Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g04 10/22 kur. 20-22
  • Nitamwambiaje Jinsi Ninavyohisi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nitamwambiaje Jinsi Ninavyohisi?
  • Amkeni!—2004
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tenda kwa Busara
  • Sifa Zako
  • Asipoitikia
  • Naweza Kumkataaje?
    Amkeni!—2001
  • Vipi Akikataa?
    Amkeni!—2004
  • Nimtendeeje Msichana Anayependezwa Nami?
    Amkeni!—2005
  • Namna Gani Asiponipenda?
    Amkeni!—1998
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2004
g04 10/22 kur. 20-22

Vijana Huuliza . . .

Nitamwambiaje Jinsi Ninavyohisi?

“Ningependa kupata jibu la swali hili, Ni nani anayepaswa kumwambia mwingine kwamba anampenda—ni mwanamume au mwanamke?”—Laura.a

TUSEME umekutana na mtu fulani hivi karibuni au umemjua kwa muda mrefu na ungependa kuanzisha uhusiano naye. Unaamini kwamba anahisi jinsi unavyohisi, lakini unafikiri kwamba anaona haya au anaogopa kukuambia. Basi, unajiuliza ikiwa inafaa kuchukua hatua ya kwanza na kumwambia jinsi unavyohisi.b

Kwanza, fikiria maoni ya watu walio karibu nawe, yaani, familia na jamii yenu. Kwa mfano, je, kulingana na desturi za kwenu, wazazi ndio wenye daraka la kukutafutia mwenzi?c Huenda ukahisi kwamba uchumba na ndoa ni mambo ya kibinafsi. Hata hivyo, Wakristo hujitahidi kuepuka kuwaudhi wengine bila sababu. Pia, wao hujitahidi kufikiria maoni ya watu wa familia na ya wapendwa wao.

Hata hivyo, katika nchi nyingi ni kawaida kwa watu wawili kujiamulia wenyewe kuanza uchumba kabla ya kuamua ikiwa watafunga ndoa. Je, ni vibaya mwanamke akichukua hatua ya kwanza na kumwambia mwanamume kwamba anampenda? Ni muhimu tena kufikiria maoni ya familia yenu na ya jamii yenu. Je, watu wengi watashtuka au kuchukizwa ukifanya hivyo?

Biblia inatoa mashauri gani mengine kuhusu habari hii? Katika nyakati za Biblia, mwanamke mmoja mcha-Mungu anayeitwa Ruthu alimfikia mwanamume anayeitwa Boazi ili kuzungumza naye kuhusu ndoa. Yehova Mungu alibariki jitihada za Ruthu! (Ruthu 3:1-13) Bila shaka, Ruthu hakuwa mtoto; alikuwa mjane mwenye umri wa kutosha kufunga ndoa. Vilevile, hakumchezea-chezea Boazi kimapenzi. Badala yake, Ruthu alifuata kwa makini sheria za Mungu kuhusu ndoa.—Kumbukumbu la Torati 25:5-10.

Huenda una umri wa kutosha kufikiria kufunga ndoa na unapendezwa na kijana fulani mwanamume. Hata hivyo, ni hatari kumweleza mtu mwingine hisia zako ikiwa hahisi jinsi unavyohisi. Ni kama kumpa mtu mwingine moyo wako. Anaweza kuutendea kwa wororo au kuuangusha chini. Kufuata kanuni za Biblia ndiyo njia bora ya kuepuka kuaibika bila sababu au kuumia kihisia.

Tenda kwa Busara

Ni rahisi kujikuta ukiwazia jinsi unavyompenda mtu fulani. Huenda hata ukawazia arusi yenu na maisha yenu ya baadaye. Lakini, ijapokuwa mawazo hayo yanaweza kufurahisha, hizo ni ndoto tu. Zinaweza kuamsha tamaa kubwa ambazo huwezi kutosheleza. Kama vile Biblia inavyosema, “tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” (Methali 13:12) Ndoto hizo zinaweza pia kuathiri maamuzi yako. Hata hivyo, andiko la Methali 14:15 linasema: “Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” Kuwa mwerevu kunamaanisha kutumia akili. Utatumiaje werevu unapohisi kwamba unampenda mtu fulani?

Kwanza, jitahidi ‘kutenda kwa ujuzi.’ (Methali 13:16) Kama vile msichana mmoja alivyosema, “huwezi kumpenda mtu kikweli kabla ya kumjua.” Kabla hujaanza kumpenda mtu fulani, chunguza kwa makini mambo anayofanya na jinsi anavyozungumza. Angalia jinsi anavyowatendea watu. Kijana mmoja anapendekeza hivi: “Waulize marafiki zake juu yake, yaani, watu wazima wanaomjua vizuri.” Je, ‘anashuhudiwa vema’ na wale walio katika kutaniko lao la Kikristo? (Matendo 16:2) Pia, msichana anayeitwa Isabel anasema: “Kwenda matembezi pamoja naye mnapokuwa katika kikundi cha watu na kujua familia yao kunaweza kukunufaisha sana.” Mnapokuwa katika kikundi cha watu ni rahisi kumchunguza bila wasiwasi mwingi.

Ili umjue mtu kwa njia hiyo, unahitaji wakati na subira. Lakini kufanya hivyo kutakuwezesha kuona mitazamo, tabia, na sifa ambazo zitaimarisha au kubadilisha hisia zako. Methali 20:11 inasema: “Kwa matendo yake, mvulana [au kijana mwanamume] hujitambulisha kama utendaji wake ni safi na mnyoofu.” Naam, muda si muda matendo yake yataonyesha sifa zake.

Basi, tumia hekima na uepuke kuharakisha kumweleza kijana huyo kwamba unampenda. Ukiharakisha mambo, naye akubali maombi yako, huenda baadaye ukagundua kwamba hafai kuwa mume wako.d Ukiisha kumweleza hisia zako, kukatisha uhusiano wenu kunaweza kumuumiza sana.

Sifa Zako

Huenda kijana huyo anakuchunguza pia! Je, wewe huonyesha kwamba una sifa zinazompendeza Mungu? Isabel anasema hivi: “Nimeona kwamba wasichana wengi hawavai vizuri. Ikiwa unataka mtu anayependa sana mambo ya kiroho akutambue, unapaswa kuvalia kwa kiasi.” Licha ya mitindo iliyopo ulimwenguni, ukijipamba “kwa mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili,” utamvutia zaidi mwanamume anayemcha Mungu.—1 Timotheo 2:9.

Pia, Biblia inawatia moyo vijana Wakristo ‘kuwa vielelezo katika kusema.’ (1 Timotheo 4:12) Jinsi unavyozungumza huonyesha mengi kukuhusu. Unapaswa kufanya nini unapopata nafasi za kuzungumza na kijana huyo? Ikiwa ana haya, huenda akaogopa na kuwa na wasiwasi. Msichana mmoja anayeitwa Abbie anasema, “Huenda wewe mwenyewe ukahitaji kuanzisha mazungumzo ili uone jinsi atakavyotenda.”

Utafanyaje hivyo? Ukizungumza kila wakati juu yako, huenda akafikiri kwamba una ubinafsi na hujui mambo mengi. Biblia inawahimiza watu ‘kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yao wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’ (Wafilipi 2:4) Ukimuuliza maswali machache yanayofaa juu yake au mapendezi yake anaweza kukueleza jinsi anavyohisi.

Haifai kuwa na “ulimi wenye ujanja” au “midomo ya uwongo.” (Zaburi 120:2) Mwanamume mwenye ufahamu atagundua ikiwa unasema uwongo. Pia, epuka kusema mambo ili kumfurahisha tu, hasa wakati ambapo mnazungumzia mambo mazito kama vile miradi yenu ya kiroho. Sikuzote uwe mnyoofu, sema kweli, na usijifanye. Ukifanya hivyo, utajua ikiwa mna miradi ileile.

Asipoitikia

Hata hivyo, baada ya kufanya jitihada hizo zote kwa unyoofu, utafanya nini asipovutiwa nawe? Huenda majuma kadhaa, au hata miezi ikapita bila yeye kuonyesha anapendezwa nawe. Je, utakata kauli mara moja kwamba ana haya tu? Jiulize hivi: ‘Ikiwa ni mwoga hivyo, je, yuko tayari kwa ajili ya ndoa? Nikiolewa naye, je, ataweza kutimiza daraka lake akiwa kichwa cha familia, au atanitarajia niwe kichwa?’ (1 Wakorintho 11:3) Pia, jiulize hivi: ‘Je, kweli yeye ni mwenye haya au hanipendi?’ Huenda jambo hilo likakufadhaisha. Lakini ukitambua kwamba hakupendi, utaepuka kupata aibu inayotokana na kumweleza jinsi unavyohisi na kumbe hakupendi.

Huenda ukahisi kwamba kijana huyo anakupenda lakini anahitaji muda mrefu ili kuonyesha jambo hilo na kwamba anahitaji tu kuchochewa kidogo. Huenda ndivyo ilivyo. Lakini ukiamua kuchukua hatua ya kwanza kumweleza hisia zako, tambua kwamba ni hatari kufanya hivyo. Unapaswa kufikiria kwa makini yale utakayosema na vilevile wakati unaofaa zaidi wa kuyasema.

Kwa mfano, huenda ukaamua kuwa inafaa zaidi kumwonyesha kwamba unapendezwa naye badala ya kusema moja kwa moja unampenda. Katika hali zenye kustarehesha na mahali panapofaa, unaweza kumwambia kwamba ungependa kumjua vizuri zaidi. Usiwe na wasiwasi hata unaposhindwa kujieleza vizuri. Hisia zako za unyoofu zinaweza kutimiza mengi zaidi ya maneno unayosema. Pia, kumbuka unamweleza tu kwamba ungependa kuanzisha uchumba, wala si kumwomba akuoe. Hata hivyo, anaweza kushangaa. Basi mpe wakati ili afikirie yale uliyomwambia.

Ikiwa umemjua vizuri kijana huyo na umejionea kwamba ni mwenye fadhili na mwenye kujali, hupaswi kuogopa kwamba ataudhika au kukuaibisha. Lakini, utafanya nini asipokubali maombi yako? Na mwanamume anapaswa kutendaje anapokabili hali kama hiyo? Makala moja ya wakati ujao itajibu maswali hayo.

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b Ingawa makala hii imeandikwa hasa kwa ajili ya vijana wa kike, vijana wa kiume na watu wengine wanaofikiria kuanzisha uchumba wanaweza pia kufaidika na mashauri haya ya Kimaandiko.

c Wengine ambao wamechaguliwa wenzi wa ndoa wamekuwa na ndoa zenye furaha. Kwa mfano, katika nyakati za Biblia, baada ya kuchaguliwa mwenzi, Isaka na Rebeka walifunga ndoa, na Isaka “akampenda.” (Mwanzo 24:67) Somo ni nini? Usipuuze haraka desturi za eneo lenu maadamu hazipingani na sheria ya Mungu.—Matendo 5:29.

d Sura za 28 hadi 31 katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, zinaweza kukusaidia kuchagua mwenzi wa ndoa anayefaa.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Ukiona jinsi anavyotenda, hilo linaweza kubadili jinsi unavyohisi

[Picha katika ukurasa wa 22]

Ukivutiwa na mtu fulani, zungumza na watu wazima wakomavu ambao wanamjua

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki