Kusikiliza kwa Macho Yako
NI NINI ufunguo wa kuwasiliana kwa matokeo na Kiziwi? Kumtazama ifaavyo ana kwa ana. Jambo hili ni la lazima Viziwi wanapozungumza. Kwa kweli unaonwa kuwa ujeuri kutazama mahali penginepo na kukatisha mawasiliano ya ana kwa ana wakati watu wawili wanapozungumza kwa kutumia lugha ya ishara. Na unaweza kuvutiaje uangalifu wa Kiziwi? Badala ya kumwita mtu huyo kwa jina, inafaa zaidi kumgonga kwa upole kwenye bega au mkono, mpungie mkono ili aone, au ikiwa yuko mbali, ashiria mtu mwingine ili avutie uangalifu wake. Ikitegemea hali, ungeweza kugongagonga sakafu au kuwasha na kuzima taa. Njia hizi na nyinginezo za kuvuta uangalifu huongezea namna ya maisha ya Viziwi na ni sehemu ya desturi ya Viziwi.
Kifungo cha Muungano cha Lugha
Wanapokutana na Kiziwi, watu fulani wamefikia mkataa wenye makosa kwamba kusoma mdomo ni kazi rahisi. Hata hivyo, Viziwi wengi hawaioni njia hii ya mawasiliano kuwa bora. Bila shaka, kuna visa vya kipekee, kwani watu fulani ni stadi sana kwa kusoma mdomo, lakini kwa ujumla halingekuwa jambo la fadhili kudhania kwamba mtu fulani ataweza kusoma mdomo wako. Labda kwa kutumia mfasiri au kuandika kwenye karatasi unalotaka kusema kungetokeza mawasiliano yenye maana.
Hata hivyo, je, halingekuwa jambo lenye kuonyesha ufikirio kujifunza lugha ya ishara ikiwa unakutana kwa ukawaida na Viziwi? Jambo hili litatokeza kifungo cha ajabu kama nini hasa miongoni mwa wale wanaoshiriki imani ileile! Ni sawa na kujifunza mambo ya msingi ya lugha nyingine katika utamaduni wenye lugha mbili. Kwa muda mrefu Mashahidi wa Yehova wametaka kufanya ujumbe kuhusu Yehova Mungu upatikane kwa watu wote. Tunapotambua kwamba Viziwi hawawezi kujifunza kusikiliza kwa njia ya kawaida, itakuwa vyema kama nini kujipatanisha na hali yao kwa kutumia lugha ya ishara!—1 Wakorintho 9:20-22.
Antonino asema kwamba alipoanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo katika Italia, mwanzoni “hakukuwa na kitia-moyo halisi na chenye kuchochea katika mazungumzo na ndugu ambao wangeweza kusikia. Kwa sababu hatukuweza kuelewana, nilihisi nimetengwa.” Washiriki wengi wa kutaniko waliitikia kwa kujifunza Lugha ya Ishara ya Italia (LIS). Viziwi wengi wenye kupendezwa wakaanza kujifunza Biblia, na mikutano iliongozwa kwa LIS. Antonino alitiwa moyo na sasa anatamani “kuzungumza na marafiki zangu wote walio Viziwi kuhusu mikutano yetu na upendo mchangamfu unaopatikana miongoni mwa watu wa Yehova.”
Ulimwenguni pote Mashahidi wa Yehova wanaanzisha makutaniko yanayotumia lugha ya ishara, ambapo Viziwi wanaweza kufurahia ushirika mchangamfu na wenye upendo wa mtu na mwenzake. Kwa miaka izidiyo 20, kumekuwa na vikundi vinavyotumia lugha ya ishara kwa ajili ya Viziwi katika Hispania. Kwa sasa kuna makutaniko 19 yenye utendaji ya Viziwi na vikundi vidogo zaidi 47 huko Marekani.
Viziwi wanaweza kutumika wakiwa wahudumu wa wakati wote (mapainia), watumishi wa huduma, na wazee na vilevile kutoa hotuba kwenye mikusanyiko, kufundisha Shule za Utumishi wa Painia, na kuongoza katika njia mbalimbali. Katika hali hii hakuna mipaka, bali fursa tu za kumsifu Yehova kwa uwezo alio nao mtu.
Uhitaji wetu wa kiasili wa uandamani na mawasiliano huonyeshwa kupitia kwa tamaduni na lugha nyingi ulimwenguni pote. Badala ya kuwaona Viziwi kuwa wamepungukiwa au wana kasoro, litakuwa jambo bora kama nini kuona yale wanayotimiza, uwezo wao na sifa ambazo hufanyiza wanadamu wote! Kwa kuwastahi wengine na kuwa tayari kubadilikana, sote twaweza kuwa na sehemu ya maana katika familia ya kibinadamu yenye watu wa aina mbalimbali lakini yenye muungano.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Unapoongea kwa kutumia lugha ya ishara, dumisha mawasiliano ya macho
[Picha katika ukurasa wa 24]
Viziwi watumikia wakiwa wahudumu wa wakati wote wenye shangwe
[Picha katika ukurasa wa 25]
Kuimba nyimbo za Ufalme katika Kihispania
[Picha katika ukurasa wa 25]
Kutoa hotuba katika mkusanyiko katika Lugha ya Ishara ya Korea
[Picha katika ukurasa wa 25]
Vichapo vinavyotegemea Biblia vyatolewa katika lugha ya ishara kwenye vidio