Uwezo wa Porojo
KUJIUA kwa mwanamke huyo kijana kulishangaza mji huo wa Uingereza ulio mtulivu. Jambo la kushangaza hata zaidi lilikuwa ni ule mkataa wa baraza lililochunguza sababu ya kujiua kwa mwanamke huyo: ‘Yeye aliuawa na porojo za kiupuuzi!’ Kwa wazi, jina la mwanamke huyo kijana, sifa zake nzuri, na hata maisha yake yaliangamizwa na maongezi ya kiupuuzi yenye nia ya kuumiza.—Rumour and Gossip—The Social Psychology of Hearsay, ya Ralph L. Rosnow na Gary Alan Fine.
Ingawa mara nyingi matokeo hayawi yenye msiba jinsi hiyo, hakuna shaka kwamba porojo zina uwezo wenye kuhofisha. Kwa upande mmoja, zaweza kusifiwa kuwa njia ya kawaida ya kubadilishana habari za maana. Kwa upande ule mwingine, zaweza kuonwa kuwa kisababishi cha misukosuko ya serikali, migawanyiko ya familia, na mharabu wa kazi-maisha.
Porojo zimelaumiwa kwa ukosefu wa usingizi usiku, maumivu ya moyo, na ugonjwa wa tumbo kutoweza kuyeyusha chakula. Bila shaka zimekuletea hangaiko la binafsi wakati mmoja au mwingine. Kwa kweli, mwandikaji William M. Jones aonya kwamba katika ulimwengu wa biashara, “ni lazima ukubali uwezekano kwamba katika kazi-maisha yako mtu fulani atajaribu kukuumiza kwa porojo zisizofaa.”
Porojo zisizofaa zinachukiwa karibu ulimwenguni pote. Miongoni mwa Wahindi Waseminole wa United States, “kuzungumza lililo baya kuhusu yeyote” kunahesabiwa kuwa sawa na kudanganya na kuiba. Katika jamii moja ya Afrika Magharibi, wenye kupiga porojo walijasiria kukatwa midomo yao au, hata vibaya zaidi, walijasiria kuuawa! Kwa kweli, katika historia yote, hatua zimechukuliwa ili kuzuia porojo.
Kati ya karne ya 15 na 18, kile kilichoitwa eti kiti cha kuchovyea majini kilitumiwa sana katika Uingereza, katika Ujerumani, na, baadaye, katika United States ili kujaribu kuwaaibisha wapiga porojo waache kupayukapayuka maneno yanayodhuru. Mtu aliyepatikana na hatia ya kosa hilo angefungwa kwenye kiti na kuchovywa ndani ya maji mara kadhaa.
Ingawa viti hivyo vya kuchovyea majini hali kadhalika na mikatale iliachwa kutumiwa, jitihada kubwa dhidi ya porojo imefanywa hata katika nyakati za leo. Kwa mfano, katika miaka ya 1960, vituo viitwavyo eti vidhibiti-porojo vilianzishwa katika United States ili kupambana na uvumi ulioelekea kuwa wenye kudhuru shughuli za serikali. Huduma za aina hiyo hiyo zimeendeshwa katika Ailandi Kaskazini na katika Uingereza. Sheria hata zimepitishwa ili kuzuia porojo ambazo zimefanyizwa ili kusababisha madhara ya kiuchumi kwa mashirika fulani ya kifedha.
Juhudi hizo zijapokuwako, porojo zaendelea kuwapo. Ziko hai na zasitawi. Wala sheria wala njia yoyote ile ya kibinadamu bado haijaweza kuzima uwezo wazo wenye kuchoma. Porojo ziko kila mahali. Kuna porojo za ujirani, porojo za ofisini, porojo za dukani, porojo za karamuni, porojo za familia. Zinapatikana katika kila tamaduni, taifa, na ustaarabu, na zimesitawi katika kila sehemu ya jamii. Mtaalamu mmoja alisema: “Porojo ni za kawaida sana karibu ziwe kama kupumua.” Yeye alisema pia kwamba: ‘Zafanyiza sehemu kubwa sana ya asili ya kibinadamu.’
Ni kweli, porojo mara nyingi hufunua upande mbaya sana wa asili ya kibinadamu, upande ambao hupendezwa na kuchafua sifa nzuri, kupotoa ukweli, na kuangamiza maisha. Hata hivyo, porojo si jambo ovu kwa asili. Kuna upande mzuri kwa mazungumzo ya vivi-hivi. Kufahamu jinsi ya kutofautisha kati ya porojo zenye kudhuru na zile zisizodhuru ndio ufunguo wa kuepuka kuwaumiza wengine—na kutoumizwa nazo wewe mwenyewe.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Utumizi wa kiti cha kuchovyea majini ulikuwa njia moja ambayo mamlaka mbalimbali za vijiji zilijaribu kuwaadhibu wapiga porojo
[Hisani]
Historical Pictures Service