Maoni ya Mkristo Kuhusu Desturi za Mazishi
KIFO kisichotarajiwa cha mpendwa hasa ni chenye kuhuzunisha. Hutokeza mshtuko ambao hufuatwa na maumivu mengi ya kihisia-moyo. Kumtazama mpendwa akifa baada ya ugonjwa wa muda mrefu wenye maumivu si jambo lisilotarajiwa, lakini mtu huendelea kuwa na huzuni na hisia nyingi za kumkosa aliyekufa.
Hata mpendwa awe alikufa katika hali gani, waliofiwa huhitaji utegemezo na faraja. Huenda Mkristo aliyefiwa pia akakabili mnyanyaso kutoka kwa wale wasisitizao afuate desturi za mazishi zisizo za Kimaandiko. Jambo hilo ni la kawaida katika nchi nyingi za Afrika na pia katika sehemu nyinginezo za dunia.
Ni nini kitakachomsaidia Mkristo aliyefiwa aepuke desturi za mazishi zisizo za Kimaandiko? Waamini wenzake wanaweza kumtegemezaje nyakati kama hizo za majaribu? Majibu kwa maswali hayo yawahusu wote wale watafutao kumpendeza Yehova, kwa kuwa “namna ya ibada iliyo safi na isiyo na unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kutazama mayatima na wajane katika dhiki yao, na kufuliza kujitunza mwenyewe bila doa kutokana na ulimwengu.”—Yakobo 1:27.
Zahusiana na Imani Fulani
Jambo la kawaida linalohusiana na desturi nyingi za mazishi ni imani kwamba wafu huendelea kuishi katika makao yasiyoonekana ya wazazi wa kale waliokufa. Waombolezaji wengi huhisi kuwa wamewajibika kushika desturi fulani ili kuwatuliza. Au wao huhofu kwamba watawaudhi majirani wanaoamini kwamba, jumuiya itapatwa na madhara iwapo haitashika desturi hizo.
Kumhofu mwanadamu hakupaswi kumfanya Mkristo wa kweli ashiriki katika desturi zisizompendeza Mungu. (Mithali 29:25; Mathayo 10:28) Biblia huonyesha kwamba wafu hawana fahamu, kwa kuwa yasema hivi: “Kwa sababu walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lolote . . . hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu uendako wewe.” (Mhubiri 9:5, 10) Kwa hiyo, Yehova Mungu aliwaonya watu wake wa nyakati za kale wasijaribu kuwatuliza wafu au kuwasiliana nao. (Kumbukumbu la Torati 14:1; 18:10-12; Isaya 8:19, 20) Kweli hizo za Biblia hupingana na desturi nyingi za mazishi zinazopendwa sana.
Namna Gani “Utakaso wa Kingono”?
Katika nchi fulani za Afrika ya kati, mwenzi aliyefiwa hutarajiwa kufanya ngono na mtu wa jamaa ya aliyekufa. Iwapo hawatafanya hivyo, inaaminiwa kwamba yule aliyekufa ataidhuru familia iliyoachwa. Desturi hiyo huitwa “utakaso wa kingono.” Lakini Biblia hufasili uhusiano wowote wa kingono nje ya ndoa kuwa “uasherati.” Kwa kuwa Wakristo lazima ‘wakimbie uasherati,’ wao hukinza kwa ujasiri desturi hiyo isiyo ya Kimaandiko.—1 Wakorintho 6:18.
Mfikirie mjane aitwaye Mercy.a Mume wake alipokufa mwaka wa 1989, watu wa jamaa walitaka afanye utakaso wa kingono pamoja na mwanamume fulani wa jamaa. Alikataa na kuwaeleza kwamba hiyo desturi ilikuwa kinyume cha sheria ya Mungu. Wakiwa wamevunjika moyo, hao watu wa jamaa walimtukana na kuondoka. Mwezi mmoja baadaye walipora nyumba yake na kutoa mabati ya paa. “Dini yako yaweza kukutunza,” wakasema.
Kutaniko lilimfariji Mercy na hata kumjengea nyumba mpya. Majirani walivutiwa sana hivi kwamba baadhi yao waliamua kushiriki katika mradi huo, mke wa chifu, aliye Mkatoliki, akiwa wa kwanza kuleta nyasi ya kuezeka paa. Mwenendo wa Mercy wa uaminifu uliwatia moyo watoto wake. Tangu wakati huo, wanne kati yao wamejiweka wakfu kwa Yehova Mungu, na mmoja wao alihudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma hivi majuzi.
Kwa sababu ya desturi ya utakaso wa kingono, Wakristo fulani wamejiachilia washurutishwe kufunga ndoa pamoja na mtu asiyeamini. Kwa mfano, mjane mmoja mwanamume aliye katika miaka yake ya 70 alioa haraka-haraka msichana mdogo kutoka kwa jamaa ya mke wake aliyekufa. Kwa kufanya hivyo, angeweza kudai kwamba alikuwa amefanya utakaso wa kingono. Hata hivyo, mwendo kama huo hupingana na shauri la Biblia kwamba Wakristo wapaswa kuoa “katika Bwana tu.”—1 Wakorintho 7:39.
Sherehe za Makesha
Katika nchi nyingi, waombolezaji hukusanyika nyumbani mwa aliyekufa na kukesha usiku kucha. Mara nyingi makesha hayo hutia ndani karamu na muziki wenye sauti ya juu. Inaaminiwa kwamba jambo hilo hutuliza wafu na kulinda familia iliyoachwa dhidi ya uchawi. Huenda hotuba zenye kurai-rai zikatolewa ili kupata upendeleo wa aliyekufa. Baada ya hotuba, huenda waombolezaji wakaimba wimbo wa kidini kabla ya mtu mwingine kusimama na kuzungumza. Huenda wakafanya hivyo hadi mapambazuko.b
Mkristo wa kweli hawezi kushiriki katika sherehe hizo za makesha za usiku kucha kwa sababu Biblia huonyesha kwamba wafu hawawezi kuwasaidia au kuwadhuru walio hai. (Mwanzo 3:19; Zaburi 146:3, 4; Yohana 11:11-14) Maandiko hulaumu zoea la uwasiliani-roho. (Ufunuo 9:21; 22:15) Hata hivyo, huenda mjane Mkristo akashindwa kuwazuia wengine wasianzishe mazoea ya uwasiliani-roho. Huenda wakasisitiza wakeshe usiku kucha nyumbani mwake. Ni nini ambacho waamini wenzi wanaweza kufanya ili kuwasaidia Wakristo waliofiwa ambao wanakabili mnyanyaso huo wa ziada?
Mara nyingi wazee wa kutaniko wameweza kuitegemeza familia ya Kikristo iliyofiwa kwa kusababu na watu wa jamaa na majirani. Baada ya kusababu kama huko, huenda watu hao wakakubali kuondoka nyumbani humo kwa amani na kukusanyika tena siku nyingine kwa ajili ya mazishi. Lakini vipi ikiwa baadhi yao wanakuwa wenye ugomvi? Huenda kuendelea kusababu nao kukatokeza jeuri. ‘Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali ni lazima afulize kujizuia mwenyewe chini ya uovu.’ (2 Timotheo 2:24) Kwa hiyo, iwapo watu wa jamaa wasiotaka kushirikiana wataka kuongoza mambo kwa nguvu, huenda mjane Mkristo na watoto wake wasiweze kuwazuia. Lakini hawatashiriki katika sherehe ya kidini ya uwongo inayofanywa nyumbani mwao, kwa kuwa wao hutii amri hii ya Biblia: “Msiwe wenye kufungwa nira isiyosawazika pamoja na wasio waamini.”—2 Wakorintho 6:14.
Kanuni hiyo pia hutumika kuhusu mazishi. Mashahidi wa Yehova hawashiriki katika kuimba, kusali, au katika desturi zenye kuongozwa na mhudumu wa dini ya uwongo. Iwapo Wakristo ambao ni washiriki wa karibu wa familia waona kuna uhitaji wa kuhudhuria ibada kama hiyo, wao hufanya hivyo lakini hawashiriki.—2 Wakorintho 6:17; Ufunuo 18:4.
Mazishi Yenye Heshima
Mazishi ambayo huongozwa na Mashahidi wa Yehova hayatii ndani desturi zikusudiwazo kutuliza wafu. Hotuba ya Biblia hutolewa ama kwenye Jumba la Ufalme, kwenye ukumbi wa mazishi, nyumbani kwa aliyekufa, ama kwenye kaburi. Kusudi la hotuba hiyo ni kufariji aliyefiwa kwa kufafanua yale Biblia isemayo kuhusu kifo na tumaini la ufufuo. (Yohana 11:25; Waroma 5:12; 2 Petro 3:13) Wimbo wenye kutegemea Maandiko waweza kuimbwa, na kumaliza mazishi kwa sala yenye kufariji.
Hivi majuzi, mazishi kama hayo yalifanywa kwa ajili ya mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyetukia kuwa dada mwenye umri mdogo zaidi wa Nelson Mandela, rais wa Afrika Kusini. Baada ya mazishi hayo, rais alimshukuru msemaji kwa moyo mweupe. Waheshimiwa na maofisa wengi wa vyeo vya juu walikuwa wamehudhuria. “Haya ndiyo mazishi yenye heshima zaidi ambayo nimewahi kuhudhuria,” akasema waziri mmoja.
Je, Mavazi ya Kuomboleza Yanakubalika?
Mashahidi wa Yehova huombolezea kifo cha wapendwa wao. Kama Yesu, huenda wakalia. (Yohana 11:35, 36) Lakini hawalioni kuwa jambo la lazima kuonyesha huzuni yao hadharani kwa ishara fulani ya nje. (Linganisha Mathayo 6:16-18.) Katika nchi nyingi, wajane hutarajiwa kuvaa mavazi maalumu ili kuwatuliza wafu. Mavazi hayo lazima yavaliwe kwa miezi kadhaa au hata mwaka baada ya mazishi, na karamu hufanywa wakati wa kuyavua.
Kutoonyesha ishara za kuomboleza huonekana kuwa kosa dhidi ya yule aliyekufa. Kwa sababu hiyo, katika sehemu za Swaziland, machifu wa makabila wamewafukuza Mashahidi wa Yehova kutoka katika nyumba na ardhi zao wenyewe. Hata hivyo, Wakristo hao waaminifu sikuzote wametunzwa na ndugu zao wa kiroho wanaoishi sehemu nyinginezo.
Mahakama Kuu ya Swaziland iliamua kwa kupendelea Mashahidi wa Yehova, ikisema kwamba wapaswa kuruhusiwa kurudi kwenye nyumba na ardhi zao. Katika kisa kingine, mjane Mkristo aliruhusiwa kubaki kwenye ardhi yake baada tu ya kuonyesha barua na utepe uliorekodiwa ambamo mume wake aliyekufa alikuwa ameeleza waziwazi kwamba mke wake hapaswi kuvaa mavazi ya kuomboleza. Hivyo, aliweza kuthibitisha kwamba kwa kweli alikuwa akimstahi mume wake.
Kuna manufaa kubwa za kutoa maagizo dhahiri juu ya mazishi kabla mtu hajafa, hasa katika sehemu ambako mazoea yasiyo ya Kimaandiko ni mambo ya kawaida. Fikiria mfano wa Victor, mkazi wa Kamerun. Aliandika programu ambayo ingefuatwa kwenye mazishi yake. Familia yake ilikuwa na watu wengi mashuhuri, waliofuata utamaduni wenye mapokeo yenye nguvu kuhusiana na wafu, yakitia ndani kuabudu mafuvu ya vichwa vya binadamu. Kwa kuwa Victor alikuwa mshiriki wa familia aliyestahiwa, alijua kwamba kulikuwa na uwezekano wa kuabudiwa kwa fuvu la kichwa chake. Kwa hiyo, alitoa maagizo dhahiri juu ya jinsi ambavyo Mashahidi wa Yehova wangeshughulikia mazishi yake. Kufanya hivyo kulifanya hali iwe rahisi kwa mjane na watoto wake, na ushahidi mzuri ukatolewa katika jumuiya.
Epuka Kuiga Desturi Zisizo za Kikristo
Watu wengine walio na ujuzi wa Biblia wameogopa kuonekana kuwa tofauti. Ili kuepuka mnyanyaso, wamejaribu kuwapendeza majirani wao kwa kujifanya waonekane kana kwamba wanashika desturi ya makesha kwa ajili ya wafu. Ingawa kuwatembelea waliofiwa ili kuwafariji kibinafsi kwastahili pongezi, jambo hilo halihitaji kwamba kufanywe ibada ndogo ya mazishi kila usiku nyumbani mwa aliyekufa kabla ya mazishi halisi. Huenda kufanya hivyo kukawakwaza watazamaji, kwa kuwa huenda jambo hilo likafanya wafikiri kwamba wanaoshiriki hawaamini kabisa yale Biblia isemayo juu ya hali ya wafu.—1 Wakorintho 10:32.
Biblia huwahimiza Wakristo watangulize ibada ya Mungu maishani na kutumia wakati wao kwa hekima. (Mathayo 6:33; Waefeso 5:15, 16) Ingawa hivyo, katika sehemu fulani, utendaji wa kutaniko umesimamishwa kwa juma moja au hata majuma mengi kwa sababu ya mazishi. Tatizo hilo haliko Afrika pekee. Ripoti kutoka Amerika ya Kusini yasema hivi kuhusiana na mazishi fulani: “Mikutano mitatu ya Kikristo ilikuwa na wahudhuriaji wachache mno. Utumishi wa shambani ukapuuzwa kwa muda wa siku kumi. Hata watu wasio Mashahidi na wanafunzi wa Biblia walishangaa na kukatishwa tamaa kuona baadhi ya ndugu na dada zetu wakishiriki katika shughuli hizo za mazishi.”
Katika jumuiya nyingine, huenda familia iliyofiwa ikawaalika nyumbani kwao marafiki wa karibu kwa ajili ya viburudisho baada ya mazishi. Lakini katika sehemu nyingi za Afrika, ambako mara nyingi wanyama hutolewa dhabihu, mamia ya watu wanaohudhuria mazishi hufika nyumbani kwa aliyekufa wakitarajia karamu. Baadhi ya washiriki wa kutaniko la Kikristo wameiga desturi hiyo, wakifanya ionekane kana kwamba wanafanya karamu za kidesturi za kutuliza wafu.
Mazishi yafanywayo na Mashahidi wa Yehova hayamwekelei mfiwa mzigo wenye kulemea wa gharama. Kwa hiyo si lazima kuwe na mpango wa pekee kwa waliohudhuria kutoa pesa za kugharimia matumizi ya mazishi yanayopita kiasi. Bila shaka, wengine kutanikoni watafurahia kutoa msaada iwapo wajane maskini hawawezi kugharimia mambo ya lazima. Ikiwa msaada huo hautoshi, huenda wazee wakapanga kutoa msaada wa kimwili kwa wanaostahili.—1 Timotheo 5:3, 4.
Desturi za mazishi hazipingani sikuzote na kanuni za Biblia. Zinapopingana, Wakristo huazimia kutenda kulingana na Maandiko.c (Matendo 5:29) Ijapokuwa jambo hilo huenda likaleta dhiki, watumishi wengi wa Mungu wanaweza kushuhudia kwamba wamekabili majaribu hayo kwa mafanikio. Wamefanya hivyo kwa nguvu za Yehova, “Mungu wa faraja yote,” na kwa msaada wenye upendo wa waamini wenzao ambao wamewafariji katika dhiki yao.—2 Wakorintho 1:3, 4.
[Maelezo ya Chini]
a Majina yamebadilishwa katika makala hii.
b Katika vikundi fulani vya lugha na utamaduni, neno “makesha” hutumiwa kumaanisha ziara fupi ya kumfariji aliyefiwa. Huenda ziara hiyo isihusishe jambo lolote lisilo la Kimaandiko. Ona gazeti la Amkeni! la Mei 22, 1979, ukurasa wa 27-28 (la Kiingereza).
c Mahali ambako yaelekea desturi za mazishi zitamletea Mkristo majaribu makali, wazee waweza kuwatayarisha wataka kubatizwa kwa yale ambayo huenda wakakabili baadaye. Wanapokutana na watu hao wapya ili kuzungumzia maswali katika kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu, wazee wapaswa kukazia uangalifu vichwa, “Nafsi, Dhambi, na Kifo” na “Kuchangamana na Dini Mbalimbali.” Vichwa hivyo viwili vina maswali ambayo wazee waweza kuchagua kuzungumzia. Wazungumziapo vichwa hivyo wazee waweza kutoa habari juu ya desturi za mazishi zisizo za Kimaandiko ili mtaka kubatizwa ajue kile ambacho Neno la Mungu hutaka afanye akikabili hali kama hizo.
[Sanduku katika ukurasa wa 23]
Walibarikiwa kwa Sababu ya Msimamo Wao Imara
Sibongili Ni mjane Mkristo jasiri anayeishi Swaziland. Baada ya kifo cha mume wake cha hivi majuzi, alikataa kufuata desturi zifikiriwazo na wengi kuwa zinawatuliza wafu. Kwa mfano, hakunyoa nywele zake. (Kumbukumbu la Torati 14:1) Washiriki wanane wa familia walikasirishwa na jambo hilo na kumnyoa kwa nguvu. Pia waliwazuia Mashahidi wa Yehova wasimtembelee Sibongili nyumbani ili kumfariji. Hata hivyo, watu wengine wenye kupendezwa na ujumbe wa Ufalme walifurahia kumtembelea na kumpelekea barua za kufariji zilizoandikwa na wazee. Siku ambayo Sibongili alitarajiwa kuvaa mavazi maalumu ya kuomboleza, jambo lenye kushangaza lilitukia. Mshiriki mashuhuri wa familia alifanya mkutano kuzungumzia kukataa kwake kukubaliana na desturi za kimapokeo za kuomboleza.
Sibongili aliripoti hivi: “Waliniuliza kama imani yangu ya kidini iliniruhusu kuonyesha huzuni yangu kwa kuvaa mavazi meusi ya kuomboleza. Baada ya kueleza msimamo wangu, waliniambia hawatanilazimisha. Nilishangaa kwamba, wote waliniomba msamaha kwa kunitenda vibaya na kwa kuninyoa kwa lazima. Wote waliniomba msamaha.” Baadaye, dada yake Sibongili alisema aliamini kwamba dini ya Mashahidi wa Yehova ndiyo ya kweli, naye akaomba funzo la Biblia.
Fikiria mfano mwingine: Mwanamume mmoja aitwaye Benjamin kutoka Afrika Kusini alikuwa na umri wa miaka 29 aliposikia juu ya kifo cha ghafula cha baba yake. Wakati huo, Benjamin pekee ndiye aliyekuwa Shahidi katika familia yake. Wakati wa mazishi, kila mtu alitarajiwa kupita penye kaburi na kutupa kiasi kidogo cha mchanga kwenye jeneza.d Baada ya mazishi, washiriki wa familia wa karibu walinyolewa. Kwa kuwa Benjamin hakushiriki katika desturi hizo, majirani na washiriki wa familia walitabiri kwamba angeadhibiwa na roho ya baba yake aliyekufa.
“Kwa sababu nilimtumaini Yehova, sikupatwa na lolote,” asema Benjamin. Washiriki wa familia walitambua kwamba hakuadhibiwa. Baada ya muda, baadhi yao walianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na kuonyesha wakfu wao kwa Mungu kwa kubatizwa. Namna gani Benjamin? Yeye alijiunga na kazi ya wakati wote ya kueneza evanjeli. Kwa miaka michache iliyopita, amekuwa na pendeleo la kutumikia makutaniko ya Mashahidi wa Yehova akiwa mwangalizi asafiriye.
[Maelezo ya chini ya Sanduku katika ukurasa wa 23]
d Watu wengine huenda wasione ubaya wowote wa kutupa maua au mchanga kaburini. Hata hivyo Mkristo angeepuka zoea hilo kama jumuiya huliona kuwa njia ya kuwatuliza wafu au ikiwa kufanya hivyo ni sehemu ya sherehe zenye kusimamiwa na mhudumu wa dini isiyo ya kweli.—Ona gazeti la Amkeni! la Machi 22, 1979, ukurasa wa 15 (la Kiingereza).