Mbegu Zilizozaa Matunda Miaka Mingi Baadaye
Barua ifuatayo ilipokewa kwa sababu ya ile makala “Magumu na Baraka za Kulea Wana Saba,” katika “Amkeni!” la Januari 8, 1999.
Ndugu na Dada Dickman Wapendwa,
Nimemaliza tu kusoma simulizi lenu, na sina budi kuwaandikia barua. Niliifahamu familia yenu miaka kadhaa iliyopita huko Mississippi [1960-1961]. Kwa hakika, nilisomea shule moja na wana wenu, na nilizoea kuja nyumbani kwenu na kucheza na wana wenu mara nyingi. Lakini haya si ndiyo mambo yaliyonivutia zaidi nilipokuwa mchanga. Hata nikiwa na umri mchanga hivyo, nilivutiwa sana na jambo la kwamba wana wenu hawakuisalimu bendera shuleni kwa sababu ya dhamiri zao za Kikristo. Ijapokuwa nilikuwa mshiriki wa Grandview Baptist Church, wakati mwana wenu mmoja aliponieleza msimamo wake, nilijua kwamba ulikuwa sawa.
Mmojawapo wa wana wenu alinipa kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana,a au labda nilikiiba. Sikumbuki nilikipataje, lakini nilikisoma chote. Wakati huo, nilikiona kuwa kitabu cha hadithi tu chenye kupendeza. Sikung’amua kamwe kwamba mbegu za kweli zilikuwa zimepandwa na kwamba hazingekua kwa miaka mingi.
Familia yangu ilihamia Kaskazini mnamo mwaka wa 1964, nami nikaacha kwenda kanisani. Unafiki wa dini ulinikatisha tamaa, kwa hiyo kwa miaka mingi sikutaka kujihusisha na mambo ya dini.
Miaka mingi baadaye, nilipoanza kufikiria sana juu ya kusudi la maisha, niling’amua kwamba nilihitaji kuwa na uhusiano na Muumba. Nilitaka kuwa na uhusiano ambao haukuwa na unafiki wa kidini. Mbegu hizo za kweli zilizopandwa miaka mingi awali zilikuwa zinaanza kuchipuka; na bado sikutambua hivyo.
Nilifikiri sana juu ya uhakika wa kwamba sikutaka kwenda mbinguni; nilitaka kuishi papa hapa duniani. Nilihisi kwamba sayari hii iliumbwa kwa njia ya kustaajabisha, sasa kwa nini Mungu aiangamize? Pia sikumfikiria Yesu kuwa Mungu. Ikiwa alikuwa Mungu, basi dhabihu yake ingekuwa hila. Mawazo, hisi, na masadikisho haya, ukipenda kuyaita hivyo, hayangeweza kupatanishwa na yale niliyokuwa nimejifunza katika Kanisa Baptisti. Basi nilianza kusali, nilisali kwa bidii, na Yehova akanijibu upesi. Mashahidi walikuja mlangoni pangu siku chache baadaye, na mara moja funzo la Biblia likaanzishwa. Hata ingawa sikuwahi kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova tangu wakati nilipofahamu familia yenu hadi nilipoanza kujifunza, sikukosa kamwe kuwaheshimu wana wenu kwa sababu ya msimamo wao kwa ajili ya mambo yaliyo sawa. Nilipoanza tu kujifunza na kutwaa ujuzi, niliyaelewa mambo yote. Ilinichukua muda wa mwaka mmoja na nusu kurekebisha maisha yangu. Hatimaye nilibatizwa mnamo mwaka wa 1975.
Wakati wowote tunapofikiria jinsi mwenendo wetu unavyoweza kutoa ushahidi bila hata sisi kujua, mimi huikumbuka familia yenu. Tunapofikiria umuhimu wa kupanda mbegu nyingi za Ufalme kwa sababu sikuzote hatujui ni wapi au ni lini zitakapokua, ninajua ukweli wa jambo hilo kwa sababu ya yale yaliyonipata.
Ningependa kuwashukuru kwa sababu ya kuwa miongoni mwa watu wa Yehova na kuishi kupatana na itikadi zenu hapo zamani. Bila nyinyi kujua mlimsaidia mtu fulani apate kweli. Mwenendo na usadikisho wenu, na wa wana wenu, ulifanya kweli ing’ae na kupenya. Nilifikiri kwamba singewahi kujua mlipo au kupata kuwashukuru. Asanteni tena.
Upendo Mwingi wa Kikristo,
L. O.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., mwaka wa 1958; sasa hakichapishwi tena.