Elimu Yenye Kusudi
“Mwelimishe mwenye hekima, naye atazidi kuwa na hekima.”—MITHALI 9:9.
1. Yehova hutazamia nini kwa watumishi wake kwa habari ya maarifa?
YEHOVA ni “Mungu wa maarifa.” (1 Samweli 2:3) Yeye huwaelimisha watumishi wake. Musa alitabiri kwamba vikundi vya watu vya wakati huo vingesema hivi juu ya Israeli: “Hakika taifa hili kubwa ni watu wenye hekima na akili.” (Kumbukumbu la Torati 4:6) Wakristo wa kweli wanapaswa vilevile wawe wenye maarifa. Wanahitaji kuwa wanafunzi bora zaidi wa Neno la Mungu. Akionyesha kusudi la funzo la jinsi hiyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Sisi . . . hatuachi kufanya maombi na dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni; mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana [Yehova, NW], mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu.”—Wakolosai 1:9, 10.
2. (a) Ni nini lililo la lazima ili kupata maarifa sahihi juu ya Mungu? (b) Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limeshughulikiaje jambo hilo?
2 Kujifunza ili kupata maarifa sahihi juu ya Mungu na makusudi yake hutaka angalau kiasi fulani cha elimu. Lakini watu wengi ambao wamekuja kujifunza kweli ya Neno la Mungu huishi katika nchi ambako walikuwa na nafasi ndogo sana au hawakuwa na yoyote ya kupokea elimu ya kilimwengu ifaayo. Walikuwa katika hali zisizofaa. Ili kushinda tatizo hilo, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limeagiza kwa miaka mingi sasa kwamba, inapohitajiwa, madarasa ya kufundisha kusoma na kuandika yapaswa kupangwa katika makundi. Zaidi ya miaka 30 iliyopita, gazeti la habari la Kibrazili Diário de Mogi lilitangaza kwa chapa makala yenye kichwa “Mashahidi wa Yehova Wapiga Vita Dhidi ya Kutoweza Kusoma na Kuandika.” Lilitaarifu hivi: “Mfunzi mwenye kustahili huanza . . . kwa saburi kuwafundisha wengine kusoma na kuandika. . . . Ni lazima wanafunzi, kwa sababu ya hali zenyewe zinazowasukuma wakiwa wahudumu wa Mungu, lazima wakuze maarifa yao ya lugha ili waweze kutoa hotuba.” Hivyo maelfu ya watu kotekote ulimwenguni wamewezeshwa wawe wanafunzi wazuri wa Neno la Mungu. Walipokea elimu hiyo ya msingi wakiwa na kusudi bora zaidi akilini.
Stadi Zinazohitajiwa Ili Kuwa Wahudumu Wenye Mafanikio
3, 4. (a) Kwa nini Wakristo wa kweli hupendezwa na elimu? (b) Hali ilikuwaje katika Israeli, na ni elimu gani ya msingi iliyo ya lazima katika makundi yetu leo?
3 Wakristo wa kweli hupendezwa na elimu, si kwa sababu wapate elimu tu, bali ili wawe watumishi wa Yehova wenye mafanikio zaidi. Kristo aliwapa Wakristo wote utume wa “kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimeamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20, NW) Ili kuwafundisha wengine, ni lazima wao wenyewe wajifunze kwanza, na hilo lataka njia nzuri za kujifunza. Ni lazima wawe na uwezo wa kuyachunguza Maandiko kwa uangalifu. (Matendo 17:11) Ili watimize utume wao, ni lazima pia waweze kusoma kwa ufasaha.—Ona Habakuki 2:2; 1 Timotheo 4:13.
4 Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, kuna sababu nzuri ya kuamini kwamba, kwa ujumla, hata vijana katika Israeli ya kale walijua jinsi ya kusoma na kuandika. (Waamuzi 8:14; Isaya 10:19) Wahudumu Wakristo leo wanahitaji kuandika habari nadhifu wanapotoa ushahidi nyumba kwa nyumba. Wao huandika barua, huandika habari kwenye mikutano, na huandika maelezo juu ya habari za funzo. Hayo yote yataka mwandiko uwezao kusomeka. Kuweka maandishi katika kundi la Kikristo kwahitaji angalau maarifa ya msingi ya hesabu.
Faida za Elimu Ifaayo
5. (a) Ni nini chanzo cha neno “shule”? (b) Wachanga wanapaswa wachukue nafasi gani?
5 Kwa kupendeza, neno “shule” (skuli) hutokana na neno la Kigiriki skho·leʹ, ambalo hapo kwanza lilimaanisha “wasaa” au utumizi wa wasaa ili kufanya utendaji wenye uzito, kama vile kujifunza. Baadaye likaja kumaanisha mahali ambapo kujifunza huko kulifanywa. Hilo laonyesha kwamba, wakati mmoja, ni ile jamii ya watu waliopendelewa tu—katika Ugiriki na mabara mengine mengi—ndiyo iliyokuwa na wasaa wa kujifunza. Jamii ya wafanyakazi kwa ujumla ilibaki bila maarifa. Leo, katika nchi zilizo nyingi watoto na vijana hupewa wakati wa kujifunza. Mashahidi vijana wapaswa kwa hakika kununua wakati ufaao ili wawe wenye maarifa na watumishi wa Yehova wenye uwezo.—Waefeso 5:15, 16.
6, 7. (a) Ni zipi baadhi ya faida za kusoma shuleni ifaavyo? (b) Kujifunza lugha ya kigeni kwaweza kuwa kwenye mafaa katika njia zipi? (c) Hali ikoje leo miongoni mwa vijana wengi wanapomaliza shule?
6 Maarifa ya msingi ya historia, jiografia, sayansi, na kadhalika yatawawezesha Mashahidi wachanga wawe wahudumu wenye maarifa ya ujumla. Kwenda kwao shule hakuta wafundisha masomo mengi tu bali pia utaratibu wa kujifunza. Wakristo wa kweli hawaachi kupata maarifa na kujifunza wanapoondoka shuleni. Hata hivyo, yale watakayopata kutokana na kujifunza kwao, yatategemea sana wao kujua jinsi ya kujifunza. Elimu ya kilimwengu na ya kundi pia yaweza kuwasaidia wakuze uwezo wao mbalimbali wa kufikiri. (Mithali 5:1, 2) Wanaposoma wataweza kutambua vema zaidi yaliyo ya maana, yanayostahili kuandikwa na kukumbukwa.
7 Kwa kielelezo, kujifunza lugha ya kigeni hakutakuza tu uwezo wa kiakili wa vijana bali pia kutawafanya wawe wenye kutumika zaidi katika tengenezo la Yehova. Katika baadhi ya matawi ya Watch Tower Society, hesabu fulani ya ndugu wachanga wameliona kuwa jambo lenye faida kuweza kusema au kusoma Kiingereza kwa ufasaha. Isitoshe, wahudumu wote Wakristo wanapaswa waweze kutamka vema lugha yao ya mama. Habari njema za Ufalme hustahili kutolewa katika njia dhahiri iliyo sahihi kisarufi. Mambo ya hakika huonyesha kwamba ulimwenguni leo vijana wengi wanapomaliza shule wangali wana tatizo la kuandika na kusema kwa usahihi na la kufanya hata hesabu zilizo rahisi zaidi; nao wana maarifa machache mno ya historia na jiografia.
Elimu ya Kutosha
8. Ni maandiko gani yanayohusu habari ya elimu ya kilimwengu na uwezo wa mtu wa kujitegemeza mwenyewe?
8 Kwa hiyo, huu unaonekana kuwa wakati ufaao wa kuzungumzia mtazamo wa Mkristo kuelekea elimu ya kilimwengu. Ni kanuni zipi za Biblia zinazohusu habari hiyo? Kwanza, katika nchi nyingi ujitiisho ufaao kwa “Kaisari” hutaka wazazi Wakristo wapeleke watoto wao shuleni. (Marko 12:17; Tito 3:1) Kwa habari ya Mashahidi wachanga, wanapaswa katika kazi yao ya shule wakumbuke, Wakolosai 3:23 linalotaarifu hivi: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa Bwana [Yehova, NW], wala si kwa wanadamu.” Kanuni ya pili inayohusika ni kwamba Wakristo wanapaswa waweze kujitegemeza wenyewe, hata ikiwa wao ni wahudumu mapainia wa wakati wote. (2 Wathesalonike 3:10-12) Ikiwa amefunga ndoa, mwanamume anapaswa aweze kuandalia ifaavyo mke na watoto wowote ambao huenda wakazaliwa, akiwa na ziada kidogo ya kuwapa wale wenye uhitaji na kutegemeza kazi ya kuhubiri ya mahali pao na ya ulimwenguni pote.—Waefeso 4:28; 1 Timotheo 5:8.
9, 10. (a) Mwelekeo waonekana kuwa nini katika mabara mengi? (b) Huenda mhudumu painia akafikiria ni nini ulio mshahara wa kutosha?
9 Mkristo mchanga anahitaji elimu ya kiasi gani ili astahi kanuni hizo za Biblia na kutimiza wajibu wake mbalimbali wa Kikristo? Hilo latofautiana kutoka nchi hadi nchi. Hata hivyo, kwa ujumla, yaonekana kwamba mwelekeo wa kawaida katika mabara mengi ni kwamba kiwango cha kwenda shule kinachohitajiwa ili kuchuma mshahara wa kadiri sasa ni cha juu zaidi ya vile ilivyokuwa miaka michache iliyopita. Ripoti zilizopokewa kutoka matawi ya Watch Tower Society katika sehemu tofauti-tofauti za ulimwengu zaonyesha kwamba katika mahali pengi ni vigumu kupata kazi zenye mishahara ya kadiri baada ya kukamilisha tu elimu ya chini zaidi inayotakwa na sheria au katika nchi fulani hata baada ya kumaliza sekondari au shule ya upili.
10 Ni nini kinachomaanishwa na “mishahara ya kadiri”? Haimaanishi kazi zenye malipo makubwa. Kamusi ya Kiswahili Sanifu hufasili “kadiri” katika muktadha huo kuwa “kiasi kinachofaa.” Kwa mfano, ni nini chaweza kuitwa “kiasi kinachofaa,” kwa wale wanaotamani kuwa wahudumu mapainia wa habari njema? Kwa ujumla wao huhitaji kazi ya muda-muda ili waepuke kuwa “mzigo” kwa ndugu zao au familia yao. (1 Wathesalonike 2:9, Habari Njema kwa Watu Wote) Mishahara yao yaweza ikasemwa kuwa “kiasi kinachofaa,” au “yenye kuridhisha,” ikiwa kile wanachochuma chawaruhusu waishi maisha ya kadiri kikiwaachia wakati na nguvu za kutosha kuweza kutimiza huduma yao ya Kikristo.
11. Kwa nini vijana wengine wameacha utumishi wa painia, na ni swali gani linalotokezwa?
11 Hali ikoje mara nyingi leo? Imeripotiwa kwamba katika nchi fulani vijana wengi wenye makusudio mazuri wameacha shule baada ya kukamilisha elimu ya chini zaidi inayotakwa ili wawe mapainia. Hawakuwa na ufundi au stadi za kilimwengu. Ikiwa hawakusaidiwa na wazazi wao, walihitaji kutafuta kazi ya muda-muda. Baadhi yao wamelazimika kukubali kazi iliyowataka wafanye kazi ya saa nyingi sana ili wajiruzuku. Kwa sababu ya kuwa wenye kuchoka sana kimwili, waliiacha huduma ya painia. Watu hao wanaweza kufanya nini ili wajitegemeze wenyewe na kurudia utumishi wa painia?
Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu Elimu
12. (a) Kwa habari ya elimu, Mkristo ataepuka maoni gani mawili yenye kupita kiasi? (b) Kwa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu na watoto wao, elimu yapaswa itimize kusudi gani?
12 Maoni yenye usawaziko kuhusu elimu yaweza kusaidia. Kwa vijana wengi wa ulimwengu, elimu ni ishara ya cheo jambo la kuwasaidia wapande cheo katika jamii, ufunguo wa mtindo-maisha wenye ufanisi, wa kufuatia vitu vya kimwili. Kwa wengine, elimu ni kazi ngumu ipaswayo kumalizwa haraka iwezekanavyo. Hakuna lolote la maoni hayo linalofaa Wakristo wa kweli. Kwa hiyo, ni nini yawezayo kuitwa “maoni yenye usawaziko”? Wakristo wanapaswa waone elimu kuwa njia ya kutimiza kusudi fulani. Katika siku hizi za mwisho, kusudi lao ni kumtumikia Yehova kwa kadiri kubwa na kwa mafanikio zaidi iwezekanavyo. Ikiwa, katika nchi wanamoishi, elimu ya chini zaidi au hata ya shule ya upili itawawezesha tu wapate kazi zitakazoandaa mapato yasiyotosha kuwategemeza wenyewe wakiwa mapainia, basi elimu au mazoezi ya ziada yaweza kufikiriwa. Hilo lingefanywa kukiwa na mradi mahususi wa utumishi wa wakati wote.
13. (a) Dada mmoja katika Ufilipino amewezaje kuendelea na utumishi wake wa painia huku akitimiza wajibu wake mbalimbali wa familia? (b) Ni onyo gani lililo la wakati wake?
13 Wengine wamefanya mitaala ya mazoezi ambayo imewapa nafasi za kazi zinazowawezesha washiriki katika utumishi wa wakati wote au waanze tena. Dada mmoja katika Ufilipino alikuwa ndiye mleta riziki wa familia, lakini alitaka kupainia. Tawi laripoti hivi: “Ameweza kufanya hivyo kwa sababu amepokea elimu ya ziada ili akastahili kuwa mhasibu mwenye cheti cha kisheria.” Ripoti hiyohiyo ya tawi ilitaarifu hivi: “Tuna wengi sana wanaojifunza shuleni na wakati huohuo wameweza kupanga ratiba zao kuweza kupainia. Kwa ujumla wao huwa wahubiri bora zaidi kwani wao ni wenye bidii ya kujifunza, maadamu hawawi wenye kufuatia mno mambo ya kilimwengu.” Maneno hayo ya mwisho yanapaswa yatupe sababu ya kufikiri. Kusudi la elimu ya ziada, mahali inapoonekana kuwa ya lazima, halipaswi kusahauliwa au kubadilishwa kuwa mradi wa kufuatia vitu vya kimwili.
14, 15. (a) Kwa nini kanuni zilizokazwa zisizonyumbuka hazipaswi kuwekwa kwa habari ya elimu? (b) Ndugu fulani wenye madaraka walipokea elimu gani ya kilimwengu, lakini ni nini limesawazisha hilo?
14 Katika nchi chache, shule za sekondari huandaa mazoezi ya kazi mbalimbali ambayo yaweza kumtayarisha Mkristo mchanga kwa ajili ya ufundi au kazi fulani ifikiapo wakati wa kuhitimu. Hata hali isipokuwa hivyo, katika mabara fulani vijana wenye kujikakamia waliopata masomo ya shuleni ya msingi tu hupata kazi ya muda-muda inayowawezesha wachume pesa za kutosha kuwawezesha kupainia. Kwa hiyo kanuni zilizokazwa zisizonyumbuka hazipaswi kuwekwa ama kuunga mkono ama kupinga elimu ya ziada.
15 Wengi wanaotumika sasa katika vyeo vyenye madaraka wakiwa waangalizi wasafirio, kwenye makao makuu ya Sosaiti, au katika mojapo matawi walikuwa na elimu ya msingi tu. Walikuwa mapainia waaminifu, hawakuacha kamwe kujifunza, walipokea mazoezi, na wamekabidhiwa madaraka makubwa zaidi. Hawajuti hata kidogo. Kwa upande ule mwingine, baadhi ya wale wa rika lao walichagua kupata elimu ya chuo kikuu wakaangukia njiani, wakiwa wamefanywa watumwa wa falsafa zenye kuharibu imani na “hekima ya dunia hii.”—1 Wakorintho 1:19-21; 3:19, 20; Wakolosai 2:8.
Kuhesabu Bei
16. (a) Ni nani anayeamua kama elimu ya ziada inatamanika, na ni nini linalopaswa kufikiriwa zaidi? (b) Ni nini kipaswacho kufikiriwa?
16 Ni nani anayeamua kama Mkristo mchanga apaswa kupata elimu au mazoezi ya ziada? Hapa kanuni ya ukichwa ya Biblia yaingia. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 6:1) Kwa msingi huo kwa hakika wazazi watataka kuwaongoza watoto wao katika chaguo la ufundi au kazi na kwa hiyo katika kiasi cha elimu kitakachohitajiwa. Katika nchi nyingi machaguo ya kielimu na ya kikazi yanapaswa yafanywe mapema zaidi wakati wa elimu ya sekondari. Huo ndio wakati ambao wazazi na vijana Wakristo wanahitaji kutafuta mwelekezo wa Yehova katika kufanya chaguo lenye hekima, wafikiria zaidi masilahi ya Ufalme. Vijana wana mapendezi na uwezo mbalimbali wa kujifunza. Wazazi wenye hekima watafikiria mambo hayo. Kazi yote yenye kufuatia haki ni yenye kuheshimika, iwe ya mikono au ya ofisini. Ingawa huenda ulimwengu ukaona kazi ya ofisini kuwa bora zaidi na kudharau mtu kufanya kazi ngumu kwa mikono, Biblia haifanyi hivyo. (Matendo 18:3) Kwa hiyo wazazi na vijana Wakristo leo, wanapoamua kukubali au kukataa mafunzo ya baada ya shule ya sekondari, baada ya kupima manufaa na hasara zayo kwa uangalifu na kwa sala, wengine kundini hawapaswi kuwachambua.
17. Wazazi wengine Mashahidi huwafanyia watoto wao chaguo gani?
17 Wazazi Wakristo wakiamua kwa utimamu kuwaandalia watoto wao elimu ya ziada baada ya shule ya upili, hiyo ni haki yao. Kipindi cha mafunzo hayo kinatofautiana kulingana na aina ya ufundi au kazi iliyochaguliwa. Kwa sababu za kifedha na ili kuwawezesha watoto wao waingie utumishi wa wakati wote haraka iwezekanavyo, wazazi wengi Wakristo wamewachagulia programu fupi za mafunzo katika shule za kujifunzia kazi au ufundi. Katika visa fulani vijana wamehitaji kuwa wanagenzi (kufundishwa) ufundi fulani wanapofanya kazi lakini sikuzote wakiwa na mradi wa maisha yaliyojaa ya utumishi kwa Yehova.
18. Mitaala ya ziada ikichukuliwa, ni nini lipaswalo kukumbukwa?
18 Ikiwa mitaala ya ziada inachukuliwa, kwa hakika kusudio halipaswi kuwa kutukuka kitaalamu au kujitengenezea kazi-maisha ya kilimwengu yenye fahari. Mitaala yapaswa ichaguliwe kwa uangalifu. Gazeti hili limekazia hatari za kisomo cha juu zaidi, na limefanya hivyo kwa haki, kwa kuwa elimu nyingi ya juu zaidi hupinga “mafundisho yenye afya” ya Biblia. (Tito 2:1, NW; 1 Timotheo 6:20, 21) Zaidi ya hayo, tangu miaka ya 1960, shule nyingi za kisomo cha juu zaidi zimekuwa mazingira yanayokuza ukosefu wa sheria na ukosefu wa maadili. “Mtumwa mwaminifu mwenye akili” amepinga kwa nguvu kuingia mazingira ya aina hiyo. (Mathayo 24:12, 45) Hata hivyo, lazima ikiriwe kwamba siku hizi vijana hukabili hatari zizo hizo katika shule za upili na vyuo vya kujifunzia ufundi na hata kazini.—1 Yohana 5:19.a
19. (a) Wale wanaoamua kuchukua mitaala ya ziada wanapaswa kuchukua hadhari jinsi gani? (b) Wengine wametumiaje elimu yao kwa faida nzuri?
19 Iwapo uamuzi ni elimu ya ziada, Shahidi mchanga angefanya vema, ikiwezekana, kuipokea akiwa bado anaishi nyumbani, hivyo aweze kudumisha tabia za Kikristo za kawaida za kujifunza, kuhudhuria mikutano, na utendaji wa kuhubiri. Tangu mwanzoni msimamo ufaao wapaswa pia uchukuliwe kuhusu kanuni za Biblia. Yapaswa ikumbukwe kwamba Danieli na Waebrania wenzake watatu walikuwa watekwa uhamishoni walipolazimishwa kupokea mafunzo ya juu zaidi katika Babuloni, lakini waliendelea kudumisha uaminifu-maadili wao. (Danieli, sura 1) Wakiwa wanaweka masilahi ya kiroho kwanza, Mashahidi wachanga katika nchi kadhaa wamechukua mitaala ili wajitayarishe wenyewe kwa ajili ya kazi ya muda-muda wakiwa wahasibu, mafundi, walimu, watafsiri, wakalimani au katika kazi nyinginezo zilizowategemeza vya kutosha katika kazi-maisha yao ya msingi ya kupainia. (Mathayo 6:33) Baadhi ya vijana hao baadaye wamekuwa waangalizi wasafirio au wafanyakazi wa hiari wa Betheli.
Watu Wenye Umoja, Walioelimishwa
20. Ni tofauti gani ya kilimwengu isiyo na nafasi miongoni mwa watu wa Yehova?
20 Miongoni mwa watu wa Yehova, iwe kazi ya mtu ni ya ofisini, ya mikono, ya ukulima, au ya utumishi mbalimbali, wote wanahitaji kuwa wanafunzi wazuri wa Biblia na walimu wenye uwezo. Stadi zinazopatwa na wote katika kusoma, kujifunza, na kufundisha zaelekea kuondosha ile tofauti ambayo ulimwengu hufanya kati ya wafanyakazi wa mkono na wa ofisini. Hilo latokeza kuwe umoja na staha kwa mmoja na mwenzake ambayo huonekana hasa miongoni mwa wafanyakazi wa hiari katika makao ya Betheli na sehemu za ujenzi za Watch Tower Society, ambako sifa za kiroho ni za maana zaidi na zahitajiwa na wote. Huko, wafanyakazi wa ofisi wenye ujuzi hufanya kazi kwa shangwe pamoja na wafanyakazi wa mkono wenye ustadi, wote wakionyeshana upendo wenye uthamini.—Yohana 13:34, 35; Wafilipi 2:1-4.
21. Lengo la Wakristo wachanga lapaswa kuwa nini?
21 Wazazi, ongozeni watoto wenu kuelekea mradi wa kuwa washiriki wenye mafaa wa sosaiti ya ulimwengu mpya! Wakristo wachanga, tumieni nafasi zenu za kupata elimu kuwa njia ya kuwatayarisha kushikilia kwa ukamili zaidi mapendeleo yenu katika kumtumikia Yehova! Mkiwa waliofundishwa, nyinyi nyote na mthibithike kuwa washiriki waliotayarishwa vema wa sosaiti ya kitheokrasi sasa na kwa umilele pia katika “dunia mpya” iliyoahidiwa na Mungu.—2 Petro 3:13; Isaya 50:4; 54:13; 1 Wakorintho 2:13.
[Maelezo ya Chini]
Tahini Kumbukumbu Yako
◻ Kwa nini Wakristo wa kweli wanapendezwa na elimu?
◻ Wakristo wa kweli wanapaswa waepuke maoni gani yenye kupita kiasi kuhusu elimu?
◻ Ni hatari zipi za elimu ya ziada zinazopasa kufikiriwa, na ni hadhari zipi zinazohitaji kuchukuliwa?
◻ Ni tofauti gani ya kilimwengu isiyo na mahali miongoni mwa watu wa Yehova?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Kwa kujifunza kwa bidii-nyendelevu, Wakristo wachanga wanaweza kuwa washiriki wenye mafaa zaidi wa sosaiti wa ulimwengu mpya
[Picha katika ukurasa wa 19]
Elimu ya ziada, ikichaguliwa, yapasa ichochewe na tamaa ya kumtumikia Yehova vizuri zaidi