Maoni ya Biblia
Je, Wafu Wapasa Kuheshimiwa?
“HISIA FULANI ILIYOIMARIKA SANA HUCHOCHEA WATU WENGI WATENDEE MAITI KWA NJIA YENYE STAHA ISIYOHISIWA WANAPOSHUGHULIKA NA MZOGA.”—ENCYCLOPÆDIA BRITANNICA.
WATU wengi huheshimu wapendwa wao waliokufa katika njia fulani. Wafu huheshimiwa kupitia matangazo ya tanzia katika magazeti ya habari, na wanasifiwa katika taabini. Katika nchi fulani maziko yenye kupangwa kwa uangalifu sana yakiwa na desturi za kidini au za kizamani ni ya kawaida. Sherehe kwa ajili ya wafu zaweza kuchukua muda wa siku, majuma au miezi kadhaa. Shule, viwanja vya ndege, barabara, na miji inaitwa kwa majina ya watu mashuhuri waliokufa. Nguzo za ukumbusho hujengwa na sikukuu huanzishwa ili kuadhimisha ukumbusho wa watu walio mashujaa.
Hata hivyo, kulingana na Neno la Mungu, wafu hawafahamu kabisa juu ya heshima yoyote wanayopewa. (Ayubu 14:10, 21; Zaburi 49:17) Wafu wako hai tu katika kumbukumbu ya wale wanaowakumbuka. Biblia husema: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Maandiko hutoa tumaini la ufufuo utakaotokea wakati ujao. (Yohana 5:28, 29; 11:25) Lakini hadi wakati huo utakapofika, wafu hawako. Kihalisi wanakuwa mavumbi.—Mwanzo 3:19; Ayubu 34:15.
Kwa kufikiria msimamo wa Biblia ulio dhahiri kuhusu hali ya wafu, je, kuna kusudi lolote linalotimizwa kwa kuwaheshimu? Je, Wakristo wapaswa kufuata desturi zinazohusiana na maziko ya wapendwa wao?
Desturi Zinazotegemea Kauli Zisizo za Kweli
Desturi nyingi, labda zilizo nyingi zaidi, zinazohusiana na wafu zimeimarika sana katika mafundisho ya kidini yasiyo ya Kibiblia. Sherehe fulani za ibada zinadai “kulinda aliyekufa na mashambulizi ya roho waovu; nyakati nyingine kusudi la sherehe za ibada limekuwa kulinda walio hai na uvutano wenye kuenea wa wafu au na nia ya wafu ya kuwadhuru,” yasema Encyclopædia Britannica. Desturi yoyote ya namna hiyo inayotegemea kauli isiyo ya kweli kwamba wafu wanaendelea kuishi katika makao yasiyoonekana huhitilafiana moja kwa moja na kweli za Kibiblia.—Mhubiri 9:10.
Watu wengi huheshimu kupita kiasi watu wao waliokufa. Namna ya ibada hii inatia ndani kuwatolea wazazi waliokufa dhabihu na sala. Watu fulani wanaoshiriki katika desturi hizo hawaoni matendo yao kuwa ibada, bali, badala ya hivyo, wanayaona kuwa semi za staha au staha yenye kina kirefu kwa wafu. Na bado, ujitoaji wa namna hii kwa wazazi waliokufa una misingi ya kidini na huhitilafiana na mafundisho ya Biblia. Yesu Kristo alisema hivi: “Ni Yehova Mungu wako ambaye lazima uabudu, na ni kwake peke yake lazima utoe utumishi mtakatifu.”—Luka 4:8.
Maoni Yaliyosawazika
Kuwaonyesha wafu heshima na staha sikuzote hakuhusiani na mafundisho ya kidini yasiyo ya kweli. Mathalani, simulizi la Biblia laeleza jinsi ambavyo Mfalme Hezekia mwaminifu alipewa heshima baada ya kufa. Watu wa Mungu “wakamzika mahali pa kupandia makaburi ya wana wa Daudi; nao Yuda wote na wenyeji wa Yerusalemu wakamfanyia heshima alipokufa.” (2 Mambo ya Nyakati 32:33) Kielelezo kingine ni cha Yesu. Biblia husema kwamba wanafunzi wake “wakauchukua mwili wa Yesu na kuufunga kwa mabendeji pamoja na manukato, sawa na jinsi Wayahudi walivyo na desturi ya kutayarisha kwa ajili ya maziko.”—Yohana 19:40.
Maandiko yana visa vingine vingi ambapo utaratibu maalumu ulifuatwa uliohusiana na mwili na maziko ya watu waliokufa. Mazoea haya hayakuwa ibada ya wafu, wala hayakutegemea itikadi yenye makosa kwamba wafu huendelea kuwa na uvutano juu ya mambo ya walio hai. Badala ya hivyo, waombolezaji walidhihirisha staha yenye kina kirefu kwa wale waliowapenda. Biblia haipingi heshima ya namna hiyo, kwa kuwa inategemea hisia za asili za kibinadamu ingawa Biblia haiungi mkono maonyesho yanayopita kiasi au ya mpagao kwenye maziko. Kwa upande mwingine, haiwatii moyo Wakristo wawe wavumilivu na wasioonyesha hisia wanapokabiliwa na kifo cha mpendwa wao.
Kwa sababu hiyo, wanapohudhuria maziko ya wapendwa wao waliokufa, Mashahidi wa Yehova huonyesha staha na heshima inayofaa kwa wafu. (Mhubiri 7:2) Inapohusu habari ya maua, ibada za maziko, na desturi nyinginezo za mahali pao, Wakristo hufanya uchaguzi wa kibinafsi kwa uangalifu kusudi waepuke mazoea yanayopingana na mafundisho ya Biblia. Katika hili, uamuzi mzuri na usawaziko vyahitajiwa. Kichapo Encyclopædia of Religion and Ethics chaeleza kwamba “sherehe ya ibada hubadili umaana wake katika vipindi mbalimbali, hivi kwamba umaana unaoambatanishwa nayo baadaye huenda ukawa tofauti na ule wa awali, na namna inavyofafanuliwa huenda isifunue jambo lolote kuhusu chanzo chake.”a
Je, Ni Vibaya Kusifu Sana?
Kanuni ya kuwa wenye usawaziko hutumika pia kuhusiana na habari ya kusifu sana wafu. Kwenye ibada za maziko, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuwafariji waliofiwa. (2 Wakorintho 1:3-5) Huenda programu rasmi ikatia ndani msemaji mmoja au zaidi. Lakini haingefaa kubadilisha pindi hiyo kuwa gwaride la wasifaji wakimhimidi kupita kiasi aliyekufa. Badala yake, maziko hutokeza fursa ya kuhimidi sifa za Mungu zenye kustaajabisha, kutia ndani fadhili zake katika kutuandalia tumaini la ufufuo.
Hata hivyo, hii haimaanishi kwamba ingekuwa vibaya kukumbuka sifa nzuri za mtu aliyekufa wakati wa hotuba ya maziko. (Linganisha 2 Samweli 1:17-27.) Mtu aliyekufa anapokuwa mwaminifu kwa Mungu mpaka kifo, anakuwa kielelezo bora cha kuigwa. (Waebrania 6:12) Ni vizuri kutafakari juu ya mwendo wa uaminifu-maadili wa watumishi wa Mungu. Kushiriki mawazo hayo pamoja na wengine wakati wa ibada ya maziko huandaa faraja kwa walio hai na kuheshimu kumbukumbu ya wafu.
Wakristo wa kweli hawaabudu wafu. Hawashiriki katika sherehe za ibada zinazopendwa na wengi ambazo huhitilafiana na kweli za Biblia. Kwa upande mwingine, watumishi wa Mungu hupinga maoni yanayopita kiasi kwamba kwa sababu wafu ni mavumbi tu, desturi zote za maziko hazitimizi kusudi lolote na si za lazima. Wao huomboleza na kuwakumbuka watu wao waliokufa. Lakini maumivu na majonzi yao hupunguzwa na kweli za Biblia kwamba wafu hawateseki na kwamba kuna tumaini la ufufuo.
[Maelezo ya Chini]
a Toleo la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1991, ukurasa wa 31, huandaa mwelekezo ufuatao: “Mkristo wa kweli apaswa afikirie hili: Je! kufuata desturi fulani kungeonyesha wengine kwamba nimechagua imani au mazoea yasiyo ya Kimaandiko? Kipindi cha wakati na mahali vingeweza kuongoza jibu la hilo. Desturi (au pambo) huenda ikawa ilikuwa na maana ya kidini bandia mamileani yaliyopita au huenda ikawa na maana hiyo leo katika nchi ya mbali. Lakini bila kuchukua wakati mwingi katika kuchunguza hilo, jiulize mwenyewe hivi: ‘Maoni ya kawaida mahali ninapoishi ni gani?’—Linganisha 1 Wakorintho 10:25-29.”
[Picha katika ukurasa wa 10]
Msafara wa mazishi ukimpa heshima Gustav wa Pili, mfalme wa Sweden, baada ya kifo chake mwaka wa 1632
[Hisani]
From the book Bildersaal deutscher Geschichteyy