Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kuboresha Maksi Mimi ni mwanafunzi shuleni, na ningependa kuwashukuru kwa ile makala “Vijana Huuliza . . . Je, Ningeweza Kufanya Vizuri Zaidi Shuleni?” (Machi 22, 1998) Ijapokuwa sikuzote maksi zangu zimekuwa juu ya wastani, kwa kweli sikuwahi kuona sababu ya kutosha kuziboresha. Lakini kwa sababu ya makala hii yenye kupendeza na kuchochea, naona waziwazi kwamba naweza kutimiza mengi zaidi kwa kuweka miradi inayofaa.
B. R., Marekani
Nina umri wa miaka 14, na kwa kweli sikupata kuelewa namna ya kujifunza. Niliamua kwamba mambo fulani hayangenifaidi wakati ujao na nikadhani hakukuwa na sababu ya kujifunza mambo hayo. Kusoma makala hii kulinifanya nibadili maoni yangu. Pia, nataka kuwashukuru kwa kueleza kwa njia yenye kutumika namna ya kujifunza!
K. F., Japani
Kusaga Meno Ile makala “Je, Wewe Husaga Meno Yako?” (Machi 22, 1998) ilifaa mahitaji yangu. Kwa kuwa nina tatizo hili, niliiona kuwa yenye kuelimisha na kutia moyo sana. Sikuwazia kamwe mngechapisha jambo fulani kuhusu habari hii. Kwa unamna-namna wa habari ya jinsi hii, mnagusa hisia za kila msomaji.
A. M. N. C., Brazili
Wanawake Nilipoanza kusoma mfululizo wa makala “Wanawake—Wana Wakati Ujao Gani?,” katika Amkeni!, la Aprili 8, 1998, machozi yalinitiririka. Sijawahi kuguswa moyo jinsi hiyo. Asanteni sana kwa kitia-moyo chenu cha kuendelea kutazamia wakati ujao ambapo kutendwa kwa njia ya uonevu kutakwisha.
C. J., Marekani
Niliguswa hisia na namna ya maisha magumu ya wanawake wengi duniani. Nilisikitika kusikia mambo yote wanawake hawa hulazimika kufanya—mara nyingi wakibeba mzigo wenye kulemea wakiwa peke yao. Mimi ni mama ya watoto wawili, na mara nyingi mimi husikitikia magumu mengi ninayoyapata. Makala hii ilinisaidia kutambua kwamba shida zangu maishani ni afadhali kuliko za wengine wengi.
K. S., Marekani
Kukabili Ujane Ningependa kueleza uthamini wangu wa moyo mweupe kwa simulizi la Barbara Schweizer, “Kupata Faraja Katika ‘Bonde la Uvuli wa Mauti.’” (Aprili 8, 1998) Sijampoteza mume, lakini nilipoteza wazazi wangu wote na kaka kwa muda usiozidi miaka mitatu. Barbara Schweizer alisema kwamba “huzuni yake ni kitu ambacho huja na kwenda.” Nilishukuru kusoma kwamba mtu fulani huhisi jinsi nihisivyo.
H. T., Hawaii
Mimi ni mweneza-evanjeli wa wakati wote mwenye umri wa miaka 17, na ijapokuwa sina matatizo yoyote makubwa, simulizi hili lilinitia moyo niwe na mtazamo wenye shangwe na wa kuazimia. Lilinifanya nielewe kwamba Yehova ananitegemeza na hataniacha kamwe.
T. C., Italia
Tiba ya Meno Yaliyoota Vibaya Asanteni kwa makala katika toleo la Aprili 8, 1998, “Tiba ya Meno Yaliyoota Vibaya—Inahusisha Nini?” Nina umri wa miaka 12 na karibuni nilianza kuvaa vifaa vya kubana meno. Sipendelei jambo hili sana. Lakini makala yenu ilielezea namna vitakavyonisaidia, na kwamba watu wengi huvaa vifaa vya kubana meno, hivyo sipaswi kuona aibu.
J. L., Kanada
Nilipendezwa sana na ile makala juu ya tiba ya meno yaliyoota vibaya! Tangu utoto nimetamani kuwa na meno mazuri. Hivi karibuni, moja ya meno yangu ya mbele lilivunjika, na ilinipasa kuvaa jino lililozibwa lililo ghali sana. Hapa Yugoslavia, mara nyingi madaktari wa meno hawana vifaa vihitajikavyo kwa kazi yao. Na madaktari wa meno wa kibinafsi wanatoza fedha nyingi sana kwa wengine wetu tusio na fedha. Jinsi ninavyotamani kwa hamu nyingi wakati ujao ambapo sote tutakuwa na meno yasiyo na kasoro!
B. E., Yugoslavia