Vijana Wauliza . . .
Porojo—Zina Madhara Gani?
“Wao [vijana wenye kubalehe] . . . hutumia wakati wao kwa kukaa-kaa hapa na pale wakielezana porojo.”—Socrates, c. 400 K.W.K.
‘JE! UMESIKIA habari za karibuni zaidi?’ ‘Je! wajua?’ ‘We! mambo yamechacha, ebu sikia jambo hili!’ ‘Je! wewe waweza kutunza siri?’ Hizi zote ni tangulizi za kawaida za kueleza watu kuhusu mambo ya faragha, kutamanisha watu mambo wasiyoyajua, au hata habari za kushangaza sana kuhusu wengine—tabia ambayo yajulikana kuwa kupiga porojo.
Kama katika siku za Socrates, vijana hasa wangali wapenda sana tabia hiyo, na watafiti wakuita kupiga porojo kuwa hali ya ulimwengu wote iliyo kati ya watu wa rangi zote, umri, na utamaduni wote. Naam, kulingana na Journal of Communication, hata watoto wadogo hupiga porojo, “kuanzia karibu wakati ule ule ambao wao waweza kuongea na waweza kuanza kutambua wengine.”
Si ni sawa kusema kwamba kupiga porojo ni tabia ya wanawake peke yao? Si sawa! Watafiti Levin na Arluke walichanganua maongezi ya kikundi cha wanachuo wa kiume na wa kike. Tokeo likawa nini? Wale wa kiume walithibitika kuwa wenye elekeo la kupiga porojo sawasawa na wale wa kike!
Ingawa hivyo, kwa nini hasa twaona kupiga porojo kuwa jambo la kuvutia sana? Je! kuna sababu nzuri ya kujihadhari na jambo hilo?
Kupiga Porojo—Kwema, Kubaya, na Kusikopendeza
Porojo ni maongezi yasiyo ya maana sana. Ingawa hivyo, karibu nyakati zote hizo huelekeza fikira si juu ya vitu, bali juu ya vikasoro, vikosa, mafanikio, na mikasa ya watu. Maongeo ya jinsi hiyo hayahitaji kwa lazima kuwa yenye madhara wala yenye kuumiza. Ingawaje, ni asili ya kibinadamu kupendezwa na watu wengine. Biblia hata hutupa mawaidha ‘tuangalie, si upendezi wa kibinafsi kuhusu mambo yetu wenyewe tu, bali pia upendezi wa kibinafsi juu ya yale ya wengine.’—Wafilipi 2:4, NW.
Basi, porojo zikidhibitiwa kwa uangalifu zaweza kuwa ni badilishano la habari zenye mafaa. Kwa kielelezo, wewe hujuaje kwamba Bi. Jones ni mgonjwa na ahitaji msaada wa kununua vitu, kwamba John rafiki yako ameshuka moyo kwa kupoteza kazi afanyayo baada ya masomo, au kwamba Sally jirani yako anahama aende mbali? Je! ni kupitia tangazo fulani lililo rasmi? Sivyo, mara nyingi sana, watu hujua mambo haya kupitia kubwabwaja maneno kwa njia isiyo rasmi—kupiga porojo, ukitaka.
Neno la awali la Kigiriki lililotumiwa katika Biblia kwa “wapiga-porojo” lilitokana na kitenzi kilichomaanisha ‘kufurikwa na maneno.’ (1 Timotheo 5:13, NW; A Greek-English Lexicon, iliyotungwa na Liddell na Scott) Twakumbushwa juu ya maneno yaliyo kwenye Mithali 10:19: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.” Kanuni ya kidhahabu ambayo huhusika katika maongezi humaanisha kufikiri kabla hujanena!
Mpaka uliopo kati ya porojo zisizo na madhara na zenye madhara waweza kuwa mwembamba sana kwa njia isiyoonekana wazi. Kutangaza kwamba ‘John hafanyi kazi tena katika lile jengo lenye maduka mengi’ kwaweza kuwa ni hatua iliyobakiza kidogo tu kuongezea kwamba ‘Yaonekana John hawezi kudumisha kazi’—hiyo ikiwa ni hatua ya kujileta karibu na uchongezi! Mara nyingi hata majaribio ya kusema jambo zuri kuhusu mtu fulani huenda kombo. Taarifa ya kwamba, ‘Judy ndiye mwanafunzi mwenye akili zaidi darasani,’ yaweza kufuatwa upesi na, ‘Lakini umepata kuona jinsi yeye huvalia nguo?’ Na mara nyingi mno, porojo zaweza kuwa zisizopendeza hata kidogo, zikawa chombo cha kusafirishia mawongo yenye uchongezi na habari za uvumi kuhusu mtu fulani.
Porojo Zisizofaa—Kwa Nini Hutukia
Basi, kwa nini mara nyingi porojo huegemea mambo yasiyofaa? Kwanza, ‘moyo ni mdanganyifu,’ na mara nyingi maongeo yasiyofaa hutosheleza mahitaji fulani ya hisia-moyo za ubinafsi.—Yeremia 17:9.
“Mtu huhisi akiwa wa maana kwa sababu ya kujua jambo fulani ambalo wengine hawajui,” akiri Connie mchanga. Na mara nyingi sana hilo “jambo fulani” huwa ni kipande cha habari zisizopendeza hata kidogo kuhusu mtu mwingine. Wengine huelekea kuhisi kwamba kukazia kikiki dosari na makosa ya wengine huficha kasoro zao wenyewe. Na bado kwa wengine, porojo ni chombo cha kuendeleza umashuhuri wao wenyewe. Wao hujitahidi kuwa wajuaji ili wawe ndio wa kwanza kuambia wengine. Ili wafurahie muda huu mfupi wa kuwa mashuhuri kuliko wengine, watasaliti siri ya rafiki yao aliye mkubwa zaidi. Kumbuka kwamba, mtu ambaye hukueleza wewe kuhusu wengine kwa kawaida ataeleza wengine kuhusu wewe.
Porojo zaweza kutumiwa kama njia ifaayo ya kufungulia kasirani, umizo, na wivu uliojazana ndani. Watu fulani hata watageukia kutunga jambo lisilo la kweli ili waumize mtu fulani ambaye wao wana hisia mbaya za ndani kuhusu yeye. (Linganisha Mithali 26:28.) Hivyo, msichana mmoja alieneza uvumi kwamba mwanashule mwenzake alikuwa mwenye mimba—yaonekana kwa sababu huyo mwanashule mwenzake alikuwa akifanya matembezi ya kirafiki pamoja na mvulana ambaye yeye pia alimpenda.
Mara nyingi, kwa kadiri kubwa porojo zisizofaa hutokana na kutofikiri wala hazitokani sana na nia ya kutaka kuumiza. Tineja mmoja alikiri hivi: “Nyakati fulani mimi hung’amua kwamba labda jambo ambalo niko karibu kusema si la kweli mia kwa mia, lakini huwa ni kama nimekolewa na uzoelevu wa jambo hili. Mimi husema mambo kabla zijaweza kujizuia—na nyakati nyingi tatizo lenyewe hunirukia mimi baadaye.”
Porojo Zisizofaa—Upanga Wenye Makali Kuwili
Hata ziwe zachochewa na nini, porojo zisizofaa ni upanga wenye makali kuwili. Kwa upande mmoja, zaweza kusababishia jina na sifa ya mtu mwingine hasara isiyoweza kurekebishwa. Kama vile gazeti ’Teen lilivyoonelea: “Ukipiga porojo kuhusu watu wengine, uwachambue, uvunje uhusiano wa watu wenye kuaminiana, utie chumvi au hata useme uwongo wa wazi, hapo labda unakuwa ukihatarisha au kuharibu mahusiano—na yawezekana sana kwamba unazuia pia mahusiano mapya ya urafiki yasifanyike.” Au kama vile Biblia iwekavyo wazo hilo: “Afunikaye kosa hutafuta kupendwa; bali yeye akashifuye neno hutenga rafiki.”—Mithali 17:9; linganisha Mithali 16:28.
Kwa upande ule mwingine, porojo zaweza kufyatuka zikamrudia na kumletea hasara mpiga-porojo yule pia. Badala ya kuvuta watu watake kumsikiliza, porojo zaweza kuzalisha hali ya kutotumainiwa. “Hakuna mmoja ambaye hupiga porojo aweza kutumainiwa kwa kupewa siri,” yasema Mithali 11:13. (Today’s English Version) Na hakika mwenye kunenewa hatafurahi ikiwa na iwapo ajua kwamba siri fulani imefichuliwa au dosari ikatangazwa. “Porojo huleta kasirani sawa na vile kwa uhakika upepo wa kaskazi huleta mvua,” yasema Mithali 25:23.—TEV.
Mtu ambaye hunena mambo ya kupuuza ubora wa wengine hujijasirisha pia kuleta hasara ya uhusiano wake na Mungu. Mara nyingi maongeo malegevu huja kuwa ni uchongezi. Na Yehova hufanya ushirika na yule tu ambaye “hakuchongea kwa ulimi wake. Yeye hakufanya ubaya wowote kwa mwandamani wake.” (Zaburi 15:1, 3, NW) Hata hivyo, tuenezapo uvumi usio na msingi, huenda kwa kweli tukawa wahusika katika uwongo—jambo ambalo Yehova Mungu achukia.—Mithali 6:16, 17.
Kuepuka Mtego wa Porojo
Kuacha kuongea kuhusu watu wengine ni jambo ambalo ni kama haliwezekani—angalau kuliacha kabisa kabisa. Lakini matatizo mengi yaweza kuepukwa ukitumia ile kanuni ya kidhahabu: “Yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.
Hii yamaanisha kukataa kusikiliza porojo zenye kudhuru! “Ni lazima wewe usiwe na ushirika pamoja na mtu ambaye ni mwenye kushawishwa na midomo yake,” yashauri Biblia. (Mithali 20:19, NW) Ukisikiliza maongeo yenye nia ya kuumiza au yenye kuleta hasara, hapo unakuwa ukiyakubali. Kama vile kijana mwenye kuitwa Rosalyn awekavyo wazo hilo: ‘Watu ambao husikiliza porojo huwa tu wakiwatia moyo wapiga-porojo.’ Zaidi ya hilo, sikuzote huwa kuna ‘donge moja tamu’ la porojo hizo ambalo huvutia sana mtu hata akawa hawezi kujinyamazia na akawa sehemu ya mfululizo ule wa uchongezi wenye kuumiza.
Kwa hiyo jaribu kunyamazisha maongeo yasiyofaa. Hii haimaanishi kwa lazima kwamba usomee watu kuhusu maovu ya porojo zenye kudhuru. Lakini waweza kujaribu kubadili habari ile, ukigeuza maongeo yale yaelekee upande tofauti, au kusema jambo fulani la kumsifu yule anayezungumzwa. Maongeo yale yenye kuumiza yakiendelea, ione hiyo kuwa ndiyo ishara ya kuomba radhi utoke kwenye maongeo hayo.
Ndiyo, huenda jambo likawa la kweli kabisa—sembuse kuwa lenye kutekenya sana hisia na lenye kusisimua, lakini je! kweli lahitaji kusemwa? Je! litaudhi, lichongee, livunjie mtu heshima, au limwaibishe? Je! ungesema jambo hilo usoni pa mtu huyo? Wewe ungehisi namna gani mtu fulani akilisema kuhusu wewe? “Ulimi wa mwenye hekima hutamka maarifa vizuri,” yasema Mithali 15:2, “bali vinywa vya wapumbavu humwaga upumbavu.”
Kwa hiyo chunga midomo yako. Yasemwa kwamba akili pana huongea habari zenye mafaa, akili za wastani huongea habari za vitu, na akili haba huongea habari za watu! Katika maongeo yako sema mambo ya namna nyingi. Kuna mambo mengi—kutia na ya kiroho—ambayo yaweza kuandaa kuni za maongeo mazuri kuliko porojo zisizofaa kitu, zenye kuumiza.a
[Maelezo ya Chini]
a Toleo hili lina makala nyingine kuhusu kuwa jeruhi wa porojo.
[Picha katika ukurasa wa 18]
Mara nyingi mpiga-porojo huona shangwe ya kuwa ndiye mtu wa pekee mwenye kuelekezewa fikira
[Picha katika ukurasa wa 19]
Ukisikiliza maongeo yenye nia ya kuumiza au yenye kuleta hasara, hapo unakuwa ukiyakubali