Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 3/22 kur. 20-23
  • Namshukuru Yehova kwa Ajili ya Wanangu Watano

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Namshukuru Yehova kwa Ajili ya Wanangu Watano
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Badiliko la Kufikiri
  • Kuwazoeza Wana Wetu Watano
  • Yale Ambayo Wanangu Wanasema
  • Sababu ya Kuwa Mwenye Shukrani
  • Magumu na Baraka za Kulea Wana Saba
    Amkeni!—1999
  • Kumkaribia Mungu Kulinisaidia Niwezane na Hali
    Amkeni!—1993
  • Jinsi Matumaini Yangu Yalivyotimizwa
    Amkeni!—2002
  • Biblia Inabadili Maisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 3/22 kur. 20-23

Namshukuru Yehova kwa Ajili ya Wanangu Watano

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA HELEN SAULSBERY

Machi 2, 1997, ilikuwa mojawapo ya siku zenye kuhuzunisha sana maishani mwangu. Marafiki wapatao 600 pamoja na washiriki wa familia walikusanyika Wilmington, Delaware, Marekani, kwa ajili ya maziko ya mume wangu mpendwa, Dean. Alikuwa mzee Mkristo na mwangalizi-msimamizi wa kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova. Nifikiriapo ile miaka 40 yenye furaha katika ndoa yetu, ninakuwa na sababu nyingi za kushukuru. Ninajua kwamba Dean yuko mahali salama sana, katika kumbukumbu la Mungu Mweza-Yote, Yehova, na kwamba tutamwona Dean wakati ujao.

DEAN alijiandikisha katika jeshi la anga baada tu ya kufuzu katika shule ya sekondari mwaka wa 1950. Hakuwa mtu wa kidini na alipinga mafundisho ya Kanisa nililopenda la Katoliki. Hata hivyo tulikubaliana kuwalea watoto wetu katika Ukatoliki. Kila usiku tulipiga magoti na kusali kimya-kimya. Nilikariri sala zangu za Kikatoliki, naye Dean alisema mambo yoyote yaliyokuwa moyoni mwake. Katika miaka iliyofuata, tukawa na wana watano wa kiume: Bill, Jim, Dean Jr., Joe, na Charlie.

Nilikuwa mhudhuriaji mwaminifu wa kanisa na sikuzote nilienda na wanangu. Nilitamaushwa na kanisa, hasa na kuhusika kwake katika Vita ya Vietnam. Kadinali Spellman aliyekufa aliwaambia hivi watu ambao huenda wangetilia shaka haki ya hatua ya Marekani: “Naunga mkono maoni ya nchi yangu yawe yanafaa au hayafai.” Mimi singekubali wanangu waende vitani, hata ingawa kanisa langu lilihusika. Na bado, ningesali kwamba angalau mmoja kati ya wanangu angekuja kuwa kasisi na kwamba mume wangu angekuwa Mkatoliki.

Badiliko la Kufikiri

Jioni moja siku ya Jumamosi nilikuwa nikishirikiana na marafiki kadhaa Wakatoliki pamoja na kasisi wa mahali hapo. Tulipokuwa tukinywa na kujifurahisha mmojawapo wa wale wanawake alimuuliza kasisi: “Baba, je, ni dhambi inayoleta mauti ikiwa baada ya kujifurahisha hivi, unashindwa kuamka asubuhi ifuatayo ili kwenda kwenye Misa?”

“La, la,” yeye akajibu. “Hilo ni sawa. Jumanne usiku sisi hufanya Misa katika nyumba ya kasisi. Kwa njia hiyo unaweza kuja kwenye Misa na kutekeleza wajibu wako.”

Nilikuwa nimefunzwa tangu utotoni kwamba lazima uende kwenye Misa siku ya Jumapili bila kujali hali. Nilipokosa kukubaliana naye, alilaani na kwa hasira akasema kuwa mwanamke hapaswi kumsahihisha padri.

Nikajiuliza, ‘Je, nimekuwa nikisali ili wanangu wawe hivyo?’ Hata ingawa nilijua kwamba mapadri wote hawakuwa hivyo, jambo hilo lilinifanya nishuku upadri.

Katikati ya miaka ya 1960, Mashahidi wa Yehova walitutembelea katika Philadelphia, Pennsylvania, na baadaye huko Newark, Delaware. Ijapokuwa nilivutiwa na bidii yao ya Kikristo, sikuzote ningesema: “Samahani. Sipendezwi kwa sababu mimi ni Mkatoliki.”

Kisha, asubuhi moja yenye baridi katika mwezi wa Novemba mwaka wa 1970, Mashahidi wakaja tena. Wakauliza swali juu ya Biblia na kisha wakasoma Zaburi 119:105: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.” Maneno hayo yaliniathiri sana. Nakumbuka nikiwazia, ‘Biblia! Huenda hilo ndilo jibu, lakini sina hata moja.’ Nilikuwa nimefunzwa kwamba Wakatoliki hawakuhitaji Biblia, kwamba ingetutatanisha, na kwamba Biblia ilikuwa ya mapadri peke yao ambao wangesoma na kuieleza. Mimi nilidhani kwamba kutokuwa nayo kulinifanya niwe Mkatoliki mwaminifu-mshikamanifu.

Siku hiyo nikakubali kutoka kwa hao Mashahidi msaada wa kujifunza Biblia kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Nilikisoma juma hilo na nikajua tu kwamba nilikuwa nimepata kweli! Mashahidi hao walirudi na Biblia mbili, moja ikiwa ni tafsiri ya Kikatoliki. Nilistaajabu kuona kwamba maandiko yaliyonukuliwa katika kile kitabu yalikuwa pia katika Biblia ile ya Kikatoliki. Kuanzia hapo nikawa na Funzo la Biblia la nyumbani lenye maendeleo, na nikabatizwa mnamo Agosti mwaka wa 1972, pamoja na dada yangu Sally, aliyekuwa ameanza kujifunza Biblia pia.

Mume wangu Dean, hakunipinga kamwe, lakini alishtuka kuniona nikipendezwa na jambo jingine tofauti na dini ya Katoliki. Daima alikuwa akisikiliza na kutazama. Hapo awali, ilionekana kwamba sikuzote nilikuwa nikiwapigia wanangu kelele ili wanisikilize. Lakini nikajifunza kwamba Biblia huonya dhidi ya “hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi.” (Waefeso 4:31, 32) Mbali na hayo, watoto hawazoezwi kwa njia hiyo ya kuwapigia kelele. Wakati mmoja, nilimsikia mume wangu akimwambia mama yake kuhusu Mashahidi wa Yehova: “Mama, watu hao huzoea kufanya wanayohubiri!” Muda mfupi baada ya hapo, mume wangu alikubali funzo la Biblia. Dean akawa Shahidi aliyebatizwa katika Januari mwaka wa 1975.

Kuwazoeza Wana Wetu Watano

Nilipoanza kwenda kwenye Jumba la Ufalme, nilifikiri kwamba mikutano ilichukua muda mrefu kwa wanangu kuhudhuria. Hivyo ningewaacha nyumbani pamoja na baba yao. Lilikuwa jambo zuri na la kufurahisha kwenda peke yangu. Lakini, msemaji mmoja alipokuwa akizungumzia urefu wa mikutano ya Kikristo, aliuliza hivi: “Je, mmewahi kufikiria juu ya kipindi cha wakati ambacho watoto wako huweza kuketi wakitazama televisheni?” Wanangu walikuwa wakitazama televisheni wakati huo-huo! Kwa hivyo nikaamua kwamba, ‘Imetosha! Wataenda nami kwenye mikutano!’ Mume wangu akaniruhusu niandamane nao kwenye mikutano, na baada ya muda akaanza kuhudhuria pia.

Hudhurio la mikutano la kawaida liliyafanya maisha ya familia yetu yawe thabiti na yenye mpango. Lakini kulikuwa na faida nyingine. Mimi na Dean tulijaribu sikuzote kuboresha ustadi wetu wa kuwalea watoto, huku tukikubali makosa yetu na kutumia kwa uangalifu miongozo ya Biblia. Hatukuruhusu kamwe kuwapo kwa viwango maradufu. Yaliyokuwa sawa kwangu na kwa mume wangu yalikuwa sawa kwa wana wetu. Ilikuwa lazima tushiriki utendaji wa kuhubiri hadharani kwa ukawaida.

Ulipofika wakati wa vitumbuizo, hatukuruhusu sinema zenye jeuri, zisizo za adili. Sikuzote tulionea shangwe utendaji wa pamoja wenye kujenga wa familia, kutia ndani mchezo wa kuteleza kwenye barafu, kuviringisha tufe, kucheza gofu, kuzuru bustani za burudani, kuwa na mandari, na kufurahia mlo wa piza Ijumaa usiku. Dean alikuwa kichwa cha familia mwenye upendo. Wakati wote wa maisha yetu ya ndoa, tulitambua kwamba hivi ndivyo maisha yapaswavyo kuwa.—Waefeso 5:22, 23.

Nilipoanza kujifunza na Mashahidi wa Yehova katika mwaka wa 1970, Billy alikuwa na umri wa miaka 12, Jimmy 11, Dean Jr. 9, Joe 7, naye Charlie 2. Walikuwa wamezoea kwenda kanisani, lakini sasa walikuwa wakijifunza Biblia. Hilo lilitusisimua. Ningewaambia: “Njooni hapa mwone! Njooni hapa!” Wangekuja, nasi tungezungumzia kwa msisimuko jambo lililokuwa jipya kwetu. Kupitia kwa funzo letu la kitabu chenye mamlaka ya juu zaidi duniani, Biblia, wana wetu walikuwa wanajifunza kumpenda Yehova na kuhisi wakiwa na daraka kumwelekea akiwa Mungu na Muumba—si kuwa na daraka tu kwa baba na mama yao.

Kabla ya kujifunza kweli ya Biblia, tulikuwa na madeni mengi. Ili kulipia baadhi ya madeni hayo, tuliuza nyumba yetu na tukakodi nyingine. Tuliuza pia gari letu jipya na kununua gari lililotumika. Tulijaribu kuishi maisha sahili iwezekanavyo. Hili liliniruhusu nibaki nyumbani pamoja na wanangu badala ya kufanya kazi ya kimwili. Tulihisi kwamba wana wetu walihitaji kuwa na mama nyumbani. Hili liliniwezesha pia kutumia wakati zaidi katika huduma ya Kikristo wanangu walipokuwa shuleni. Hatimaye, katika Septemba mwaka wa 1983, nikawa painia (mhudumu wa wakati wote). Ni kweli kwamba, wana wetu hawakuwa na vitu bora zaidi kimwili sikuzote, lakini bado hawakuhisi wakiwa wamenyimwa isivyofaa. Kila mmoja wao alihudhuria chuo cha ufundi na walijifunza kazi za kilimo cha bustani, useremala, urekebishaji wa magari, na sanaa za maandishi. Kwa hivyo walikuwa wametayarishwa kujipatia riziki.

Nyakati nyingi ningefikiria maisha yetu ya familia na kujiambia, ‘Ijapokuwa tuna vitu vichache kimwili, nawazia kwamba familia yetu ni baadhi ya familia zenye furaha zaidi duniani.’ Upesi, Dean akaanza kujitahidi kufikia madaraka katika kutaniko, nao vijana wakafanya hivyo pia. Katika mwaka wa 1982, Dean aliwekwa kuwa mzee wa Kikristo. Miaka minane baadaye, katika mwaka wa 1990, mwana wetu wa kwanza, Bill, akawekwa kuwa mzee. Joe naye akawekwa mwaka huo-huo, Dean Jr. katika mwaka wa 1991, Charlie katika mwaka wa 1992, naye Jim katika mwaka wa 1993.

Najua kwamba kuna mambo ambayo hatukufanya vema tukiwa wazazi, na si jambo rahisi kukumbuka mambo tuliyofanya vema. Rafiki mmoja aliwauliza wanangu mambo wanayokumbuka kuhusu miaka yao ya mapema wakiwa Wakristo na hasa kanuni za Biblia walizojifunza tangu mazoezi yao ya mapema ambazo zimewasaidia kujitahidi kustahili kuwa wazee wa Kikristo. Maelezo yao huuchangamsha moyo wangu.

Yale Ambayo Wanangu Wanasema

Bill: “Yale tuliyosoma katika andiko la Waroma 12:9-12 huathiri fikira zangu. Andiko hilo lasema hivi kwa sehemu: ‘Katika upendo wa kidugu iweni na shauku nyororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wenye kuongoza. . . . Iweni wenye kuwaka roho. . . . Shangilieni katika tumaini.’ Wazazi wangu waliweza kuonyesha linalomaanishwa na kupenda watu. Ungeweza kuona kwamba kuonyesha wengine upendo kuliwaletea furaha. Hali hii ya upendo iliyokuwa nyumbani kwetu ilifanya kweli za Biblia ziwe sehemu ya kufikiri kwetu. Hilo ndilo lililotufanya tuishike kweli. Wazazi wangu waliipenda kweli ya Biblia kabisa. Kama tokeo, haikuwa vigumu kwangu kuipenda kweli, na wala haijawa kamwe vigumu kuishikilia kweli hiyo.”

Jim: “Mojawapo ya kanuni za kwanza zinazokuja kwenye akili yangu ni Mathayo 5:37: ‘Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, La yenu, La; kwa maana lizidilo hayo ni kutoka kwa yule mwovu.’ Sikuzote mimi na ndugu zangu tulijua yale wazazi wetu walitazamia tufanye, walikuwa mifano bora ya namna ambavyo Wakristo wanapaswa kuwa. Sikuzote wote wawili walitenda kwa upatano. Hawakubishana kamwe. Na ikiwa walikosa kukubaliana juu ya jambo lolote, sisi hatukujua hilo kamwe. Walikuwa na muungano, jambo ambalo bila shaka lilituvutia sote. Hatukutaka kuwatamausha Mama na Baba na, zaidi ya wote, Yehova.”

Dean: “Mithali 15:1 husema: ‘Jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.’ Baba alikuwa mwenye tabia ya upole. Hata sikumbuki nikibishana naye wakati wowote ule—hata nilipokuwa tineja. Sikuzote alikuwa mpole sana, hata alipokuwa amekasirika. Nyakati nyingine aliniadhibu kwa kunizuilia katika chumba changu au kwa kuniondolea mapendeleo fulani, lakini hatukubishana kamwe. Hakuwa tu baba yetu. Alikuwa pia rafiki yetu, nasi hatukutaka kumwaibisha.”

Joe: “Katika 2 Wakorintho 10:5, Biblia husema juu ya ‘kuingiza kila fikira katika utekwa ili kuifanya iwe tiifu kwa Kristo.’ Nyumbani kwetu tulifunzwa kutii viwango na maagizo ya Yehova. Kweli ilikuwa maisha yetu. Kuhudhuria mikutano kulikuwa njia ya maisha. Hata sasa siwazii kamwe kukosa mikutano ili nifanye jambo jingine. Huduma ya Kikristo ilikuwa pia sehemu ya kawaida ya maisha yetu—halikuwa kamwe chaguo. Marafiki zetu walikuwa katika Jumba la Ufalme. Hakukuwa na uhitaji wa kutafuta marafiki penginepo. Ni jambo gani zaidi awezalo baba kuwafanyia wanawe kuliko kuwaleta kwenye barabara iongozayo kwenye uhai!”

Charlie: “Mithali 1:7 ni lenye kutokeza katika akili yangu. Lasema hivi: ‘Kumcha BWANA ni chanzo cha maarifa, bali wapumbavu hudharau hekima na adabu.’ Wazazi wangu walitusaidia kumwona Yehova kuwa halisi na kuelewa umuhimu wa kusitawisha hofu na upendo kumwelekea. Wangesababu nasi, kwa kutuambia: ‘Usifanye hili kwa sababu tunakwambia tu. Wewe wafikirije? Unafikiri Yehova anahisije anapoona hili? Unafikiri Shetani anahisije?’

“Tulisaidiwa kuona uhakika wa jambo. Baba na Mama hawangeweza kuwa nasi kila wakati. Lile ambalo wangeweza kufanya tu ni kukaza kikiki kweli za Biblia katika mioyo na akili zetu. Tulipokuwa shuleni, kazini, na hata tulipokuwa na marafiki zetu hatukuwa na wazazi. Hofu hiyo ifaayo ya Yehova ilitokeza tofauti kubwa maishani mwetu—na ndivyo ilivyo hadi leo.

“Mama pia, alizungumza sikuzote juu ya huduma yake ya upainia na mambo mazuri yaliyoonwa aliyokuwa akipata. Sikuzote alikuwa na habari zenye kujenga sana kuhusu huduma, na hilo lilikuwa na tokeo bora kwetu. Tulisitawisha upendo kama wake kuelekea watu, nasi tukaja kuthamini kwamba utendaji wa mlango kwa mlango unaweza kuleta shangwe sana.”

Sababu ya Kuwa Mwenye Shukrani

Wanangu wameoa sasa, nami nina wakwe watano wazuri sana, wote wakiwa wanamtumikia Yehova kwa uaminifu. Nimebarikiwa pia kuwa na wana watano zaidi—naam, wajukuu wa kiume! Wote wakiwa wanalelewa ili wampende Yehova na kuuweka kwa uthabiti Ufalme wake mahali pa kwanza maishani mwao. Tunasali kwamba siku moja watakuja kuwa wazee, kama baba zao walivyo na kama vile babu yao alivyokuwa.

Muda mfupi baada ya kifo cha Dean, mmoja kati ya wanangu aliandika: “Nitamkosa sana baba yangu, kwa kuwa analala sasa. Sasa hana maumivu yoyote. Hateseki. Hakuna tena kupasuliwa, wala sindano, wala chupa za kumlisha—ana amani tu. Sikumwambia kwaheri kabla hajafa. Sikuzote mambo hayafanyiki unavyopanga. Ninaweza kusema tu kwamba nimeazimia kuishi maisha yangu ili niweze kuwapo wakati wa ufufuo ili kumkaribisha!”

Jinsi ninavyomshukuru Yehova kwa ajili ya mume wangu mpendwa na kwa tumaini hakika la ufufuo! (Yohana 5:28, 29) Na jinsi ninavyomshukuru Yeye kwa ajili ya wanangu watano!

[Picha katika ukurasa wa 23]

Helen Saulsbery na familia yake leo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki