Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 10/8 kur. 5-8
  • Sababu Inayofanya Muziki Utuathiri

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sababu Inayofanya Muziki Utuathiri
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mambo Yanayohusu Muziki
  • Upatano, Kutopatana, na Melodia
  • Muziki na Ubongo
  • Muziki, Maneno ya Wimbo, na Wewe
  • Ninaweza Kuwekaje Muziki Mahali Pao Panapofaa?
    Amkeni!—1993
  • Jilinde na Muziki Usiofaa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Ninaweza Kuwa na Usawaziko Jinsi Gani Kuhusu Muziki?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Je, Utafanya Maamuzi Yenye Hekima?
    Amkeni!—2011
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 10/8 kur. 5-8

Sababu Inayofanya Muziki Utuathiri

MUZIKI na lugha ni mambo yanayofanywa na wanadamu peke yao. Ingekuwa vigumu kuwazia ulimwengu usio na mambo hayo. “Lugha pamoja na muziki ni mambo yanayofanywa na wanadamu ulimwenguni pote,” chasema kitabu The Musical Mind. Hayo ni mambo yanayohusu uhitaji tulio nao wa kuwasiliana. Kwa hiyo, inaweza kusemwa kwamba kama ilivyo na lugha, muziki “unaposema” hisia-moyo zetu “husikiliza.”

Ni kwa nini na kwa njia gani muziki husema kwa hisia-moyo zetu? Ili kujibu swali hilo, tunahitaji kufikiria: (1) mambo yenyewe yanayohusu muziki na jinsi ubongo wetu huyashughulikia; (2) hisia-moyo zetu na malezi yetu, ambayo huathiri jinsi tunavyoitikia muziki; na (3) lugha, ambayo inaweza kuathiri pia itikio letu.

Mambo Yanayohusu Muziki

Sifa mbalimbali za ala za muziki tofauti-tofauti mara nyingi hurejezewa kuwa “mambo yanayohusu muziki.” Mambo hayo hutia ndani toni ya ala. Kwa kielelezo, tarumbeta sikio imefafanuliwa kuwa yenye “fahari” au nzito na mlio wake huwa tofauti kabisa na wa tarumbeta “yenye kiburi.” Ijapokuwa zote mbili ziko katika kikundi kimoja cha ala za muziki wa kupuliza, kila moja hutokeza alama za juu za noti au ulinganifu wa sauti, wenye nguvu zinazotofautiana. Jambo hili ndilo huipa kila ala ya muziki “sauti” yake ya pekee. Waimbaji hutumia sifa hizi ili kutokeza mawimbi-sauti kusudi wachochee hisia-moyo za wasikilizaji.

Labda jambo la kwanza tunalofahamu ni mfuatano wa muziki—labda tunapokuwa tungali katika tumbo la uzazi, tukisikiliza mpigo wa moyo wa mama. Imesemwa kwamba huenda namna tunavyoitikia mfuatano wa muziki kukaathiriwa na mpigo wetu wa moyo au kupumua pasipo kutambua. Kwa sababu hiyo, si sadfa kwamba watu wengi hupendelea muziki wenye mwendo wa mapigo 70 na 100 kwa dakika—yanayolingana na mpigo wa moyo wa wastani wa mtu mzima mwenye afya nzuri. Angalau jambo hilo ndilo linalodokezwa katika jarida Perceptual and Motor Skills.

Mambo mengi ya namna mbalimbali yahusuyo muziki yaweza kutambuliwa wakati milio na melodia zinazotokezwa na ala tofauti-tofauti zinapofikiriwa. Mlio wenye kugusa wa tarumbeta katika kizio cha pili cha koncheto ya Mozart ya tarumbeta waweza kuchochea hisia-moyo za ndani kabisa. Mlio wa huzuni wa filimbi ya Kijapani shakuhachi waweza kugusa moyo kwa njia ya werevu. Sauti ya mkwaruzo ya saksafoni hufanya melodia ya muziki wa jazi ibaki akilini mwa watu wengi. Kwa kawaida besi ya tuba katika bendi ya Ujerumani huchochea hisia changamfu sana. Tuni zenye kuchangamsha za fidla zinazocheza msowero wa mwimbaji Strauss huchochea wasikilizaji wengi watake kuanza kucheza dansi. Kunakuwa na matokeo kama hayo kwa sababu “muziki hunena kwa mwanadamu mzima,” kulingana na Clive E. Robbins, wa kituo cha Nordoff-Robbins Music Therapy Center, huko New York.

Upatano, Kutopatana, na Melodia

Upatano hutokeza milio inayopendeza, ilhali kutopatana hutokeza milio isiyofurahisha. Lakini je, uliwahi kujua kwamba mambo hayo hukamilishana katika muziki wa aina fulani? Muziki unaosikika kuwa wenye upatano huenda ukawa na kutopatana kwingi sana kuliko ambavyo ungewazia. Kuingiliana daima kati ya upatano na kutopatana hutokeza ongezeko la fadhaa inayobadilika-badilika, ingawa mara nyingi haionekani, inadhihirishwa kwa hisia-moyo zetu. Kubadilika-badilika huku kwa kihisia-moyo hutuliza, ilhali muziki usiopatana peke yake unaweza kusumbua na kuchochea hisia zisizopendeza—kama vile kukwaruza kucha za vidole kwenye kibao au kwenye ubao wa kuandikia. Kwa upande mwingine, ikiwa muziki unapatana tu, unaweza kuchosha.

Melodia ni mpangilio wa tuni za noti mojamoja zinazofuatana. Kulingana na vichapo fulani, neno hilo latokana na neno la Kigiriki meʹlos, linalomaanisha “wimbo.” Kulingana na kamusi, melodia ni muziki unaopendeza, sauti yoyote inayopendeza.

Hata hivyo, melodia inayopendeza haifanyizwi tu na mfuatano wa sauti zozote. Kwa kielelezo, muda mrefu unaopita kati ya noti zenye kufuatana waweza kufanya melodia iwe yenye kutokeza lakini isipendeze. Kwa upande mwingine, noti zenye kufuatana kwa muda mfupi zaweza kufanyiza melodia yenye kupendeza. Mpangilio tofauti-tofauti wa noti na muda ulioko katikati hufanya melodia iwe ya kuhuzunisha au ya kufurahisha. Kama ilivyo na upatano, melodia hutokeza fadhaa, zinazoathiri hisia-moyo zetu kwa sababu ya kuongezeka na kupungua kwa sauti—yaani, ukubwa au udogo wa sauti.

Mambo hayo yote yanapounganishwa, hutokeza kani zenye nguvu zinazoweza kutuliza au kuchochea hisia-moyo zetu. Hii ni kwa sababu ya njia mbalimbali ambazo ubongo wetu hutambua na kutokeza muziki.

Muziki na Ubongo

Watu fulani wanadokeza kwamba lugha na mantiki ni utendaji unaotukia hasa kwenye upande wa kushoto wa ubongo, ilhali muziki hutokezwa kwenye upande wa kulia wa ubongo, ambao hushughulika hasa na hisia-moyo. Kama jambo hilo ni kweli au sivyo, ni wazi kwamba muziki huchochea maitikio yanayojitokeza yenyewe kutoka kwa wasikilizaji. Jarida Perceptual and Motor Skills yaueleza jinsi hii: “Muziki una uwezo wa kutokeza hisia kwa njia ya haraka na yenye matokeo. Jambo ambalo lingehitaji kufafanuliwa kwa sentensi nyingi katika kitabu . . . , mara nyingi laweza kujulishwa kwa mdundo mmoja tu au tuni kadhaa za muziki zinazovumishwa wakati mmoja.”

Kuhusu utendeano ulioko kati ya kuona na kusikia na itikio kwa kila moja, kitabu Music and the Mind chatoa maoni haya yenye kupendeza: “Kuna uhusiano wa karibu zaidi kati ya kusikia na kuamshwa kwa hisia-moyo kuliko ulivyo kati ya kuona na kuamshwa kwa hisia-moyo. . . . Kutazama mnyama aliyejeruhiwa au mtu anayeteseka ambaye yuko kimya kwaweza kutokeza itikio dogo sana la kihisia-moyo kwa mtazamaji. Lakini mara waanzapo kupiga yowe, kwa kawaida hisia za mtazamaji huguswa sana.”

Muziki, Maneno ya Wimbo, na Wewe

Kikundi kimoja cha watu wenye maoni sawa kinadai kwa dhati kwamba wimbo hususa una matokeo yaleyale kwa wasikilizaji wote. Hata hivyo, kikundi kingine chasema kwamba itikio kwa melodia au wimbo hudhihirisha hali ya akili ya sasa ya mtu au jambo lililoonwa wakati uliopita. Mfano wa hilo waweza kuwa wakati mtu fulani ambaye amefiwa na mpendwa wake anaposikia wimbo fulani, labda kwenye mahali pa ibada. Wimbo huo waweza kuleta kumbukumbu na kusababisha huzuni au hata kufanya machozi yaanze kumlenga-lenga mtu aliyefiwa. Wengine wasiokuwa katika hali hiyo waweza kuimba wimbo huohuo kwa moyo wenye shangwe.

Pia fikiria ufafanuzi wa tarumbeta sikio na tarumbeta uliotolewa mapema. Huenda usikubali kwamba tarumbeta sikio hutoa sauti yenye fahari. Huenda ukaisikia kuwa yenye kusumbua, ilhali tarumbeta huenda ikaamsha hisia-moyo za ndani kabisa. Kila mmoja wetu ana chemchemi ya pekee ya hisia inayoweza kuchochewa na muziki—hivyo tunauitikia kwa njia yetu wenyewe.

Muziki husaidia kuunganisha maneno au mawazo na kwa hisia-moyo. Kwa sababu hiyo, matangazo machache ya biashara katika televisheni au redio huonyeshwa bila kuandamana na muziki. Mara nyingi maneno hayo huwa hayana maana sana. Hata hivyo, ikiwa muziki wa chini chini unaofaa watumiwa, tangazo la biashara litaathiri hisia-moyo za msikilizaji. Ni kweli kwamba kusudi la matangazo mengi ya biashara ni kufanya watu wanunue vitu kwa kusukumwa na hisia-moyo wala si kwa kutumia akili!

Ilhali matangazo ya biashara yaweza kuathiri isivyofaa pesa za umma, kuna upande mbaya zaidi kuhusu uwezo wa maneno ya nyimbo na muziki. Jarida Journal of Youth and Adolescence ladokeza kwamba kupitia maneno ya nyimbo yanayorudiwa-rudiwa, watunzi wa nyimbo huwafunza vijana wabalehe wapuuze maoni ya watu wengine na “kushikilia sana kauli yao.” Kulingana na kichapo kingine, jumbe zinazotolewa na “maneno ya nyimbo za rapu yanayobishaniwa . . . , yaliyo wazi zaidi kuliko yale ya nyimbo zenye mdundo mzito,” zaweza kupenya ndani kabisa ya hisia-moyo za msikilizaji na kutokeza tabia ya kujitenga na watu.

Je, itikio lisilofaa lingeweza kuepukwa ikiwa mtu angesikiliza muziki tu na kupuuza maneno ya wimbo? Ni kweli kwamba kwa kiasi kikubwa, ni vigumu kusikia maneno ya muziki wenye mdundo mzito na wa rapu. Kwa hakika, mara nyingi karibu hayaeleweki sauti ya muziki inapokuwa ya juu kupita kiasi. Lakini, kuwe kuna maneno yanayoeleweka au la, ujumbe ungali katika mdundo unaofuatana na melodia inayorudiwa!

Jinsi gani hivyo? Naam, baadhi ya majina peke yake hutokeza dhana. Zaidi ya hilo, mara nyingi aina yenyewe ya muziki ndiyo huwa ujumbe. Ni ujumbe gani unaotokezwa? Jarida moja la vijana lasema: “Unaonekana kuwa dhana ya mamlaka, uwezo wa kusababisha tokeo hususa, na ushindi wa kingono.” Jingine lasema: “Vichwa vya msingi . . . ni uasi unaopita kiasi, jeuri, utumizi mbaya wa dawa za kulevya, ngono za ovyoovyo, upotovu, na Ibada ya Shetani.”

Vijana fulani wanadai kwamba ingawa hiyo yaweza kuwa ni kweli, hawaathiriwi kwa njia isiyofaa. Watatoa hoja kwamba muziki huo unafaa kwa sababu unawasaidia ‘wajitambue wenyewe.’ Je, unafanya hivyo? Jarida Journal of Youth and Adolescence lasema: “Ile hasira, mambo yenye uhasama yanayokaziwa, na mamlaka ambayo vijana fulani wanajihusisha nayo katika muziki wenye mdundo mzito yaweza kufurahisha hasa siku iishapo kwa vijana wasiofua dafu shuleni baada ya kuvumilia siku moja wakiwa shuleni na kuambiwa kwamba hawajafuzu.” Kisha laongezea: “Jambo lililo kinyume na hilo au la kushangaza ni kwamba jitihada ya vijana ya kutafuta usalama zaidi huhusisha kushiriki njia ya umma ya kuwasilisha habari. Badala ya kutafuta mambo ya pekee kikweli wanapokuwa peke yao, vijana wanaobalehe hujitahidi kupata dhana iliyo tayari inayotolewa na viwanda vya biashara.” Yaani, mtu mwingine anawaambia vijana hawa mambo wanayohitaji kufikiri na jinsi wanavyopaswa kuhisi.

Acheni tuchunguze maonyesho ya muziki wa roki. Yanaathirije umati mkubwa unaohudhuria? Kitabu Music and the Mind chajibu: “Hakuna shaka kwamba kwa kuchangamsha hisia za umati na kwa kuhakikisha kwamba hisia hizo zinafikia kilele wakati uleule badala ya pindi mbalimbali, muziki unaweza kuchangia sana kutofanya uamuzi unaofaa, kufuata hisia za wakati huo bila ufahamu wowote, jambo lililo hatari sana linaloonyesha tabia ya umati.” Baadhi ya mambo yanayoonekana kwenye maonyesho ya muziki wa roki yasiyodhibitiwa hudhihirisha ukweli wa taarifa hiyo.

Kwa hiyo, ili kuepuka kuchafua akili na moyo, lazima tuteue sana muziki. Tunaweza kufanyaje hivyo? Makala yetu ya kumalizia itajibu swali hilo.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mara nyingi muziki huwafanya wasikilizaji watake kucheza dansi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki