Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 2/22 kur. 17-19
  • Kwa Nini Porojo Ni Mbaya?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Porojo Ni Mbaya?
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sababu Inayotufanya Tupige Porojo
  • Mitego ya Porojo Yenye Kudhuru
  • Kuzuia Porojo Zenye Kudhuru
  • Kusikiliza—Upande Mwingine wa Porojo
  • Ninaweza kuzuiaje porojo?
    Amkeni!—2007
  • Porojo Ina Ubaya Gani?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Porojo—Zina Madhara Gani?
    Amkeni!—1990
  • Porojo—Kwa Nini Zavutia?
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 2/22 kur. 17-19

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Porojo Ni Mbaya?

“Katika shule yetu ya sekondari, porojo imeenea kama ugonjwa wa kuambukiza. Hatuna tatizo la dawa za kulevya; au bunduki, au kupigana—tatizo ni porojo. Hilo ndilo tatizo kubwa.”—Michelle mwenye umri wa miaka 16.a

Watu fulani husema porojo inapendeza. Wengine husema porojo inadhuru. Kwa kawaida inapatikana kwa wingi kwenye magazeti na katika programu za televisheni. Pia porojo hufanya mazungumzo mengi yawe machangamfu. Porojo ni nini? Porojo ni mazungumzo ya kawaida juu ya watu na mambo yao ya kibinafsi.

Labda hakuna jambo linalonasa akili zetu upesi sana kuliko maneno haya, “Je, umesikia jambo ambalo limetokea?” Maneno yanayofuata yaweza kuwa kweli au uwongo—au labda ukweli kidogo na uwongo kidogo. Vyovyote vile, kishawishi cha kupiga porojo chaweza kuwa chenye nguvu. “Si jambo rahisi kuwa mtu asiyependezwa na mambo ya watu wengine,” asema Lori mwenye umri wa miaka 17. “Wewe na rafiki zako mnahisi ya kwamba unapopata habari yenye kuvutia, lazima uwaambie.”

Sababu Inayotufanya Tupige Porojo

Ni kwa nini tunavutiwa sana na porojo? Jambo la kwanza ni kwamba wanadamu ni viumbe wa kijamii. Yaani, watu hupendezwa na watu wengine. Hivyo basi, ni jambo tu la kiasili kupata kwamba baada ya muda maongezi yetu yatageukia mambo mapya katika maisha ya marafiki na watu tunaowafahamu.

Je, hilo ni jambo baya? Si wakati wote. Mara nyingi, maongezi ya kawaida huwa na habari zenye mafaa, kama vile ni nani anayefunga ndoa, ni nani aliyejifungua, na ni nani mgonjwa. Hata Wakristo wa karne ya kwanza walizungumza juu ya mambo mapya yaliyohusu maisha ya waamini wenzao. (Waefeso 6:21, 22; Wakolosai 4:8, 9) Kwa kweli, maongezi ya kawaida juu ya rafiki na watu tunaofahamiana nao ni sehemu muhimu ya jinsi tunavyowasiliana na kudumisha uhusiano mzuri.

Mitego ya Porojo Yenye Kudhuru

Ingawa hivyo, nyakati nyingine mazungumzo juu ya maisha ya wengine hayachochewi na hali ya kuwahangaikia. Kwa mfano, Deidra mwenye umri wa miaka 18 asema hivi: “Watu hupiga porojo ili wapendwe na wengine. Wanafikiri [watapendwa] kwa kujua habari nzuri kuliko ile ambayo wameambiwa.” Ile tamaa ya kuwapendeza wengine huenda hata ikamsukuma mpiga porojo apotoe mambo ya hakika. “Ikiwa unajua kisa chenyewe, una uwezo wa kukibadilisha,” aeleza Rachel mwenye umri wa miaka 17. “Ni kama hadithi uliyoibuni, na waweza kuipotosha jinsi upendavyo.” Nyakati nyingine, porojo isiyo ya kweli hutumiwa kama njia ya kulipiza kisasi. “Wakati mmoja nilieneza uvumi usio wa kweli kuhusu rafiki yangu,” asema Amy mwenye umri wa miaka 12. “Nilifanya hivyo kwa sababu alisema jambo fulani kunihusu.” Tokeo likawa nini? “Mwanzoni nilifikiri, Lo, nilikuwa nimemtendea jinsi alivyonitendea.” Hata hivyo, Amy aendelea kueleza: “Baada ya muda uvumi huo ukaenea zaidi, nikaanza kuhisi uchungu kuliko ule uchungu ambao ningalipata kama ningalinyamaza tu.”

Kama mtaalamu mmoja wa akili asemavyo, ni rahisi kuona namna porojo iwezavyo kuwa “kama moto uwezao kuenea kwa haraka.” (Linganisha Yakobo 3:5, 6.) Hili litukiapo, matokeo yaweza kuwa mabaya sana. Kwa mfano, namna gani ikiwa jambo ambalo lilipasa kuwekwa kama siri linaenezwa? Na namna gani ikiwa porojo hiyo si ya kweli na katika kuisambaza unaiharibu sifa njema ya mtu fulani? “Mmoja wa marafiki wangu alianza uvumi wa kwamba mimi hutumia dawa za kulevya, jambo ambalo si la kweli,” asema Bill mwenye umri wa miaka 12. “Jambo hilo liliniumiza sana.”

Kuzuia Porojo Zenye Kudhuru

Biblia ina sababu nzuri inaposema kwamba “mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi.” (Mithali 18:21) Naam, maneno yetu yaweza kuwa kama vyombo vya kujengea au kama silaha za kuharibu. Inasikitisha kwamba watu wengi leo hutumia ulimi wao kama silaha za kuharibu. Wao ni kama watu fulani wanaofafanuliwa na mtunga-zaburi Daudi kuwa “waliounoa ulimi wao kama upanga, wameielekeza mishale yao, maneno ya uchungu, wapate kumpiga mkamilifu faraghani.”—Zaburi 64:2-4. Wanaotaka kumpendeza Mungu hawapaswi kueneza ripoti zisizo za kweli, kwa kuwa Biblia hutaarifu kwamba “midomo ya uongo ni chukizo kwa BWANA.” (Mithali 12:22) Kuanzisha na kueneza kimakusudi uvumi unaojua kuwa si wa kweli ni kusema uwongo, na Biblia husema kwamba Wakristo wanahitaji ‘kuweka mbali ukosefu wa lililo kweli’ na ‘kusema kweli kila mmoja pamoja na jirani yake.’—Waefeso 4:25. Kwa hiyo kabla hujasema jambo fulani juu ya mtu mwingine, jiulize hivi: ‘Je, kweli ninajua mambo ya hakika? Je, yale nitakayoyasema yatamfanya msikilizaji wangu amdharau yule tunayeongea juu yake? Na ikiwa ni hivyo, nia yangu ya kusema mambo haya ni gani?’ Kumbuka hili: Hata ikiwa jambo fulani ni la kweli hiyo peke yake haitupi sababu ya kulieneza—hasa ikiwa habari hiyo itadhuru sifa ya mwingine.

Swali jingine la kujiuliza ni hili, ‘Kupiga porojo kutaathirije sifa yangu?’ Ndiyo, kwa kupiga porojo unasema jambo fulani kujihusu. Kwa mfano, Kristen asema hivi: “Ikiwa waweza kutumia wakati mwingi ukizungumza juu ya watu wengine, basi maisha yako ni lazima yawe hayapendezi.” Lisa aligundua kwamba sifa yake ya kuwa mpiga porojo ilimfanya rafiki yake wa karibu akose kumwamini. “Ilifikia hatua ambapo rafiki yangu alitilia shaka uaminifu wangu,” yeye asema. “Lilikuwa jambo baya sana—nikalazimika kuthibitisha kwamba angeweza kuniamini.”

Unapojulikana kuwa mpiga porojo, huenda watu wakakuona kama mtu anayeweza kudhuru, na huenda wasipendezwe tena kushirikiana nawe. Mithali moja ya Biblia hutaarifu hivi: “Mpiga porojo huzungukazunguka akifunua siri; usishirikiane na mtu afunuaye midomo yake sikuzote.” (Mithali 20:19, Beck) Lakini, je, ulijua kwamba waweza kuchangia porojo yenye kudhuru hata bila kutamka neno lolote?

Kusikiliza—Upande Mwingine wa Porojo

Angalau watu wawili wanahitajiwa ili kushiriki katika porojo—msemaji na msikilizaji. Ingawa huenda ikaonekana kwamba mwenye kusikiliza hana hatia kama msemaji, Biblia yatoa mwelekezo tofauti kuhusu jambo hilo. Twasoma hivi katika Mithali 17:4: “Mtenda mabaya husikiliza midomo ya uovu; na mwongo hutega sikio lake kusikiliza ulimi wa madhara.” Basi msikilizaji wa porojo ana hatia nzito. “Katika njia fulani ni jambo baya hata zaidi kusikiliza porojo kuliko kuisema,” asema mwandikaji Stephen M. Wylen. Kwa nini iwe hivyo? “Kwa sababu ukiwa msikilizaji mwenye hamu,” Wylen aendelea kusema, “unamtia moyo msemaji kuendelea.”

Basi yakupasa ufanye nini, usikiapo porojo yenye kuumiza? Bila kujionyesha kuwa mwadilifu, waweza kusema tu: ‘Acha tuyabadili mazungumzo’ au, ‘kwa kweli sipendi kuzungumza jambo hili. Isitoshe, yeye hayupo hapa ili ajitetee.’

Namna gani ikiwa watu wanajitenga nawe kwa sababu unakataa kushiriki kwa mazungumzo yao? Katika njia fulani hili laweza kukulinda. Jinsi gani? Kumbuka kwamba mtu anayekupigia porojo juu ya wengine yaelekea atawapigia wengine porojo juu yako. Kwa hiyo, waweza kujiepusha na huzuni nyingi kwa kuwa karibu na vijana na watu wazima wasiobomoa wengine kwa usemi wao. Wylen asema: “Hasara yoyote unayopata kwa kuepuka kupiga porojo, baada ya muda utapata kwamba hujapoteza chochote ila fursa ya kujiletea taabu. Mwishowe utaweza kuwasaidia wengine kwa sababu utapata sifa ya kuwa mtu anayeweza kutumainika.” Jambo muhimu zaidi ni kuwa utajifanyia jina zuri pamoja na Mungu. Yeye anapendezwa na jinsi tunavyosema juu ya wengine, kwa kuwa Yesu Kristo alionya hivi: “Kila usemi usio na faida ambao watu husema, watatoa hesabu kuhusu huo Siku ya Hukumu; kwa maana kwa maneno yako wewe utatangazwa kuwa mwadilifu, na kwa maneno yako utahukumiwa.”—Mathayo 12:36, 37. Ni mwendo wa hekima basi, kutii onyo hili la upole la mtume Paulo: ‘Fanya iwe shabaha yako kuishi kwa utulivu na kushughulika na mambo yako mwenyewe.’ (1 Wathesalonike 4:11) Kufanya hivyo kutakusaidia udumishe uhusiano mzuri na wengine na msimamo mzuri pamoja na Mungu.

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

“Njia Kubwa Zaidi Ulimwenguni ya Kupigia Porojo”

Je, umepata habari ya karibuni? Kuanzishwa kwa njia ya kupeleka habari kwa kompyuta, E-mail, kumefanya porojo ienezwe kupitia tekinolojia ya kisasa. Kwa kweli, mwandikaji Seth Godin anaiita E-mail “njia kubwa zaidi ulimwenguni ya kupigia porojo.” Ingawa anakiri manufaa zake, anaonya hivi: “Mtu fulani anaweza kuanzisha jambo ambalo ni hakika au ambalo lina makosa, na linaweza kwa ghafula kufikia maelfu ya watu.”

Ujumbe wa E-mail waweza kuwafikia watu wengi sana—na upesi sana. Godin asema: “Hiyo ndiyo njia mpya ya kwanza ya mawasiliano inayounganisha umaana wa jambo lililofikiriwa kimbele pamoja na uharaka na udharura kama ule wa simu.” Hivyo basi, unapopeleka ujumbe kupitia E-mail, hakikisha kwamba kusudi la ujumbe wako liko wazi. Na kamwe usiwapelekee rafiki zako habari ambayo haijathibitishwa.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mtu anayekupigia porojo juu ya wengine . . . yaelekea atawapigia wengine porojo juu yako

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki