Vijana Huuliza . . .
Namna Gani Asiponipenda?
“Nina wasiwasi na nataabika. Nimempenda. Lakini sijui kama ananipenda. Nifanyeje? Je, nimwambie ninavyohisi? La, la, siwezi kufanya hivyo! Wengine watasemaje kunihusu?”—Huda.a
HUDA, mwanamke kijana wa Lebanoni, alimpenda mtu fulani, na huyo mtu hakumpenda. Hilo ni tatizo la kawaida. Mwanamke mwingine kijana, aliyeitwa Zeina, alipatwa na jambo kama hilo. Akumbuka hivi: “Nilizoea kumwona kila siku kwa sababu alikuwa jirani yetu. Alivutia sana na alikuwa na sura nzuri. Kwa hiyo nilimpenda.”
Bila shaka, hakuna ubaya wowote wa kuwa na hisia zenye nguvu kuelekea mtu fulani—tukijua kuwa huyo ni mtu ambaye Mkristo angeweza kufunga ndoa naye. (Mithali 5:15; 1 Wakorintho 7:39) Wala si vibaya kwa mwanamke kijana kutaka kufunga ndoa na kuwa na familia. Lakini namna gani ukimpenda mtu anayefaa ambaye hajui kama unampenda au hakuonyeshi upendo?
Maumivu ya Mahaba
Kama Huda, waweza kuhisi ukiwa umechanganyikiwa kihisia-moyo. Mpumbao wa kihisia-moyo wenye kuchangamsha waweza kufuatwa upesi na ukosefu wa uchangamfu wenye kulemaza. “Nyakati fulani nilihisi kuwa msichana aliye na furaha zaidi ulimwenguni, na nyakati nyingine nilihisi kuwa aliye na huzuni zaidi,” akasema Zeina. Upendo wa upande mmoja tu waweza kuwa chanzo cha hangaiko, ukosefu wa usingizi usiku, na hata mshuko-moyo.
Biblia yasema hivi kwenye Mithali 13:12: “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua.” Na matarajio yasipotimizwa kamwe, jambo hili laweza kuumiza! Waweza kujipata ukifikiria juu ya mtu huyu wakati wote, ukiwa na hamu ya kusikia habari yoyote kumhusu. Waweza kubuni njia za kuelekeza uangalifu wake kwako au kutafuta kisababu tu cha kukufanya uwe pamoja naye. Na unapokuwa naye, waweza kupata ugumu wa kujiendesha kwa njia ya kawaida.
Mambo yaweza kuwa yenye kutatanisha hasa wakati ambapo mtu unayetaka kumwonyesha shauku mara kwa mara anakupa uangalifu hususa na kisha nyakati nyingine kutenda kana kwamba hapendezwi nawe hata kidogo. Na ukimwona akielekeza uangalifu mwingi kwa mtu mwingine au akiwaonyesha wengine fadhili na hisani kidogo tu, hisia za wivu zaweza kujitokeza. Biblia yasema hivi: “Ghadhabu ni kali, na hasira ni gharika; lakini ni nani awezaye kusimama mbele ya wivu”?—Mithali 27:4.
Huda alikiri hivi: “Nilihisi uchungu wenye wivu usioweza kuelezeka hivi kwamba ikiwa singerekebisha mambo, ningeshikwa na kichaa.” Pia tokeo laweza kuwa kujichukia. Huda alisema hivi: “Nilijilaumu kwa kumpenda mtu ambaye hakunipenda na kwa kujitesa mwenyewe.”
Ingawa mwanamke kijana katika nchi za Magharibi aweza kujihisi huru kumfikia tu mwanamume kijana na kumwambia juu ya hisia zake, si wanawake wote vijana wana mwelekeo huo. Na katika tamaduni fulani, lingeonwa kuwa jambo lisilofaa au hata lenye kushtua kwa msichana kuchukua hatua kama hiyo. Basi, unaweza kufanya nini ikiwa umempenda mtu asiyekupenda?
Kuchunguza kwa Makini Hisia Zako
Kwanza, jaribu kuchunguza hisia zako kwa utulivu na kihalisi. Biblia huonya: “Mwenye kujitumainia moyo wake ni mjinga.” (Mithali 28:26) Kwa sababu gani? Kwa sababu mara nyingi sana maoni ya moyo wetu huwa yamepotoka. (Yeremia 17:9) Na kile tuwezacho kufikiri kuwa ni upendo mara nyingi hugeuka kuwa kitu kingine. “Nilihitaji uangalifu na upendo,” akakiri Huda. “Nilihitaji mtu wa kunipenda na kunitunza. Kutoka utotoni sikuwahi kupendwa kamwe. Hilo liliniathiri sana.” Ikiwa unatoka katika mazingira ya familia yasiyo na upendo au yenye kudhulumu, hali kadhalika waweza kutaka kupendwa na kutambuliwa. Lakini je, uhusiano wa kimahaba ndio suluhisho?
Kwa kusikitisha, watu wasiokuwa na furaha na wapweke mara nyingi huwa wenzi wa ndoa wasiofaa. Wanaingia maisha ya ndoa wakitarajia kupata wanachohisi wanakihitaji sana. Hata hivyo, furaha ya kweli huja kutokana na kutoa, si kupokea. (Matendo 20:35) Na mwanamke huwa ametayarishwa vizuri zaidi kushughulikia ndoa ikiwa ahisi uradhi na ‘kufuliza kuangalia, si masilahi ya kibinafsi ya mambo yake mwenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.’—Wafilipi 2:4.
Unapohisi washurutishwa sana kufunga ndoa, waweza kuvutiwa kwa urahisi kupita kiasi na uangalifu wowote unaotoka kwa watu wa jinsia tofauti. Nyakati nyingine tamaa ya mapenzi ya mwanamke kijana husitawishwa na marafiki na familia. Jamii fulani husisitiza kwamba msichana aolewe mara tu afikishapo umri wa kuolewa. Kitabu Women in the Middle East chasema hivi: “Ikiwa mwanamke akaribia miaka thelathini na bado ni mseja, jambo hilo husababisha hangaiko kubwa kwa familia yake.” Kwa sababu heshima ya familia yahusika, baba aweza kujaribu kuwaoza binti zake wanapokuwa wachanga iwezekanavyo.
Hata hivyo, kanuni za Biblia ni muhimu kuliko utamaduni. Na Maandiko huwahimiza vijana wangoje mpaka wanapokuwa ‘wamepita mchanuko wa ujana’ kabla ya kufunga ndoa. (1 Wakorintho 7:36) Hivyo, namna gani ikiwa wahisi marafiki au wazazi wako wanakusababishia msongo usio wa lazima wa kufunga ndoa? Biblia hutuambia kwamba msichana Mshulami mwenye kumhofu Mungu aliwaagiza kwa uzito waandamani wake ‘wasiyachochee mapenzi, wala kuyaamsha, hata yatakapoona vema yenyewe.’ (Wimbo Ulio Bora 2:7) Labda kujieleza mwenyewe kwa njia iliyo imara kama hiyo kungeleta matokeo, hasa ikiwa wazazi wako ni wenye kumhofu Mungu.
Kukabili Ukweli
Ingawa hivyo, mwishowe lazima ukabili ukweli kuhusu mtu unayehisi wampenda. Huenda isiwe rahisi kufanya hivyo na kwaweza kusababisha maumivu ya kihisia-moyo. Lakini Maandiko huonya kwa upole hivi: “Inunue kweli, wala usiiuze.” (Mithali 23:23) Jiulize mwenyewe, ‘Je, nina msingi wowote mzuri wa kumpenda? Namjua kadiri gani mtu huyu? Najua nini kuhusu mawazo, hisia, maoni, mazoea, maadili, uwezo, vipawa, na mtindo wake wa maisha?’
Jambo jingine la kufikiria ni kama mtu huyo amekuonyesha upendezi wowote wa kweli ama la. Nyakati nyingi, fadhili au urafiki tu hueleweka vibaya. “Alijaribu kuwa mwenye fadhili,” akasema Huda, “lakini niliyaelewa maneno na matendo yake kuwa upendezi wa kibinafsi kwa sababu nilitaka hivyo. Nilipong’amua kwamba hakupendezwa nami, nilifedheheka sana. Nilihisi kwamba sikustahili upendezi wake na kwamba nilikuwa na kasoro fulani.”
Labda umehisi namna hivyo kutokana na jambo lililokupata linalofanana na hilo. Hata hivyo, ng’amua kwamba kwa sababu tu hukufaa machoni pa mtu huyo haimaanishi kwamba hutafaa machoni pa mtu mwingine. Isitoshe, huyu si mwanamume kijana pekee ulimwenguni!
Kushinda Msononeko
Ijapokuwa hivyo, yaweza kuchukua muda kushinda msononeko wako. Ni nini kiwezacho kusaidia? Njia moja ni kuzungumza na ‘rafiki’—Mkristo mkomavu atakayekusikiliza. (Mithali 17:17) Labda kuna dada aliye na umri mkubwa kutanikoni ambaye ungeweza kuongea naye. Wazazi Wakristo waweza pia kuchangia sehemu kubwa katika kuandaa msaada na utegemezo. Akumbuka Zeina: “Mwanamke fulani Mkristo katika kutaniko letu alitambua msononeko wangu na alikuwa mkomavu wa kutosha kunisaidia. Nilijihisi nimestareheka kuwa pamoja naye na kumweleza kila kitu. Alinitia moyo niongee na wazazi wangu. Kwa hiyo niliongea nao, na walinielewa na kunisaidia.”
Kumbuka pia, nguvu za sala. (Zaburi 55:22) Asema Huda: “Sala zangu kwa Yehova zilinisaidia kuondoa uchungu wangu. Pia nilisoma makala zenye kusaidia katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!” Kwa kuongezea, ni muhimu kwamba usijitenge na wenzako. (Mithali 18:1) Jihusishe na watu wengine. “Jambo jingine lililonisaidia,” akumbuka Zeina, “ni kwamba nilikuwa na shughuli nyingi kisha nikawa painia [mweneza-evanjeli wa wakati wote]. Pia nilishiriki zaidi na wanawake wengine kutanikoni. Nilisaidiwa kufanya maendeleo ya kiroho.”
Biblia husema juu ya “wakati wa kupenda,” na yawezekana kwamba baada ya muda utakutana na mtu atakayekupenda vilevile. (Mhubiri 3:8) Yehova Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya kuonea shangwe raha za upendo wa ndoa, na mwishowe wewe pia waweza kupata uandalizi huu ulio bora kutoka kwa Mfanyi wetu Mtukufu. Katika wakati ulioko, kwa nini usitumie vizuri miaka yako ya useja, ambayo ‘haina mahangaiko,’ kama asemavyo mtume Paulo? (1 Wakorintho 7:32-34) Kwa vyovyote vile, waweza kuhakikishiwa utimizo kwa ahadi hii ya Biblia: “Waufumbua mkono wako [Yehova], wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.”—Zaburi 145:16.
[Maelezo ya Chini]
a Majina yamebadilishwa ili kulinda haki za wanaohusika.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Nyakati nyingine fadhili hueleweka vibaya