Mamilioni Watahudhuria—Namna Gani Wewe?
ZAIDI ya watu milioni nane ulimwenguni pote huhudhuria mikusanyiko ya wilaya ya Mashahidi wa Yehova kila mwaka. Mwaka huu, Mikusanyiko 27 ya Wilaya ya siku tatu ya “Neno la Mungu la Kiunabii” imepangwa kufanywa katika Afrika Mashariki. Yaelekea kwamba kutakuwa na mkusanyiko karibu na mahali unapoishi. Tunakutia moyo uwepo programu inapoanza kwa muziki saa 3:30 asubuhi siku ya Ijumaa.
Programu ya asubuhi itatia ndani hotuba ya kukaribisha pamoja na hotuba ya msingi yenye kichwa “Sikiliza Neno la Mungu la Kiunabii.” Wakati wa alasiri mfufulizo wenye kichwa “Pendezwa na Kusoma Neno la Mungu” utaandaa madokezo yenye kutumika kuhusu jinsi ya kufanya usomaji wa Biblia uwe wenye kunufaisha na kufurahisha. Hotuba ya kumalizia siku hiyo, “Wapiganao na Mungu Hawatashinda,” itapitia vita vinavyopiganwa katika nyakati za kisasa dhidi ya wapiga-mbiu wa Ufalme wa Mungu.
Programu ya Jumamosi asubuhi itatia ndani hotuba ya ubatizo, na kutakuwa na fursa ya kubatiza wale wanaostahili. Katika kipindi cha alasiri, ripoti zenye kutia moyo zitatolewa za jinsi ambavyo watu wameitikia kweli ya Biblia katika nchi fulani-fulani za Amerika ya Latini, Afrika, Ulaya Mashariki, na pia katika nchi kubwa mno ya Kazakhstan huko Asia. Kichwa cha hotuba hiyo ni “‘Vitu Vinavyotamaniwa’ Vinaijaza Nyumba ya Yehova.” Programu ya Jumamosi itafikia tamati kwa hotuba mbili, “Maandiko ya Kiunabii Hututahadharisha Tuwe Wenye Kulinda” na “Neno la Kiunabii Wakati wa Mwisho.” Hotuba ya kumalizia itakazia kitabu cha Biblia cha Danieli na itatoa sababu za kusikiliza unabii wake.
Jumapili asubuhi mfululizo wa muda wa saa moja wenye sehemu tatu, “Maneno ya Kiunabii kwa Ajili ya Wakati wa Mwisho” utazungumzia unabii wa Habakuki. Utaona jinsi kitabu hiki cha Biblia chenye sura chache kinavyoweza kuwatia moyo Wakristo leo. Baadaye drama yenye mavazi kamili, kuhusu simulizi la Biblia la Yakobo na Esau, itakazia kichwa “Kuthamini Urithi Wetu wa Kiroho.” Programu ya Jumapili asubuhi itafikia tamati kwa hotuba yenye kuchochea yenye kichwa “Urithi Wetu Wenye Thamani Humaanisha Nini Kwako?” Kisha alasiri, utafurahia hotuba ya watu wote “Kufanya Vitu Vyote Kuwa Vipya—Kama Ilivyotabiriwa.”
Panga sasa kuhudhuria. Kwa habari juu ya mahali karibu na unapoishi, wasiliana na Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova lililo karibu au andikia wachapishaji wa gazeti hili. Gazeti-jenzi letu, Mnara wa Mlinzi, katika toleo la Februari 15, 1999 liliorodhesha mahali pote pa mikusanyiko katika Burundi, Kenya, Kongo (Kinshasa), Rwanda, Tanzania, na Uganda.