Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kujiua kwa Vijana Ningependa kuwashukuru kwa ajili ya makala mfululizo “Vijana wa Leo Wana Tumaini Gani?” (Septemba 8, 1998) Niliguswa sana hadi nikalia. Nimejaribu kujiua mara kadhaa. Lakini ninafurahi kwamba sikufaulu.
A. Z., Jamhuri ya Cheki
Hizi zilikuwa makala zenye kutoa uelewevu juu ya habari inayohitaji kushughulikiwa kwa busara. Mapema mwaka huu nilijaribu kujiua nilipoelezwa na daktari kuwa nilikuwa na mshuko-moyo. Asanteni kwa habari hii ya wakati wake. Iliokoa uhai wangu.
R. P., Uingereza
Inasikitisha sana kwamba, wanadarasa wenzangu wawili wamejaribu kujiua. Mmoja wao alifanya hivyo kwa sababu alipofikiri juu ya wakati ujao, yeye hakuona jambo lolote lenye kutumainisha—ila tu magumu yaliyohitaji kushindwa. Kwa hiyo makala hii ilikuwa yenye kutumika, kwa kuwa ilieleza kwa njia ya wazi sana na hususa jinsi wakati wetu ujao unavyoweza kuwa na kusudi.
R. D., Hispania
Makala yenu iliugusa moyo wangu. Ilikuwa kana kwamba Yehova alikuwa akiongea nami kama Baba mwenye upendo. Nilipokuwa mtoto, nilitendwa vibaya na baba yangu. Nimekuwa nikihisi sifai na mara nyingi nimefikiria kujiua. Lakini sasa, kama makala yenu ilivyodokeza, ninakuza tamaa ya “uhai ulio halisi.”—1 Timotheo 6:19.
S. R., Brazili
Asanteni, hasa kwa sababu ya manukuu kutoka kwa vijana, mengi yake yakiwa na utatuzi wa matatizo kwa maneno machache tu.
W. H., Ujerumani
Kuchuma Pesa Asanteni sana kwa ajili ya wakati mliotumia kuchapisha makala yenye kuelimisha yenye kichwa “Vijana Huuliza. . . Naweza Kuchumaje Pesa?” (Agosti 22, 1998) Ilikuwa vigumu kwangu kupata kazi ya kuajiriwa. Lakini nilifuata mapendekezo yenu na ndipo nilipopata kazi hatimaye!
S. D., Ghana
Lugha ya Ishara Baada ya kusoma makala yenu “Lugha Ambayo Waiona!” (Septemba 8, 1998), ilinilazimu kuwaandikia ili kuwashukuru. Makala kama hii hutusaidia kuwaelewa wengine walio katika hali zinazotofautiana na zetu. Nina rafiki aliyezaliwa akiwa kiziwi, na nimekuwa nikitaka kujifunza lugha ya ishara. Lakini kwa sababu moja au nyingine, sijafaulu kamwe kupata wakati wa kujifunza. Sitaahirisha tena kamwe kujifunza lugha hiyo!
M. E., Uingereza
Ningependa kuwashukuru kwa ajili ya jitihada yenu kubwa ya kuwategemeza viziwi. Niliwapa maofisa wa serikali nakala kadhaa za makala yenu. Waliomba nakala zaidi, kwa sababu makala hiyo iliandikwa kwa njia bora sana! Nilimwonyesha pia mwanamke aliyempinga binti yake kiziwi kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Baada ya kusoma makala hiyo, alitokwa na machozi ya shangwe. Sasa anaunga mkono jitihada za binti yake za kuhudhuria mikutano na hata ameahidi kumlipia nauli ya kwenda kwenye mkusanyiko wa Kikristo!
E. R., Mexico
Nimelazimika kuwajulisha jinsi ambavyo nilithamini makala hiyo. Nilikuwa na mradi wa kujifunza Lugha ya Ishara ya Marekani ili nisaidie katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova la mahali hapa la lugha ya ishara. Lakini nilikuwa nimevunjika moyo. Makala hiyo ilinipa kitia-moyo nilichohitaji ili kufikia mradi wangu!
N. D., Marekani
Ilivutia sana kujifunza kwamba Viziwi kwa hakika hufikiri katika lugha yao ya ishara. Kwa kuwa nina uwezo wa kusikia, nitakuwa mwangalifu kutafuta njia zinazofaa zaidi za kuwasiliana na Viziwi.
P. H., Marekani