Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Matatizo ya Likizo Nilifurahia sana makala “Jinsi Uwezavyo Kuepuka Matatizo ya Likizo.” (Juni 22, 1998) Nilijifunza mengi. Kwa mfano, sikujua kamwe kwamba kukaa bila utendaji fulani kwa vipindi virefu kwaweza kuongeza hatari ya kuganda kwa damu.
L. G., Marekani
Wanadamu—Je, Wao Ni Wanyama Tu wa Hali ya Juu? Ningependa kuwashukuru sana kwa ajili ya mfululizo wa makala “Wanadamu—Je, Wao Ni Wanyama Tu wa Hali ya Juu?” (Juni 22, 1998) Makala hizi zimefikiriwa na kuandikwa vizuri sana. Manukuu yenyewe ya vyanzo vyenye kujulikana yanafanya makala hizo ziwafae wataalamu. Mwishowe mtu anakubali tu kwamba tuliumbwa na Mungu.
A. D., Slovakia
Makala hizi zilikuwa zenye kuvutia. Bila shaka gazeti la Amkeni! huelewa jinsi ya kueleza kweli za ndani na zenye kutatanisha kwa sentensi zilizo sahili na zisizokanushika.
C. L. D., Ujerumani
Picha ya jalada ya makala hizo na mambo yaliyomo yalikuwa yenye kuvutia sana. Tunathamini sana jitihada zenu za daima za kuitetea kweli ya Biblia dhidi ya nadharia zenye hila. Katika kazi ya kuhubiri, toleo hili la Amkeni! liliamsha sana kupendezwa miongoni mwa vijana; na watu wengi wenye kukubali sababu walilipokea.
M. M., Italia
Roboti Yachunguza Mihiri Baada tu ya kusoma mfululizo wa makala zinazoonyesha pengo kubwa lililopo kati ya mwanadamu na wanyama, nilifikia makala yenye kichwa “Roboti Yachunguza Mihiri” katika gazeti hilo. (Juni 22, 1998) Makala hiyo ilieleza kwa njia dhahiri na isiyokanushika kama nini habari hii juu ya pengo la kiakili lililopo kati ya mwanadamu na wanyama!
G. D. M., Marekani
Namna Gani Asiponipenda? Leo nilipokea toleo la Amkeni! la Juni 22, na nilipoona makala “Vijana Huuliza . . . Namna Gani Asiponipenda?,” mara moja nilimshukuru Yehova kwa kujibu sala zangu. Nimeazimia kuichunguza makala hii pamoja na mama yangu na kutumia mashauri hayo maishani mwangu. Kwa kweli, mfululizo wa makala “Vijana Huuliza. . . .” ni uandalizi wenye upendo wa Yehova Mungu.
K. M., Kenya
Mimi ni mwanamke mwenye umri wa miaka 22, nami hufurahia kila toleo la gazeti lenu; lakini hii ilikuwa mara ya kwanza kwangu kuguswa moyo sana na makala moja. Nilipoanza kuisoma, nilianza kutokwa na machozi. Wakati fulani uliopita nilikuwa nahisi tu vile mnavyoeleza, nikawa na maswali mengi kuhusu hisia hizo. Makala hii ilinisaidia kufahamu mambo kwa njia iliyo wazi zaidi.
R. B., Lithuania
Niliposoma makala hiyo, nilifikiri, ‘Mtu alijuaje ninavyohisi?’ Nilifurahi sana kujua kwamba kwa fadhili Yehova anafahamu kila jambo. Gazeti hili limekuja leo, na hata ingawa ni katikati ya usiku, nilitaka kuwaandikia mara moja.
A. N., Japani
Ijapokuwa makala hiyo ilitayarishwa hasa kwa ajili ya wanawake, ilinifaidi sana. Juma moja awali, nilikuwa nimekataliwa vibaya sana na msichana mmoja, jambo ambalo liliniumiza. Makala yenu ilinisaidia kuchanganua hisia zangu. Ilinifariji na, jambo kubwa zaidi, ilinionyesha kwamba ninapochagua mke, ninahitaji kufikiria juu ya kutoa, wala si kupokea.
P. H. S., Brazili
Jamii ya Wakorea hukazia sana umuhimu wa msichana kuolewa mara tu anapofikia umri wa kuolewa. Si jambo rahisi kwa mwanamke Mkristo kusubiri hadi ‘anapopita mchanuko wa ujana’ kabla hajaolewa. (1 Wakorintho 7:36) Asanteni kwa ajili ya shauri hilo bora.
S. C., Korea