Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Hangaiko la Habari Nawaandikia ili kuwashukuru kwa mfululizo wa makala “Hangaiko la Habari—Lakuathirije?” (Januari 8, 1998) Napenda kusoma, lakini ni sasa tu ambapo nimetambua kwamba nina wasiwasi wa kutaka kujua kila kitu. Makala hizi zilinisaidia kuwa na maoni yaliyosawazika.
M. E., Italia
Ningependa kuwapongeza kwa makala zenye habari nyingi. Nitathamini sana mkiniruhusu kunakili utangulizi wa makala hiyo katika kijarida cha shirika letu la kielimu na tekinolojia ya uandishi wa habari. Ule unaoitwa mfumo wa habari umesongamana, na ni kupitia kwa makala kama hizi ambapo mtu aweza kupashwa habari kwa njia ya unyoofu juu ya namna ya kukabiliana na kizazi cha habari.
G. D., Ghana
Idhini ilitolewa ya kunakili makala hiyo.—Mhariri.
Kumhofu Mungu? Nahisi msukumo wa kueleza jinsi nilivyopendezwa na makala “Maoni ya Biblia: Unaweza Kumhofuje Mungu wa Upendo?” (Januari 8, 1998) Kwa muda fulani nilikuwa nikitafakari swali hilo. Nilielewa kwamba kumhofu Mungu kulimaanisha kuwa na hofu inayofaa ya kutompendeza. Lakini, nilihisi uhitaji wa kuielewa habari hii kikamili. Kisha nikasoma makala hiyo. Hatimaye nikapata habari yenye kuridhisha juu ya kinachomaanishwa na kumhofu Mungu!
M. J. T., Marekani
Ukosefu wa Haki Warekebishwa Asanteni kwa makala “Mahakama ya Ulaya Yasahihisha Ukiukwaji wa Sheria.” (Januari 8, 1998) Kusikia juu ya ndugu zetu wakienda mahakamani ili wasilazimishwe kuingia katika utumishi wa kijeshi kulinikumbusha juu ya jinsi ndugu zetu walivyopata haki ya kuhubiri kutoka mlango hadi mlango siku za Jumapili. Habari kama hizo hunisaidia nisichukue pendeleo hili kivivi-hivi kamwe.
S. V., Marekani
Wainka Baada ya kusoma makala “Jinsi Wainka Walivyopoteza Milki Yao Yenye Fahari” (Januari 8, 1998), nalazimika kuwashukuru sana kwa simulizi hilo lenye kuelezwa vizuri na la kuhuzunisha. Jitihada zenu nyinyi Mashahidi za kuleta ujumbe wenye kufariji kwa wazao wa Wainka bila shaka zitawaliwaza sana. Asante Amkeni!, kwa kusema kweli.
S. B., Nigeria
Nina umri wa miaka kumi, na ningependa kutoa shukrani kwa makala hiyo. Nilishangazwa na barabara ya kilometa nyingi iliyojengwa na Wainka. Pia nilipendezwa na namna walivyopeleka ujumbe.
F. C., Marekani
Watoto Waondokapo Nyumbani Ninawashukuru kwa mfululizo wa makala “Watoto Waondokapo Nyumbani.” (Januari 22, 1998) Kuruhusu watoto wangu ninaowathamini waondoke kumekuwa jambo lenye kuumiza na la polepole. Hata hivyo, mlisema kweli. Maisha ya mzazi ambaye watoto wake wameondoka huboreka kwa kupita kwa wakati na kwa uelewevu. Sisi wazazi twaweza kufanya upya vifungo vyetu vya ndoa pamoja na wenzi wetu.
A. E., Kanada
Makala hizo zilijibu sala zangu. Kuondoka nyumbani kwa watoto kwaweza kuwa chanzo cha uchungu na hitilafiano. Lakini kwa shauri zuri la makala hii, amani na upendo zaweza kushinda.
P. N., Ufaransa
Nilihisi kana kwamba makala hizo ziliandikwa kwa ajili yangu hasa. Hivi karibuni niliondoka nyumbani ili kutumika katika eneo ambalo lina uhitaji wa waeneza-evanjeli wa wakati wote. Makala hizi zilinisaidia kuona namna wazazi wangu wanavyohisi na kushinda hisia zangu mwenyewe za hatia kwa kuwaacha. Zaidi ya hilo, nitatumia shauri katika sehemu inayosema “Neno kwa Watoto Walio Watu Wazima—Wasaidieni Wazazi Wenu Kuwaacha Mwende.” Hata ingawa niko mbali sana, nitaweza kuhisi ukaribu na wazazi wangu. Asanteni kwa makala kama hizi ambazo sikuzote hufika kwa wakati unaofaa.
G. U., Italia