Kupoteza Kiungo cha Mwili—Jinsi Uwezavyo Kupunguza Hatari Hiyo
VISA vingi vya kupoteza viungo vya mwili vyaweza kuzuiwa! Na ndivyo ilivyo hata kwa watu wanaougua maradhi ya mishipa (PVD). Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, mara nyingi PVD husababishwa na ugonjwa wa kisukari.a Kwa uzuri, ugonjwa wa kisukari unaweza kudhibitiwa.
“Mlo ni muhimu sana katika kutibu ugonjwa wa kisukari iwe umeagizwa utumie insulini au la,” kichapo The Encyclopædia Britannica chasema. Dakt. Marcel Bayol, wa Kings County Hospital huko New York City, aliliambia gazeti la Amkeni! hivi: “Ikiwa watu wenye kuugua kisukari wanakuwa waangalifu kwa hali yao, na kuzingatia mlo wao, na kufuata mwelekezo wa kitiba, watapunguza hatari ya kupoteza kiungo cha mwili.” Wale walio na ugonjwa wa kisukari kisichohitaji insulini na ambao hufuata shauri hili huenda wakapata nafuu baada ya muda.b
Mazoezi Ni Muhimu
Mazoezi ni muhimu pia. Mazoezi husaidia mwili kudumisha vipimo vya glukosi, au sukari katika viwango vya kawaida. Ugonjwa wa PVD unapogunduliwa, kufanya mazoezi husaidia kudumisha nguvu, miendo, na mzunguko wa damu kwenye sehemu zenye madhara. Mazoezi pia husaidia kupunguza maumivu makali kwenye misuli ya shavu la mguu—maumivu ambayo huenda yakahisiwa na wale wanaougua PVD wanapotembea au kufanya mazoezi. Hata hivyo, wenye maradhi haya wanapaswa kuepuka kufanya mazoezi yanayokaza na kushtua miguu. Mazoezi yanayofaa zaidi yanatia ndani matembezi, kuendesha baiskeli, kupiga makasia, kuogelea, na mazoezi ya majini yanayofanya upumue kwa kasi. Mtu apaswa kupata ushauri wa daktari kabla ya kufuata utaratibu maalum wa mlo au mpango maalum wa kufanya mazoezi.
Bila shaka, mtu yeyote anayetaka kuwa na afya njema ataepuka kuvuta sigareti. PVD ni mojawapo tu ya magonjwa mengi yanayosababishwa au kuzidishwa na uvutaji wa sigareti. “Uvutaji wa sigareti ni kisababishi kikuu cha kukatwa viungo, hasa ikiwa mvutaji anaugua kisukari na PVD,” asema Dakt. Bayol. Huchangia kwa kadiri gani? Kichapo kimoja cha kuwasaidia waliokatwa viungo vya mwili waishi maisha ya kawaida chasema kwamba “uwezekano wa wavutaji wa sigareti kukatwa kiungo cha mwili ni mara 10 zaidi ya wale wasiovuta sigareti.”
Kutunza Viungo vya Mwili Vinavyougua
Maradhi ya PVD yanaweza kupunguza mzunguko wa damu kwenye viungo vya mwili, hali inayoweza kutokeza ugonjwa unaoitwa neuropathy—kufa, au kufa ganzi kwa neva. Hivyo basi viungo vya mwili huwa katika hatari ya kujeruhiwa, hata wakati ambapo mtu anapumzika tu kitandani. Kwa mfano, kwa kuwa mgonjwa hawezi kuhisi maumivu yoyote, anaweza kuchomeka vibaya sana iwapo blanketi yake ya umeme au kitu chenye kupasha joto kitatoa joto jingi kupita kiasi! Hiyo ndiyo sababu watengenezaji wa vifaa hivyo huwatahadharisha wanaougua kisukari wawe waangalifu wanapotumia vifaa hivyo.
Viungo vya mwili vinavyougua pia huweza kuambukizwa kwa urahisi. Mkwaruzo mdogo tu waweza kutokeza vidonda, au hata sehemu hiyo kuoza. Hivyo utunzaji wa miguu ni muhimu, na hii hutia ndani kuvaa viatu visivyofinya na vinavyotoshea vizuri na kudumisha miguu na nyayo zikiwa safi na kavu. Hospitali nyingi zina kliniki za kutibu miguu ambazo huwaelimisha wagonjwa juu ya utunzaji wa miguu.
Wakati ambapo maradhi ya PVD yamefikia hali ambayo inahitaji upasuaji, kwa kawaida madaktari wapasuaji hujaribu kuepuka kukata kiungo cha mwili. Mojawapo ya tiba ya badala ni katheta ya puto. Daktari wa mishipa huingiza katheta iliyo na ncha yenye puto. Hewa huingizwa katika puto, na kisha puto hupanua mishipa iliyoziba. Tiba nyingine ni upasuaji wa kuondoa mishipa ya damu iliyoharibiwa na ugonjwa na mahali pake kuweka mishipa iliyotolewa sehemu nyingine ya mwili.
Barbara, mwenye umri wa miaka 54, amevumilia ugonjwa wa kisukari kinachohitaji insulini tangu alipokuwa na umri wa miaka minne. Baada ya kujifungua mtoto wa kwanza, miguu yake ilishikwa na maradhi ya PVD. Baadhi ya madaktari walimshauri akatwe miguu hiyo. Hata hivyo, Barbara alimpata daktari mashuhuri wa mishipa aliyetumia mbinu ya katheta yenye puto kuboresha mzunguko wa damu kwenye miguu yake. Mbinu hiyo ilifanikiwa kwa muda fulani, lakini hatimaye Barbara alihitaji kufanyiwa upasuaji wa kubadili mshipa, ambao ulifaulu. Sasa Barbara hutunza miguu yake kwa uangalifu sana.
Epuka Jeraha
Jeraha ni kisababishi cha pili cha kupoteza viungo vya mwili. Kwa kuwa jeraha halichagui kiungo fulani hususa cha mwili, hilo laweza kuharibu sehemu yoyote ya mwili. Hata hivyo, kuwa na maoni ya kimungu juu ya maisha kwaweza kupunguza sana hatari ya mtu kujeruhiwa. Wakristo wanapaswa kuiona miili yao kuwa zawadi kutoka kwa Mungu, wawe wanafanya kazi, wanaendesha gari, au wanafurahia tafrija. Hivyo, watatii matakwa yote ya usalama na kuepuka kuhatarisha maisha yao kwa upumbavu.—Waroma 12:1; 2 Wakorintho 7:1.
Ni hatua gani zinazochukuliwa ili kupunguza hatari ya kujeruhiwa katika nchi zenye mabomu yaliyotegwa ardhini? Serikali nyingi zimefadhili mipango ya kuwaelimisha watu kuhusu hatari za mabomu ya kutegwa ardhini. Kulingana na ripoti ya katibu-mkuu wa Umoja wa Mataifa, mipango hii huelimisha “watu walio hatarini . . . jinsi ya kupunguza hatari za kuyakanyaga wanapoishi na kufanya kazi katika maeneo yenye mabomu hayo.”
Kwa kusikitisha, “watu huzoea kuishi kwenye sehemu za mabomu yaliyotegwa ardhini na kuanza kuyapuuza,” yasema ripoti moja ya Umoja wa Mataifa. “Nyakati nyingine mawazo ya kidini huwatia [watu] moyo wawe na maoni ya kwamba mambo kama haya ni mipango ya Mungu.” Hata hivyo, Neno la Mungu haliungi mkono maoni ya kwamba hiyo ni mipango ya Mungu. Kinyume na hilo, Biblia huwatia watu moyo wazingatie tahadhari na usalama.—Kumbukumbu la Torati 22:8; Mhubiri 10:9.
Hivyo, kwa kutahadhari na kuchukua hatua zinazofaa kulinda afya yako, unaweza kupunguza sana hatari ya kupoteza kiungo cha mwili. Lakini namna gani wale ambao tayari wamepoteza viungo? Je, bado wanaweza kufurahia maisha bora?
[Maelezo ya Chini]
a Maradhi ya mishipa ya sehemu za chini kabisa za mwili yanaweza pia kusababishwa au kuzidishwa ikiwa mtu huvaa mavazi yanayobana sehemu za chini za mwili au viatu visivyomtosha au ikiwa ameketi (hasa akiwa amekingamanisha miguu) au kusimama kwa muda mrefu.
b Watu wenye ugonjwa wa kisukari kinachohitaji insulini wanahitaji kupigwa sindano ya insulini kila siku. Mara nyingi wale wanaougua ugonjwa wa kisukari kisichohitaji insulini wanaweza kudhibiti hali yao kwa kuzingatia mlo na kufanya mazoezi. Katika Marekani, asilimia 95 ya watu wanaougua kisukari wana aina ile isiyohitaji insulini.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Kuvuta sigareti huongeza sana hatari ya kupoteza kiungo cha mwili, hasa kwa wale wanaougua maradhi ya mishipa
[Picha katika ukurasa wa 5]
Mazoezi yanayofaa na mlo mzuri hujenga mfumo wa mishipa wenye afya