Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Magenge ya Mitaani Niliguswa moyo na makala zilizohusu magenge ya mitaani katika toleo la Amkeni! la Aprili 22, 1998. Sasa hivi mimi niko katika shule ya kuadibisha. Mama yangu ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, lakini mimi niliacha kwenda mikutanoni muda fulani uliopita. Kisha nikaanza kushirikiana na marafiki wasiofaa na pia nikajiingiza katika mfululizo wa wizi wa kutumia nguvu. Hiyo ndiyo sababu mama yangu alinipelekea nakala hii ya Amkeni! Mwanzoni nilifikiri, ‘Mambo haya tena!’ Lakini nilipoendelea kulitazama gazeti hili, nilivutiwa sana nikalisoma lote. Wakati nilipomaliza kulisoma, mawazo yangu yalikuwa yamebadilika. Kamwe sikufikiri kwamba Amkeni! lingeweza kunisaidia sana jinsi hiyo. Nataka nijirekebishe na nianze kuhudhuria mikutano tena. Sitaki kurudia makosa yangu tena na nataka nimtumikie Yehova muda wote wa maisha yangu.
M. S., Japani
Mimi ni mzazi asiye na mwenzi na nina mwana mwenye umri wa miaka 11 na binti mwenye umri wa miaka 9, na tunaishi katika eneo lenye magenge mengi. Nililisoma gazeti hili na mara moja nikalijadili pamoja na watoto wangu. Kupitia msaada wa makala hiyo, walitambua kwamba kujiunga na genge kamwe si njia ya badala ya kupata upendo au maisha ya familia yaliyo salama.
B. S., Marekani
Natoa shukrani tele kwa ajili ya makala hizo. Mara nyingi mimi huwahangaikia wapwa wangu ambao ni matineja, na habari mlizoandaa zimekuwa msaada mkubwa sana.
I. M. M., Brazili
Makala hizo zilitolewa kwa wakati ufaao kwa sababu wanadarasa wenzangu wako katika hatua ya kuanzisha genge. Baadhi yao hawana uhakika kama kweli wajiunge na genge au sivyo, kwa sababu kiongozi wa genge hilo aliwalazimisha waandike maandishi machafu kumhusu mkuu wa shule. Asante sana kwa kuwasaidia vijana katika nyakati hizi zenye magumu.
B. C. G., Mexico
Kusongwa Sana na Marafiki Ningependa kuelezea tu jinsi ambavyo niliithamini makala ya “Vijana Huuliza . . . Naweza Kuepukaje Kusongwa Sana na Rafiki Yangu?” (Aprili 22, 1998) Ingawa mimi ni mtu mzima ambaye ameolewa, wakati wote mimi huzifurahia makala hizi za vijana. Makala hii hasa ilifaa sana hali fulani ambayo inatupata na mume wangu hivi kwamba niliisoma mara tano mfululizo bila kuacha kusoma. Ilinisaidia kutambua kwamba hata Yesu alikuwa na uhitaji wa kuwa na wakati wa kibinafsi.
P. A., Trinidad
Kwa sababu ya kutoelewana katika mambo madogo-madogo, nyakati nyingine mimi na rafiki yangu huacha kuzungumziana, na hili hunifanya nihuzunike sana hivi kwamba siwezi kumakinika. Baada ya kuisoma makala hiyo mara kadhaa, nilitambua kwamba ninamsonga sana rafiki yangu na simpi wakati wa kufanya mambo mengine. Ninaona kwamba ni mimi hasa niliyeandikiwa makala hii, kwa sababu ilinionyesha njia nyingi za kuboresha mahusiano yangu na wengine.
R. S., India
Tiba ya Meno Yaliyoota Vibaya Hivi majuzi nilipoenda kumwona daktari wa meno, nilimpa nakala ya Amkeni!, Aprili 8, 1998, yenye makala kuhusu tiba ya meno yaliyoota vibaya. Huyo daktari wa meno baadaye alishukuru, akasema kwamba makala hiyo ilikuwa yenye kuelimisha na wazi, na iliandikwa kwa njia iliyo rahisi kueleweka. Aliongezea kusema kwamba amewapa baadhi ya wagonjwa nakala za makala hiyo ili iwasaidie kuelewa mpango wa matibabu yao.
T. P., Uingereza
Masimulizi ya Maisha ya Grace Marsh Ningependa kushukuru sana kwa ajili ya simulizi la Grace Marsh katika Amkeni! (Aprili 22, 1998) Nilijengwa na kutiwa moyo niliposoma juu ya ujasiri wake wa kuendelea kuhubiri japo upinzani. Hilo lilinifanya nithamini hata zaidi uhuru wa kuhubiri tulio nao ambao ulitokezwa na jitihada za akina ndugu wakati uliopita.
C. F., Marekani