Elimu—Gharama Yake? Faida Yake
JE! UNGEPENDA watoto wako wawe na elimu nzuri? ‘Bila shaka,’ unasema. ‘Elimu nzuri inamtayarisha mtu kwa maisha bora. Mtu aliyeelimishwa ana faida nyingi zaidi ya mtu mwenye elimu ndogo.’ Hivi ni kweli. Wazazi Wakristo, pamoja na wengine, wanataka watoto wao wapate elimu bora iwezekanavyo.
Lakini “elimu bora iwezekanavyo” inatia nini? Mkristo anajua kwamba inatia masomo ya kidunia na ya kiroho. Elimu ya kiroho inaendelea maishani mwetu mwote, lakini elimu ya kawaida ya kidunia inapasa kuendelea kwa kadiri gani? Je! kijana Mkristo anapaswa kuridhika na elimu ya kidunia ya msingi? Au je, anapaswa kwenda kwenye chuo cha elimu au chuo kikuu? Hilo si ulizo rahisi kujibu, kwa sababu, ingawa elimu yote inaleta faida, vile-vile inagharimu kitu. Namna gani?
Elimu ya Msingi
Elimu huanza kabla mtoto hajaenda shuleni. Mzazi Mkristo mwenye hekima humzoeza mtoto tangu utotoni. Anapaswa kuzoezwa katika nini? Mtume Paulo alimkumbusha Timotheo kwamba yeye alikuwa amezoezwa “tangu utoto” ayajue “maandiko matakatifu,” sehemu ya Biblia iliyokuwapo wakati huo. (2 Timotheo 3:15) Kwa hiyo, wazazi wanaweza kuwafunza watoto wao juu ya Yehova Mungu, Yesu Kristo, umaana wa ufalme wa Mungu, na kweli nyingine za Biblia, watoto wanapokuwa wangali wachanga.
Iwapo mtoto mchanga aweza kujifunza mambo hayo, basi kwa wazi anaweza pia kuanza kujifunza kusoma na kuandika, na wazazi wenye hekima wanachukua wakati wa kufunza hayo pia. Kwa hiyo, elimu ya mtoto inapasa kuanza mapema.
Je! hiyo inagharimu cho chote? Inagharimu fedha chache sana, lakini inagharimu wakati na nishati (nguvu) zaidi. Hata hivyo, inastahili kabisa. Kwa kupewa elimu hiyo ya mapema, mtoto anaweza kusitawisha upendo wa kutoka moyoni kwa ajili ya Yehova na kusitawisha upesi ufundi wa msingi wa kujifunza.
Katika nchi nyingi serikali inatoa elimu ya kidunia ya msingi kwa watoto wanapokuwa wenye umri wa miaka kama sita. Hata ingawa elimu hiyo inalipiwa kwa sehemu kubwa kwa fedha za kodi, kwaweza kuwa gharama nyingine inayohusika. Uvutano ambao wazazi hawawezi kuuongoza unaanza kufanyiza namna ya kuwaza kwa mtoto. Kwa mara ya kwanza maishani mwake, mtoto huyo anatenganishwa na wazazi wake kwa saa kadha katika siku. Huenda akachangamana na watoto ambao bado hawajafunzwa inavyofaa njia za Kikristo, na, hivyo, lazima wazazi wake wawe na hakika kwamba yeye hasahau mazoezi yake ya kwanza.
Je! gharama hiyo inastahili? Wazazi wengi wanafikiri ndivyo ilivyo. Shuleni, watoto wanapata elimu nyingi katika sehemu mbalimbali za maarifa. Huenda pia wakaanza kujifunza ufundi ambao utakuwa na thamani maisha yao yote. Na, ingawa wanaishi nyumbani, wana nafasi ya kuonyesha upendo wao kwa Yehova wanapokuwa mbali na ulinzi wa wazazi wao.
Hata hivyo, kuna bei ambayo wazazi Wakristo wenye hekima hawataki kuilipa. Wao hawawakazi watoto wao wajifunze kwa bidii sana hata kwamba wawe hawana nishati (nguvu) au wakati mchache sana unaobaki, au wawe hawana kabisa, wa kujifunza “maandiko matakatifu” au kumtumikia Mungu. Kwa sababu gani? Kwa sababu, ingawa elimu ya kidunia ina thamani hasa, ni elimu tu yenye msingi wa “maandiko matakatifu” inayoweza kumfanya mtu ‘awe na hekima ya kumpa wokovu.’ (2 Timotheo 3:15) Ni nini ya maana zaidi: elimu ya kidunia inayomtayarisha mtu kwa ajili ya miaka michache ya maisha? au elimu inayomtayarisha mtu kwa ajili ya uzima wa milele?
Vyuo vya Elimu na Vyuo Vikuu
Katika nchi nyingi, baada ya kumaliza masomo ya shule ya msingi kwa kawaida vijana wanaendelea na masomo ya sekondari. Kufikia hapo wazazi wengi Wakristo, wakikumbuka jinsi Yesu alivyozoezwa awe seremala, wanawatia moyo watoto wao wapate mazoezi ya kazi fulani. (Marko 6:3) Wanajua kwamba wakati vijana hao watakapokuwa wakubwa, watakuwa na madaraka, na sasa ni wakati unaofaa wa kuanza kuwatayarisha kuyachukua madaraka hayo,—1 Timotheo 5:4, 8.
Wengine hutaka kujua kama wanapaswa kuwaelekeza watoto wao kwenye elimu ya chuo kikuu. Kwa sababu gani? Katika nchi yenye umaskini, elimu ya chuo kikuu huenda ikaonekana kuwa njia bora ya kufanikiwa. Huenda ikaonekana kuwa yenye kutoa ulinzi wa kifedha, na hata zaidi. Mwalimu mmoja Mnaigeria alisema: “Akina baba . . . wanataka watoto wao wawe madaktari wa tiba, wahandisi, wachora ramani za majengo, wahasibu ili wainue cheo cha jamaa zao katika ujamii.”
Hata hivyo, je, hayo ndiyo mambo ambayo mzazi Mkristo anapaswa kuweka kwanza anapofanya mipango ya elimu ya mtoto wake? Wazazi wengi wanafikiri sivyo. Wanapendelea kutafuta njia nyinginezo za kuwatayarisha watoto wao kwa ajili ya maisha. Kwa sababu gani? Kwa sababu faida za elimu ya chuo kikuu mara nyingi hazistahili gharama.
Gharama
Gazeti Nigeria Daily Times lilisema hivi juu ya gharama ya kifedha: “Ujamii mwingi umejitoza kodi . . . nyingi sana; wazazi wamejinyima vitu vya anasa na nyakati nyingine bidhaa wanazohitaji sana, nao vijana walioajiriwa kazi wenye mapato wametumia sehemu kubwa za mapato yao, wote wakijitahidi kuhakikisha kwamba watoto wao, watoto wanaowatunza na wao wenyewe wanapata matunda ya elimu ya juu.”
Je! lingekuwa jambo la hekima kwa wazazi Wakristo kujinyima hivyo ili kuwapeleka watoto wao kwenye chuo kikuu? Pengine unaweza kuchukua gharama hiyo ya kifedha. Je! kuna bei nyingine inayopasa kufikiriwa? Mara nyingi, ni ndiyo. Kwa mfano, wazazi wa kijana mmoja walimruhusu asafiri mpaka Ulaya kwa masomo ya chuo kikuu. Je! masomo yake huko yalifanya awe na ulinzi wa kifedha, au kuinua cheo cha jamaa yake nyumbani? Hapana. Kwa kusihiwa na “marafiki” wake wapya kwenye chuo kikuu, yeye alitumia dawa za kulevya kupita kiasi akafa. Mwafrika mwingine kijana alikwenda kwenye chuo kikuu kimoja katika Marekani. Alirudishwa nyumbani ikiwa inaogopwa kwamba ubongo wake unavuja damu, kwa sababu ya matumizi ya dawa za kulevya na vileo. Wazazi wa wanaume hao vijana walilipa bei kubwa kama nini!
Wazazi wengine Wakristo wamelipa bei kubwa pia. Mwanamume mmoja kijana alijiandikisha katika chuo kikuu kimoja nchini mwao, lakini mbali na nyumbani. Yeye aliacha kushirikiana na Wakristo wenzake akaacha kumtumikia Yehova. Mambo yote aliyokuwa amejifunza “tangu utoto” aliyaacha, na sasa hata anatilia shaka mafundisho ya Biblia.
Inasikitisha kwamba mwanamume huyo kijana hayuko peke yake. Kuna wengine waliolelewa wamtumikie Mungu ambao sasa wanaamini mageuzi ya viumbe, wasioamini kuwapo kwa Mungu na wenye kuchambua kweli ya Biblia. Je! hiyo ni kwa sababu Biblia ina kosa na falsafa ya kisasa ni sahihi? Hata kidogo. Ni kwa sababu waliendelea kushambuliwa na mawazo yasiyo ya kimungu chuoni walipokuwa wametenganishwa na Wakristo wengine. Kwa hiyo imani yao ilidhoofika na mwishowe ikafa. Jambo la kusikitisha ni kwamba mara nyingi waliwekwa katika hali hiyo na wazazi wao.
“Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri,” ndivyo alivyosema mtume Paulo. (1 Wakorintho 15:33, NW) Baadhi ya mashirika mabaya zaidi kwa Mkristo—yaani, ya kiroho na kiadili—yamepatikana katika makao ya vyuo vikuu. Mambo yaliyotangulia kutajwa yanaonyesha yanayoweza kutendeka wakati vijana wasio na ujuzi, wakiwa mbali na jamaa zao, wanakuwa katika mazingira ya uasherati, dawa za kulevya au matumizi mabaya ya vileo, matendo mabaya, na mawazo ya kisiasa ya uasi. Je! heshima yenye kuongezeka ya jamaa au uwezekano wa kuwa na kazi yenye mapato makubwa zaidi inastahili bei ambayo huenda ikalipwa?
Maoni Yaliyosawazika
Lakini, huenda ikabishwa kwamba si kila mtu anayekwenda kwenye chuo kikuu anayepoteza imani yake ya Kikristo au kuuawa na matumizi ya kupita kiasi ya dawa za kulevya. Hiyo ni kweli. Wengine waliofuzu (waliohitimu) wamekuwa washiriki wa kundi la Kikristo wenye kuthaminiwa na wenye kufanya kazi kwa bidii. Lakini ebu fikiri, ni kweli pia kwamba si kila mtoto anayecheza kwenye barabara yenye motokaa nyingi atakayeuawa na motokaa yenye kupita. Wengine wanaokoka na kukua. Lakini je, ungewaruhusu watoto wako wacheze barabarani katikati ya motokaa kwa sababu hiyo?
Je! hiyo maana yake ni kwamba ni kosa kwenda kwenye masomo ya chuo kikuu? Hilo ni jambo ambalo kila mzazi anapaswa kuamulia mtoto wake mwenyewe. Hata hivyo, katika kufanya hivyo, anapaswa kufikiria mambo yaliyotangulia kutajwa. Huenda ikawa kwamba mwanafunzi huyo atakaa nyumbani na kwenda chuoni. Au pengine anaweza kukaa na watu wa ukoo ambao wataangalia sana ni nani marafiki wake na kumtia moyo sana aendelee kutimiza madaraka yake ya Kikristo. Lakini kwa kufikiria hali zote, je, wakati na jitihada itastahili? Je! kutamtayarisha vizuri zaidi amtumikie Mungu wake?
Wazazi wengi wana maoni kwamba faida zinazoweza kupatikana za elimu ya chuo kikuu hazistahili gharama za misiba mikubwa inayoweza kutokea, sana sana watoto wanapokwenda katika mji au nchi nyingine pasipo ulinzi. Badala yake, wanawaongoza watoto wao kwenye kazi fulani. Kwa mfano, anapokuwa katika shule ya sekondari, je, kuna mitaala fulani ya kazi mbalimbali inayoweza kumsaidia kijana ajifunze ufundi fulani ambao utamsaidia ajiruzuku akiisha kufuzu? Katika nchi nyingine kuna shule za kazi fulani-fulani zinazochukua muda wa mwaka mmoja ambako mtu anaweza kujifunza ufundi fulani, au ule ambao mtu alijifunza katika shule ya sekondari anaweza kuusitawisha zaidi.
Vilevile wazazi hao wamefikiria kwa uzito yale wanayotaka watoto wao wafanyie maisha yao. Je! wanataka waletee jamaa heshima? wawe tajiri: au kuweza kuwaangalia wazazi watakapozeeka? Kwa jamaa isiyo na imani ya Kikristo, miradi hiyo inafahamika. Lakini hakika Mkristo ana miradi bora zaidi.
Mtume Paulo alionya hivi: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu.” (1 Timotheo 6:9) Vilevile Yesu alionya hivi: “Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.” (Mathayo 6:24) Je! hukubali kwamba sababu moja wanafunzi wengi wa chuo kikuu wanapoteza imani yao ni kwamba wengi wao ‘wanatumikia mali,’ au ‘wanataka kuwa na mali’? Kwa kushindwa kutia moyoni shauri la Biblia kuhusu nia yao kuelekea mali, wanajifanya wenye kushambulika kwa urahisi na mawazo mengine yenye kuharibu imani na mwenendo.
Mtume Yohana alisema: “Dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.” (1 Yohana 2:17) Ikiwa unaamini hilo, basi utampa mtoto wako elimu ambayo kwanza kabisa itamtayarisha kufanya mapenzi ya Mungu. ‘Lakini,’ huenda wengine wakasema, ‘maisha leo ni magumu sana, na kijana—sana sana ikiwa anatoka kwenye hali ya umaskini—anahitaji msaada wote anaoweza kupata.’ Hiyo ni kweli. Lakini Mungu ametuahidi kwamba tukiweka ufalme wake kwanza maishani mwetu, tutaongezewa mambo yote mengine tunayohitaji. (Mathayo 6:33) Je! tunaweza kuomba msaada bora zaidi ya huo?
Mfalme Daudi, kabla hajawa mfalme, alilazimishwa kuishi akiwa mtoro jangwani. Kwa hiyo, yeye alijua maana ya kutokuwa na cho chote. Hata hivyo yeye alisema: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.” (Zaburi 37:25) Mungu anaweza kutusaidia sasa sawa na alivyoweza katika siku za Daudi ikiwa tunaweka kwanza ufalme wake maishani mwetu.
Hakika, basi, elimu bora zaidi tunayoweza kuwapa watoto wetu itakuwa ni usawazisho wa mafundisho ya kiroho na ya kidunia. Elimu ya kidunia ina thamani. Lakini ikiwa kuifuatia kunamaanisha kujinyima mambo ya kiroho, basi haistahili gharama hiyo. Kwa habari ya elimu ya watoto wetu, ni vema kufuata shauri la mtume Paulo: “Muda ubakio si mwingi; basi tokea sasa . . . wale wautumiao ulimwengu huu, [na wawe] kama hawautumii sana; kwa maana [tamasha] ya ulimwengu huu [inapita].”—1 Wakorintho 7:29-31.
Matokeo ya elimu iliyosawazika yanafurahisha wazazi wote. Watoto wanakuwa wenye imani yenye nguvu, wakimsifu Mungu na kuwaheshimu wazazi wao. Vijana wengi Wakristo, ambao wamelelewa katika njia hiyo, sasa wanatumikia wakiwa wahubiri wa wakati wote au wamisionari, na maisha zao zinaridhisha kweli kweli. Wazazi wao wanajivunia hao kama nini! Kwa kweli ‘wanamkumbuka Muumba wao siku za ujana wao,’ na kwa njia hiyo wanaonyesha imani yao Kwake, badala ya kuuonyesha imani ulimwengu huu.—Mhubiri 12:1.
Mfumo huu utakapokwisha hatimaye, vijana ambao wamepokea na kutwaa elimu ya kimungu iliyosawazika wataokoka, pamoja na wazazi wao wenye kumwogopa Mungu, ili wamtumikie Mungu milele. Je! hilo ndilo unalotakia mtoto wako? Basi msaidie apate elimu itakayomfaidi kwa umilele.—Yohana 17:3.
[Blabu katika ukurasa wa 20]
Je! faida zinazoweza kuletwa na elimu ya chuo kikuu zinastahili bei ambayo huenda ikalipwa?
[Blabu katika ukurasa wa 21]
Wazazi, mnatumaini watoto wenu watafanyia nini maisha zao?
[Blabu katika ukurasa wa 22]
Ikiwa kufuatia elimu ya kidunia kunamaanisha kujinyima mambo ya kiroho, basi haistahili gharama hiyo