Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 8/8 kur. 18-20
  • Muungano wa Kidini Katika Ndoa—Sababu Ni wa Maana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Muungano wa Kidini Katika Ndoa—Sababu Ni wa Maana
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kusudi la Ndoa
  • Ndoa Bora
  • Uvutio na Kanuni Zilezile
  • Vipi Juu ya Watoto?
  • “Katika Bwana” Kweli Kweli
  • Ndoa—Zawadi Kutoka kwa Mungu Mwenye Upendo
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Ndoa​—Zawadi Kutoka kwa Mungu
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Biblia Inasema Nini Kuhusu Ndoa?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Mwongozo wa Mungu Katika Kuchagua Mwenzi wa Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 8/8 kur. 18-20

Maoni ya Biblia

Muungano wa Kidini Katika Ndoa—Sababu Ni wa Maana

FAMILIA yaketi kula chakula cha jioni. Baba anapotoa sala, mama aomba kimya-kimya kwa mungu mwingine. Katika familia nyingine mke huabudu kanisani, lakini mume wake huhudhuria ibada kwenye sinagogi. Kuna familia ambapo mzazi mmoja huwafundisha watoto kuhusu Baba Krismasi, huku mwingine akiwaeleza juu ya sikukuu iitwayo Hanukkah.

Kulingana na uchunguzi wa hivi karibuni, hali kama hizo zimekuwa za kawaida zaidi kwa kuwa watu wengi zaidi wanafunga ndoa na mtu asiye wa dini yao. Uchunguzi mmoja waonyesha kwamba huko Marekani, sasa asilimia 21 ya Wakatoliki hufunga ndoa na watu wasio wa dini yao; miongoni mwa Wamormon, asilimia 30; kwa Waislamu, asilimia 40; na kwa Wayahudi, zaidi ya asilimia 50. Kwa kufikiria uhasama ambao umekuwako kati ya dini kwa karne nyingi, watu fulani huona ndoa ya watu wa dini tofauti kuwa ushindi dhidi ya kutovumiliana. Mwandishi wa habari wa gazeti moja aliandika hivi: “Ndoa za mseto wa aina yoyote zapasa kutukuzwa.” Je, hayo ndiyo maoni ya Biblia?

Na itambuliwe kwamba Biblia haiungi mkono ubaguzi wa kijamii au wa kikabila. Neno la Mungu hukuza kutobaguana kwa kijamii. Mtume Petro alisema waziwazi kuhusu jambo hili: “Kwa hakika nahisi kwamba Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Na wakati huohuo, Biblia hufundisha kwamba waabudu wa kweli wa Yehova wanapaswa kufunga ndoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Kwa nini?

Kusudi la Ndoa

Mungu alikusudia ndoa iwe kifungo mahususi cha ukaribu. (Mwanzo 2:24) Alipoanzisha mpango wa ndoa, Mungu alikuwa akifikiria mengi zaidi ya uandamani. Yehova alipowapa watu wawili wa kwanza mgawo wa kulea watoto na kutunza makao yao ya kidunia, alionyesha kwamba walipaswa kufanya kazi kwa ukaribu katika kutimiza mapenzi yake. (Mwanzo 1:28) Kwa kushirikiana katika kumtumikia Mungu katika jambo hili, mwanamume na mwanamke hawangefurahia tu uandamani, bali pia urafiki wa karibu na wa kudumu.—Linganisha Malaki 2:14.

Yesu aligusia urafiki huo aliposema maneno yanayojulikana vema: “Wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.” (Mathayo 19:6) Yesu alitumia lugha ya sitiari kulinganisha muungano wa ndoa na nira inayofunga pamoja wanyama wawili wa mizigo ili kuvuta au kusongeza mzigo uleule. Ebu wazia mkazo unaowapata wanyama wawili waliofungiwa nira wanapovuta kuelekea pande tofauti-tofauti! Vivyo hivyo, wale wanaofunga ndoa na mtu asiye katika imani ya kweli huenda wakapata mkazo wa kuishi kupatana na kanuni za Biblia huku mwenzi akipinga. Kwa kufaa, Biblia husema: “Msiwe wenye kufungwa nira isiyosawazika pamoja na wasio waamini.”—2 Wakorintho 6:14.

Ndoa Bora

Muungano katika ibada ya kweli waweza kuimarisha sana ndoa. Mwandishi mmoja alisema: “Kuabudu pamoja ni mojawapo ya mambo muhimu ya familia zenye hali nzuri na furaha.” Mhubiri 4:9, 10 husema: “Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja; maana wapata ijara njema kwa kazi yao. Kwa maana wakianguka, mmoja wao atamwinua mwenzake.”

Kwa kufanya ibada yao iwe jambo kuu maishani mwao, wenzi wa ndoa Wakristo wanaungana si kimwili tu bali pia kiroho. Wanaposali pamoja, kujifunza Neno la Mungu pamoja, kukutana na Wakristo wenzao, na kushiriki imani yao na wengine, wanafanyiza kifungo cha kiroho ambacho hufanya wawe na ukaribu zaidi katika ndoa yao. Mwanamke mmoja Mkristo alisema hivi: “Ibada ya kweli ni njia ya maisha. Siwezi kuwazia kuolewa na mtu ambaye hashiriki msimamo unaohusu jinsi nilivyo.”—Linganisha Marko 3:35.

Wale wanaofunga ndoa “katika Bwana” wanaweza kutarajia wenzi wao waige mwenendo wa Yesu. Waume Wakristo wanapaswa kuwatendea wake zao kama vile Yesu alivyolitendea kutaniko kwa njia ya upendo. Wake Wakristo wanapaswa kuwastahi waume zao. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:25, 29, 33) Wakristo hufanya hivyo si kwa kutamani tu kuwapendeza wenzi wao bali pia ili kumpendeza Mungu, ambaye atawatoza hesabu wenzi wa ndoa kwa namna wanavyotendeana.—Malaki 2:13, 14; 1 Petro 3:1-7.

Kushikamana na itikadi zilizowekwa ambazo wanashiriki pia husaidia wenzi Wakristo kutatua tofauti zao kwa njia ya amani. Biblia huwashauri Wakristo wazingatie, “si masilahi ya kibinafsi ya mambo [yao] wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.” (Wafilipi 2:4) Bila kujali mapendezi ya kibinafsi, wenzi ambao wameunganishwa na imani hutegemea Neno la Mungu kuwa mamlaka ya pamoja ya kutatua tofauti zozote. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa njia hii wanatii shauri la Biblia kwa Wakristo la kuwa katika “akili ileile.”—1 Wakorintho 1:10; 2 Wakorintho 13:11; Wafilipi 4:2.

Uvutio na Kanuni Zilezile

Ni kweli kwamba kuna mengi zaidi yanayotakikana kwa uhusiano kuliko kushiriki tu imani ileile. Uvutio wa watu wawili ni jambo ambalo huchangia. (Wimbo Ulio Bora 3:5; 4:7, 9; 5:10) Lakini ili ndoa idumu, ni muhimu kufuata kanuni zilezile. Kulingana na kitabu Are You the One for Me? “wenzi wa ndoa ambao hufuata kanuni zilezile wana uwezekano mkubwa zaidi wa kuanzisha uhusiano wenye furaha, wenye upatano, na wa kudumu.”

Kwa kusikitisha, watu wanaovutiana huenda wasishughulikie tofauti kubwa kati yao mpaka baada ya ndoa. Kwa kulinganisha, ebu wazia ukinunua nyumba kwa sababu tu unapenda jinsi inavyoonekana. Hata hivyo, baada ya kuhamia ndani, unakuta kwamba msingi wake si imara. Msingi usio imara unafanya sehemu zote za nyumba hiyo zenye kupendeza ziwe bure. Vivyo hivyo, huenda mtu akavutiwa na mtu mwingine wa imani tofauti anayeonekana kuwa wanafaana—lakini baada ya ndoa huenda uhusiano huo ukageuka kuwa na kasoro kubwa sana.

Fikiria magumu fulani yawezayo kutokea baadaye katika ndoa za dini mbili: Familia itaabudu wapi? Watoto watalelewa katika dini gani? Familia itategemeza kifedha dini gani? Je, mwenzi mmoja wa ndoa atasisitiza kushiriki katika desturi na sikukuu fulani za kidini ambazo yule mwingine anaziona kuwa za kipagani? (Isaya 52:11) Kila ndoa hutaka kila mwenzi afanye marekebisho yafaayo; hata hivyo, kuridhiana kanuni za Biblia—hata kwa kuhifadhi ndoa—hakukubaliki na Mungu.—Linganisha Kumbukumbu la Torati 7:3, 4; Nehemia 13:26, 27.

Ili kudumisha amani katika ndoa, wenzi fulani katika ndoa zilizogawanyika kidini hufuatia dini zao wenyewe. Ingawa hivyo, kwa kusikitisha hali ya kila mtu kufuata dini yake hutokeza pengo la kiroho katika ndoa. Mwanamke mmoja Mkristo aliyeolewa na mwanamume ambaye hakushiriki imani yake alisema: “Ijapokuwa tulikuwa tumefunga ndoa kwa miaka 40, kwa kweli mume wangu hakunijua.” Tofauti na hilo, Mungu huwa wa muhimu katika ndoa ambamo wenzi wote wawili huabudu “kwa roho na kweli.” Kama Biblia isemavyo kishairi, “kamba ya nyuzi tatu haikatiki upesi.”—Yohana 4:23, 24; Mhubiri 4:12.

Vipi Juu ya Watoto?

Watu fulani wanaofikiria ndoa ya dini mbili waweza kuhisi kwamba wanaweza kuwafundisha watoto wao dini mbili na kuwaruhusu watoto hao wajichagulie dini. Ni kweli kwamba wazazi wote wawili wana haki ya kisheria na ya kiadili ya kuwazoeza watoto wao kidini, na hatimaye watoto wajiamulie wenyewe.a

Biblia huwaagiza watoto wawatii wazazi wao “katika muungano na Bwana.” (Waefeso 6:1) Mithali 6:20 husema hivi: “Mwanangu, shika maagizo ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” Badala ya kupata mafundisho mbalimbali, watoto wanaolelewa na wazazi walio na itikadi moja wanaungana katika ile ambayo Biblia huiita “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja.”—Waefeso 4:5; Kumbukumbu la Torati 11:19.

“Katika Bwana” Kweli Kweli

Ikiwa kushiriki kanuni zilezile ndio ufunguo wa ndoa yenye mafanikio, je, lingekuwa jambo la hekima kufunga ndoa na mtu yeyote tu anayedai kuwa Mkristo? Biblia hujibu: “Yeye ambaye husema akaa katika muungano na [Yesu] yuko chini ya wajibu yeye mwenyewe pia kuendelea kutembea kama vile huyo alivyotembea.” (1 Yohana 2:6) Hivyo, Mkristo anayefikiria ndoa angetafuta Mkristo mwenzi anayejitahidi kikweli kumfuata Yesu. Mtu huyo anayetarajiwa kuwa mwenzi angekuwa ameweka maisha yake wakfu kwa Mungu na kubatizwa. Angeiga utu wenye upendo wa Yesu na jinsi alivyohubiri Ufalme wa Mungu kwa bidii. Kama ilivyokuwa kwa Yesu, angekazia kufanya mapenzi ya Mungu maishani mwake.—Mathayo 6:33; 16:24; Luka 8:1; Yohana 18:37.

Kwa kungoja kwa saburi mwenzi anayefaa miongoni mwa familia ya waabudu wa Mungu, wale wanaofikiria ndoa huweka kiolezo cha kutanguliza mapenzi ya Mungu maishani mwao. Kiolezo cha namna hiyo hatimaye kitachangia ndoa yenye furaha na yenye kuridhisha zaidi.—Mhubiri 7:8; Isaya 48:17, 18.

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala “Maoni ya Biblia: Je, Watoto Wapaswa Kuchagua Dini Yao Wenyewe?” katika toleo la Amkeni! la Machi 8, 1997, ukurasa wa 26-27. Pia, ona ukurasa wa 24-25 wa kichapo Mashahidi wa Yehova na Elimu, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., 1995.

[Sanduku katika ukurasa wa 20]

Msaada kwa Familia Zilizogawanyika Kidini

Wenzi wengi wa ndoa leo wamegawanyika kidini kwa sababu mbalimbali. Huenda watu fulani walichagua mwenzi wa dini tofauti. Lakini wenzi wengi walianza kwa kushiriki dini ileile na baadaye wakagawanyika kidini mwenzi mmoja alipoanza kufuatia ibada nyingine. Huenda kukawa na mambo mengine ambayo husababisha migawanyiko ya kidini katika familia. Hata hivyo, bila kujali sababu hizo, nadhiri za ndoa hazipasi kuvunjwa wala kupuuzwa kwa sababu tu wenzi wanakosa kukubaliana kuhusu dini wanayochagua. Biblia hustahi utakatifu wa ndoa na ndoa zenye kudumu, hata wakati wenzi wanapokuwa hawajaungana katika ibada. (1 Petro 3:1, 2) Mtume Paulo aliandika: “Ikiwa ndugu yeyote ana mke asiyeamini, na bado ni mwenye kukubali kukaa pamoja naye, asimwache.” (1 Wakorintho 7:12) Kanuni zinazopatikana katika Biblia zinapotumiwa zinaweza kusaidia wenzi wowote wa ndoa wafurahie amani katika uhusiano wenye upendo na staha.—Waefeso 5:28-33; Wakolosai 3:12-14; Tito 2:4, 5; 1 Petro 3:7-9.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki