na elimu? La. Kwa wazi ilimaanisha kwamba elimu yao haikuwa kutoka shule za Kiebrania za elimu ya chuo kikuu katika Yerusalemu. Maandishi ya watetezi hawa wawili walio jasiri wa Ukristo baadaye yalithibitisha uhakika wa kwamba walikuwa wamesoma vizuri, walikuwa wanaume wenye akili, wenye uwezo wa kufafanua Maandiko waziwazi. Elimu yao ilitia ndani maagizo yenye kutumika katika kushughulikia mahitaji ya kimwili ya familia zao. Wao walikuwa wenzi katika ile iliyokuwa kwa wazi biashara yenye faida ya uvuvi.—Marko 1:16-21; Luka 5:7, 10.
Kwa kutofautisha, Luka, mwanafunzi aliyeandika moja ya Gospeli vilevile kitabu cha Matendo, alipokea elimu ya hali ya juu zaidi. Alikuwa tabibu. (Wakolosai 4:14) Malezi yake ya kitiba hutoa namna ya uandishi iliyo tofauti kwa maandishi yake yenye kupuliziwa.—Ona Luka 4:38; 5:12; Matendo 28:8.
Kabla hajawa Mkristo, mtume Paulo aliagizwa katika sheria ya Kiyahudi, chini ya ukufunzi wa msomi mojawapo mwenye akili sana wa wakati huo, Gamalieli. (Matendo 22:3) Elimu ya Paulo yaweza kulinganishwa na elimu ya chuo kikuu leo. Zaidi, katika jamii ya Wayahudi lilifikiriwa kuwa jambo lenye kuheshimika kwa wachanga kujifunza kazi, hata wakati elimu ya chuo kikuu ilipofuatiwa katika miaka ya baadaye. Kwa wazi Paulo alipokea mazoezi akiwa mtengeneza-hema alipokuwa mvulana mchanga. Stadi za namna hiyo zilimwezesha ajitegemeze katika huduma yake ya wakati wote.
Hata hivyo, Paulo alitambua kwamba kwa kuhusianishwa na thamani yenye kuzidi ya ujuzi wa Mungu, elimu ya kilimwengu—ijapokuwa ni ya lazima—ni yenye thamani ndogo. Kulingana na hayo, Biblia hukazia umaana zaidi katika kujipatia ujuzi juu ya Mungu na Kristo. Wakristo hufanya vema leo kujitwalia maoni haya yaliyosawazika juu ya elimu ya kilimwengu.—Mithali 2:1-5; Yohana 17:3; Wakolosai 2:3.
Kuchunguza kwa Uangalifu Jambo Hili
Wakristo fulani wamepata kwamba kufuatia elimu ya ziada, kwa njia ya kitaaluma ama mafunzo ya weledi, kumewasaidia kutunza mahitaji ya kimwili ya familia zao. Kutunza mahitaji ya familia ya mtu ni jambo linalofaa, kwa kuwa ‘kuandalia wale walio wake mwenyewe’ ni wajibu mtakatifu. (1 Timotheo 5:8) Kupata stadi zinazohitajiwa ili kufanya hivi ni jambo linaloonyesha hekima itumikayo.
Hata hivyo, wale wanaohisi uhitaji wa kujipatia elimu zaidi ile ya msingi ili kutimiza lengo hili wapaswa kupima manufaa na madhara. Manufaa yawezekanayo hutia ndani kutayarishwa ili kupata kazi ambayo itawezesha mtu ajitegemeze mwenyewe na familia vya kutosha huku akiendelea kwa bidii kufuatia utumishi wa Kikristo. Kwa kuongezea, huenda akaweza kusaidia wengine kwa njia ya kimwili, ‘akiwa na kitu fulani cha kugawa kwa mtu aliye katika uhitaji.’—Waefeso 4:28.
Ni nini baadhi ya madhara? Haya yangeweza kutia ndani kupata mafundisho yanayomomonyoa imani katika Mungu na katika Biblia. Paulo aliwashauri Wakristo wawe wenye hadhari juu ya “yenye kuitwa ‘ujuzi’ isivyo kweli” na “falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu.” (1 Timotheo 6:20, 21; Wakolosai 2:8) Bila kukana, kupata namna fulani za elimu kwaweza kudhuru imani ya Mkristo. Wale wanaofikiria mazoezi ya ziada au mafunzo wapaswa kujua hatari ya mavutano ya namna hiyo yenye madhara.
Musa, ambaye ‘alifunzwa katika hekima yote ya Wamisri,’ alidumisha imani yenye nguvu licha ya kupokea elimu ambayo bila shaka ilitia ndani ibada ya miungu mingi, mafundisho yenye kumshushia Mungu staha. (Matendo 7:22) Hivyohivyo, Wakristo leo ni waangalifu wasije wakashindwa na mavutano yasiyofaa katika mazingira yoyote wanayojipata ndani yake.
Hatari nyingine iwezekanayo katika kufuatia elimu ya ziada ni kwamba ujuzi hututumuka, au hutokeza majivuno. (1 Wakorintho 8:1) Wengi hutafuta ujuzi kupitia elimu kwa sababu za kibinafsi, na hata ufuatiaji wa elimu wa moyo mweupe ungeweza kutokeza hisia za ubora na umashuhuri wa kibinafsi. Mitazamo ya namna hiyo haimpendezi Mungu.—Mithali 8:13.
Fikiria Mafarisayo. Washiriki wa farakano hili la kidini lililokuwa mashuhuri walionea fahari maarifa yao na uadilifu wa kudhania. Walikuwa wamesoma sana mkusanyo mkubwa wa mapokeo ya kirabi, na waliwadharau watu wa kawaida, ambao hawakuwa wamesoma sana, wakiwaona kuwa wasio na ujuzi, wa kudharaulika, hata waliolaaniwa. (Yohana 7:49) Mbali na hili, walipenda pesa. (Luka 16:14) Vielelezo vyao vyaonyesha kwamba inapofuatiwa kwa nia mbaya, elimu inaweza kumfanya mtu awe mwenye kiburi au imwongoze awe mwenye kupenda pesa. Kwa hiyo, katika kuamua aina na kiwango cha elimu kitakachofuatiwa, Mkristo angefanya vema kujiuliza, ‘Nia zangu ni gani?’
Jambo la Uchaguzi wa Kibinafsi
Kama ilivyokuwa kweli katika karne ya kwanza, kuna namna nyingi sana za malezi ya kielimu miongoni mwa Wakristo leo. Chini ya mwongozo wa wazazi wao, vijana wachanga wanaomaliza elimu yao ya lazima wanaweza kuchagua kufuatia elimu ya kilimwengu ya ziada. Hivyohivyo, watu wazima wanaopendezwa kuboresha njia zao za kuandalia familia zao wanaweza kuona elimu hiyo ya ziada kuwa njia iwezekanayo ya kufikia lengo hilo.a Pande nyingine za elimu ya kitaaluma na ya kidesturi hukazia kusitawisha uwezo wa akili wa kawaida badala ya stadi za kitaaluma au za weledi. Hivyo, mtu anaweza kupata kwamba hata baada ya kutenga kando wakati katika kujipatia elimu ya namna hiyo, anakosa stadi zinazohitajiwa ili kupata kazi. Kwa sababu hii, wengine huchagua kufuatia mafunzo katika programu za weledi au shule za ufundi, kwa kusudi la kujazia kwa utayari nafasi halisi za kazi.
Kwa vyovyote vile, maamuzi kama hayo ni ya aina ya kibinafsi. Wakristo hawapaswi kukosoa au kuhukumu mtu na mwenzake juu ya jambo hili. Yakobo aliandika: “Wewe ni nani uwe ukihukumu jirani yako?” (Yakobo 4:12) Ikiwa Mkristo anafikiria kufuatia shule ya ziada, atafanya vema kuchunguza nia zake mwenyewe ili kuhakikisha kwamba mapendezi ya kichoyo, ya kufuatia vitu vya kimwili si ndiyo kani inayomsukuma kufanya hivyo.
Inaonekana kwamba Biblia hutia moyo maoni yaliyosawazika kuelekea elimu. Wazazi Wakristo hutambua thamani yenye kuzidi ya elimu ya kiroho yenye kutegemea Neno la Mungu lililopuliziwa na hutoa shauri lililosawazika kwa watoto wao kuhusu elimu ya ziada. (2 Timotheo 3:16) Wakiwa wanaona maisha kwa njia halisi, wanakiri thamani ya elimu ya kilimwengu katika kujipatia stadi zilizo za lazima kwa ajili ya watoto wao waliokua ili kujiandalia wao wenyewe na familia zao za wakati ujao. Kwa hiyo, katika kuhakikisha kama elimu ya ziada itafuatiwa, na kwa kiwango gani, kila Mkristo anaweza kufanya maamuzi timamu ya kibinafsi yenye kutegemea ujitoaji kwa Yehova Mungu, ambao ni “wenye manufaa kwa mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja.”—1 Timotheo 4:8.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari kamili kuhusu somo hili, ona Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1992, ukurasa wa 10-21, na broshua Elimu na Mashahidi wa Yehova, vyote viwili vimechapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Blabu katika ukurasa wa 20]
‘Tushike hekima kamili na busara.’—Mithali 3:21
[Blabu katika ukurasa wa 21]
Katika kufikiria ikiwa utafuatia elimu ya ziada, Mkristo angefanya vema kujiuliza, ‘Nia zangu ni gani?’