Je, Kupatana Kwawezekana?
“Ni rahisi kuanza kutafuta talaka kwa ghafula,” chasema kitabu “Couples in Crisis,” “lakini lazima kuwe na ndoa nyingi ambazo kwa msingi zinafaa na ambazo zingeweza kufanikiwa ikiwa matatizo yangetatuliwa.”
MAONI hayo yapatana na fundisho la Yesu Kristo la kale kuhusu talaka. Ijapokuwa alisema kwamba mwenzi asiye na hatia anaruhusiwa kuchukua talaka kwa msingi wa kukosa uaminifu katika ndoa, hakusema kwamba ilikuwa lazima kufanya hivyo. (Mathayo 19:3-9) Huenda mwenzi mwaminifu akawa na sababu za kutaka kuokoa ndoa. Huenda mume mkosaji akawa bado anampenda mke wake bado.a Huenda akawa ni mume mwenye kujali na baba mwenye kujitoa anayeandaa mahitaji ya familia yake kwa kudhamiria. Kwa kufikiria mahitaji yake na yale ya watoto, huenda mwenzi mwaminifu akaamua kutafuta kupatana badala ya talaka. Ikiwa ndivyo, ni mambo gani yanayoweza kufikiriwa, na magumu ya kujenga ndoa upya yanaweza kukabiliwaje kwa mafanikio?
Kwanza ujue kwamba wala talaka wala kupatana si rahisi. Zaidi ya hayo, kumsamehe tu mwenzi mzinzi hakuelekei kutatatua matatizo ya msingi katika ndoa. Kwa kawaida ili kuokoa ndoa, kujichunguza kwa undani, mawasiliano ya waziwazi, na kazi ngumu hutakikana. Mara nyingi wenzi wa ndoa hupuuza kiasi cha wakati kinachotakikana na jitahada zinazotakikana kujenga upya ndoa iliyovunjika. Hata hivyo, wengi wamevumilia na kama tokeo wamekuwa na ndoa zilizo imara.
Maswali ya Kujibiwa
Ili kufanya uamuzi unaotegemea habari fulani, mwenzi mwaminifu anapaswa kuchanganua hisia zake na mambo tofauti-tofauti anayoweza kuchagua. Huenda akafikiria mambo yafuatayo: Je, anataka kurudi? Je, amekomesha kabisa kufanya uzinzi, au anasitasita kukomesha uhusiano huo? Je, ameomba radhi? Ikiwa ndivyo, je, ametubu kikweli, amejuta kwa moyo mweupe kuhusu jambo alilofanya? Au je, anaelekea kunilaumu kwa kosa lake? Je, anajuta kikweli kwa madhara ambayo amesababisha? Au badala ya hivyo, amefadhaika tu kwa sababu uhusiano wake haramu umefunuliwa na kuvurugwa?
Vipi kuhusu wakati ujao? Je, ameanza kurekebisha mitazamo na matendo yalioongoza kwenye uzinzi? Je, ameazimia kwa dhati kutorudia kosa hilo? Au bado ana mwelekeo wa kucheza kimahaba na kuwa na uhusiano wa kihisia-moyo usiofaa na watu wa jinsia tofauti? (Mathayo 5:27, 28) Je, amejitoa kikamili kujenga ndoa upya? Ikiwa ndivyo, anafanya nini kuhusu jambo hilo? Majibu yafaayo kwa maswali haya yaweza kuwa msingi wa kuamini kwamba inawezekana kurudisha uhusiano wa ndoa.
Mawasiliano Muhimu
“Pasipo mashauri,” asema mwandishi mmoja wa Biblia, “makusudi hubatilika.” (Mithali 15:22) Kwa hakika inakuwa hivyo mwenzi asiye na hatia anapohitaji kuzungumza kuhusu ukosefu huo wa uaminifu pamoja na mwenzi wake. Bila kuingilia mambo ya ndani sana isivyo lazima, wangeweza kuwa na mazungumzo yaliyo wazi na ya umakini ambayo yangeweza kutokeza ukweli kuhusu kilichotokea na kumaliza kutoelewana. Jambo hili laweza kuzuia wenzi wasizidi kutengana kwa sababu ya kutoelewana na kuwa na uchungu wa moyo wa muda mrefu. Ni kweli kwamba mume na mke wataona mazungumzo hayo kuwa yenye kutia uchungu. Lakini wengi wameona kwamba yanachangia fungu muhimu katika hatua ya kuaminiana tena.
Hatua nyingine muhimu kuelekea kupatana kwa njia yenye matokeo ni kujaribu kutambua sehemu zenye matatizo katika ndoa—mambo ambayo huenda wenzi wote wawili wakahitaji kuyafanyia kazi. Zelda West-Meads, ashauri hivi: “Baada ya kuzungumzia hali zenye kuhuzunisha, baada ya kuamua kwamba kwa kweli jambo hilo limemalizika, kwamba bado mnataka kubaki katika ndoa, tatueni kosa lililotokea na kuifanya upya ndoa [hiyo].”
Labda mlichukuliana kivivihivi. Huenda mlipuuza shughuli za kiroho. Labda hamkuwa mkitumia wakati wa kutosha pamoja. Labda hukumwonyesha mwenzi wako upendo mwingi, shauku nyororo, pongezi, na heshima aliyohitaji. Kukadiria upya miradi na maadili yenu mkiwa pamoja kutachangia fungu kubwa kuwaleta karibu zaidi na kutazuia kukosa uaminifu wakati ujao.
Kufanyia Kazi Msamaha
Kujapokuwa jitihada za moyo mweupe, huenda mwenzi aliyekosewa asione likiwa jambo rahisi kumsamehe mume wake, sembuse mwanamke yule mwingine. (Waefeso 4:32) Ingawa hivyo, inawezekana kuachilia mbali uchungu wa moyo hatua kwa hatua. Kitabu kimoja cha marejezo chashauri kwamba “mwenzi mwaminifu anapaswa kutambua kwamba wakati hufika ambapo wanahitaji kuacha kufikiria mambo hayo na kuanza maisha upya.” “Ni muhimu kutoendelea kutaja dhambi za zamani za mwenzi wako ili ku[mwa]dhibu kila mara mnapobishana.”
Wenzi wengi wameona kwamba kwa kujitahidi kupunguza au kuondoa hisia zenye uchungu mwingi, hatimaye wameacha kuhisi uhasama kuelekea mkosaji. Hiyo ni hatua ya maana katika kujenga ndoa upya.
Jifunze Kumwamini Tena
“Je, tutaweza kuaminiana tena?” akasema kwa maumivu mwanamke mmoja mwenye wasiwasi. Hangaiko lake ni halali kwa sababu udanganyifu wa mzinzi umeharibu—au angalau ukadhuru vibaya sana—kuaminiana. Kama vile chombo cha kuwekea maua chenye thamani, ni rahisi kuvunja tumaini lakini ni vigumu kulijenga. Uhakika ni kwamba wenzi wanapaswa kuaminiana na kustahiana, si kuendeleza tu uhusiano bali kuufanya usitawi.
Kwa kawaida itatia ndani kujifunza kumwamini mtu tena. Badala ya kudai kuaminiwa bila kujali hisia za mwenzake, mwenzi mwenye hatia anaweza kusaidia kujenga upya imani kwa kuwa wazi na kufuatia haki kabisa kuhusu utendaji wake. Wakristo wanatiwa moyo ‘waweke mbali ukosefu wa lililo kweli na kusema kweli’ mtu na mwenzake. (Waefeso 4:25) Ili kuaminiwa tena, huenda hapo mwanzoni “ukampa [mwenzi] wako ratiba sahihi kuhusu mipango yako hasa,” asema Zelda West-Meads. “Mwambie [mwenzi] wako mahali unapoenda, wakati utakaporudi na uhakikishe kwamba upo mahali uliposema utakuwapo.” Mipango ikibadilika, umwarifu.
Huenda kujistahi tena kukahitaji wakati na jitihada. Mwenzi mwenye hatia anaweza kusaidia kwa kuwa mwenye shauku nyingi na mwenye kupongeza sana—akimwambia mke wake mara nyingi kwamba anathaminiwa na kupendwa. Mshauri wa ndoa anayeheshimiwa ashauri hivi: “Mpe sifa kwa yote anayofanya.” (Mithali 31:31, Today’s English Version) Mke pia kwa upande wake, anaweza kujistahi tena kwa kufikiria mambo fulani maishani ambayo yeye hufanya vyema.
Inahitaji Wakati
Kwa kufikiria maumivu makali sana yanayosababishwa na kukosa uaminifu, haishangazi kwamba baada ya miaka mingi inawezekana kumbukumbu zilizo dhahiri na zenye kuhuzunisha zikawako. Hata hivyo, maumivu yanapopungua hatua kwa hatua, unyenyekevu, saburi, na uvumilivu kwa upande wa wote zitasaidia kujenga upya imani na staha.—Waroma 5:3, 4; 1 Petro 3:8, 9.
“Maumivu mabaya sana ya miezi michache ya kwanza hayadumu,” chatoa uhakikisho kitabu To Love, Honour and Betray. “Hatimaye [hu]pungua . . . Hatimaye unakuta kwamba siku, majuma, miezi na hata miaka inaweza kupita bila wewe kuyafikiria.” Unapoendelea kutumia kanuni za Biblia katika ndoa yako na kutafuta msaada na mwongozo wa Mungu, bila shaka utapata matokeo yenye kutuliza ya “amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora.”—Wafilipi 4:4-7, 9.
“Ninapokumbuka,” aripoti Pedro, “jambo hilo limebadili mwendo wa maisha yetu. Bado twahitaji kufanya marekebisho machache kwa ndoa yetu mara kwa mara. Lakini tumeokoka masaibu hayo. Bado tumefunga ndoa. Na tuna furaha.”
Lakini vipi ikiwa mwenzi asiye na hatia hana sababu ya kumsamehe yule asiye mwaminifu? Au vipi ikiwa anamsamehe mwenzi wake (kwa kiwango cha kuachilia uchungu wa moyo) na bado akiwa na sababu halali aamua kuchukua talaka inayokubaliwa na Biblia?b Talaka inaweza kumdai mtu mambo gani? Twakukaribisha ufikirie mambo yanayohusika katika talaka, na vilevile jinsi ambavyo wengine wamekabiliana nayo.
[Maelezo ya Chini]
a Ili kusahilisha mambo, kwa ujumla tutamtaja mwenzi mwaminifu kuwa mke. Hata hivyo, kanuni zinazozungumziwa pia zawahusu waume ambao wake zao si waaminifu.
b Tafadhali ona makala “Maoni ya Biblia: Uzinzi—Kusamehe au Kutosamehe?” katika toleo la Amkeni! la Agosti 8, 1995.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
MSAADA WA MAANA
Kwa kufikiria mambo mengi yanayoweza kuzingatiwa, huenda ikanufaisha kutafuta msaada kutoka kwa mshauri mwenye uzoefu na usawaziko. Kwa kielelezo, Mashahidi wa Yehova, wanaweza kuwafikia wazee wa kutaniko walio na fadhili na huruma.—Yakobo 5:13-15.
Washauri, marafiki, na jamaa wanatiwa moyo wasisisitize juu ya mapendezi yao wenyewe au kutetea au kulaumu uamuzi uliochukuliwa wa ama talaka iliyo na msingi wa Kimaandiko ama kupatana. Mwanamke mmoja Mkristo aliyetalikiwa anasihi hivi: “Toeni tu utegemezo mwingi, na mtuache tuamue la kufanya.”
Shauri lapaswa kutegemea Biblia peke yake. “Msiwaambie jinsi wanavyopaswa kuhisi au wasivyopaswa kuhisi,” adokeza mtu mmoja aliyetalikiwa. “Badala ya hivyo, waruhusuni wajieleze kwa uhuru.” Hisia-mwenzi, shauku ya kidugu, na huruma nyororo zitasaidia kupunguza majeraha makubwa sana yaliyosababishwa na usaliti wa ndoa. (1 Petro 3:8) Mshauri mwenye uzoefu alisema hivi: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; bali ulimi wa mwenye haki ni afya.”—Mithali 12:18.
Mume mmoja mwaminifu asema hivi: “Nilihitaji mtu mwenye kunielewa, maneno ya kufariji, na kutiwa moyo.” “Na mke wangu alitamani kupata mwelekezo hususa na kupongezwa kwa jitihada alizokuwa akifanya—msaada unaoonekana ambao ungemsaidia aendelee.”
Ikiwa baada ya kufikiria sana kwa uangalifu na kwa sala mtu aamua kumtaliki mwenzi wake au kutengana akiwa na sababu ya Kimaandiko, shauri lisitolewe katika njia inayoweza kumfanya mtu huyo ahisi kuwa na hatia. Badala ya hivyo, mtu huyo aweza kusaidiwa ashinde hisia za hatia zisizo na msingi.
“Ikiwa wataka kuwa chanzo bora cha kutoa faraja,” asema mhasiriwa mmoja, “usisahau kamwe hisia-moyo za kibinadamu zenye kina kirefu zinazohusika.”
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
SABABU INAYOFANYA WENGINE WASIACHANE
Katika jumuiya nyingi, kuna wake ambao hawana chaguo jingine ila kubaki na mume mzinzi asiyetubu. Kwa kielelezo, wanawake fulani Wakristo wanaoishi katika maeneo yenye mizozo au yenye kiwango cha chini cha kiuchumi wamebaki pamoja na mume asiye mwaminifu kwa ndoa ambaye huendelea kutunza watu wa nyumba yake katika mambo fulani-fulani, hata ingawa huenda asiwe mwamini. Kama tokeo, wana makao, ulinzi unaohitajiwa, mapato yenye kutegemeka, na uthabiti wa kiasi fulani wa kuwa na baba nyumbani—hata ingawa huenda asiwe mwaminifu. Wamesababu kwamba kwa kubaki pamoja, ijapokuwa si jambo linalopendeza au lililo rahisi, kumewawezesha—katika hali zao hususa—kudhibiti maisha yao kwa kiwango kikubwa kuliko jinsi ambavyo wangefanya ikiwa wangeng’ang’ana kivyao.
Baada ya kuvumilia hali hiyo—nyakati nyingine kwa miaka mingi—baadhi ya wake hawa hatimaye wamepata shangwe ya kuona waume wao wakibadili njia zao na kuwa Wakristo waaminifu na wenye upendo.—Linganisha 1 Wakorintho 7:12-16.
Kwa hiyo, wale wanaoamua kubaki na mwenzi—hata ikiwa si mwenye kutubu—hawapaswi kuchambuliwa. Wamelazimika kufanya uamuzi mgumu na wanapaswa kupewa msaada wowote na utegemezo wanaohitaji.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
NI NANI MWENYE KULAUMIKA?
Ni kweli kwamba katika visa fulani huenda kutokamilika kwa mwenzi kuwe kulichangia mkazo katika uhusiano, lakini Biblia husema kwamba “kila mmoja hujaribiwa kwa kuvutwa na kutongozwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetungika mimba, huzaa dhambi; nayo, dhambi, wakati imetimilika, hutokeza kifo.” (Yakobo 1:14, 15) Ijapokuwa kunaweza kuwa na mambo mbalimbali yanayochangia uzinzi, ‘tamaa ya mtu mwenyewe’ ndiyo hasa kisababishi cha msingi. Ikiwa kasoro za mwenzi husababisha matatizo ya ndoa, kwa hakika kufanya uzinzi si njia ya kuzitatua.—Waebrania 13:4.
Badala yake, matatizo ya ndoa yanaweza kutatuliwa mume na mke wakitumia daima kanuni za Biblia. Inatia ndani “kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake.” Pia wanapaswa kudumu katika kudhihirisha sifa kama vile “shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu.” La maana zaidi, wanapaswa ‘kujivika wenyewe upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.’—Wakolosai 3:12-15.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Kusikiliza kwa umakini mtu na mwenzake kwaweza kusaidia wenzi wajenge ndoa upya