Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 2/8 kur. 5-7
  • Porojo—Kwa Nini Zavutia?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Porojo—Kwa Nini Zavutia?
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Porojo—Mbadilishano wa Habari
  • Kufaana na Wengine
  • Porojo za Vyombo vya Utangazaji Habari
  • “Niliisikia Kupitia Mzabibu”
  • Porojo Zenye Nia ya Kuumiza—Ni Uchongezi
  • Porojo—Zina Madhara Gani?
    Amkeni!—1990
  • Uwezo wa Porojo
    Amkeni!—1992
  • Kwa Nini Porojo Ni Mbaya?
    Amkeni!—1999
  • Ninaweza kuzuiaje porojo?
    Amkeni!—2007
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 2/8 kur. 5-7

Porojo—Kwa Nini Zavutia?

KATIKA Kichina, zinaitwa shén-tán; katika Kifinlandi, juoru; katika Kiitaliano, pettegolézzo; katika Kihispania, chisme. Naam, porojo ziko ulimwenguni pote. Katika lugha fulani, porojo zaweza kuwa na maana isiyofaa kabisa. Katika Kiingereza neno “porojo” kwa msingi humaanisha “mazungumzo ya kiupuuzi,” kuzungumza-zungumza juu ya mambo yasiyo ya maana sana.

Hata hivyo, kwa kupendeza, neno la Kiingereza limepata maana isiyofaa. Hivyo, “porojo” mara nyingi hufuatwa na maneno “-enye nia ya kuumiza” au “-enye kudhuru.” Hii ni kwa sababu mazungumzo ya kiupuuzi mara nyingi hugeuka kuwa mazungumzo yenye kudhuru au yenye kuanzisha udhia. Yaweza hata yakageuka kuwa uchongezi kabisa, ambao umefafanuliwa kuwa “matamko ya mashtaka bandia au masingizio ambayo huvunja heshima na kuharibu sifa nzuri ya mwingine.” Basi haishangazi kwamba mithali moja ya kale husema: “Porojo huleta hasira kama vile upepo wa kaskazini haukosi kuleta mvua.”—Mithali 25:23, Today’s English Version.

Basi, kwa kufikiria uwezo wazo wa kudhuru, kwa nini sisi mara nyingi huziona porojo kuwa zisizozuilika, na zenye kuvutia sana? Mtu anaweza kutofautishaje kati ya porojo zenye kudhuru na zisizodhuru?

Porojo—Mbadilishano wa Habari

Kuna sababu ya msingi kwa porojo: Watu hupendezwa na watu. Kiasili, basi, tuna mwelekeo wa kuzungumza juu ya watu wengine. Kama vile Max Gluckman, mwanaanthropolojia, alivyosema wakati mmoja: “Kila siku, na kwa sehemu kubwa ya kila siku, wengi wetu hujishughulisha na porojo. Mimi nafikiri kwamba kama tungeweka rekodi ya jinsi tunavyotumia wakati wetu baada ya kuamka asubuhi, kupiga porojo kungekuwa kwa pili baada ya ‘kazi’—kwa wengine wetu—katika nambari.”

Yanapokuwa na kiasi na yenye fadhili, mazungumzo ya vivi-hivi yaweza kutumika kwa kubadilishana habari za maana, yakiwa njia ya kupata habari za matukio ya karibuni zaidi. Yanaweza kutia ndani mambo yasiyodhuru kama vile ni nani aliyeolewa, nani aliye mjamzito, na ni nani aliyekufa, au yaweza kuwa tu mazungumzo ya ucheshi yasiyo na nia ya kuumiza.

Hata hivyo, mara nyingi, mazungumzo ya kiupuuzi hupita mpaka wa kuwa na adabu na heshima. Mambo ya hakika yanarembeshwa, yanatiwa chumvi, au kupotoshwa. Aibu hufanywa kuwa chanzo cha ucheshi. Usiri huingiliwa. Mambo ya siri hufichuliwa. Sifa nzuri hudhuriwa au kuharibiwa. Mambo yanayostahili sifa yanafunikwa kwa malalamiko, manong’onezo, na kutafuta-tafuta makosa. Jambo la kwamba hakuna ubaya uliokusudiwa haliwezi kutuliza yule aliyezungumzwa juu yake. Hivyo porojo zenye kudhuru zimefananishwa na matope yenye kutupwa kwenye ukuta ulio safi. Huenda yasikwame kwenye ukuta, lakini huacha alama chafu sikuzote.

Kufaana na Wengine

Sababu nyingine ambayo huenda tukavutwa kwa urahisi katika porojo ni tamaa yetu ya asili ya kupendwa na kukubaliwa na wengine. “Kwa sababu moja au nyingine,” akaandika mwanasaikolojia John Sabini na Maury Silver, “una wajibu wa kuzungumza; na porojo ni njia ya kupendeza, iliyo rahisi, na inayokubalika ulimwenguni pote ya kutimiza wajibu huo.” (Moralities of Everyday Life) Kwa kadiri fulani, basi, porojo ni za maana katika kuendeleza mazungumzo, njia ya kufaana na wengine.

Tatizo ni kwamba watu huelekea kusisimuliwa na habari zisizofaa kuliko zile zinazofaa. Wengine hata ni kama hufurahia kushtuliwa na habari za kuogofya na zile mbaya kabisa. Hivyo porojo huvutia usikivu kweli kweli—kadiri habari izidivyo kuwa yenye kutisha na kuaibisha sana, ndivyo inavyovutia zaidi. Mara nyingi huwa hakuna kuhangaikia kuthibitisha masemekano hayo yenye kushtua.

Porojo za Vyombo vya Utangazaji Habari

Aina hii ya porojo huvutia upungufu mwingine wa kibinadamu—udadisi wa kupita kiasi. Sisi hupenda mambo ya siri. Tunafurahia kujua habari zote. Huko mapema kuanzia mwaka 1730, wakati Benjamin Franklin alipoanza kuandika safu juu ya porojo katika Pennsylvania Gazette, ilifahamika kwamba watu wangelipia porojo.

Porojo za vyombo vya utangazaji habari zaendelea kuwako—na kusitawi. Katika Ulaya meza za kuuzia magazeti kwa kweli hujaa kupita kiasi magazeti yenye habari kuhusu familia za kifalme, washindani wa magari, na watu wengine maarufu wa kitaifa. Hivyo makala moja ya gazeti iliiita porojo biashara kubwa.

Lakini je! inafaa kuwa mdadisi sana juu ya kile kinachotukia katika nyumba za faragha za watu wengine, vyumba vyao vya kulalia, na akilini mwao? Je! kusoma na kuona vitabu vinavyoelekea kuamsha tamaa za kingono kwaweza kweli kuwa kwenye afya njema? Bila shaka, porojo za vyombo vya habari hufanya udadisi upite mipaka inayofaa.

“Niliisikia Kupitia Mzabibu”

Uvumi usio na msingi na habari zisizo za kweli pia zimechochea porojo zenye kudhuru. Wakati wa Vita ya Wenyewe kwa Wenyewe ya Amerika, kamba za simu zilizokuwa na nyuzi kama za mzabibu zilizokuwa ndefu kweli kweli ziliwekwa kati ya vituo vya kijeshi. Hivyo “mzabibu” ukawa ndio ishara ya habari zisizohakikishwa bado, na maneno “Niliisikia kutoka kwa mzabibu” yakawa ndiyo kisababu chenye kupendwa na wengi cha kupitisha uvumi usio na msingi.

Kwa kusikitisha, mzabibu mara nyingi huzaa matunda machungu. Uvumi umekuwa kisababishi cha hofu ya ghafula, kifo, na hasara nyingi. Gharama kwa biashara pekee imekuwa isiyohesabika. Kampuni moja yenye mikahawa mingi ya kutayarisha vyakula vyepesi ilijaribu kwa muda wa zaidi ya mwaka mmoja kumaliza uvumi wa kwamba maandazi yao yalikuwa na funza. Kampuni moja iliyojulikana kwa utengenezaji bidhaa za sabuni ilitumia miaka—na mamilioni ya dola—ikijaribu kukomesha uvumi wa kwamba mfano wayo wa shirika ulikuwa alama ya Shetani na kwamba kampuni yenyewe ilihusika katika ibada ya kishetani.

Hata hivyo, ni watu mmoja mmoja ambao hupata maumivu ya moyoni na hasara kubwa zaidi kutokana na porojo. Na bado, kwa sababu hadithi potovu huwa zenye kuvutia, watu wanaelekea kuziendeleza bila kujali ukweli au matokeo yazo.

Porojo Zenye Nia ya Kuumiza—Ni Uchongezi

Wivu na chuki huwa ndio sababu ya aina ya porojo yenye uharibifu zaidi—porojo zenye nia ya kuumiza, au uchongezi. Neno la Kigiriki la “mchongezi” ni di·aʹbo·los, neno linalotafsiriwa katika Biblia kuwa Ibilisi. (Ufunuo 12:9) Jina hilo lafaa, kwa vile Shetani ni mchongezi mkuu wa Mungu. Kama vile Shetani, wengine husema juu ya watu wakiwa na makusudio mabaya. Wakati mwingine kusudi ni kulipiza kisasi, kutokana na maudhiko au wivu. Kwa vyovyote vile, wao hutafuta kuendeleza matamanio yao wenyewe kwa kuua jina zuri la wengine.

Ingawa porojo zenye nia ya kuumiza, au uchongezi, kwa wazi ni aina ya porojo yenye kulaumika sana, kujiingiza katika aina yoyote ya porojo zenye kuumiza, na zenye kuanzisha matata ni kukosa adili na kutochukua daraka. Basi, mtu awezaje kuzuia mazungumzo yasiyodhuru yasigeuke kuwa uchongezi wenye kudhuru?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Porojo za kirafiki mara nyingi hutumikia kusudi la kubadilishana habari za maana na kuendeleza mazungumzo

[Picha katika ukurasa wa 6]

Porojo zenye kudhuru ni kama matope yenye kutupwa kwenye ukuta safi. Huenda yasikwame kwenye ukuta, lakini huacha alama chafu sikuzote

[Picha katika ukurasa wa 7]

Watu wengine hupiga porojo ili wawavutie wengine

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki